Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unaweza Kumkaribia Mungu Jinsi Gani?

Unaweza Kumkaribia Mungu Jinsi Gani?

Jifunze Kutoka Katika Neno La Mungu

Unaweza Kumkaribia Mungu Jinsi Gani?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Je, Mungu anasikiliza sala zote?

Yehova anawakaribisha watu wa mataifa yote wamkaribie katika sala. (Zaburi 65:2) Lakini hasikilizi sala zote. Kwa mfano, Waisraeli walipokataa kuacha matendo maovu, Mungu alikataa kusikiliza sala zao. (Isaya 1:15) Pia, sala za mwanamume anayemtendea vibaya mke wake zinaweza kuzuiwa. (1 Petro 3:7) Hata hivyo, Mungu atawasikiliza watu wanaotenda dhambi nzito ikiwa watatubu.—Soma 2 Mambo ya Nyakati 33:9-13.

2. Tunapaswa kusali jinsi gani?

Sala ni pendeleo na sehemu ya ibada yetu, kwa hiyo tunapaswa kusali tu kwa Yehova. (Mathayo 4:10; 6:9) Kwa kuwa sisi si wakamilifu, tunapaswa kusali katika jina la Yesu kwa sababu yeye ndiye amechaguliwa kuwa “njia.” (Yohana 14:6) Yehova hataki turudie-rudie sala ambazo tumekariri au zilizoandikwa, lakini anataka tusali kutoka moyoni.—Soma Mathayo 6:7; Wafilipi 4:6, 7.

Muumba wetu hata anaweza kusikia sala zinazotolewa kimya-kimya. (1 Samweli 1:12, 13) Anataka tusali kila pindi, kama vile asubuhi na jioni, wakati wa chakula, na tunapopatwa na matatizo.—Soma Zaburi 55:22; Mathayo 15:36.

3. Kwa nini Wakristo wanakutana pamoja?

Si rahisi kumkaribia Mungu kwa sababu tunaishi kati ya watu wasiomwamini Mungu na wanaodhihaki ahadi yake ya kuleta amani duniani. (2 Timotheo 3:1, 4; 2 Petro 3:3, 13) Kwa hiyo, tunahitaji kuwa na ushirika wenye kujenga pamoja na waamini wenzetu.—Soma Waebrania 10:24, 25.

Unaweza kumkaribia Mungu ikiwa utafanya urafiki na watu wanaompenda. Mikutano ya Mashahidi wa Yehova inatoa fursa za kufaidika na imani ya wengine.—Soma Waroma 1:11, 12.

4. Unaweza kumkaribia Mungu jinsi gani?

Unaweza kumkaribia Yehova kwa kutafakari mambo ambayo umejifunza katika Neno lake. Tafakari juu ya matendo yake, miongozo yake, na ahadi zake. Kutafakari na kusali kutakusaidia kuthamini kikweli upendo na hekima ya Mungu.—Soma Yoshua 1:8; Zaburi 1:1-3.

Unaweza kumkaribia Mungu ikiwa tu utamtegemea na kumwamini. Lakini imani ni kama kitu kilicho hai ambacho kinahitaji kutunzwa. Ni lazima uendelee kuitia imani yako nguvu kwa kutafakari mambo ambayo umejifunza.—Soma 1 Wathesalonike 5:21; Waebrania 11:1, 6.

5. Utafaidika jinsi gani kwa kumkaribia Mungu?

Yehova anawajali wale wanaompenda. Anawalinda na chochote kinachoweza kuhatarisha imani yao na tumaini lao la uzima wa milele. (Zaburi 91:1, 2, 7-10) Anatuonya ili tusifuate njia ya maisha inayoweza kufanya tuwe wagonjwa au tukose furaha. Yehova anatufundisha njia iliyo bora zaidi ya maisha.—Soma Zaburi 73:27, 28; Yakobo 4:4, 8.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 17 ya kitabu hiki,Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.