Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Uishi Kulingana na Sala ya Mufano—Sehemu ya 1

Uishi Kulingana na Sala ya Mufano—Sehemu ya 1

‘Jina lako litakaswe.’ —MT. 6:9.

1. Katika mahubiri, namna gani tunaweza kutumia sala yenye kuwa kwenye Mathayo 6:9-13?

WATU wengi wanaweza kutaja sala ya Baba yetu neno kwa neno. Wakati tunahubiri nyumba kwa nyumba, mara nyingi tunatumia sala hiyo ili kusaidia wenye nyumba waelewe kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ya kweli kabisa yenye italeta mabadiliko makubwa duniani. Ao tunaweza kutumia ombi la kwanza la sala hiyo ili kuonyesha kwamba Mungu iko na jina la pekee, lenye linapaswa kutakaswa, ao kuonwa kuwa takatifu.—Mt. 6:9.

2. Tunajua namna gani kwamba Yesu hakutuomba turudilie sala ya mufano neno kwa neno kila wakati tunasali?

2 Je, Yesu alimaanisha kwamba kila wakati tunasali tunapaswa kurudilia sala hiyo neno kwa neno, kama vile wale wenye kujiita kuwa Wakristo wanafanya? Hapana. Mbele tu atoe sala hiyo ya mufano, Yesu alisema hivi: ‘Munaposali, musiseme mambo yaleyale tena na tena.’ (Mt. 6:7) Wakati mwingine, Yesu alirudilia sala hiyo kwa kutumia maneno mengine. (Lu. 11:1-4) Kwa kufanya hivyo, alitusaidia kujua mambo yenye tunapaswa kuomba, na yenye kuwa ya lazima sana. Ndiyo sababu sala hiyo inaitwa sala ya mufano.

3. Tutafikiria maulizo gani wakati wa kuzungumuzia sala ya mufano?

3 Katika habari hii na ile yenye kufuata, tutazungumuzia sala ya mufano. Wakati wa kuzungumuzia habari hizo, ujiulize hivi: ‘Namna gani sala ya mufano inaweza kunisaidia kufanya sala zangu zikuwe muzuri zaidi? Tena, ni muzuri zaidi kujiuliza hivi: Ninaishi kulingana na sala ya mufano?’

“BABA YETU ULIYE MBINGUNI”

4. Maneno “Baba yetu” inatukumbusha nini, na ni katika njia gani Yehova ni “Baba” ya Wakristo wenye kuwa na tumaini la kuishi duniani?

4 Maneno “Baba yetu” inatukumbusha kwamba tuko katika ‘ushirika muzima wa akina ndugu’ wenye wanapendana sana. (1 Pet. 2:17) Kwa kweli, hilo ni pendeleo nzuri sana! Wakristo wenye kuwa na tumaini la kuishi mbinguni, wamefanywa kuwa watoto wa Mungu; kwa hiyo, wanastahili kabisa kumuita Yehova “Baba.” (Rom. 8:15-17) Wakristo wenye kuwa na tumaini la kuishi milele duniani wanaweza pia kumuita Yehova “Baba.” Yeye ndiye amewapatia uzima, na anatimiza kwa upendo mahitaji ya waabudu wake wa kweli. Wale wenye kuwa na tumaini la kuishi hapa duniani watakuwa kabisa watoto wa Mungu kisha kufikia ukamilifu na kuonyesha uaminifu wao wakati wa jaribu la mwisho.—Rom. 8:21; Ufu. 20:7, 8.

5, 6. Ni zawadi gani nzuri zaidi yenye wazazi wanaweza kuwapatia watoto wao, na kila mutoto iko na daraka gani? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

5 Wakati wazazi wanafundisha watoto wao namna ya kusali na kuwasaidia wamuone Yehova kuwa Baba wa mbinguni mwenye kutuhangaikia, wanawapatia zawadi nzuri. Mwangalizi mumoja wa muzunguko katika Afrika Kusini anasema hivi: “Tangu wakati binti zetu walizaliwa, nilikuwa ninasali pamoja nao kila usiku wakati nilikuwa nyumbani. Mara nyingi binti zetu wanasema kwamba hawakumbuke kabisa maneno yenye nilikuwa ninasema katika sala hizo. Lakini, wanakumbuka hali, mazungumuzo yenye heshima pamoja na Baba yetu, Yehova, na namna walijisikia kuwa salama. Wakati walikuwa na uwezo wa kusali peke yao, niliwatia moyo wakuwe wanasali kwa sauti ili nisikie namna wanamuelezea Yehova mawazo yao na namna wanajisikia. Kufanya hivyo kulinipatia nafasi nzuri ya kujua kwa kiasi fulani mambo yenye ilikuwa ndani ya mioyo yao. Kisha, niliwasaidia kutumia mambo ya lazima yenye kupatikana katika sala ya mufano ili sala zao zikuwe na musingi muzuri.”

