Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Uishi Kulingana na Sala ya Mufano—Sehemu ya 2

Uishi Kulingana na Sala ya Mufano—Sehemu ya 2

‘Baba yenu anajua ni vitu gani munavyohitaji.’—MT. 6:8.

1-3. Sababu gani dada mumoja alikuwa hakika kwamba Yehova anajua mahitaji yetu?

DADA Lana hawezi kusahau hata siku moja jambo lenye lilitokea katika Alemanye, mwaka wa 2012. Iko hakika kwamba Yehova alijibu sala zake mbili. Alitoa sala ya kwanza wakati alikuwa katika treni yenye ilikuwa inamupeleka kwenye uwanja wa ndege. Aliomba Yehova amusaidie ili apate nafasi ya kuhubiri. Alitoa sala ya pili wakati alifika kwenye uwanja wa ndege na kuambiwa kwamba atasafiri siku yenye kufuata. Lana aliomba Yehova amusaidie kwa sababu alikuwa ametumia karibu feza zake zote, na hakuwa na nafasi ya kulala.

2 Wakati alikuwa hajamaliza kutoa sala yake ya pili, alisikia mutu fulani anamusalimia hivi: “Jambo, Lana, unafanya nini hapa?” Mutu huyo, ni kijana fulani mwanaume mwenye alisomaka naye zamani. Alikuwa pamoja na mama yake na tate (nkambo) yake, na walikuwa wanamusindikiza kwenye uwanja wa ndege ili aende Afrika Kusini. Kisha kusikia hali ya dada Lana, Elke pamoja na mama yake walimualika kwa furaha nyumbani kwao. Elke pamoja na mama yake walimuonyesha Lana ukaribishaji na waliendelea kumuuliza maulizo juu ya imani yake na juu ya utumishi wake wa wakati wote.

3 Siku yenye ilifuata, kisha kula chakula kizuri cha asubuhi, Lana alijibia maulizo yao mengi yenye kutegemea Biblia na akawaomba adresi yao ili Shahidi mwengine awatembelee. Lana alirudia kwao vizuri na akaendelea kufanya kazi yake ya upainia. Iko hakika kwamba ‘Musikiaji wa sala’ alijua mahitaji yake na akamusaidia.—Zab. 65:2.

4. Tutazungumuzia mahitaji gani?

4 Wakati magumu yenye hatukuwazia inatufikia, tunaomba Yehova musaada palepale, na anafurahi wakati anasikia sala zetu. (Zab. 34:15; Met. 15:8) Lakini, ikiwa tunafikiri sana juu ya sala ya mufano, tunaweza kuona kwamba katika sala hiyo, kuna mahitaji mengine ya lazima zaidi yenye wakati fulani hatukazie uangalifu. Kwa mufano, fikiria namna mahitaji yetu ya kiroho inazungumuziwa kwenye ombi tatu za mwisho katika sala hiyo ya mufano. Je, kuna mambo mengine yenye tunaweza kufanya ili tuishi kulingana na ombi hili la ine: ‘Utupe leo mukate wetu kwa ajili ya siku hii?’—Soma Mathayo 6:11-13.

‘UTUPE LEO MUKATE WETU KWA AJILI YA SIKU HII’

5, 6. Sababu gani ombi ‘utupe mukate wetu kwa ajili ya siku hii’ ni la lazima hata kama tuko na chakula cha kutosha kwa ajili ya siku nyingi?

5 Kumbuka kwamba Yesu alitufundisha kusali ili tupate mukate “wetu;” wala si mukate “wangu.” Ndugu Victor, mwangalizi wa muzunguko katika Afrika, anasema hivi: “Kila mara ninamushukuru kabisa Yehova kwa sababu mimi na bibi yangu hatuhangaikie sana namna ya kupata chakula kwa ajili ya kesho na mahitaji mengine ya lazima. Ndugu zetu wanatuhangaikia kwa upendo kila siku. Lakini ninasali kwa ajili ya wale wenye kutusaidia ili wajue namna ya kupiganisha matatizo ya kupata feza yenye wanapambana nayo.”

6 Ikiwa tuko na chakula cha kutosha kwa ajili ya siku nyingi, tunaweza kufikiria pia ndugu wenye kuwa masikini ao wenye wamepatwa na misiba fulani. Tunasali kwa ajili yao, lakini pia tunapaswa kutenda kulingana na sala zetu. Kwa mufano, tunaweza kuchangia vitu vyetu vyenye tuko navyo pamoja na waabudu wenzetu wenye kuwa katika uhitaji. Pia, tunaweza kuendelea kutoa michango kwa ajili ya kazi ya ulimwenguni pote, kwa sababu tunajua kwamba feza zenye tunatoa zinatumiwa muzuri.—1 Yoh. 3:17.

