Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Kweli Yesu Alikufa Juu ya Msalaba?

Je, Kweli Yesu Alikufa Juu ya Msalaba?

Je, Kweli Yesu Alikufa Juu ya Msalaba?

KITABU kimoja cha marejeo kinasema: “Msalaba ndio alama ya Ukristo inayojulikana sana.” Kazi ya sanaa na michoro mingi ya kidini inamwonyesha Yesu akiwa ametundikwa kwenye msalaba. Kwa nini msalaba unatumiwa sana katika dini zinazodai kuwa za Kikristo? Je, kweli Yesu alikufa msalabani?

Wengi watasema Biblia inajibu swali hilo. Kwa mfano, tafsiri ya Union Version inasema kuwa wakati wa kuuawa kwa Yesu, watazamaji walimdhihaki, wakimwambia “shuka msalabani.” (Mathayo 27:40, 42) Tafsiri nyingine nyingi za Biblia zinasema vivyo hivyo. Biblia Habari Njema inasema hivi kumhusu Simoni wa Kirene: “[Askari] wa[li]mlazimisha achukue msalaba wa Yesu.” (Marko 15:21) Katika mistari hiyo, neno “msalaba” limetafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki staurosʹ. Je, kuna sababu nzuri ya kulitafsiri neno hilo kuwa msalaba? Neno la awali lilimaanisha nini?

Je, Neno Staurosʹ Lilimaanisha Msalaba?

Kulingana na msomi wa Kigiriki W. E. Vine, neno staurosʹ “linamaanisha hasa nguzo au mti ulionyooka. Wahalifu waliuawa kwa kutundikwa kwenye miti kama hiyo. Awali, nomino staurosʹ na kitenzi stauroō, maneno yanayomaanisha kufungia kwenye mti au nguzo, yalimaanisha kitu tofauti na msalaba unaotumiwa katika makanisa, ambao una mbao mbili zilizokingamana.”

Kamusi fulani ya Biblia (The Imperial Bible-Dictionary) inasema kuwa neno staurosʹ “kwa kufaa lilimaanisha mti, nguzo iliyonyooka, au kipande cha mhimili kinachoweza kutumiwa kutundika kitu chochote juu yake, au kinachoweza kutumiwa kutengenezea ua.” Kamusi hiyo inaongeza: “Hata kati ya Waroma inaonekana kuwa mwanzoni neno crux (neno la Kilatini ambalo limetafsiri kuwa cross katika Kiingereza) lilimaanisha nguzo iliyonyooka.” Kwa hiyo, haishangazi kuwa kitabu kimoja cha marejeo (The Catholic Encyclopedia) kinasema hivi: “Vyovyote vile, ni wazi kwamba mwanzoni msalaba ulikuwa nguzo iliyonyooka, ambayo sehemu yake ya juu ilikuwa imechongwa.”

Kuna neno lingine la Kigiriki, xyʹlon, ambalo waandikaji wa Biblia walitumia kuelezea kifaa ambacho Yesu aliuawa juu yake. Kamusi fulani (A Critical Lexicon and Concordance to the English and Greek New Testament) inafafanua xyʹlon kuwa “kipande cha mbao au mti.” Inaendelea kusema kwamba neno xyʹlon, sawa na staurosʹ “linamaanisha tu mti au nguzo iliyonyooka ambayo Waroma waliwapigilia kwa misumari wale waliosemekana kuwa wamesulubiwa.”

Hiyo ndiyo sababu tafsiri ya Union Version inasema hivi kwenye Matendo 5:30: “Mungu wa baba zetu alimfufua Yesu, ambaye ninyi mlimwua mkimtundika katika mti [xyʹlon].” Katika Biblia nyingine pia neno staurosʹ limetafsiriwa kuwa “msalaba,” huku katika Biblia hizohizo neno xyʹlon likitafsiriwa kuwa “mti.” Kwenye Matendo 13:29, tafsiri ya Union Version inasema hivi kumhusu Yesu: “Walipokwisha kumaliza yote aliyoandikiwa, wakamtelemsha katika ule mti [xyʹlon], wakamweka kaburini.”

