Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

“Mazao Saba” ya ile Nchi Nzuri

“Mazao Saba” ya ile Nchi Nzuri

“Mazao Saba” ya ile Nchi Nzuri

KATIKA Biblia, Israeli inatajwa kuwa nchi yenye milima na mabonde, maeneo tambarare ya pwani na nyanda za juu, mito na mabubujiko ya maji. Ikiwa na aina mbalimbali za udongo na hali ya hewa tofauti-tofauti, kutia ndani majangwa upande wa kusini na milima yenye theluji upande wa kaskazini, nchi hiyo ilitokeza mazao ya aina mbalimbali. Wakati Musa alipozungumza na Waisraeli ili kuchochea hamu yao kuhusu ile “nchi nzuri” ambayo wangemiliki, aliifafanua kuwa “nchi ya ngano na shayiri na mizabibu na tini na makomamanga, nchi ya mizeituni ya mafuta na asali,” akitaja mazao saba hususa yaliyokuzwa katika nchi hiyo.—Kumbukumbu la Torati 8:7, 8.

Hata leo, usemi “mazao saba” bado unatumiwa kuelezea mazao ya nchi hiyo. Pindi kwa pindi, mazao hayo yameonekana kwenye sarafu na stempu ili kuonyesha kwamba nchi hiyo ina rutuba. Mazao hayo yalikuzwa jinsi gani nyakati za Biblia? Yalihusiana jinsi gani na maisha ya watu? Acheni tuone.

“Ngano na Shayiri” Ingawa ngano na shayiri zilipandwa mwishoni mwa mwaka, shayiri ilikomaa mwezi mmoja kabla ya ngano. Mganda wa mazao ya kwanza ya shayiri ulipelekwa kwenye hekalu kama toleo kwa Yehova wakati wa Sherehe ya Mkate Usiotiwa Chachu, mwezi wa Machi (Mwezi wa 3) au Aprili (Mwezi wa 4). Nalo toleo la mikate ya ngano lilitolewa wakati wa Sherehe ya Majuma, au Pentekoste, mwezi wa Mei (Mwezi wa 5).—Mambo ya Walawi 23:10, 11, 15-17.

Kwa karne nyingi, na hata hivi karibuni, wakulima nchini Israel walipanda mbegu za nafaka yao kwa kuzitawanya kwa mkono kutoka kwenye mkunjo wa vazi lao. Mbegu za shayiri zilitawanywa tu juu ya udongo, lakini za ngano zilihitaji kufunikwa kwa udongo. Ili kuzifunika, wakulima walitumia ng’ombe wa kuvuta mizigo kukanyanga-kanyanga eneo lenye mbegu hizo au kulilima tena.

Mara nyingi Biblia inazungumzia kupanda, kuvuna, kupura, kupepeta, na kusaga nafaka. Nguvu nyingi zilitumiwa kufanya kazi hizo zote. Kila siku, nafaka iliyovunwa ilisagiwa nyumbani na kuwa unga, kisha kutumiwa kuoka mikate kwa ajili ya familia. Jambo hilo linatusaidia kuelewa agizo la Yesu kwamba tusali kwa ajili ya “mkate wetu wa kila siku.” (Mathayo 6:11, Biblia Takatifu) Nyakati za Biblia, chakula cha kawaida kilikuwa mkate uliookwa kwa unga wa nafaka nzima ya ngano au shayiri.—Isaya 55:10.

“Mizabibu na Tini na Makomamanga” Baada ya kuwaongoza watu wake nyikani kwa miaka 40, Musa aliwachochea wawe na hamu ya jambo fulani, yaani, kula mazao ya Nchi ya Ahadi. Miaka 40 mapema, wapelelezi walikuwa wamewaletea Waisraeli waliokuwa wamepiga kambi nyikani mazao gani ili kuthibitisha kwamba Nchi ya Ahadi ilikuwa yenye rutuba? “Chipukizi lenye kishada kimoja cha zabibu” lililokuwa zito sana hivi kwamba ilibidi ‘wawili kati ya wanaume hao walichukue kwa ufito.’ Pia, walileta tini na makomamanga. Hivyo vilikuwa vitu vyenye kutamanika kama nini kwa wasafiri hao wa jangwani! Huo ulikuwa mwonjo tu wa mambo mazuri ambayo wangekuja kufurahia!—Hesabu 13:20, 23.

Ili mizabibu iendelee kuzaa kwa wingi ilihitaji kutunzwa sana—ilihitaji kumwagiliwa maji, kupunguzwa matawi, na kuvunwa. Shamba la mizabibu lililotunzwa vizuri lilikuwa na matuta yaliyotengenezwa vizuri, lilizingirwa kwa ukuta, na lilikuwa na kibanda cha mlinzi. Waisraeli walijua vizuri kazi waliyopaswa kufanya kwenye shamba la mizabibu na pia walifahamu matokeo ya kutolitunza vizuri.—Isaya 5:1-7.