7. Yesu alitoa mufano gani ili kuonyesha kwamba hatupaswe ‘kuhangaika kamwe juu ya kesho’?

7 Wakati alizungumuzia mukate kwa ajili ya siku hii, Yesu alipenda kumaanisha mahitaji yetu ya leo. Kwa hiyo, alionyesha namna Mungu anavalisha maua. Alisema hivi: ‘Je, yeye hataona ni afazali zaidi awavike [awavalishe], ninyi wenye imani kidogo? Kwa hiyo musihangaike kamwe na kusema, . . . Tutavaa nini?’ Alimalizia maneno yake kwa kurudilia shauri hili la maana: ‘Musihangaike kamwe juu ya kesho.’ (Mt. 6:30-34) Hilo linaonyesha kwamba hatupaswe kupenda vitu vya kimwili, lakini tunapaswa kutosheka na mahitaji ya lazima ya kila siku. Mahitaji hayo inaweza kuwa makao yenye kufaa, kazi ya kutusaidia kutimiza mahitaji ya familia, na hekima ya kutusaidia kupambana na matatizo ya afya. Hata hivyo, ikiwa tunasali tu kwa ajili ya mahitaji ya kimwili, hilo litaonyesha kwamba tunapenda vitu vya kimwili, kuliko kukazia mahitaji ya kiroho yenye kuwa ya lazima zaidi.

8. Maneno ya Yesu ‘utupe mukate wetu kwa ajili ya siku hii’ inapaswa kutukumbusha mahitaji gani ya lazima? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

8 Maneno ya Yesu ‘utupe mukate wetu kwa ajili ya siku hii’ inapaswa kutukumbusha kwamba tunahitaji chakula cha kiroho. Bwana wetu alisema hivi: ‘Mwanadamu ataishi, si kwa mukate tu, bali kwa kila neno linalotoka katika kinywa cha Yehova.’ (Mt. 4:4) Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kusali ili Yehova aendelee kutupatia chakula cha kiroho kwa wakati wenye kufaa.

‘UTUSAMEHE MADENI YETU’

9. Ni katika njia gani zambi zetu ni “madeni”?

9 Sababu gani Yesu alitumia neno “madeni,” na wakati mwengine akatumia neno ‘zambi’? (Mt. 6:12; Lu. 11:4) Kumepita zaidi ya miaka 60, gazeti Munara wa Mulinzi lilieleza waziwazi hivi: “Wakati tunafanya zambi, hilo linafanya tukuwe na deni la Mungu. . . . Kwa sababu ya zambi yetu Mungu anaweza kutuomba ao kutunyanganya uzima wetu. . . . Anaweza kutunyanganya amani yake, na kuvunja urafiki muzuri wenye tulikuwa nao pamoja naye. . . . Tunapaswa kumupenda, na tunafanya hivyo kwa kumutii; na wakati tunafanya zambi, tunashindwa kulipa deni letu la kumupenda, kwa sababu Mungu anachukia zambi.”—1 Yoh. 5:3.

10. Ni nini inafanya Yehova asamehe zambi zetu, na tunajisikia namna gani kuhusu jambo hilo?

10 Tunashukuru Yehova kwa sababu alitutolea zabihu ya ukombozi ya Yesu ili kusamehe zambi zetu! Kila siku, tunahitaji Yehova atusamehe. Hata kama zabihu hiyo ililipwa kumepita karibu miaka 2000, tunapaswa kuiona kuwa ya lazima, na yenye faida hata leo. “Bei ya ukombozi” kwa ajili ya uzima wetu ‘ni yenye samani sana’ hivi kwamba hakuna kitu chenye mwanadamu mwenye hakamilike anaweza kufanya ili kuilipa. (Soma Zaburi 49:7-9; 1 Petro 1:18, 19.) Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kumushukuru Yehova kwa ajili ya zawadi hiyo kubwa. Pia, maneno ‘zambi zetu,’ wala si ‘zambi zangu,’ inapaswa kutukumbusha kwamba waabudu wote wa Yehova wanahitaji zabihu ya ukombozi. Ni wazi kwamba, Yehova anapenda tuhangaikie mahitaji yetu ya kiroho, na pia ile ya wengine, bila kusahau wale wenye wametukosea. Kwa kawaida, zambi hizo ni makosa madogo-madogo yenye kutupatia nafasi ya kuonyesha kwamba tunapenda kabisa ndugu na dada zetu, na kwamba tuko tayari kuwasamehe kama vile Mungu pia anatusamehe.—Kol. 3:13.

