Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Uendelee Kuwa Mwaminifu kwa Ufalme wa Mungu

Uendelee Kuwa Mwaminifu kwa Ufalme wa Mungu

“Wao si sehemu ya ulimwengu.”YOHANA 17:16.

NYIMBO: 63, 129

1, 2. (a) Kuwa mwaminifu kwa Yehova na kutojiingiza katika mambo ya ulimwengu huu, kunapatana namna gani? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.) (b) Watu wengi wanaonyesha uaminifu kwa mambo gani, na hilo linaleta matokeo gani?

WATUMISHI wa Yehova hawajiingize katika mambo yenye kugawanya watu kama vile, kupenda sana inchi yao, rangi ya ngozi, ao desturi. Sababu gani? Kwa sababu wanamupenda Yehova, wako waaminifu kwake, na wanamuheshimu. (1 Yohana 5:3) Hata kama tulitoka wapi ao tunaishi wapi, tunatii kanuni za Mungu. Jambo la lazima sana kuliko mambo mengine yote, ni kuwa mwaminifu kwa Yehova na Ufalme wake. (Mathayo 6:33) Ndiyo sababu tunaweza kusema kwamba hatuko “sehemu ya ulimwengu.”—Soma Yohana 17:11, 15, 16; Isaya 2:4.

2 Leo, watu wengi katika dunia wanaonyesha uaminifu kwa inchi yao, kabila yao, desturi yao, ao hata kwa vikundi fulani vya wachezaji. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, hilo limefanya wengi kati yao wakuwe na roho ya mashindano, kuchukiana, na wakati fulani kuua watu wenye kuwa waaminifu kwa upande mwingine. Hata kama hatujiingize katika mambo hayo, inaweza kuwa na matokeo mabaya juu yetu na juu ya familia yetu, na tunaweza kutendewa mubaya sana. Mungu alitupatia uwezo wa kujua ikiwa mambo iko sawa ao hapana; ndiyo sababu wakati serikali zinachukua maamuzi mabaya, inaweza kuwa vyepesi kwetu kuunga mukono upande fulani. (Mwanzo 1:27; Kumbukumbu la Torati 32:4) Unajisikia namna gani wakati serikali zinafanya hivyo? Je, unaunga mukono upande fulani ao unaepuka kufanya hivyo?

Wakristo wa kweli hawaone kwamba sehemu fulani ya ulimwengu wa Shetani ni nzuri kuliko ingine

3, 4. (a) Wakati wa vita, sababu gani hatuunge mukono upande fulani? (b) Tutazungumuzia nini katika habari hii?

3 Wakati wa vita, watu wengi wanaunga mukono upande fulani kwa sababu wakubwa wa serikali wanawasadikisha kwamba wanainchi wazuri wanapaswa kupigania inchi yao. Lakini sisi tunafuata mufano wa Yesu. Ndiyo sababu hatujiingize katika mambo ya politike, na hatupigane vita. (Mathayo 26:52) Wakristo wa kweli hawaone kwamba sehemu fulani ya ulimwengu wa Shetani ni nzuri kuliko sehemu ingine. (2 Wakorintho 2:11) Tunakataa kujiingiza katika mambo ya ulimwengu huu.—Soma Yohana 15:18, 19.

Kwa sababu hatukamilike, ndugu na dada fulani wanaweza kuwa wangali na mawazo mabaya juu ya watu wenye kuwa tofauti nao. (Yeremia 17:9; Waefeso 4:22-24) Katika habari hii, tutajifunza kanuni zenye zitatusaidia kupiganisha na kupata ushindi juu ya tabia hizo zote zenye kugawanya watu. Tutazungumuzia pia namna tunaweza kujizoeza ili kubaki waaminifu kwa Ufalme kwa kuona watu namna Yehova na Yesu wanawaona.

SABABU GANI HATUUNGE MUKONO SEHEMU FULANI YA ULIMWENGU

5, 6. Wakati Yesu alikuwa duniani, alikuwa na maoni gani juu ya watu, na sababu gani?

5 Wakati unaona kwamba ni vigumu kuepuka kujiingiza katika mambo ya politike ao kuunga mukono upande fulani katika ulimwengu huu, ujiulize hivi: ‘Ingekuwa Yesu, angefanya nini?’ Wakati Yesu alikuwa duniani, kulikuwa uadui na mabishano kati ya watu wa Yudea, Galilaya, na Samaria. Tufikirie mifano fulani. Wayahudi na Wasamaria hawakuwa wanazungumuza. (Yohana 4:9) Mafarisayo na Masadukayo hawakuwa wanaelewana katika mambo mengi. (Matendo 23:6-9) Wayahudi wenye walijifunza Sheria walizarau sana watu wenye hawakujifunza Sheria hiyo. (Yohana 7:49) Tena, wengi walichukia wakusanya-kodi na Waroma. (Mathayo 9:11) Lakini Yesu hakujiingiza katika mambo hayo. Hata kama sikuzote alikuwa anafundisha kweli juu ya Yehova na alijua kwamba Israeli lilikuwa taifa la pekee la Mungu, hakuwafundisha wanafunzi wake hata kidogo kwamba walikuwa watu wa hali ya juu kuliko wengine. (Yohana 4:22) Lakini, aliwafundisha kupenda watu wote.—Luka 10:27.

