Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Yesu Aliishi Jinsi Gani?

Yesu Aliishi Jinsi Gani?

Yesu Aliishi Jinsi Gani?

“Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.”—YOHANA 4:34.

YESU alisema maneno hayo katika hali ambayo inafunua mengi kuhusu jambo lililokuwa muhimu zaidi maishani mwake. Katika kipindi chote cha asubuhi, Yesu na wanafunzi wake walikuwa wamesafiri katika nchi yenye milima-milima ya Samaria. (Yohana 4:6) Wanafunzi wake walifikiri kwamba kufikia wakati huo Yesu alikuwa na njaa, hivyo wakampa chakula. (Yohana 4:31-33) Lakini Yesu akawaeleza kifupi kuhusu kusudi lake maishani. Kufanya kazi ya Mungu lilikuwa jambo muhimu zaidi maishani mwake kuliko kula. Kwa maneno na matendo yake, Yesu alionyesha kuwa aliishi ili kufanya mapenzi ya Mungu. Hayo yalitia ndani nini?

Kuhubiri na kufundisha kuhusu Ufalme wa Mungu Biblia inaeleza kazi ambayo Yesu alifanya maishani mwake kwa kusema: “Akaenda akizunguka katika Galilaya yote, akifundisha . . . na kuhubiri habari njema ya ufalme.” (Mathayo 4:23) Yesu hakuwahubiria tu, au kuwatangazia, watu Ufalme wa Mungu. Bali aliwafundisha, akawafafanulia mambo, na kutoa hoja zenye kusadikisha. Kichwa kikuu cha ujumbe wake kilikuwa Ufalme.

Katika huduma yake yote, Yesu aliwafundisha wasikilizaji wake Ufalme wa Mungu ni nini na yale ambayo utafanya. Ona kweli zifuatazo kuhusu Ufalme na Maandiko yanayoonyesha maneno ya Yesu kuhusu kweli hizo.

▪ Ufalme wa Mungu ni serikali ya kimbingu, na Yehova alimchagua Yesu kuwa Mfalme.—MATHAYO 4:17; YOHANA 18:36.

▪ Ufalme utatakasa jina la Mungu na kufanya mapenzi yake yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.—MATHAYO 6:9, 10.

▪ Chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu, dunia nzima itabadilishwa na kuwa paradiso.—LUKA 23:42, 43.

▪ Hivi karibuni Ufalme wa Mungu utakuja na kutekeleza kusudi la Mungu kuelekea dunia. *—MATHAYO 24:3, 7-12.

Kufanya miujiza Yesu alijulikana hasa kuwa “Mwalimu.” (Yohana 13:13) Hata hivyo, katika utumishi aliofanya kwa miaka mitatu na nusu, Yesu alifanya miujiza kadhaa pia. Alifanya miujiza hiyo ili kutimiza makusudi mawili hivi. Kwanza, miujiza hiyo ilisaidia kuthibitisha kuwa alitumwa na Mungu. (Mathayo 11:2-6) Pili, ilionyesha yale ambayo angefanya wakati ujao kwa kiwango kikubwa hata zaidi akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Hebu ona baadhi ya miujiza aliyofanya.

▪ Alituliza bahari iliyochafuka na upepo uliovuma kwa nguvu.—MARKO 4:39-41.

▪ Aliwaponya wagonjwa, kutia ndani vipofu, viziwi, na vilema.—LUKA 7:21, 22.

▪ Alifanya chakula kiwe kingi na hivyo kulisha umati wenye njaa.—MATHAYO 14:17-21; 15:34-38.

▪ Katika pindi tatu hivi, alifufua wafu.—LUKA 7:11-15; 8:41-55; YOHANA 11:38-44.

Hebu wazia jinsi maisha yatakavyokuwa chini ya utawala wa Mfalme huyo mwenye nguvu!

Kufunua sifa za Yehova Mungu Inapohusu kuwafundisha wengine kumhusu Yehova, hakuna mtu anayeweza kufanya hivyo vizuri zaidi kuliko Mwana wa Mungu, ambaye alikuja kuitwa Yesu Kristo. Akiwa “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote,” Yesu aliishi pamoja na Yehova huko mbinguni kwa muda mrefu kuliko kiumbe mwingine yeyote wa roho. (Wakolosai 1:15) Fikiria nafasi alizokuwa nazo za kuelewa njia ya kufikiri ya Baba yake na kujifunza makusudi, kanuni, na njia Zake.

Kwa hiyo, kwa kufaa Yesu alisema: “Hakuna anayemjua Mwana ni nani ila Baba; na hakuna anayemjua Baba ni nani ila Mwana, na yule ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Luka 10:22) Alipokuwa mwanadamu hapa duniani, Yesu alifunua sifa za Baba yake kwa hamu na bila kulazimishwa. Aliongea na kufundisha kwa njia ya kipekee kwa kuwa alikumbuka mambo aliyojionea mwenyewe alipokuwa katika makao ya roho pamoja na Mungu Aliye Juu Zaidi.—Yohana 8:28.

Yale ambayo Yesu alifanya yanaweza kulinganishwa na kazi ambayo hufanywa na transfoma ya umeme. Mashine hiyo inaweza kupokea umeme mwingi na kuupunguza ili kutokeza umeme kidogo unaofaa kwa ajili ya matumizi ya kawaida. Alipokuwa duniani, Yesu alifundisha mambo aliyokuwa amejifunza kutoka kwa Baba yake kwa njia rahisi ambayo wanadamu wa hali ya chini wangeweza kuyaelewa na kuyatumia.

Fikiri njia mbili muhimu ambazo Yesu alifunua sifa za Baba yake.

▪ Katika mafundisho yake Yesu alijulisha ukweli kumhusu Yehova—Jina lake, kusudi lake, na njia zake.—YOHANA 3:16; 17:6, 26.

▪ Kupitia matendo yake, Yesu alifunua sifa nyingi nzuri za Yehova. Yesu alionyesha sifa za Yehova kwa ukamili sana hivi kwamba ni kama alikuwa akisema: ‘Mkitaka kujua jinsi Yehova alivyo, mnitazame.’—YOHANA 5:19; 14:9.

Tunavutiwa na jinsi Yesu alivyoishi. Tunaweza kufaidika sana kwa kuchunguza kwa nini alikufa na kutenda kulingana na mambo tunayojifunza.

[Maelezo ya Chini]

^ Ili ujifunze mengi kuhusu Ufalme wa Mungu na kwa nini tunasema kwamba hivi karibuni utakuja, ona sura ya 8, “Ufalme wa Mungu Ni Nini?,” na sura ya 9, “Je, Tunaishi Katika ‘Siku za Mwisho’?,” za kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.