Ikiwa unapenda Mungu akusamehe, ukuwe mwenye kusamehe wengine (Ona fungu la 11)

11. Sababu gani ni jambo la lazima tukuwe na tabia ya kusamehe wengine?

11 Jambo lenye kuhuzunisha ni kwamba, kwa sababu ya kutokamilika, wakati fulani tunaweza kuwekea wengine kinyongo. (Law. 19:18) Ikiwa tunaelezea ndugu na dada makosa yenye wengine wametufanyia, wamoja kati yao wanaweza kutuunga mukono na hilo linaweza kuleta mugawanyiko katika kutaniko. Ikiwa tunaacha hali hiyo iendelee, hilo litaonyesha kwamba hatupendezwe na rehema ya Mungu na zabihu ya ukombozi. Ikiwa tuko na tabia ya kukataa kusamehe wengine, Yehova pia hatatusamehe. (Mt. 18:35) Yesu alikazia jambo hilo kisha kuzungumuzia sala ya mufano. (Soma Mathayo 6:14, 15.) Pia, ili Yehova atusamehe, tunapaswa kujikaza kuepuka kuwa na zoezi la kufanya zambi nzito. Tuzungumuzie sasa ombi lingine lenye linaweza kutusaidia kuepuka zoezi la kufanya zambi.—1 Yoh. 3:4, 6.

“USITUINGIZE KATIKA JARIBU”

12, 13. (a) Ni jambo gani lilimupata Yesu kisha tu kubatizwa? (b) Sababu gani hatupaswe kulaumu wengine wakati tunaangukia katika jaribu? (c) Yesu alionyesha nini kwa kubakia mwaminifu mupaka kifo?

12 Kufikiria jambo lenye lilimupata Yesu kisha tu ubatizo wake, kunaweza kutusaidia tuelewe sababu gani ni jambo la lazima tusali hivi: “Usituingize katika jaribu.” Kisha Yesu kubatizwa, roho ya Mungu ilimuongoza katika jangwa. Sababu gani? ‘Ili ajaribiwe na Ibilisi.’ (Mt. 4:1; 6:13) Je, hilo linapaswa kutushangaza? Hapana, ikiwa tunaelewa sababu kubwa yenye ilimufanya Mungu amutume Mwana wake duniani. Yesu alikuja ili kujibu maulizo yenye ilitokezwa wakati Adamu na Eva walikataa utawala wa Mungu. Iliomba muda fulani upite ili kujibu maulizo hayo. Kwa mufano, je, mwanadamu alikuwa na kasoro ao kosa fulani wakati Mungu alimuumba? Ingewezekana mwanadamu mukamilifu atetee utawala wa Mungu hata kama anajaribiwa na ‘ule muovu’? Je, wanadamu wangepata matokeo mazuri ikiwa wangekataa utawala wa Mungu kama vile Shetani alionyesha? (Mwa. 3:4, 5) Iliomba muda upite ili kujibu maulizo hayo; kufanya hivyo, kungesaidia pia viumbe wote wenye akili waelewe kwamba Yehova anatumia vizuri mamlaka yake.

13 Yehova ni mutakatifu; ndiyo sababu hawezi kumujaribu mutu yeyote ili afanye mambo mabaya. Lakini, Ibilisi ndiye ‘Mujaribu.’ (Mt. 4:3) Ibilisi anaweza kutokeza hali za kuingiza watu katika majaribu. Hata hivyo, kila mutu anapaswa kuamua ikiwa atajiacha aangukie katika jaribu ao hapana. (Soma Yakobo 1:13-15.) Kwa upande wake, Yesu alipinga bila kukawia kila jaribu lenye alipata kwa kutaja maandiko yenye kupatikana katika Neno la Mungu. Kwa kufanya hivyo, Yesu alitetea utawala wenye haki wa Mungu. Lakini Shetani aliendelea kumujaribu. Alingojea “wakati mwingine unaofaa.” (Lu. 4:13) Yesu aliendelea kumupinga Shetani na hakumuruhusu avunje uaminifu wake. Kristo alitetea utawala wenye haki wa Yehova na alionyesha kwamba mwanadamu mukamilifu anaweza kubakia mwaminifu hata kama anajaribiwa namna gani. Hata hivyo, Shetani anajaribu kuwatega wafuasi wa Yesu, na wewe pia.

