Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Umutegemee Yehova Sikuzote!

Umutegemee Yehova Sikuzote!

‘Mumutegemee nyakati zote [nyinyi watu].’ZAB. 62:8.

1-3. Ni nini ilimusaidia mutume Paulo amutegemee kabisa Yehova? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

ILIKUWA hatari kuwa Mukristo katika muji wa Roma. Wafuasi wa Kristo waliteswa sana kwa sababu walishitakiwa kwamba waliunguza muji wa Roma katika mwaka wa 64, na kwamba waliwachukia watu wengine. Ikiwa ungekuwa Mukristo wakati huo, kila siku ungekuwa katika hatari ya kukamatwa na kuteswa. Inawezekana ndugu na dada zako fulani wa kiroho waliraruliwa (kupasuliwa vipande-vipande) na wanyama, ao walitundikwa kwenye miti na kuunguzwa wangali wazima ili watoe mwangaza usiku.

2 Inawezekana mutume Paulo alifungwa huko Roma kwa mara ya pili katika hali hiyo yenye muvurugo. Je, mutume Paulo alipata musaada kutoka kwa Wakristo wengine? Inawezekana mwanzoni mutume Paulo alikuwa na wasiwasi, kwa sababu alimuandikia Timotheo hivi: “Katika kujitetea kwangu mara ya kwanza hakuna yeyote aliyekuja upande wangu, bali wote waliniacha—hilo lisihesabiwe kwao.” Hata hivyo, mutume Paulo alielewa kwamba hakuachiliwa kabisa. Aliandika hivi: ‘Lakini Bwana alisimama karibu na mimi na kutia nguvu ndani yangu.’ Kwa kweli, Bwana Yesu alimupatia mutume Paulo nguvu zenye alikuwa nazo lazima. Musaada huo ulikuwa na matokeo gani? Mutume Paulo alisema hivi: ‘Na mimi nilikombolewa kutoka katika kinywa cha simba.’—2 Tim. 4:16, 17. *

3 Bila shaka kukumbuka jambo hilo kulimutia nguvu mutume Paulo, na kulimusaidia akuwe na tumaini kwamba Yehova atamupatia nguvu ili avumilie majaribu ya wakati huo, na mateso mengine yenye angepata. Ndiyo sababu, hakusita kusema hivi: “Bwana atanikomboa kutoka katika kila tendo la uovu.” (2 Tim. 4:18) Bila shaka, mutume Paulo alikuwa amejifunza kwamba hata kama wanadamu wanaweza kumusaidia kwa kiasi fulani, Yehova na Mwana wake wanaweza kumusaidia kabisa-kabisa!

TUKO NA NAFASI ZA KUONYESHA KWAMBA ‘TUNAMUTEGEMEA YEHOVA’

4, 5. (a) Ni nani anaweza sikuzote kukutolea musaada wenye unahitaji? (b) Namna gani unaweza kufanya urafiki wako pamoja na Yehova ukuwe wenye nguvu?

4 Kuna siku ulijisikia kwamba umeachiliwa wakati ulipambana na hali ngumu? Pengine ulikosa kazi, ulipambana na mikazo kwenye masomo, ulikuwa na ugonjwa fulani, ao ulipambana na hali zingine zenye kuhuzunisha. Pengine uliomba musaada, lakini ulivunjika moyo kwa sababu wengine hawakukupatia musaada wenye ulikuwa nao lazima. Bila shaka, kuna magumu fulani yenye wanadamu hawawezi kumaliza. Katika hali kama hizo, je shauri la Biblia lenye kutuomba ‘tumutegemee Yehova’ halina faida yoyote? (Met. 3:5, 6) Ao halina maana yoyote? Jibu ni hapana kabisa! Mungu anaweza kukutolea musaada wa kweli kabisa. Biblia iko na mifano mingi yenye kuonyesha jambo hilo.

5 Usisirike ikiwa watu hawakupatie musaada wenye unahitaji wakati wa magumu. Lakini, kama vile mutume Paulo, uone magumu yenye unapata kuwa nafasi za kuonyesha kwamba unamutegemea Yehova kabisa. Pia hali hiyo inakutolea nafasi ya kuona katika maisha yako namna Yehova anakuhangaikia. Jambo hilo litakusaidia umutegemee kabisa na kufanya urafiki wako pamoja naye ukuwe wa kweli zaidi.

