Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Uendelee Kungojea!

Uendelee Kungojea!

Hata ikikawia, uendelee kuitarajia [kuingojea]!’ —HABAKUKI 2:3.

NYIMBO: 128, 45

1, 2. Watumishi wa Yehova wako na mutazamo gani?

TANGU zamani, watumishi wa Yehova wamekuwa wakingojea utimizo wa unabii mbalimbali. Kwa mufano, nabii Yeremia alingojea utimizo wa unabii wenye kuonyesha kwamba Wababiloni wataharibu Yuda, na unabii huo ulitimia katika mwaka wa 607 mbele ya kuzaliwa kwa Yesu. (Yeremia 25:8-11) Nabii Isaya alitabiri kwamba Yehova atakomboa Wayahudi kutoka Babiloni na kuwarudisha katika inchi yao. Alisema hivi: ‘Wenye furaha ni wale wote wanaoendelea kumutarajia [kumungojea].’ (Isaya 30:18) Pia, nabii Mika alingojea utimizo wa ahadi za Yehova. Alisema hivi: ‘Nitaendelea kumutazamia Yehova.’ (Mika 7:7) Kwa miaka mingi, watumishi wa Mungu walikuwa hakika kwamba Masiya ao Kristo mwenye aliahidiwa atakuja.—Luka 3:15; 1 Petro 1:10-12. * (Ona maelezo ya chini.)

2 Sisi pia tunangojea utimizo wa unabii mbalimbali juu ya Ufalme wa Yehova. Yesu, Mufalme wa Ufalme huo, ataokoa hivi karibuni watumishi wa Mungu kutoka katika ulimwengu huu wenye hatari. Ataharibu watu wabaya na kuondoa mateso yote. (1 Yohana 5:19) Kwa hiyo, tunapaswa kuendelea kungojea kwa sababu siku ya Yehova inaweza kuja wakati wowote, na tunapaswa kufanya nguvu yetu yote ili tukuwe tayari kwa ajili ya siku hiyo.

3. Ikiwa tumengojea mwisho kwa miaka mingi, tunaweza kuanza kujiuliza ulizo gani?

3 Tunangojea kwa hamu sana wakati mapenzi ya Mungu itafanyika hapa duniani. (Mathayo 6:10) Lakini, ikiwa tumengojea mwisho kwa miaka mingi, tunaweza kuanza kujiuliza hivi: ‘Sababu gani tuendelee kungojea mwisho wenye utafika hivi karibuni?’

SABABU GANI TUENDELEE KUNGOJEA?

4. Sababu gani tunapaswa ‘kuendelea kukesha’?

4 Yesu aliamuru wafuasi wake ‘waendelee kukesha.’ Ndiyo sababu ni jambo la maana sana tuendelee kungojea mwisho wenye utakuja hivi karibuni. (Mathayo 24:42; Luka 21:34-36) Pia, tengenezo la Yehova linaendelea kutukumbusha kwamba ‘tungojee na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova’ na kwamba tuendelee kukazia katika akili ahadi ya Yehova ya dunia mupya.—Soma 2 Petro 3:11-13.

5. Taja jambo lingine lenye kuonyesha sababu gani tuendelee kungojea siku ya Yehova.

5 Wafuasi wa Yesu wa wakati wa mitume walipaswa kuendelea kungojea siku ya Yehova. Kwa hiyo, ni jambo la lazima zaidi kufanya hivyo leo. Sababu gani? Kwa sababu alama yenye Yesu alitoa imeonyesha kwamba yeye ni Mufalme wa Ufalme wa Mungu tangu mwaka wa 1914, na kwamba tunaishi katika siku za mwisho, ao ‘umalizio wa mufumo wa mambo.’ Kwa mufano, kama vile tu Yesu alitabiri, ulimwengu unaendelea kuharibika zaidi na habari njema ya Ufalme inaendelea kuhubiriwa katika dunia yote. (Mathayo 24:3, 7-14) Yesu hakuonyesha siku za mwisho zitachukua muda gani; kwa hiyo, tunapaswa kuwa tayari kwa sababu mwisho unaweza kuja wakati wowote.

