Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Siri ya Furaha ya Familia

How Children Change a Marriage

How Children Change a Marriage

Charles: * “Mimi na Mary tulifurahi sana binti yetu alipozaliwa. Lakini kwa miezi kadhaa baada ya kuzaliwa kwake sikuweza kulala vizuri. Tulikuwa na mipango mbalimbali kuhusu jinsi ya kumtunza, lakini yote haikufaulu.”

Mary: “Baada ya mtoto wetu kuzaliwa, sikuwa na uhuru wa kufanya mambo niliyotaka. Ghafla, mambo muhimu katika maisha yangu yakawa kumnyonyesha mtoto, kumbadili nepi, au kujaribu kumbembeleza anyamaze. Hilo lilikuwa badiliko kubwa katika maisha yangu. Miezi kadhaa ilipita kabla ya uhusiano wangu na Charles kurudia hali ya kawaida.”

WATU wengi watakubali kwamba kupata mtoto ni mojawapo ya mambo yanayoleta shangwe nyingi zaidi katika maisha. Biblia inawataja watoto kuwa “thawabu” kutoka kwa Mungu. (Zaburi 127:3) Pia, wazazi wapya kama vile Charles na Mary, wanajua kwamba watoto wanaweza kubadili maisha ya ndoa katika njia zisizotazamiwa. Kwa mfano, mwanamke anapojifungua kwa mara ya kwanza anaweza kumkazia uangalifu sana mtoto wake na kushangaa jinsi mwili na moyo wake unavyoitikia mahitaji madogo-madogo ya mtoto. Naye baba ya mtoto huyo anaweza kushangazwa na uhusiano wa karibu uliopo kati ya mke wake na mtoto wao, lakini anaweza pia kuwa na wasiwasi kwamba anapuuzwa.

Kwa kweli, kuzaliwa kwa mtoto kunaweza kuchangia matatizo katika ndoa. Matatizo ya kihisia na mambo mengine ambayo hayakuwa yametatuliwa hapo mwanzoni, yanaweza kuwa wazi zaidi kwa sababu ya ugumu wa kuwa mzazi.

Wazazi wapya wanaweza kufanya nini ili kukabiliana na miezi kadhaa ya kwanza yenye shughuli nyingi ambayo mtoto atahitaji uangalifu wao wote? Wenzi wa ndoa wanaweza kufanya nini ili kudumisha uhusiano wao wa karibu? Na wanaweza kushughulikia jinsi gani kutoelewana kuhusu jinsi ya kumlea mtoto wao? Acheni tuchunguze kila moja ya matatizo hayo na kufikiria jinsi kanuni za Biblia zinavyoweza kuwasaidia wenzi wa ndoa kutatua matatizo hayo.

TATIZO LA 1: Kwa ghafla wazazi wanalazimika kutumia wakati mwingi kumtunza mtoto.

Mama hutumia wakati mwingi kumtunza na kufikiria mahitaji ya mtoto wake mchanga. Huenda mama huyo akahisi ameridhika kihisia anapotimiza jukumu lake la kumtunza mtoto. Wakati huohuo, mume wake anaweza kuhisi kuwa amepuuzwa. Manuel, anayeishi Brazili anasema hivi: “Haikuwa rahisi kwangu kukabiliana na hali ya mke wangu ya kumkazia fikira zaidi mtoto wetu kuliko mimi. Mwanzoni mke wangu alikazia fikira uhusiano kati yetu wawili, kisha ghafla akaanza kumkazia fikira mtoto wetu.” Unaweza kukabiliana jinsi gani na badiliko hilo?

Siri ya mafanikio: Uwe na subira.

“Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili,” inasema Biblia. Upendo “hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki.” (1 Wakorintho 13:4, 5) Mtoto anapozaliwa, mume na mke wanaweza kutumia jinsi gani shauri hilo?