6 Hatuwezi kushangaa kusikia kwamba binti za ndugu huyo walifanya maendeleo mazuri ya kiroho. Leo, ni wenye furaha katika ndoa zao, na wanamutumikia Mungu katika utumishi wa wakati wote pamoja na bwana zao. Zawadi nzuri zaidi yenye wazazi wanaweza kuwapatia watoto wao ni kuwasaidia wakuwe na urafiki wa sana pamoja na Yehova. Lakini, kila mutoto iko na daraka la kufanya urafiki huo uendelee. Kila mutoto anaweza kufanya hivyo kwa kujifunza kulipenda jina la Mungu, na kuliheshimu sana.—Zab. 5:11, 12; 91:14.

‘JINA LAKO LITAKASWE’

7. Sisi watu wa Mungu tuko na pendeleo gani, na hilo linatuchochea kufanya nini?

7 Tuko na pendeleo nzuri sana la kujua jina la pekee la Mungu na kuwa “watu kwa ajili ya jina lake.” (Mdo. 15:14; Isa. 43:10) Tunasali hivi kwa Baba yetu wa mbinguni: ‘Jina lako litakaswe.’ Kusali hivyo kunaweza kukuchochea umuombe Yehova akusaidie ili uepuke kufanya ao kusema jambo lolote lenye linaweza kuchafua jina lake takatifu. Hatupendi kuwa kama Wakristo fulani wa wakati wa mitume wenye hawakuishi kulingana na mambo yenye walihubiri. Mutume Paulo aliandika hivi juu yao: “Jina la Mungu linafanyiwa makufuru [matukano] katikati ya mataifa kwa sababu yenu.”—Rom. 2:21-24.

8, 9. Toa mufano wenye kuonyesha namna Yehova anawabariki wale wenye kupenda jina lake litakaswe.

8 Tunapenda kulitakasa jina la Mungu. Kisha kifo cha kushitukia cha bwana yake, dada mumoja wa inchi ya Norvège alibakia peke yake pamoja na mutoto mwanaume wa miaka mbili. Dada huyo anasema hivi: “Ilikuwa kipindi kigumu sana katika maisha yangu. Nilisali kila siku, karibu kila saa, ili nipate nguvu ya kutuliza akili yangu. Sikupenda kumupatia Shetani nafasi ya kumuchekelea Yehova kwa kuchukua uamuzi mubaya ao kwa kukosa uaminifu. Nilipenda kulitakasa jina la Yehova, na nilipenda mutoto wangu amuone tena baba yake katika Paradiso.”—Met. 27:11.

9 Je, Yehova alijibu sala za dada huyo? Ndiyo. Kuwa pamoja na ndugu na dada kwa ukawaida kulimutia nguvu. Kisha miaka tano, aliolewa na muzee wa kutaniko. Sasa, mutoto wake iko na miaka 20, na ni ndugu mwenye kubatizwa. Dada huyo anasema hivi: “Ninafurahi sana kwa sababu bwana yangu alinisaidia kumulea mutoto huyo.”

10. Inaomba nini ili jina la Mungu litakaswe kabisa?

10 Inaomba nini ili jina la Mungu litakaswe kabisa na lisikuwe na uchafu wowote? Inaomba Yehova awaharibu wale wote wenye kupinga kimakusudi utawala wake. (Soma Ezekieli 38:22, 23.) Wanadamu watafikia ukamilifu hatua kwa hatua. Tunangojea kwa hamu sana wakati viumbe wote wenye akili wataona jina la Yehova kuwa takatifu! Mwishowe, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo ‘atakuwa vitu vyote kwa kila mutu.’—1 Kor. 15:28.