6. Ni nini inaonyesha kwamba ulimwengu utakuwa mubaya zaidi kadiri tunakaribia mwisho?

6 Je, ‘umalizio wa mufumo wa mambo’ unazungumuzia wakati unaokuja, ni kusema, wakati ulimwengu utaharibika zaidi kuliko leo? Biblia inasema kwamba watu wataendelea kuwa wabaya zaidi “katika siku za mwisho.” (2 Timotheo 3:1, 13; Mathayo 24:21; Ufunuo 12:12) Kwa hiyo, hata kama ulimwengu uko mubaya sana leo, tunajua kwamba utaendelea kuwa mubaya zaidi.

7. Andiko la Mathayo 24:37-39 linatufundisha nini kuhusu hali ya ulimwengu katika siku za mwisho?

7 Watu fulani wanaweza kufikiri kwamba mbele ‘ziki kubwa’ ianze, kutakuwa vita katika kila inchi, na kwamba watu wengi watakuwa wagonjwa ao kutakuwa njaa kubwa. (Ufunuo 7:14) Lakini, ikiwa mambo hayo inatokea, kila mutu atakuwa amejionea kwamba unabii wa Biblia uko unatimia. Hata watu wenye hawapendezwe na ujumbe wa Biblia wanaweza kujionea jambo hilo. Ukumbuke, Yesu alisema kwamba katika siku za mwisho, watu wengi ‘hawatajali.’ Wataendelea kuishi kama kawaida na watajisikia mubaya wakati siku ya Yehova itakuja. (Soma Mathayo 24:37-39.) Kwa hiyo, hatupaswe kufikiri kuwa ulimwengu utaharibika zaidi mbele ya ‘ziki kubwa,’ na kwamba hali hiyo itafanya watu walazimike kuamini kwamba mwisho unakaribia.—Luka 17:20; 2 Petro 3:3, 4.

Tuko hakika kwamba tunaishi katika ‘umalizio wa mufumo wa mambo’

8. Kwa sababu tunaelewa vizuri alama yenye Yesu alitoa, tuko hakika na jambo gani?

8 Alama yenye Yesu aliwatolea wafuasi wake ilikuwa onyo lenye kuwa wazi juu ya wakati wenye wangekuwa wanaishi ndani. Wafuasi wa Yesu walikuwa wamejulishwa mbele ya wakati. (Mathayo 24:27, 42) Tangu mwaka wa 1914, sehemu nyingi za alama yenye Yesu alitoa zimeendelea kutimia. Tuko hakika kwamba tunaishi katika siku za mwisho, ni kusema, ‘umalizio wa mufumo wa mambo.’ Yehova amekwisha kupanga wakati wa kuharibu ulimwengu muovu wa Shetani.

9. Sababu gani tunapaswa kuendelea kungojea mwisho wenye utafika hivi karibuni?

9 Kwa hiyo, sababu gani tunapaswa kuendelea kungojea mwisho wenye utakuja hivi karibuni? Kwa sababu tunamutii Yesu Kristo. Pia, tunaelewa muzuri zaidi kwamba alama yenye Yesu alitoa juu ya siku za mwisho inaendelea kutimia. Tunaamini kwamba mwisho unakaribia, si kwa sababu tunakubali kila jambo lenye tunasikia, lakini ni kwa sababu tuko hakika kwamba unabii wa Biblia unaendelea kutimia. Tunapaswa kuendelea kukesha na kuwa tayari kwamba mwisho utafika hivi karibuni.

TUNAPASWA KUNGOJEA MUPAKA WAKATI GANI?

10, 11. (a) Sababu gani Yesu aliwaambia wanafunzi wake ‘waendelee kukesha’? (b) Yesu aliwaambia wafuasi wake wafanye nini ikiwa mwisho haufike mbio kama vile waliwazia? (Ona picha kwenye mwanzo wa habari hii.)

10 Wakristo wengi kati yetu wamemutumikia Yehova kwa uaminifu na wamengojea siku yake kwa miaka mingi. Hata kama tumengojea kwa muda wa miaka mingi, tunapaswa kuendelea kungojea siku hiyo yenye itakuja hivi karibuni. Tunapaswa kuwa tayari wakati Yesu atakuja kuharibu ulimwengu huu muovu wa Shetani. Ukumbuke shauri lenye Yesu alitolea wanafunzi wake. Aliwaambia hivi: ‘Muendelee kutazama, muendelee kukesha, kwa maana hamujue wakati uliowekwa ni gani. Ni kama mutu anayesafiri kuenda ngambo, ambaye aliacha nyumba yake na kuwapa mamlaka watumwa wake, kila mumoja kazi yake, na kuamuru mutunza-mulango aendelee kukesha. Kwa hiyo muendelee kukesha, kwa maana hamujue bwana wa nyumba anakuja wakati gani, kama ni wakati wa jioni [mangaribi] ao katikati ya usiku . . . ao asubuhi na mapema, ili anapofika kwa gafula, asiwakute mukiwa mumelala usingizi. Lakini lile ninalowaambia ninyi ninawaambia wote, muendelee kukesha.’—Marko 13:33-37.

