Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Wakristo Wote Waaminifu Wanaenda Mbinguni?

Je, Wakristo Wote Waaminifu Wanaenda Mbinguni?

Wasomaji Wetu Wanauliza . . .

Je, Wakristo Wote Waaminifu Wanaenda Mbinguni?

▪ Wengi wamesoma maneno haya ya Yesu yenye kufariji: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yohana 3:16) Je, Yesu alimaanisha kwamba waabudu wote waaminifu wa Baba yake, Yehova Mungu, wangeenda mbinguni ndio waweze kufurahia uzima milele?

Ona maneno ya Yesu yenye kuamsha fikira: “Hakuna mtu ambaye amepanda kuingia mbinguni ila yule aliyeshuka kutoka mbinguni, Mwana wa binadamu.” (Yohana 3:13) Andiko hilo linamaanisha kwamba waabudu waaminifu wa zamani, kama vile Noa, Abrahamu, Musa, na Daudi, hawakwenda mbinguni. (Matendo 2:34) Hivyo basi, wote hao walienda wapi? Kwa ufupi: Watu waaminifu waliomtumikia Mungu zamani wamo makaburini, ambamo wamelala fofofo katika kifo wakingojea ufufuo.—Mhubiri 9:5, 6; Matendo 24:15.

Yesu ndiye wa kwanza kutaja kwamba watu fulani wangeishi mbinguni baada ya kufa. Aliwaambia mitume wake kwamba angewatayarishia mahali mbinguni. (Yohana 14:2, 3) Hilo lilikuwa jambo jipya kwa watu wa Mungu. Baadaye mtume Paulo alieleza kwamba baada ya Yesu kufa na kufufuliwa kwenda mbinguni, ‘aliwazindulia wanafunzi wake njia mpya na yenye uzima’—njia ambayo hakuna mwingine aliyekuwa amewahi kuipitia.—Waebrania 10:19, 20.

Je, hilo linamaanisha kwamba kuanzia wakati huo na kuendelea wote walio waaminifu kwa Mungu wangeenda mbinguni? Hapana, kwa kuwa wale wanaofufuliwa kwenda mbinguni, wanaenda huko kwa sababu ya mgawo, au kazi, ambayo inapewa wanadamu fulani tu. Alipokuwa na mitume wake katika jioni yao ya mwisho pamoja, Yesu aliwaambia kwamba katika Ufalme wake wa mbinguni ‘wangeketi kwenye viti vya ufalme ili kuhukumu.’ Hivyo, mgawo wao ungekuwa kutawala pamoja na Yesu mbinguni.—Luka 22:28-30.

Kando na mitume, kuna wanadamu wengine pia ambao wangepewa mgawo huo mzuri. Katika maono, mtume Yohana alimwona Yesu akiwa mbinguni pamoja na kikundi cha watu waliofufuliwa ambao wanatajwa kuwa ‘ufalme na makuhani watakaotawala dunia.’ (Ufunuo 3:21; 5:10) Walikuwa wangapi? Kama inavyokuwa katika serikali nyingi, ni watu wachache tu wanaokuwa katika utawala. Na hivyo ndivyo ilivyo kuhusiana na Ufalme wa mbinguni. Yesu, Mwana-Kondoo wa Mungu, anatawala pamoja na watu 144,000 ambao “walinunuliwa kutoka kati ya wanadamu.”—Ufunuo 14:1, 4, 5.

Ni kweli kwamba watu 144,000 ni wachache wakilinganishwa na idadi ya waaminifu wote, wa wakati huu na uliopita pia. Lakini jambo hilo linaeleweka kwa sababu wale 144,000 wanafufuliwa kwenda mbinguni kwa ajili ya kazi hususa takatifu. Kama ungetaka kujenga nyumba, je, ungeajiri mafundi wote katika eneo lenu ambao wana ujuzi wa kujenga? Hapana. Ungeajiri tu idadi ya mafundi ambao wangehitajika kufanya kazi hiyo. Vivyo hivyo, si waaminifu wote wanaochaguliwa na Mungu kwa ajili ya pendeleo hilo la pekee la kutawala pamoja na Kristo mbinguni.

Serikali hiyo ya mbinguni itatimiza yale ambayo Mungu alikusudia mwanzoni kuwahusu wanadamu. Yesu na watawala wenzake 144,000 watasimamia kazi ya kuigeuza dunia yote kuwa paradiso, ambapo idadi kubwa sana ya watu waaminifu wataishi milele kwa furaha. (Isaya 45:18; Ufunuo 21:3, 4) Idadi hiyo itatia ndani wale walio katika kumbukumbu la Mungu, ambao watafufuliwa.—Yohana 5:28, 29.

Kila mwabudu mwaminifu wa Yehova—wa wakati huu au uliopita—anaweza kupokea zawadi nzuri ya uzima wa milele. (Waroma 6:23) Wachache watapokea uhai mbinguni kwa sababu ya mgawo fulani hususa, na walio wengi watapokea uhai katika dunia itakayokuwa paradiso.