‘UFALME WAKO UJE’

11, 12. Katika mwaka wa 1876, Wakristo wa kweli walielewa jambo gani?

11 Mbele Yesu arudi mbinguni, mitume wake walimuuliza hivi: “Bwana, je, unarudishia Israeli ufalme wakati huu?” Jibu la Yesu lilionyesha kwamba wakati ulikuwa haujafika ili wanafunzi wake wajue ni wakati gani Ufalme wa Mungu ungeanza kutawala. Aliwaambia wanafunzi wake wakazie uangalifu kazi ya maana yenye walipaswa kufanya, ni kusema, kuhubiri habari njema. (Soma Matendo 1:6-8.) Hata hivyo, Yesu alifundisha wafuasi wake wangojee Ufalme wa Mungu. Ndiyo sababu, kuanzia wakati wa mitume, Wakristo wanasali Ufalme huo uje.

12 Wakati muda ulikaribia ili Yesu aanze kutawala katika Ufalme wa Mungu, Yehova aliwasaidia watu wake waelewe ni katika mwaka gani jambo hilo lingetokea. Katika mwaka wa 1876, Charles Taze Russell aliandika habari fulani katika gazeti Bible Examiner (Le scrutateur de la Bible). Habari hiyo yenye kichwa, “Nyakati za Mataifa: Zitaisha Wakati Gani?” ilionyesha kwamba mwaka wa 1914 ungekuwa wa maana sana. Habari hiyo ililinganisha “nyakati saba” zenye kuzungumuziwa katika unabii wa Danieli na “nyakati zilizowekwa za mataifa” zenye Yesu alizungumuzia. *Dan. 4:16; Lu. 21:24.

13. Ni jambo gani lilitokea katika mwaka wa 1914, na mambo yenye imetokea tangu wakati huo inaonyesha nini?

13 Katika mwaka wa 1914, inchi za Ulaya zilianza kupigana vita; na vita hiyo ilienea katika dunia yote. Kufikia mwisho wa mwaka wa 1918, njaa kubwa ilikuwa imetokea na homa kali iliua watu wengi zaidi kuliko wale wenye walikufa wakati wa vita. Kwa hiyo, “alama” yenye Yesu alitoa ili kuonyesha kuwapo kwake kusikoonekana akiwa Mufalme mupya wa dunia ilianza kuonekana. (Mt. 24:3-8; Lu. 21:10, 11) Tuko na ushuhuda mwingi wenye kuonyesha kwamba Bwana Yesu Kristo ‘alipewa taji’ katika mwaka wa 1914. ‘Alienda akishinda na kukamilisha ushindi wake.’ (Ufu. 6:2) Alisafisha mbingu wakati alipigana vita na Shetani na mashetani wake, na kuwatupa kwenye ujirani wa dunia. Kuanzia wakati huo, wanadamu wamejionea namna maneno haya yenye kuongozwa na roho ya Mungu inatimia: “Ole wa dunia na wa bahari, kwa sababu Ibilisi ameshuka kwenu, akiwa na hasira kali, akijua kwamba ana kipindi kifupi cha wakati.”—Ufu. 12:7-12.

14. (a) Sababu gani tunapaswa kuendelea kusali Ufalme wa Mungu uje? (b) Tuko na pendeleo gani?

14 Unabii wenye kupatikana kwenye Ufunuo 12:7-12 unatusaidia kuelewa sababu gani mambo mabaya sana imeanza kutokea duniani tangu wakati Ufalme wa Mungu ulianza kutawala. Yesu, Mufalme wa Ufalme wa Mungu, alianza kutawala katikati ya maadui wake. Tutaendelea kusali Ufalme wa Mungu uje mupaka wakati Yesu atakamilisha ushindi wake na kumaliza mambo yote mabaya duniani. Pia, tunapaswa kuishi kulingana na sala hiyo kwa kuunga mukono utimizo wa sehemu ya lazima sana ya “alama” hiyo, ni kusema, kuhubiri habari njema. Yesu alitabiri hivi: ‘Hii habari njema ya Ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayoikaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.’—Mt. 24:14.

‘MAPENZI YAKO YATENDEKE DUNIANI’

15, 16. Tunaomba mapenzi ya Mungu ifanyike duniani. Namna gani tunaweza kuishi kulingana na ombi hilo?