NI LAZIMA TUMUTEGEMEE MUNGU ILI TUKUWE MARAFIKI WAKE

6. Sababu gani inaweza kuwa vigumu kumutegemea Yehova wakati wa magumu?

6 Unaweza kuwa na magumu fulani yenye inakusumbua. Umefanya yako yote kuhusu magumu hayo, na umesali ili kumuomba Yehova musaada. Unaweza sasa kuwa na amani na kutumaini kwamba Yehova atakusaidia? Bila shaka! (Soma Zaburi 62:8; 1 Petro 5:7.) Ikiwa unapenda kuwa na urafiki muzuri pamoja na Yehova, ni jambo la lazima ujifunze kumutumainia. Lakini, inaweza kuwa vigumu kutumaini kwamba Yehova atakutolea musaada wenye unahitaji. Sababu gani? Sababu moja ni kwamba, kila mara Yehova hajibiake sala palepale.—Zab. 13:1, 2; 74:10; 89:46; 90:13; Hab. 1:2.

7. Sababu gani Yehova hajibiake sala zetu zote palepale?

7 Sababu gani Yehova hajibiake sala zetu zote palepale? Kukumbuka kwamba Yehova anafananisha uhusiano wetu pamoja naye na ule wa muzazi na watoto wake. (Zab. 103:13) Mutoto hawezi kutumaini kabisa kwamba muzazi atamupatia kila kitu chenye anaomba ao kufanya hivyo palepale. Anaweza kupenda apate kitu fulani palepale na kisha anaonyesha kwamba hakipendi tena. Wakati fulani, anapaswa kungojea muda fulani wenye kufaa mbele ya kupata vitu vingine. Pia, mutoto anaweza kuomba vitu vyenye havitamuletea yeye ao watu wengine faida. Zaidi ya hilo, ikiwa muzazi anapatia mutoto palepale kila kitu chenye anamuomba, hilo linaweza kufanya uhusiano wao ugeuke na kuwa kama ule wa bwana na mutumwa wake. Kwa hiyo, muzazi anakuwa mutumwa wa mutoto. Vilevile, Yehova anaweza kuacha wakati upite mbele ya kujibia sala zetu, na anafanya hivyo kwa faida yetu. Yehova ni Muumbaji wetu mwenye hekima, Bwana mwenye upendo, na Baba yetu wa mbinguni; kwa hiyo, anajua vizuri mahitaji yetu na anaamua wakati wenye kufaa kabisa ili kututimizia mahitaji hayo. Ikiwa Yehova anajibia sala zetu zote palepale, hilo linaweza kuharibu urafiki wetu pamoja naye.—Linganisha na Isaya 29:16; 45:9.

8. Kwa sababu Yehova anajua uwezo wetu, anatuahidi nini?

8 Jambo lingine la kufikiria ni kwamba Yehova anajua vizuri sana uwezo wetu. (Zab. 103:14) Kwa hiyo, hatuombe tuvumilie kwa nguvu zetu wenyewe, lakini anatusaidia kama vile baba anamusaidia mutoto wake. Bila shaka, wakati fulani, tunaweza kuona kwamba hatuna tena nguvu za kuendelea kuvumilia. Lakini Yehova anatuhakikishia kwamba hataacha hata kidogo watumishi wake wapate mateso yenye hawawezi kuvumilia. Bila shaka, ‘ataifanya njia ya kutokea.’ (Soma 1 Wakorintho 10:13.) Kwa hiyo, tuko na sababu nzuri za kumutegemea Yehova kwa sababu anajua vizuri mateso yenye tunaweza kuvumilia.

9. Tunapaswa kufanya nini ikiwa tunasali kwa Yehova, lakini hajibie sala zetu palepale?

9 Ikiwa tunasali, lakini hatupate jibu palepale, tuendelee kumungojea Yehova, kwa sababu yeye anajua vizuri wakati wa kujibia sala zetu. Kumbuka kwamba yeye pia iko anavumilia, kwa sababu iko na hamu sana ya kuja kutukomboa. ‘Yehova anaendelea kutarajia [kungojea] kuwaonyesha ninyi kibali, na kwa hiyo atasimama ili kuwaonyesha ninyi rehema. Kwa maana Yehova ni Mungu wa [haki]. Wenye furaha ni wale wote wanaoendelea kumutarajia.’—Isa. 30:18.

“KINYWA CHA SIMBA”

10-12. (a) Ni hali gani zinaweza kufanya ikuwe vigumu kwa Mukristo kuchunga mutu wa familia mwenye kuwa na ugonjwa wa kukawia? (b) Kumutegemea Yehova wakati wa magumu kunaweza kuwa na matokeo gani juu ya urafiki wa mutu pamoja na Yehova? Toa mufano.