Yehova na Yesu hawaone kwamba rangi fulani ya ngozi, inchi fulani, ao luga fulani ni nzuri sana kuliko ingine

6 Sababu gani Yesu hakuona kwamba watu fulani ni wa hali ya juu kuliko wengine? Kwa sababu yeye na Baba yake wako na maoni yenye kuwa tofauti na ya wanadamu. Wakati Yehova aliumba dunia, alipenda ijae watu wa rangi mbalimbali ya ngozi. (Mwanzo 1:27, 28) Kwa hiyo, Yehova na Yesu hawaone kwamba rangi fulani ya ngozi, inchi fulani, ao luga fulani ni nzuri sana kuliko ingine. (Matendo 10:34, 35; Ufunuo 7:9, 13, 14) Tunapaswa kuiga mufano wao muzuri sana.—Mathayo 5:43-48.

7, 8. (a) Tunaunga mukono upande gani, na sababu gani? (b) Tunapaswa kujua jambo gani kuhusu magumu ya wanadamu?

7 Sababu gani hatuunge mukono utawala ao serikali fulani ya wanadamu? Kwa sababu tunaunga mukono Ufalme wa Yehova. Yeye ni Mutawala wetu. Katika shamba la Edeni, Shetani alisema kwamba Yehova anatawala mubaya wanadamu. Shetani alipenda wanadamu waamini kwamba namna yake ya kuongoza mambo ndiyo nzuri kuliko ya Mungu. Yehova anatupatia uhuru wa kujichagulia upande wenye tutaunga mukono. Lakini, wewe utaunga mukono upande gani? Je, unamutii Yehova kwa sababu unaamini kwamba namna yake ya kuongoza mambo ndiyo nzuri zaidi? Unasadiki kabisa kwamba ni Ufalme wake tu ndio utamaliza magumu yetu? Ao unafikiri kwamba watu wanaweza kujiongoza vizuri bila Mungu?—Mwanzo 3:4, 5.

8 Kwa mufano, ikiwa mutu fulani anakuuliza maoni yako juu ya chama fulani cha politike, kikundi cha watu wenye kupigania mabadiliko, ao mambo mengine kama hayo, utamujibu namna gani? Vikundi fulani vinaweza kuwa na nia nzuri na kupenda kusaidia watu. Lakini tunajua kwamba ni Ufalme wa Yehova tu ndio utamaliza magumu yote ya wanadamu na ukosefu wa haki. Pia, katika kutaniko tunafuata muongozo wa Yehova, kuliko kila mutu kujiamulia mambo yenye anafikiri kuwa ni ya muzuri zaidi. Ndiyo sababu ndugu na dada katika kutaniko ni wenye umoja.

9. Wakristo fulani wa wakati wa mitume walikuwa na tatizo gani, na walipaswa kufanya nini?

9 Wakati wa mitume, Wakristo fulani katika muji wa Korintho walikuwa wanabishana na kusema hivi: “‘Mimi ni wa Paulo,’ ‘Lakini mimi ni wa Apolo,’ ‘Lakini mimi ni wa Kefa,’ ‘Lakini mimi ni wa Kristo.’” Wakati mutume Paulo alipata habari juu ya mabishano hayo, alihuzunika sana. Hilo lilikuwa tatizo kubwa sana, kwa sababu amani ya kutaniko ilikuwa katika hatari. Ndiyo sababu aliuliza ndugu na dada zake hivi: ‘Kristo amegawanyika?’ Kisha mutume Paulo aliwashauri hivi: ‘Nawahimiza ninyi, akina ndugu, kupitia jina la Bwana wetu Yesu Kristo kwamba nyote museme kwa upatano, na kwamba kusikuwe na migawanyiko katikati yenu, bali kwamba muunganishwe vema katika akili ileile na katika njia ileile ya kufikiri.’ Sisi pia tunapaswa kutii shauri hilo leo. Tunapaswa kuepuka kabisa kuwa na migawanyiko katika kutaniko.—1 Wakorintho 1:10-13; soma Waroma 16:17, 18.