14. Tunapaswa kufanya nini ili tusiangukie katika jaribu?

14 Kwa sababu maulizo yenye ilitokezwa juu ya utawala wa Mungu inapaswa kujibiwa, Yehova anamuruhusu Mujaribu atumie ulimwengu huu ili kutujaribu. Mungu haingize mutu katika jaribu. Lakini, anatutumainia na anapenda kutusaidia. Hata hivyo, kwa sababu tuko na uhuru wa kuchagua, Yehova anatuachia nafasi ya kuamua ikiwa tutabakia waaminifu kwake ao hapana. Ili kubaki waaminifu, tunapaswa kufanya mambo mawili: kuendelea kuwa macho kiroho na kuendelea kusali. Namna gani Yehova anajibia sala zetu?

Uendelee kuwa nguvu kiroho na kuhubiri kwa bidii (Ona fungu la 15)

15, 16. (a) Taja hali fulani zenye tunapaswa kuepuka. (b) Wakati tunaangukia katika jaribu, sababu gani hatupaswe kumulaumu Shetani?

15 Yehova anatupatia roho yake takatifu, na roho hiyo inaweza kutupatia nguvu na kutusaidia ili tusiangukie katika jaribu. Pia, kupitia Neno lake na kutaniko, Mungu anatuonya mbele ya wakati juu ya hali zenye tunapaswa kuepuka, kama vile kutumia wakati, feza, na nguvu nyingi juu ya vitu vya kimwili vyenye haviko vya lazima zaidi. Ndugu Espen na dada Janne bibi yake, wanaishi katika inchi moja tajiri ya Ulaya. Kwa miaka mingi walikuwa mapainia wa kawaida katika eneo moja la inchi yao lenye kuwa na lazima kubwa ya wahubiri. Wakati walizaa mutoto wao wa kwanza, walisimamisha kazi ya upainia, na leo wamezaa mutoto wa pili. Ndugu Espen anasema hivi: “Kila mara tunasali ili Yehova atusaidie tusiangukie katika jaribu, zaidi sana katika kipindi hiki ambamo hatuwezi tena kupitisha wakati mwingi katika mambo ya kiroho. Tunamuomba Yehova atusaidie tuendelee kuwa nguvu kiroho na kuhubiri kwa bidii.”

16 Kuangalia pornografia ni jaribu lingine lenye linavuma sana katika siku zetu. Ikiwa tunaangukia katika jaribu hilo, hatuwezi kumulaumu Shetani. Sababu gani? Kwa sababu Shetani na ulimwengu wake hawawezi kutukaza kufanya jambo fulani lenye hatupendi. Wakristo fulani wameangukia katika jaribu hilo kwa sababu waliendelea kufikiria mambo mabaya. Lakini, tunaweza kuepuka jaribu hilo kama vile ndugu na dada wengi wamefanya.—1 Kor. 10:12, 13.

‘UTUKOMBOE KUTOKANA NA ULE MUOVU’

17. (a) Namna gani tunaweza kuishi kulingana na ombi ‘utukomboe kutokana na ule muovu’? (b) Tunangojea kitulizo gani hivi karibuni?

17 Ili kuishi kulingana na ombi ‘utukomboe kutokana na ule muovu,’ tunapaswa kujikaza ili tusikuwe “sehemu ya ulimwengu [wa Shetani].” Hatupaswe ‘kupenda ulimwengu [wa Shetani] ao vitu vilivyo katika ulimwengu.’ (Yoh. 15:19; 1 Yoh. 2:15-17) Tunapaswa kuendelea kupigana sana ili kufanya hivyo. Bila shaka, tutapata kitulizo wakati Yehova atajibu ombi hilo kwa kumuondoa Shetani na kuharibu ulimwengu wake muovu! Lakini, tunapaswa kukumbuka kwamba, wakati Shetani alitupwa duniani kutoka mbinguni, alijua kwamba iko na kipindi kifupi cha wakati. Kwa sababu ya hasira, anajikaza sana ili kuvunja ushikamanifu wetu. Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kusali ili Yehova atukomboe kutokana na ule muovu.—Ufu. 12:12, 17.

18. Ili tuweze kuokoka mwisho wa ulimwengu wa Shetani, tunapaswa kuendelea kufanya nini?

18 Unapenda kuishi katika ulimwengu wenye hauna Shetani? Kwa hiyo, uendelee kusali ili Ufalme wa Mungu uje kutakasa jina la Mungu na kufanya mapenzi yake ifanyike hapa duniani. Umutegemee Yehova akutimizie mahitaji yako ya kiroho na ya kimwili. Kwa hiyo, uazimie kuishi kulingana na sala ya mufano.