Mume mwenye hekima huonyesha upendo kwa mke wake kwa kujitahidi kuelewa mabadiliko ya kiakili na ya kimwili ambayo mama anaweza kuwa nayo baada ya kujifungua. Akifanya hivyo, ataweza kutambua kwa nini huenda hisia za mke wake zikabadilika-badilika ghafla. * Adam, anayeishi Ufaransa na ambaye ni baba ya binti mwenye umri wa miezi 11, anasema hivi: “Nyakati nyingine ni vigumu kukabiliana na badiliko la hisia la mke wangu. Lakini ninajitahidi kukumbuka kwamba havunjiki moyo kwa sababu yangu, badala yake, ni kwa sababu ya mfadhaiko unaosababishwa na hali yetu mpya.”

Je, nyakati nyingine mke wako anakosa kuelewa jitihada zako za kutaka kumsaidia? Ikiwa ndivyo, usikasirike haraka. (Mhubiri 7:9) Badala yake, kwa subira tanguliza mahitaji yake, na kwa kufanya hivyo utaepuka kukasirika.​—Methali 14:29.

Kwa upande mwingine, mke mwenye utambuzi atamtia moyo mume wake katika jukumu lake jipya. Atamshirikisha katika kumtunza mtoto, kwa subira akimwonyesha jinsi ya kumbadili mtoto nepi au jinsi ya kuosha chupa za kunyonyeshea, ingawa huenda akaonekana kama hafanyi kazi hiyo vizuri mwanzoni.

Ellen, mama mwenye umri wa miaka 26, anakubali kwamba alihitaji kufanya marekebisho fulani kuhusu jinsi anavyomtendea mume wake. Anasema hivi: “Nilipaswa kujizuia ili nisimwone mtoto kuwa wangu peke yangu. Pia, nilipaswa kukumbuka kwamba sipaswi kutazamia mengi kutoka kwa mume wangu anapojaribu kutumia mapendekezo ninayompa ya jinsi ya kumtunza mtoto.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Wake, ikiwa waume zenu wanafanya jambo fulani kwa njia tofauti na yenu, epukeni kuwalaumu au kufanya kazi hiyo upya. Mpongeze anapofanya kazi hiyo vizuri. Ukifanya hivyo, utamsaidia ajiamini na hivyo kumtia moyo aendelee kukusaidia. Waume, punguzeni shughuli zisizo muhimu sana ili muwe na wakati mwingi iwezekanavyo wa kuwasaidia wake zenu, hasa katika ile miezi kadhaa ya kwanza baada ya mtoto kuzaliwa.

TATIZO LA 2: Uhusiano wenu mkiwa mume na mke unadhoofika.

Wazazi wengi wapya huchoka kwa sababu ya kukosa usingizi na matatizo mengine yasiyotazamiwa, hivyo wao hujitahidi sana kuwa na uhusiano wa karibu. Vivianne, mama ya watoto wawili wadogo ambaye ni Mfaransa, anasema hivi: “Mwanzoni, nilikazia uangalifu sana jukumu langu nikiwa mama hivi kwamba nilikuwa karibu kusahau jukumu langu nikiwa mke.”

Kwa upande mwingine, mume anaweza kukosa kutambua kwamba mimba imemuathiri mke wake kimwili na kihisia. Mtoto anaweza kutumia wakati na nguvu ambazo nyote wawili mlitumia ili kudumisha uhusiano mzuri kihisia na kingono. Hivyo basi, wenzi wa ndoa wanaweza kufanya nini ili kuhakikisha kwamba mtoto wao mpendwa hawatenganishi?

Siri ya mafanikio: Mhakikishie mwenzi wako kwamba unampenda.

Ikieleza kuhusu ndoa, Biblia inasema hivi: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake nao watakuwa mwili mmoja.” * (Mwanzo 2:24) Yehova Mungu alikusudia kwamba hatimaye watoto wangewaacha wazazi wao. Kwa upande mwingine, anatarajia kifungo cha ndoa kati ya mume na mke kiwe cha kudumu. (Mathayo 19:3-9) Kuthamini jambo hilo kunaweza kuwasaidia jinsi gani wenzi wa ndoa waliopata mtoto watangulize mambo yanayofaa zaidi?