10. Mutume Paulo aliwakumbusha Wakristo nini, na hilo linatufundisha nini?

10 Mutume Paulo aliwakumbusha Wakristo watiwa-mafuta kwamba wao ni raia wa mbinguni na kwamba hawapaswe kukaza akili yao juu ya “vitu vilivyo duniani.” (Wafilipi 3:17-20) * (Ona maelezo ya chini.) Wakristo watiwa-mafuta ni mabalozi ao waambasadere wa Mungu na Kristo. Wakati ambasadere iko katika inchi ingine, hajiingize katika politike na mambo mengine ya inchi hiyo. Vilevile, Wakristo watiwa-mafuta hawapaswe kujiingiza katika politike na katika mambo mengine ya ulimwengu huu. (2 Wakorintho 5:20) Wale wenye kuwa na tumaini la kuishi milele duniani wanapaswa pia kuwa waaminifu kwa Ufalme na kuepuka kujiingiza katika mambo ya ulimwengu huu.

UJIZOEZE KUWA MWAMINIFU KWA UFALME WA YEHOVA

11, 12. (a) Ikiwa tunapenda kuendelea kuwa waaminifu kwa Ufalme wa Mungu, tunapaswa kuepuka mawazo gani? (b) Dada mumoja alikuwa na mawazo gani juu ya watu fulani, na ni nini ilimusaidia aachane kabisa na mawazo hayo?

11 Katika sehemu nyingi za dunia, watu wanavutiwa sana na wale wenye waliishi ao kukomaa pamoja nao, wenye kuwa na desturi moja, ao wenye kuzungumuza luga moja. Kwa kawaida wanajivunia nafasi kwenye walitoka. Lakini sisi tunapaswa kuepuka mambo hayo. Tunapaswa kubadilisha mawazo yetu na tunapaswa kuzoeza zamiri yetu ili tuendelee kuepuka kujiingiza katika mambo yote ya ulimwengu huu. Ni nini itatusaidia kufanya hivyo?

12 Kwa mufano, dada Mirjeta * (ona maelezo ya chini) alizaliwa katika inchi yenye ilikuwa inaitwa Yugoslavia. Nafasi kwenye alikomalia, watu walichukia Waserbia. Wakati alijifunza juu ya Yehova, alielewa kwamba Yehova haone kwamba watu wa kabila fulani kuwa ni wa hali ya juu kuliko wengine, na kwamba ni Shetani ndiye anapenda watu wachukiane. Kwa hiyo, alijikaza sana kubadilisha mawazo yake. Lakini wakati makabila mbalimbali ya eneo lao ilianza kupigana vita, dada Mirjeta akaanza tena kuchukia Waserbia. Hakupenda hata kuwahubiria. Kwa sababu alijua kwamba ni mubaya kufanya hivyo, alisali kwa Yehova ili amusaidie aachane kabisa na mawazo hayo. Alimuomba pia amusaidie ili aanze kazi ya upainia. Dada Mirjeta anasema hivi: “Nimetambua kwamba jambo lenye lilinisaidia kabisa ni kukazia uangalifu kazi ya kuhubiri. Wakati ninahubiri, ninajikaza kuiga upendo wa Yehova, na nimeona kwamba hilo linanisaidia kuachana polepole na mawazo yangu mabaya.”

13. (a) Ni jambo gani lilimufikia dada Zoila, na alifanya nini? (b) Mufano wa dada Zoila unaweza kutufundisha nini?

13 Dada Zoila alitoka Meksiko na kuhamia Ulaya. Alikuwa katika kutaniko moja na ndugu na dada wengine kutoka sehemu zingine za Amerika ya Kusini. Dada Zoila anasema kwamba ndugu na dada fulani walikuwa wanacheka inchi, desturi, na miziki ya inchi yake. Alivurugika sana, kwa hiyo alisali ili Yehova amusaidie asivunjike moyo. Ungefanya nini ikiwa ungekuwa katika hali kama yake? Wengi kati ya ndugu na dada zetu wanaendelea kujikaza ili kujizuia wakati watu wengine wanazarau nafasi kwenye walitoka. Kwa hiyo, tunapaswa kuepuka kabisa kusema ao kufanya jambo fulani lenye linaweza kuonyesha kwamba watu fulani ni wa hali ya juu kuliko wengine. Tunaepuka kuleta migawanyiko katika kutaniko ao mahali pengine.—Waroma 14:19; 2 Wakorintho 6:3.

Umuombe Yehova akusaidie kuona watu wengine namna yeye anawaona

14. Ni nini inaweza kukusaidia kuona watu namna Yehova anawaona?

14 Sisi wote tunajua kwamba watumishi wa Yehova wanaishi katika umoja; kwa hiyo, hatupaswe kufikiri kwamba nafasi ao inchi fulani ni nzuri zaidi kuliko ingine. Lakini, inawezekana familia yako na watu wenye mulikomaa nao wamekuchochea upende nafasi kwenye ulitoka. Pengine ungali na mawazo mabaya juu ya watu wa inchi, desturi, luga, ao watu wa rangi ingine ya ngozi. Ni nini inaweza kukusaidia ubadilishe mawazo yako? Fikiria sana namna Yehova anaona watu wenye kujivunia inchi yao, ao wenye wanawaza kwamba wao ni wazuri kuliko wengine. Wakati wa ibada ya familia ao wakati wa funzo lako la pekee, tafuta katika vichapo vyetu habari zaidi juu ya jambo hilo. Kisha, umuombe Yehova akusaidie kuona watu namna yeye anawaona.—Soma Waroma 12:2.