10 Kama mutume Paulo, wakati unapambana na majaribu makali, unaweza kujisikia kuwa uko katika ao karibu kuingia katika “kinywa cha simba.” Wakati kama huo, inaweza kuwa vigumu sana kumutegemea Yehova, lakini ni jambo la lazima sana kufanya hivyo. Kwa mufano, wazia unachunga mutu wa familia mwenye iko na ugonjwa wenye kukawia. Pengine umemuomba Yehova akupatie hekima na nguvu. * Hauone kwamba kisha kufanya hivyo, umepata kiasi fulani cha amani kwa sababu unajua kwamba macho ya Yehova iko juu yako na kwamba atakutolea yote yenye unahitaji ili uendelee kuvumilia kwa uaminifu?—Zab. 32:8.

11 Hali fulani zinaweza kufanya uone kwamba Yehova hakusaidie. Pengine waganga wanatoa maoni yenye kuachana juu ya ugonjwa huo. Ao watu wa jamaa wenye ulitumainia kwamba watakusaidia wanaweza kufanya hali iharibike zaidi. Endelea kumutegemea Yehova ili kupata nguvu. Endelea kumukaribia. (Soma 1 Samweli 30:3, 6.) Wakati unatambua namna Yehova iko anakusaidia, urafiki wako pamoja naye utakuwa wenye nguvu zaidi.

12 Dada Linda * alifikia kujionea ukweli wa mambo hayo miaka fulani kisha kusaidia kuchunga wazazi wake wagonjwa katika miaka yao ya mwisho-mwisho. Anasema hivi: “Wakati huo, mimi, bwana yangu, na ndugu yangu mudogo, mara nyingi tulikosa jambo la kufanya. Wakati fulani, tuliona kwamba hakuna mutu wa kutusaidia. Hata hivyo, wakati tunakumbuka mambo yenye ilipita, tunaelewa kabisa kwamba Yehova alikuwa pamoja na sisi. Hata wakati ilionekana kwamba tumekosa kabisa jambo la kufanya, alitupatia nguvu na alitutolea musaada wenye tulihitaji.”

13. Namna gani kumutegemea Yehova kumemusaidia dada fulani apambane na majaribu makali?

13 Kumutegemea kabisa Yehova kunaweza pia kutusaidia wakati tunapambana na majaribu makali. Tuchukue mufano wa dada Rhonda. Dada huyo alikuwa na bwana mwenye haiko Shahidi. Wakati bwana huyo alikuwa anafanya mipango ili kuvunja ndoa yao, ndugu mudogo ya dada Rhonda aliambiwa kwamba iko na ugonjwa hatari sana wenye kuitwa lupus (ugonjwa wenye kuharibu chembe za kukinga mwili). Kisha miezi fulani, bibi ya ndugu yake huyo alikufa. Wakati dada Rhonda alipata kitulizo fulani kisha kupatwa na majaribu hayo makali, alianza kazi ya upainia wa kawaida. Kisha muda mufupi mama yake pia alikufa. Ni nini ilimusaidia dada Rhonda apambane na majaribu hayo? Anaeleza hivi: “Nilizungumuza na Yehova kila siku, nilimuambia hata mambo madogo-madogo. Kufanya hivyo kulinisaidia nimuone kuwa mutu wa kweli kabisa. Nilijifunza kumutegemea kabisa Yehova kuliko kujitegemea mimi mwenyewe ao watu wengine. Na musaada wenye Yehova alinitolea ulikuwa wa kweli kabisa, ni kusema, alitimiza mahitaji yangu yote. Kwa hiyo, nilijifunza kutumika pamoja na Yehova.”

Hata katika familia, majaribu yanaweza kutokea na kufanya urafiki wetu pamoja na Yehova ukuwe katika hatari (Ona fungu la 14-16)

14. Mukristo mwaminifu anapaswa kuwa na tumaini gani wakati mutu wa jamaa yake anatengwa na kutaniko?

14 Tuzungumuzie hali ingine. Wazia kwamba mutu fulani wa jamaa yako anatengwa na kutaniko. Kujifunza Biblia kumekusaidia uelewe namna watengwa wanapaswa kutendewa. (1 Kor. 5:11; 2 Yoh. 10) Lakini, wakati fulani unaweza kuona kwamba ni vigumu ao haiwezekane kuunga mukono uamuzi huo. * Je, unaweza kutumaini kwamba Baba yako wa mbinguni atakupatia nguvu zenye uko nazo lazima ili uheshimu kabisa muongozo wa Biblia juu ya watengwa? Je, unaona hali hiyo kuwa nafasi ya kuendelea kumukaribia zaidi Yehova na kufanya urafiki wako pamoja naye ukuwe wenye nguvu zaidi?