Vivianne, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Nilifikiria maneno ya andiko la Mwanzo 2:24, na mstari huo ulinisaidia kutambua kwamba nilikuwa ‘mwili mmoja’ na mume wangu bali si na mtoto wangu. Niliona umuhimu wa kuimarisha ndoa yetu.” Theresa, mama ya binti mwenye umri wa miaka miwili, anasema hivi: “Ninapoanza kuhisi kwamba uhusiano wangu na mume wangu umeanza kudhoofika, mimi hujitahidi mara moja kumkazia uangalifu, hata ikiwa ni kwa muda mfupi tu kila siku.”

Ikiwa wewe ni mume, unaweza kufanya nini ili kuimarisha ndoa yako? Mwambie mke wako unampenda. Na uthibitishe maneno yako kwa matendo. Fanya jitihada za kuondoa shaka zozote ambazo mke wako anaweza kuwa nazo. Sarah, mama mwenye umri wa miaka 30, anasema hivi: “Mke anapaswa kujua kwamba bado anathaminiwa na kupendwa, hata ingawa mwili wake hauko kama ulivyokuwa zamani kabla ya kupata mimba.” Alan, baba ya wavulana wawili ambaye anaishi Ujerumani, anaona umuhimu wa kumtegemeza mke wake kihisia. Anasema hivi: “Nyakati zote nimejaribu kumtia moyo mke wangu anapohuzunika.”

Inaeleweka kwamba baada ya mtoto kuzaliwa, uhusiano wa kingono kati ya mume na mke unavurugika. Hivyo, mume na mke wanapaswa kuzungumza kuhusu mahitaji yao. Biblia inasema kwamba mabadiliko hayo katika uhusiano wa kingono kati ya mume na mke yanapaswa kufanywa kwa “makubaliano.” (1 Wakorintho 7:1-5) Jambo hilo linahitaji mawasiliano. Ikitegemea jinsi mlivyolelewa au utamaduni wenu, huenda mkasita kuzungumza kuhusu ngono. Lakini mazungumzo kama hayo ni muhimu mnapoendelea kukabiliana na majukumu mbalimbali ya kuwa wazazi. Mwe wenye huruma, subira, na wanyofu. (1 Wakorintho 10:24) Hivyo, mtaepuka kutoelewana, na badala yake kuimarisha upendo kati yenu.​—1 Petro 3:7, 8.

Wenzi wa ndoa wanaweza kuimarisha upendo kati yao kwa kuwa na shukrani. Mume mwenye hekima atatambua kwamba si rahisi kuona kazi nyingi ambazo mke wake aliyejifungua karibuni anafanya. Vivianne anasema hivi: “Siku inapoisha, mara nyingi ninaona kana kwamba sijatimiza lolote—hata ingawa nilikuwa na shughuli nyingi za kumtunza mtoto!” Hata ingawa ana shughuli nyingi, mke mwenye utambuzi atakuwa mwangalifu asipuuze yale ambayo mume wake anafanya kwa ajili ya familia.z—Methali 17:17.

JARIBU KUFANYA HIVI: Inapowezekana ninyi akina mama pumzikeni kidogo wakati ambapo mtoto amelala. Mkifanya hivyo, mtapata nguvu zaidi zitakazowasaidia kuendelea na maisha yenu ya ndoa. Akina baba, inapowezekana, amkeni usiku kumlisha au kumbadili mtoto nepi ili mke wako aweze kupumzika. Thibitisha upendo wako kwa mke wako kwa kumwandikia ujumbe mfupi, kumtumia ujumbe mfupi kwa simu, au kumpigia simu. Mkiwa mume na mke, tengeni wakati wa kuzungumza ana kwa ana. Zungumzeni mambo yanayowahusu nyote wawili, si kumhusu mtoto tu. Imarisheni urafiki wenu, na hivyo mtaweza kukabiliana vizuri zaidi na matatizo ya kuwa wazazi.

TATIZO LA 3: Kutoelewana kuhusu jinsi ya kumlea mtoto wenu.

Mume na mke wanaweza kugundua kwamba malezi yao yanaweza kuwafanya wasielewane. Mama mmoja Mjapani anayeitwa Asami na mume wake, Katsuro, walikabili tatizo hilo. Asami anasema, “Nilihisi mume wangu alikuwa akimwendekeza sana binti yetu, naye alihisi nilikuwa mkali kupita kiasi.” Mnaweza kuepuka jinsi gani hali hiyo ya kutoelewana?