15 Kumepita karibu miaka 6000, mapenzi ya Mungu ilikuwa inafanyika kabisa katika dunia. Wakati huo Yehova alisema kwamba kila kitu chenye aliumba “kilikuwa chema sana.” (Mwa. 1:31) Kisha Shetani akamuasi Yehova; na kuanzia wakati huo, wanadamu wadogo sana ndio wanafanya mapenzi ya Yehova. Lakini, leo tuko na pendeleo la kuwa kati ya Mashahidi wa Yehova karibu milioni 8 wenye kusali mapenzi ya Mungu ifanyike duniani, na kujikaza kuishi kulingana na sala ya mufano. Wanafanya hivyo kupitia namna yao ya kuishi, na kupitia bidii yao katika kazi ya kufanya wanafunzi.

Je, unawasaidia watoto wako waishi kulingana na ombi: Mapenzi ya Mungu yatendeke duniani? (Ona fungu la 16)

16 Kwa mufano, dada mumoja mwenye alibatizwa katika mwaka wa 1948, na ambaye ni misionere katika Afrika, anasema hivi: “Kupatana na sehemu hiyo ya sala ya mufano, ninasali kila mara ili watu wote wenye kuwa mufano wa kondoo wahubiriwe na kusaidiwa kumujua Yehova mbele mwisho ufike. Pia, mbele ya kuhubiria mutu, ninaomba Yehova anipatie hekima ili niguse moyo wake. Tena, kuhusu watu wenye kuwa mufano wa kondoo wenye wamekwisha kupatikana, ninasali ili Yehova abariki bidii yenye tunafanya ili kuwasaidia.” Haishangaze kuona kwamba dada huyo mwenye miaka 80 anapata matokeo mazuri katika mahubiri, na kwa musaada wa Wakristo wengine, amesaidia watu wengi wakuwe Mashahidi wa Yehova. Bila shaka, unafikiria mifano ya ndugu na dada wengine ambao wanajikaza kufanya mapenzi ya Yehova hata kama hawana tena nguvu za kutosha kwa sababu wamezeeka.—Soma Wafilipi 2:17.

17. Unajisikia namna gani wakati unafikiria namna mapenzi ya Mungu itafanyika duniani?

17 Tutaendelea kusali mapenzi ya Mungu ifanyike mupaka wakati Yehova ataharibu wale wote wenye kupinga Ufalme wake. Kisha, tutaona mapenzi ya Mungu inafanyika kwa kiasi kikubwa wakati mamiliare ya watu watafufuliwa ili waishi katika paradiso duniani. Yesu alisema hivi: ‘Musistaajabie [musishangae] jambo hili, kwa sababu saa inakuja ambayo wale wote walio ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [yangu] na kutoka.’ (Yoh. 5:28, 29) Ni pendeleo kubwa sana kuishi wakati huo na kuwapokea wapendwa wetu waliokufa! Mungu “atafuta [atapanguza] kila chozi kutoka katika macho [yetu].” (Ufu. 21:4) Watu wengi kati ya wale wenye watafufuliwa watakuwa “wasio waadilifu,” ni kusema, watu wenye walikufa bila kujifunza ukweli juu ya Yehova na Mwana wake. Itakuwa pendeleo kubwa kuwafundisha watu hao mapenzi ya Mungu na kusudi lake. Kwa kufanya hivyo, tutawasaidia wastahili kupata “uzima wa milele.”—Mdo. 24:15; Yoh. 17:3.

18. Wanadamu wanahitaji kabisa nini?

18 Kupitia Ufalme wa Mungu, jina la Mungu litatakaswa na hilo litaleta amani na umoja ulimwenguni pote. Kwa hiyo, Mungu atatimiza mahitaji ya lazima zaidi ya wanadamu wakati atajibu kabisa ombi tatu za kwanza za sala ya mufano. Lakini, kungali mambo mengine ya lazima katika sala ya mufano. Tutazungumuzia mambo hayo katika habari yenye kufuata.

^ fu. 12 Ili kupata mafasirio mengi zaidi yenye kuonyesha namna unabii huo ulitimia wakati Ufalme wa Mungu wenye kuongozwa na Masiya ulianza kutawala katika mwaka wa 1914, ona kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? ukurasa wa 215-218.