15. Katika bustani ya Edeni, sababu gani Adamu alikosa kutii amri ya Yehova?

15 Kuhusu jambo hilo, fikiria kidogo Adamu, mwanaume wa kwanza. Je, aliamini kabisa kwamba angekosa kumutii Yehova na kuendelea kuishi? Hapana, kwa sababu Maandiko yanasema kwamba Adamu “hakudanganywa.” (1 Tim. 2:14) Lakini, sababu gani alikosa kutii? Bila shaka, Adamu alikula tunda lenye Eva alimupatia kwa sababu alipenda kumufurahisha bibi yake. Alisikiliza sauti ya bibi yake kuliko kutii sauti ya Yehova, Mungu wake.—Mwa. 3:6, 17.

16. Tunapaswa kumupenda nani sana, na sababu gani?

16 Je, hilo linamaanisha kwamba hatupaswe kuwapenda watu wa jamaa yetu? Bila shaka jibu ni hapana! Lakini, ni Yehova tu ndiye tunapaswa kupenda sana. (Soma Mathayo 22:37, 38.) Kufanya hivyo kunawaletea faida watu wa jamaa yetu, iwe wanamutumikia Yehova ao hapana. Kwa hiyo, uendelee kutia nguvu upendo wako na tumaini lako kwa Yehova. Na ikiwa unavurugika sana kwa sababu mutu wa jamaa yako ametengwa, umufungulie Yehova moyo wako katika sala. * (Rom. 12:12; Flp. 4:6, 7) Tumia hali hiyo yenye kuvunja moyo kuwa nafasi ya kufanya urafiki wako pamoja na Yehova ukuwe wa kweli kabisa. Kufanya hivyo kutakusaidia umutegemee Yehova na hilo litakusaidia upate matokeo mazuri zaidi.

WAKATI TUNANGOJEA

Onyesha kwamba unamutegemea Yehova kwa kuendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kazi yake (Ona fungu la 17)

17 Sababu gani mutume Paulo ‘alikombolewa kutoka katika kinywa cha simba’? Anasema hivi: “Ili kupitia mimi kazi ya kuhubiri itimizwe kwa ukamili na mataifa yote yaisikie.” (2 Tim. 4:17) Kama mutume Paulo, wakati tunaendelea kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya kuhubiri, tuko hakika kwamba Yehova ‘atatuongezea’ vitu vingine vyote vya lazima. (Mt. 6:33) Kwa sababu sisi ni wahubiri wa Ufalme, ‘tumekabiziwa [tumepewa] habari njema,’ na Yehova anatuona kuwa ‘wafanyakazi wenzake.’ (1 Tes. 2:4; 1 Kor. 3:9) Tukihubiri kwa bidii kulingana na uwezo wetu, itakuwa mwepesi zaidi kungojea Yehova ajibie sala zetu.

18. Ni katika njia gani tunaweza kumutegemea Yehova na kufanya urafiki wetu pamoja naye ukuwe wenye nguvu?

18 Basi, huu ndio wakati wa kufanya urafiki wetu pamoja na Yehova ukuwe wenye nguvu. Ikiwa hali fulani inatusumbua sana, tutumie nafasi hiyo ili kumukaribia Yehova zaidi. Kwa hiyo, ujifunze sana Neno la Mungu, usali kwa ukawaida, na ukuwe na mengi ya kufanya katika mambo ya kiroho. Ukifanya hivyo, unaweza kuwa hakika kwamba Yehova atakusaidia upambane na majaribu ya sasa na ile yenye inaweza kutokea wakati unaokuja.

^ fu. 2 Inawezekana mutume Paulo alikombolewa moja kwa moja kutoka katika “kinywa cha simba” ao kutoka katika hali zingine zenye hatari.

^ fu. 10 Habari fulani zimechapishwa ili kusaidia Wakristo wagonjwa na wale wenye kuwachunga wapambane vizuri na hali hiyo. Ona Amuka! ya tarehe 8 Mwezi wa 2, 1994; ya tarehe 8 Mwezi wa 2, 1997; ya tarehe 22 Mwezi wa 5, 2000; na ya tarehe 22 Mwezi wa 1, 2001.

^ fu. 12 Majina fulani yamebadilishwa.

^ fu. 14 Ona habari yenye kichwa “Sababu Gani Kutengwa na Kutaniko Ni Mupango Wenye Upendo?” katika gazeti hili.

^ fu. 16 Habari fulani zimechapishwa ili kusaidia watu wa jamaa waendelee kuwa waaminifu wakati mutu wa jamaa yao anamuacha Yehova. Ona Munara wa Mulinzi wa tarehe 1 Mwezi wa 9, 2006, ukurasa wa 17-21 na Munara wa Mulinzi wa tarehe 15 Mwezi wa 1, 2007, ukurasa wa 17-20.