Kushambuliwa kwa dini za uongo kunaweza kufanywa haraka na wakati wowote

11 Wakati wafuasi wa Yesu walielewa kwamba ameanza kutawala katika mwaka wa 1914, walijua kwamba mwisho unaweza kuja wakati wowote. Kwa hiyo, walihubiri kwa bidii ili kujitayarisha kwa ajili ya mwisho huo. Yesu alisema kwamba anaweza kuja nyuma, ni kusema, “wakati wa jioni” ao “asubuhi na mapema.” Ikiwa ni hivyo, wafuasi wake wanapaswa kufanya nini? Yesu alisema: ‘Muendelee kukesha.’ Kwa hiyo, hata kama tumengojea kwa miaka mingi, hilo halimaanishe kwamba mwisho ungali mbali ao kwamba hautakuja wakati wetu.

12. Nabii Habakuki alimuomba Yehova nini, naye alimujibu nini?

12 Nabii Habakuki aliendelea kungojea na kutangaza kwamba muji wa Yerusalemu utaharibiwa. Manabii wengine wenye waliishi mbele yake, walikuwa wametangaza ujumbe huo kwa miaka mingi. Inawezekana ubaya na ukosefu wa haki wenye nabii Habakuki aliona ulikuwa mwingi zaidi kuliko zamani. Aliomba Yehova amusaidie. Alisema hivi: ‘Ee Yehova, nililie musaada mupaka wakati gani?’ Hata kama hakumwambia mwisho utakuja wakati gani, Yehova alimuahidi nabii Habakuki hivi: ‘Hautachelewa!’ Alimwambia pia hivi: ‘Uendelee kutarajia [kungojea].’—Soma Habakuki 1:1-4; 2:3.

13. Nabii Habakuki angekuwa na mawazo gani, na hilo lingemuletea hatari gani?

13 Wazia kwamba nabii Habakuki anachoka kungojea na kusema hivi: ‘Nimengojea kwa miaka mingi uharibifu wa muji wa Yerusalemu. Mwisho ungali mbali sana. Si lazima niendelee kuhubiri kuhusu mwisho huo. Wengine wanaweza kufanya kazi hiyo.’ Mambo ingekuwa namna gani ikiwa angewaza hivyo? Angepoteza urafiki wake na Yehova. Na ikiwa hangekuwa tayari wakati mwisho ulikuja, angepoteza maisha yake.

14. Sababu gani tutakuwa wenye shukrani kuona kwamba Yehova ametutolea shauri la kuendelea kungojea ule mwisho?

14 Wazia kwamba uko katika dunia mupya. Matukio yote yenye Yehova alisema zamani juu ya siku za mwisho imetimia kabisa. Kwa hiyo, unamutumainia Yehova zaidi, na unakuwa hakika kabisa kwamba atafanya mambo mengine yote yenye ameahidi. (Soma Yoshua 23:14.) Unakuwa mwenye shukrani sana kwa sababu Yehova alichagua wakati wenye kufaa ili kuleta mwisho na kwa sababu alishauria watumishi wake waendelee kungojea.—Matendo 1:7; 1 Petro 4:7.

TUNAENDELEA KUHUBIRI KWA KUNGOJEA

Unahubiri habari njema kwa bidii? (Ona fungu la 15)

15, 16. Sababu gani tunapaswa kufanya yetu yote ili kuhubiri wakati huu wa mwisho?

15 Tengenezo la Yehova litaendelea kutukumbusha kwamba tukazie akili yetu juu ya kazi ya Yehova katika maisha yetu. Vikumbusho hivyo vinatusaidia tukuwe na mengi ya kufanya katika kazi ya Mungu, na vinatusaidia pia tutambue waziwazi kwamba ujumbe wetu ni wa haraka. Tuko hakika kwamba alama yenye Yesu alitoa inaendelea kutimia leo, na kwamba mwisho unakaribia sana. Kwa hiyo, tunamutia Yehova pa nafasi ya kwanza katika maisha yetu na tunaendelea kuhuburi habari njema ya Ufalme kwa bidii.—Mathayo 6:33; Marko 13:10.