Kulingana na maana ya msingi ya maneno ya Kigiriki staurosʹ na xyʹlon, kamusi (Critical Lexicon and Concordance) ambayo tayari imenukuliwa inasema: “Maneno yote mawili yanapingana na maoni ya sasa kuhusu msalaba, ambayo yanatokana na picha za msalaba ambazo tumeziona mara nyingi.” Kwa maneno mengine, kile ambacho waandikaji wa vitabu vya Injili walikifafanua kwa kutumia neno staurosʹ ni tofauti kabisa na kile ambacho watu hukiita msalaba leo. Kwa hiyo, kwa kufaa Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inatumia maneno “mti wa mateso” katika Mathayo 27:40-42 na katika maandiko mengine ambapo neno staurosʹ limetumiwa. Vivyo hivyo, tafsiri, Complete Jewish Bible, imetumia maneno “mti ambao watu waliuawa juu yake.”

Chanzo cha Msalaba

Ikiwa kwa kweli Biblia haisemi kuwa Yesu aliuawa juu ya msalaba, basi kwa nini makanisa yote yanayodai kufundisha na kufuata Biblia, kama vile Katoliki, Protestanti, na Othodoksi, yanapamba majengo yao kwa msalaba na kuutumia kama alama ya imani yao? Msalaba ulipataje kuwa alama ya kidini inayotumiwa sana?

Jibu ni kuwa msalaba unatukuzwa sio tu na watu wanaoenda makanisani ambao wanadai kuifuata Biblia, bali pia ulitukuzwa na watu ambao hawakufuata Biblia kamwe, na ambao ibada yao ilikuwapo zamani kabla ya kutokea kwa makanisa ya “Kikristo.” Vitabu mbalimbali vya marejeo vya kidini vinasema kuwa watu walianza kutumia misalaba zamani za kale, ikiwa katika maumbo na miundo mbalimbali. Kwa mfano, mara nyingi maandishi ya kale ya michoro ya Misri na pia michoro ya miungu yao, inaonyesha umbo la herufi T ikiwa na duara juu. Msalaba huo unaitwa ansate, au msalaba wenye kishikio, ambao unafikiriwa kuwa ishara ya uhai. Baada ya muda, msalaba huo ulikubaliwa na kutumiwa sana na Kanisa la Koptiki na makanisa mengine.

Kulingana na kitabu fulani cha marejeo (The Catholic Encyclopedia), “inaonekana msalaba wa zamani zaidi ni ule unaoitwa msalaba wa ‘gamma’ (crux gammata), ambao watu wa Mashariki na wanafunzi wanaochunguza vitu vya kale wanaujua kwa jina lake la Kihindi cha zamani, swastika.” Msalaba huo ulitumiwa sana miongoni mwa Wahindu nchini India na Wabudha kotekote barani Asia, na bado unaonekana kwenye mapambo mbalimbali katika maeneo hayo.

Haijulikani ni wakati gani hasa msalaba ulianza kutumiwa kama alama ya “Ukristo.” Kamusi ya Vine (Expository Dictionary of New Testament Words) inasema: “Kufikia katikati ya karne ya 3 W.K., makanisa yalikuwa yameacha, au yalikuwa yamepotosha, mafundisho fulani ya imani ya Kikristo. Ili kuongeza sifa ya kanisa lililoasi, wapagani walikubaliwa katika makanisa ingawa hawakuwa wameweka imani katika mafundisho ya Kikristo, na katika mambo mengi waliruhusiwa kuendelea kuwa na alama na mifano yao ya kipagani,” kutia ndani msalaba.

Waandishi fulani hutaja tukio la mwaka wa 312 W.K. wakati ambapo inasemekana kuwa Konstantino, aliyeabudu jua, aliona njozi ya msalaba ukiwa juu ya uso wa jua na pia maneno ya Kilatini “in hoc vince” (kwa huu shinda). Wakati huo alikuwa katika mojawapo ya shughuli zake za kivita. Baadaye, alama hiyo ya “Kikristo” iliwekwa kwenye bendera, ngao, na kwenye silaha za jeshi lake. (Ona picha upande wa kushoto.) Inadaiwa kuwa Konstantino aligeuza imani na kuwa Mkristo, ingawa alibatizwa miaka 25 baadaye, akiwa karibu kufa. Watu fulani walitilia shaka nia yake. “Badala ya kufuata mafundisho ya Yesu Mnazareti, Konstantino alijaribu kubadili Ukristo uwe dini ya watu wote ambayo ingeweza kukubaliwa na raia zake,” kinasema kitabu The Non-Christian Cross.

