Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Unikumbuke Kwa Ajili ya Wema, Ee Mungu Wangu”

“Unikumbuke Kwa Ajili ya Wema, Ee Mungu Wangu”

Mkaribie Mungu

“Unikumbuke Kwa Ajili ya Wema, Ee Mungu Wangu”

“NILIHISI kuwa kwa sababu Yehova ananijua vema, hawezi kunipenda wala kunikubali.” Hivyo ndivyo alivyoandika mwanamke Mkristo mwaminifu ambaye amekuwa akipambana na hisia za kujiona kuwa hafai. Je, umewahi kuhisi kama mwanamke huyo, kwamba hustahili kutambuliwa au hata kukubaliwa na Mungu? Ikiwa ndivyo, basi huenda maneno yaliyo katika Nehemia 13:31 yakakufariji.

Nehemia, ambaye katika karne ya tano K.W.K., alikuwa gavana wa Wayahudi, alifanya yote aliyoweza kumpendeza Mungu. Aliongoza kazi ya ujenzi wa kuta za Yerusalemu ingawa kulikuwa na upinzani kutoka kwa maadui. Alihakikisha Sheria ya Mungu inafuatwa, akawasaidia waliokandamizwa, na akajitahidi kujenga imani ya Waisraeli wenzake. Je, Mungu alitambua mema ambayo mwanamume huyu mwaminifu alifanya? Je, Nehemia alikubaliwa na Yehova? Tunaweza kupata jibu katika maneno ya kumalizia ya kitabu kinachoitwa kwa jina lake.

Nehemia anasali: “Unikumbuke kwa ajili ya wema, Ee mungu wangu.” * Je, Nehemia anahangaika kuwa Mungu hatatambua matendo yake mema, au atamsahau? Hapana. Bila shaka, Nehemia anajua yale ambayo waandishi wa Biblia waliomtangulia wamesema kuhusu jinsi Yehova anavyopendezwa kikweli na waabudu wake waaminifu na matendo yao mazuri. (Kutoka 32:32, 33; Zaburi 56:8) Hivyo, anamwomba Mungu afanye nini? Kitabu kimoja cha marejeo kinataja kuwa neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘-kumbuka’ linamaanisha “kupenda kitu na pia kuchukua hatua kuhusiana na kitu kinachokumbukwa.” Akiwa na imani katika nguvu ya sala, Nehemia anamwomba Yehova amkumbuke kwa upendo na kumbariki.—Nehemia 2:4.

Je, Yehova atajibu sala ya Nehemia kwa kumkumbuka? Kwa njia moja, tayari amefanya hivyo. Kwa kuwa Yehova aliona inafaa sala ya Nehemia iandikwe na kuwa sehemu ya Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu, jambo hilo linatuhakikishia kuwa Yehova anamkumbuka Nehemia kwa upendo. Lakini “msikiaji wa sala” atafanya mengi zaidi ya kujibu sala ya kutoka moyoni ya Nehemia.—Zaburi 65:2.

Mungu atambariki Nehemia kwa sababu ya mema yote aliyotenda kwa ajili ya ibada safi. (Waebrania 11:6) Katika ulimwengu mpya wenye uadilifu unaokuja ambao Yehova ametuahidi, atambariki Nehemia kwa kumfufua kutoka kwa wafu. * (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Wakati huo, Nehemia ambaye atakuwa na tazamio la kuishi milele katika dunia paradiso, ataona kwamba kwa kweli Yehova amemkumbuka kwa ajili ya wema.

Sala ya Nehemia inaonyesha ukweli wa maneno haya ya Mfalme Daudi: “Wewe mwenyewe utambariki mtu yeyote aliye mwadilifu, Ee Yehova; kana kwamba kwa ngao kubwa, utawazunguka pande zote kwa kibali chako.” (Zaburi 5:12) Ndiyo, Mungu anatambua na kuthamini jitihada zetu za kutoka moyoni za kutaka kumpendeza. Ukijitahidi kufanya yote uwezayo ili kumpendeza, unaweza kuwa na hakika kwamba atakukumbuka kwa upendo na atakubariki kwelikweli.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa Mwezi wa Februari:

Nehemia 1-13

[Maelezo ya Chini]

^ Hii ni sala ya mwisho kati ya sala nne zilizo katika kitabu hiki cha Biblia ambapo Nehemia anamwomba Mungu ili matendo yake ya uaminifu yapate kibali mbele zake.—Nehemia 5:19; 13:14, 22, 31.

^ Kwa habari zaidi kuhusu kusudi la Mungu kwa wanadamu waaminifu hapa duniani, ona sura 3 na 7 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.