16 Wakati tunahubiria wengine habari njema, tunawasaidia waokoke uharibifu wa ulimwengu huu wa Shetani wenye utakuja hivi karibuni. Kati ya misiba mikubwa yenye imefanyika katika bahari, kuna musiba wenye ulifanyika mwaka wa 1945 wakati mashua (bateau) yenye iliitwa Wilhelm Gustloff ilizama. Maelfu ya watu walikufa. Dada mumoja na bwana yake waliokolewa. Dada huyo anakumbuka kwamba wakati mashua hiyo ilikuwa inazama, mwanamuke mumoja alikuwa analia hivi: “Sakoshe zangu! Sakoshe zangu! Vitu vyangu vya kujipamba! Vyote viko katika kabine. Nimepoteza kila kitu!” Lakini, watu wengine wenye walikuwa katika mashua hiyo walielewa kwamba jambo la lazima sana ilikuwa ni kuokoa uzima wa watu na kwa hiyo, walitumika kwa bidii. Leo, maisha ya watu iko katika hatari. Sisi pia tunapaswa kuiga watu hao wenye walijitolea ili kuokoa uzima wa watu kwa kukaza akili yetu juu ya kazi ya kuhubiri, kwa sababu inapaswa kufanywa kwa haraka. Tunapaswa kufanya nguvu yetu yote ili kusaidia watu waokoke mwisho wa ulimwengu huu muovu.

Chukua maamuzi yenye hekima, na uendelee kukaza akili yako juu ya kazi ya kuhubiri, kwa sababu inapaswa kufanywa kwa haraka (Ona fungu la 17)

17. Sababu gani tunapaswa kuwa hakika kwamba mwisho unaweza kufika wakati wowote?

17 Tunaelewa vizuri kwamba unabii wa Biblia unaendelea kutimia, na kwamba mwisho wa ulimwengu huu muovu unakaribia sana. Tunangojea wakati “zile pembe kumi” na ‘munyama mwitu’ watageukia dini ya uongo, ni kusema, Babiloni Mukubwa. (Ufunuo 17:16) Hatupaswe kufikiri kwamba kungali wakati mwingi sana mbele jambo hilo litokee. Usisahau kwamba Mungu ‘atatia hilo ndani ya mioyo yao’ ili washambulie dini ya uongo, na kwamba shambulizi hilo linaweza kutokea wakati wowote na kwa kushitukia! (Ufunuo 17:17) Mwisho wa ulimwengu muovu wa Shetani unakaribia sana. Kwa hiyo, tunapaswa kutii shauri hili la Yesu: ‘Mujiangalie ninyi wenyewe kwamba mioyo yenu isilemewe kamwe na kula kupita kiasi na kunywa sana na mahangaiko ya maisha, na kwa gafula siku hiyo ikuwe juu yenu mara moja kama mutego.’ (Luka 21:34, 35; Ufunuo 16:15) Tuendelee basi kukesha na kufanya kazi ya Yehova kwa bidii, na kutumaini kwamba ‘atatenda kwa ajili ya mutu anayeendelea kumutarajia.’—Isaya 64:4.

18. Tutajibu ulizo gani katika habari yenye kufuata?

18 Wakati tunaendelea kungojea mwisho wa ulimwengu huu muovu, tunapaswa kutii shauri la mwanafunzi Yuda. Alisema hivi: ‘Wapendwa, kwa kujijenga wenyewe juu ya imani yenu iliyo takatifu zaidi, na kusali mukiwa na roho takatifu, mujitunze katika upendo wa Mungu, huku mukiingojea rehema ya Bwana wetu Yesu Kristo kwa kutazamia uzima wa milele.’ (Yuda 20, 21) Lakini, namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tunangojea kwa hamu ulimwengu mupya wa Mungu wenye utakuja hivi karibuni? Tutajibu ulizo hilo katika habari yenye kufuata.

^ fu. 1 Ili ujue unabii fulani wa Biblia juu ya Masiya na namna ulitimia, soma kitabu Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kwenye ukurasa wa 200