Tangu wakati huo, misalaba yenye maumbo na miundo mbalimbali imetumiwa. Kwa mfano, kamusi fulani ya Biblia (The Illustrated Bible Dictionary) inasema kuwa ule unaoitwa msalaba wa Mt. Anthony “ulikuwa na umbo linalofanana na herufi kubwa ya T. Watu fulani wanafikiri kuwa umbo la msalaba huo lilitokana na alama ya mungu Tamuzi [wa Wababiloni].” Pia kulikuwa na msalaba wa Mt. Andrew, ambao una umbo la herufi ya X, na ule msalaba tunaojua ambao una mbao mbili zilizokingamana. Msalaba huu wenye mbao mbili zilizokingamana unaitwa msalaba wa Kilatini, na “katika mapokeo unaonwa [kimakosa] kuwa aina ya msalaba ambao Bwana wetu alikufa juu yake.”

Wakristo wa Karne ya Kwanza Waliamini Nini?

Biblia inaonyesha kuwa katika karne ya kwanza, wengi waliomsikia Yesu waliamini na kukubali thamani ya kifo chake cha kidhabihu chenye kuokoa uhai. Biblia inasema kwamba baada ya mtume Paulo kuwahubiria Wayahudi huko Korintho na kuwathibitishia kuwa Yesu ndiye Kristo, “Krispo, ofisa-msimamizi wa sinagogi akawa mwamini katika Bwana, na ndivyo na watu wote wa nyumba yake. Na wengi kati ya Wakorintho waliosikia wakaanza kuamini na kubatizwa.” (Matendo 18:5-8) Badala ya kuanzisha matumizi ya alama au mfano fulani wa kidini katika ibada yao, Paulo aliwashauri Wakristo wenzake ‘waikimbie ibada ya sanamu’ na zoea lingine lolote linalotokana na ibada ya kipagani.—1 Wakorintho 10:14.

Wanahistoria na watafiti hawajapata uthibitisho wowote unaoonyesha kuwa Wakristo wa mapema walitumia msalaba. Inapendeza kuwa kitabu History of the Cross kinamnukuu mwandishi mmoja aliyeandika mwishoni mwa karne ya 17 ambaye aliuliza: “Je, Yesu anaweza kufurahi kuwaona wanafunzi Wake wakitukuza mfano wa kitu kilichotumiwa katika hukumu ya kifo na ambacho juu yake [inasemekana] kuwa Aliteseka bila hatia, huku akiidharau aibu?” Ungesema nini?

Hatuhitaji kutumia vitu au mifano ili ibada yetu ikubaliwe na Mungu. Paulo aliuliza: “Hekalu la Mungu lina upatano gani na sanamu?” (2 Wakorintho 6:14-16) Hakuna mahali ambapo Maandiko yanadokeza kuwa ibada ya Mkristo inapaswa kutia ndani kutumia mfano wa kifaa ambacho kilitumiwa kumtundikia Yesu.—Linganisha Mathayo 15:3; Marko 7:13.

Hivyo basi, ni alama gani inayowatambulisha Wakristo wa kweli? Si msalaba wala alama nyingine yoyote, bali ni upendo. Yesu aliwaambia wafuasi wake hivi: “Ninawapa ninyi amri mpya, kwamba mpendane; kama vile ambavyo nimewapenda ninyi, ninyi nanyi mpendane vivyo hivyo. Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu, mkiwa na upendo kati yenu wenyewe.”—Yohana 13:34, 35.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Kile ambacho waandikaji wa Biblia walifafanua kwa kutumia neno staurosʹ ni tofauti kabisa na kile ambacho watu hukiita msalaba leo

[Picha katika ukurasa wa 18]

Mchoro wa karne ya 17 wa mtu aliyeuawa kwenye staurosʹ, kutoka katika kitabu “de Cruce” cha Lipsius

[Picha katika ukurasa wa 19]

Mchoro wa ukutani wa Wamisri (yapata karne ya 14 K.W.K.) Unaoonyesha msalaba wa ansate, ishara ya uhai

[Hisani]

© DeA Picture Library / Art Resource, NY

[Picha katika ukurasa wa 19]

Msalaba wa gamma kwenye Hekalu la Laxmi Narayan la Wahindu

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 20]

From the book The Cross in Tradition, History, and Art (1897)