Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Yehova Ana Hisia?

Je, Yehova Ana Hisia?

Mkaribie Mungu

Je, Yehova Ana Hisia?

IKIWA jibu ni ndiyo, basi swali lingine linazuka: Je, mwenendo au matendo yetu yanaweza kuathiri hisia za Mungu, yaani, tunaweza kumhuzunisha au kumfurahisha kupitia matendo yetu? Wanafalsafa fulani wa kale walisema haiwezekani. Walisema kwamba hakuna mtu anayeweza kuathiri hisia za Mungu na hivyo lazima iwe Mungu hana hisia. Lakini Biblia inatufundisha jambo tofauti, kwamba Yehova ana hisia na anajali sana yale tunayofanya. Fikiria maneno yaliyo katika Zaburi 78:40, 41.

Zaburi sura ya 78 inaeleza kifupi jinsi Mungu alivyoshughulika na taifa la Israeli la kale. Baada ya kulikomboa kutoka utumwani Misri, Yehova alianzisha uhusiano wa kipekee pamoja na taifa hilo. Aliwaahidi kuwa ikiwa wangeendelea kutii sheria zake, ‘wangekuwa mali yake ya pekee’ na angewatumia katika njia ya kipekee ili kutimiza kusudi lake. Watu walikubali na wakaingia katika agano la Sheria. Je, walitenda kulingana na agano hilo walilofanya pamoja na Mungu?—Kutoka 19:3-8.

Mtunga zaburi anasema: “Jinsi walivyomwasi mara nyingi nyikani!” (Mstari wa 40) Mstari unaofuata unaongezea: ‘Walimjaribu Mungu tena na tena.’ (Mstari wa 41) Ona kwamba mwandishi huyo anaeleza jinsi Waisraeli walivyorudia-rudia mwenendo wao wa uasi. Roho hiyo ya kukosa heshima na uasi ilianza mapema—wakiwa nyikani, muda mfupi baada ya kukombolewa kutoka Misri. Waisraeli walianza kumnung’unikia Mungu, wakitilia shaka kama alikuwa na uwezo na nia ya kuwatunza. (Hesabu 14:1-4) Kitabu kimoja cha marejeo ya watafsiri wa Biblia kinasema kwamba neno “walivyomwasi” linaweza “kutafsiriwa kuwa ‘waliamua mioyoni mwao kumwasi Mungu’ au ‘kusema “Hapana” kwa Mungu.’” Hata hivyo, kwa rehema zake, Yehova aliwasamehe watu wake walipotubu. Lakini, baadaye wangerudia mwenendo wao wa zamani na kumwasi Mungu tena, na kuendeleza uasi wao.—Zaburi 78:10-19, 38.

Yehova alihisi jinsi gani wakati watu wake wasio na msimamo walipomwasi? Mstari wa 40 unasema: ‘Walimhuzunisha.’ Tafsiri nyingine ya Biblia inasema “walimfanya kuwa na sababu ya kuhuzunika.” Kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinaeleza: “Maana tunayopata hapa ni kuwa mwenendo wa Waebrania ulisababisha maumivu—sawa tu na vile mwenendo wa mtoto asiyetii na mwenye kuasi unavyosababisha maumivu kwa mzazi.” Kama vile mtoto mtundu anavyoweza kuwafanya wazazi wake waumie moyoni, ndivyo Waisraeli waasi ‘walivyomtia uchungu Mtakatifu wa Israeli.’—Mstari wa 41.

Tunaweza kujifunza nini kutokana na zaburi hii? Ni jambo lenye kutia moyo kuona kuwa Yehova ana uhusiano wa karibu na waabudu wake na havunji uhusiano huo haraka. Wakati uleule, inafariji kujua kwamba Yehova ana hisia na kuwa mwenendo wetu unaweza kuathiri hisia zake. Kujua mambo hayo kuna matokeo gani kwako? Je, kunakuchochea utake kufanya mema?

Badala ya kutenda dhambi na kumfanya Yehova aumie moyoni, tunaweza kuchagua kufuata njia inayofaa na kuufurahisha moyo wake. Na hilo ndilo hasa analotaka kutoka kwa waabudu wake: “Uwe na hekima, mwanangu, na kuufanya moyo wangu ushangilie.” (Methali 27:11) Hakuna jambo lingine lenye thamani zaidi tunaloweza kumpa Yehova kuliko kuishi maisha yanayofurahisha moyo wake.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Julai (Mwezi wa 7):

Zaburi 60-86

[Blabu katika ukurasa wa 10]

Hakuna jambo lingine lenye thamani tunaloweza kumpa Yehova kuliko kuishi maisha yanayofurahisha moyo wake