Ili kubaki waaminifu kwa Yehova, tunapaswa kumutii hata kama watu wanatutendea namna gani (Ona fungu la 15, 16)

15, 16. (a) Watu fulani watatutendea namna gani kwa sababu sisi ni tofauti nao? (b) Namna gani wazazi wanaweza kusaidia watoto wao wabaki waaminifu kwa Yehova?

15 Tunataka kumutumikia Yehova na zamiri safi; kwa hiyo, wakati fulani tunapaswa kuonyesha kwamba tuko tofauti kabisa na wafanyakazi wenzetu, wanafunzi wenzetu, majirani, ao watu wa jamaa yetu. (1 Petro 2:19) Yesu alisema kwamba watu watatuchukia kwa sababu tuko tofauti nao. Tukumbuke kwamba wengi kati ya wale wenye kutupinga hawajue jambo lolote juu ya Ufalme wa Mungu. Ndiyo maana hawaelewe sababu gani ni jambo la lazima tukuwe waaminifu kwa Ufalme kuliko kuwa waaminifu kwa serikali za wanadamu.

16 Ili kubaki waaminifu kwa Yehova, tunapaswa kumutii hata kama watu wanasema ao kututendea nini. (Danieli 3:16-18) Ni vigumu sana kuwa tofauti na watu wengine, zaidi sana kwa vijana. Wazazi, muwasaidie watoto wenu wakuwe na ujasiri kwenye masomo. Watoto wenu wanaweza kuogopa kukataa kusalimu bendera ao kukataa kufanya sikukuu zingine za inchi. Wakati wa ibada ya familia, munaweza kujifunza namna Yehova anaona mambo hayo. Muwafundishe namna wanaweza kueleza waziwazi na kwa heshima mambo yenye wanaamini. (Waroma 1:16) Pia, ikiwa ni lazima, muwasaidie kwa kuzungumuza na walimu wao na kuwaelezea mambo yenye munaamini.

FURAHIA VITU VYOTE VYENYE YEHOVA ALIUMBA

17. Tunapaswa kuepuka kuwa na mawazo gani, na sababu gani?

17 Kwa kawaida tunafurahia chakula, luga, na mambo kama vile hali ya hewa, milima, miti, na vitu vingine vyenye kupatikana kwenye tulikomalia. Lakini, je, tunawaza kwamba kila mara mambo yenye tunapenda ni ya muzuri zaidi kuliko ile yenye wengine wanapenda? Yehova anapenda tufurahie vitu mbalimbali vyenye aliumba. (Zaburi 104:24; Ufunuo 4:11) Kwa hiyo, sababu gani tukazie tu kwamba mambo yenye tunapenda ni ya muzuri zaidi kuliko ya wengine?

Yehova anapenda watu wa namna zote waishi milele

18. Sababu gani ni jambo la lazima tuwaone watu wengine namna Yehova anawaona?

18 Yehova anapenda watu wa namna zote wajifunze kumujua, wamuabudu, na waishi milele. (Yohana 3:16; 1 Timotheo 2:3, 4) Kwa hiyo, wakati ndugu zetu wako na mawazo yenye kuwa tofauti na yetu, tutakuwa tayari kuwasikiliza, ikiwa mawazo hayo haivunje kanuni za Yehova. Tukifanya hivyo, tutakuwa na furaha na tutaendelea kuishi kwa umoja na ndugu na dada zetu. Kama vile tumeona, kwa sababu tuko waaminifu kwa Yehova na kwa Ufalme wake, hatujiingize katika mambo ya ulimwengu. Tunachukia kiburi na roho ya mashindano yenye kuwa katika ulimwengu huu wa Shetani. Tunamushukuru sana Yehova kwa sababu ametufundisha kupenda amani na kuwa wanyenyekevu! Tunajisikia kama mutunga-zaburi mwenye aliandika hivi: ‘Tazama! Jinsi ilivyo vema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!’—Zaburi 133:1.

^ fu. 10 Inawezekana ndugu na dada fulani wa kutaniko la Filipi walikuwa na uraia wa Roma. Kwa hiyo, walikuwa na faida nyingi kuliko ndugu na dada wenye hawakuwa na uraia huo.

^ fu. 12 Majina fulani imebadilishwa.