Wakati wa kuvuna zabibu, divai ilianza kutengenezwa. Vishada vya zabibu vilikanyangwa-kanyangwa katika mtungi au kufinywa ndani ya shinikizo la divai. Umajimaji uliotoka ulichemshwa ili kupata sukari au kuachwa uchachuke na kuwa divai. Nchi ya Israeli ilikuwa na hali nzuri ya hewa na udongo mzuri kwa ukuzi wa zabibu na utengenezaji wa divai. *

Huenda watu wanaoishi mbali na maeneo ambako tini zinakuzwa wameona tu tini zilizokaushwa au kushinikizwa. Tini ambazo zimetoka tu kuchunwa zinaonekana kuwa tofauti kabisa na zile zilizokaushwa au kushinikizwa—ni tamu na zenye umajimaji mwingi. Ili kuzihifadhi baada ya kile kipindi kifupi cha uvunaji, lazima tini zikaushwe kwa jua na kutiwa ndani ya pakiti. ‘Keki za tini zilizoshinikizwa’ zimetajwa mara nyingi katika Biblia.—1 Samweli 25:18.

Unapotoa ganda gumu la komamanga lililoiva, unapata mamia ya “matunda madogo,” yaliyo tayari kuliwa au kutengeneza maji matamu, yenye kuburudisha na mazuri kwa afya. Makomamanga yalithaminiwa sana hivi kwamba pindi moja maumbo yake yalishonwa kwenye pindo za mavazi ya kuhani mkuu na pia kuchorwa kwenye nguzo za hekalu la Sulemani kama mapambo.—Kutoka 39:24; 1 Wafalme 7:20.

‘Zeituni na Asali’ Tafsiri fulani za Biblia zinataja mzeituni au matunda yake karibu mara 60, na zeituni zilikuwa chanzo muhimu cha chakula na mafuta. Mashamba ya mizeituni bado yanapatikana katika sehemu nyingi nchini Israel. (Kumbukumbu la Torati 28:40) Hata leo, kazi ya kuvuna zeituni Oktoba (Mwezi wa 10), inafanywa na familia nzima katika jamii nyingi. Wavunaji wanapigapiga matawi ya mizeituni ili kutikisa na kuangusha zeituni, kisha kuzikusanya. Zeituni hizo zinahifadhiwa na kutumiwa kama chakula cha familia kwa mwaka mzima au kupelekwa kwenye shinikizo la mafuta la jamii. Mamia ya mashinikizo mbalimbali ya kale yamechimbuliwa na waakiolojia katika maeneo tofauti-tofauti. Leo, inapendeza kuona mafuta ya zeituni yenye rangi hafifu ya kijani-kibichi yakitiwa ndani ya chupa kwa ajili ya matumizi ya nyumbani ya mwaka mzima au kuuzwa. Mafuta ya zeituni yalitumiwa kupikia, kujipodoa, na pia kama mafuta-taa.

Asali ambayo Musa alitaja inaweza kuwa ama asali inayotengenezwa na nyuki au umajimaji mtamu unaotengenezwa kutokana na tende na zabibu. Asali inayotengenezwa kutokana na matunda hayo bado inatumiwa kama sukari. Lakini asali inayotajwa katika masimulizi ya Biblia kuhusu Samsoni na Yonathani, ni asali ya nyuki iliyotolewa kwenye masega. (Waamuzi 14:8, 9; 1 Samweli 14:27) Uvumbuzi wa hivi karibuni wa mizinga ya nyuki zaidi ya 30 huko Tel Rehov, kaskazini mwa Israel, unaonyesha kwamba Waisraeli walikuwa wakifuga nyuki hata siku za Sulemani.

Leo, yeyote anayetembelea soko lenye kuvutia nchini Israel—lenye maduka ya kuokea mikate na vibanda vya matunda na mboga—ataona kwamba bidhaa mbalimbali zinazotokana na yale “mazao saba” zinapatikana kwa wingi. Bila shaka, mazao hayo saba ni baadhi tu ya mazao mengi sana yanayokuzwa katika nchi hiyo. Njia za kisasa za kilimo zimewawezesha wakulima kukuza mimea kutoka nchi nyingine. Kupatikana kwa wingi kwa mazao hayo ni jambo linaloonyesha wazi kwamba eneo hilo dogo linafaa kuitwa “nchi nzuri.”—Hesabu 14:7.

[Maelezo ya Chini]

^ Zabibu pia zilikaushwa na kuwa zabibu kavu.—2 Samweli 6:19.

[Picha katika ukurasa wa 11]

Ngano

[Picha katika ukurasa wa 11]

Shayiri

[Picha katika ukurasa wa 12]

Zabibu

[Picha katika ukurasa wa 12, 13]

Tini

[Picha katika ukurasa wa 12]

Makomamanga

[Picha katika ukurasa wa 13]

Zeituni

[Picha katika ukurasa wa 13]

Asali