Siri ya mafanikio: Zungumza na mume au mke wako, na mtegemezane.

Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Kwa sababu ya kimbelembele mtu husababisha tu pambano, lakini wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.” (Methali 13:10) Je, unajua ni mambo gani ambayo mwenzi wako anafahamu kuhusu kulea watoto? Ikiwa utangoja hadi mtoto wenu azaliwe ndipo mzungumzie mambo ya msingi kuhusu kumzoeza mtoto, huenda mtaishia kuvutana badala ya kutatua matatizo kwa njia nzuri.

Kwa mfano, mmekubaliana nini kuhusu maswali yanayofuata: “Tunaweza kumfundisha jinsi gani mtoto wetu tabia nzuri kuhusiana na kula na kulala? Je, tutapaswa kumchukua mtoto kila anapolia wakati wa kulala? Tunapaswa kukabiliana jinsi gani na ugumu wa kumfundisha mtoto wetu jinsi ya kutumia choo?” Bila shaka, maamuzi mnayofanya yatakuwa tofauti na ya wazazi wengine. Ethan, ambaye ni baba ya watoto wawili, anasema, “Mnapaswa kuzungumzia mambo ili mweze kukubaliana. Kisha kwa pamoja mtaweza kushughulikia mahitaji ya mtoto wenu.”

JARIBU KUFANYA HIVI: Fikiria njia ambazo wazazi wako walitumia walipokulea. Amua ni njia gani ambazo ungependa kutumia unapomlea mtoto wako. Pia, amua ikiwa kuna njia yoyote ambayo ungependa kuepuka usiirudie. Zungumza na mwenzi wako wa ndoa kuhusu maamuzi unayofikia.

Mtoto Anaweza Kubadili Kabisa Maisha ya Ndoa

Kama vile wanasarakasi wawili wanavyohitaji wakati na subira wanapofanya mazoezi ili kufaulu katika onyesho lao, vivyo hivyo ninyi mnahitaji wakati ili muweze kushughulikia majukumu yenu mapya mkiwa wazazi. Mwishowe, mtaweza kuwa na uhakika mnaposhughulika na majukumu yenu.

Kulea watoto kutapima jinsi ambavyo umejitoa katika ndoa yenu na kunaweza kubadili uhusiano wenu. Hata hivyo, kutakupa pia nafasi ya kukuza sifa nzuri. Ikiwa utatumia shauri lenye hekima la Biblia, hali yako itakuwa kama ile ya baba anayeitwa Kenneth. Anasema hivi: “Kulea watoto kumekuwa na matokeo mazuri kwangu na kwa mke wangu. Sasa hatuna ubinafsi na tunapendana na kuelewana.” Bila shaka, mabadiliko kama hayo yanafaa katika ndoa.

^ fu. 3 Majina katika makala hii yamebadilishwa.

^ fu. 11 Majuma machache baada ya kujifungua akina mama wengi hushuka moyo kidogo. Lakini kwa wengine, hali hiyo ya kushuka moyo huwa mbaya sana. Kwa habari zaidi kuhusu jinsi ya kutambua na kukabiliana na hali hiyo, ona makala “Nilipambana na Ugonjwa wa Kushuka Moyo Baada ya Kujifungua,” katika toleo la Amkeni! la Julai 22, 2002 (22/7/2002), na makala “Kuelewa Mshuko wa Moyo Baada ya Kujifungua,” katika toleo la Amkeni! la Juni 8, 2003 (8/6/2003), yaliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Unaweza kusoma makala hizo katika Intaneti www.watchtower.org.

^ fu. 19 Kulingana na kitabu cha mtaalamu mmoja, neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘shikamana’ katika andiko la Mwanzo 2:24 linaweza kumaanisha ‘kuambatana na mtu kwa upendo na ushikamanifu.’

JIULIZE . . .

  • Katika juma lililopita, nimefanya nini ili kumwonyesha mwenzi wangu wa ndoa kwamba ninathamini anachofanya kwa ajili ya familia yetu?

  • Mara ya mwisho kuwa na mazungumzo ya ana kwa ana na mwenzi wangu ambayo hayakuhusu kulea watoto, ilikuwa lini?