Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

Biblia Inabadili Maisha

NI NINI kilichomsukuma msichana fulani aanze tena kufuata kanuni za Biblia alizokuwa amefundishwa tangu utotoni? Soma yale anayosema.

“Sasa Nina Kusudi la Kweli Maishani.”​—LISA ANDRÉ

MWAKA WA KUZALIWA: 1986

NCHI: LUXEMBOURG

HISTORIA: MTOTO MPOTEVU

MAISHA YANGU YA ZAMANI: Nililelewa Bertrange, mji mdogo, safi, na wenye ufanisi ulio karibu na jiji la Luxembourg. Mimi ndiye mtoto wa mwisho katika familia ya watoto watano. Wazazi wangu ni Mashahidi wa Yehova, na walijitahidi sana kutufundisha sote kufuata kanuni za Kikristo.

Mwanzoni mwa miaka yangu ya utineja, nilianza kuwa na mashaka sana kuhusu mafundisho ya Mashahidi wa Yehova. Kwanza, nilipuuza mashaka hayo, lakini pole kwa pole imani yangu ikadhoofika. Wazazi wangu walifanya kila walichoweza ili kuniongoza katika njia inayofaa, lakini nikakataa msaada wao. Bila wao kujua, nilishirikiana na vijana ambao hawakuheshimu mamlaka. Nilitamani uhuru ambao walionekana kuwa nao. Tulikuwa na sherehe nyingi, tukafanya ngono kiholela, tukatumia dawa za kulevya, na kunywa pombe kupita kiasi. Mwanzoni, nilifurahia kushirikiana na watu walioonekana kufurahia maisha kikamili.

Hata hivyo, sikuwa na furaha ya kweli. Maisha yangu hayakuwa na kusudi nilipokuwa nikishirikiana na vijana hao; hawakujali chochote. Ingawa hivyo, nilisumbuliwa na mambo kama vile kuenea kwa ukosefu wa haki duniani. Kadiri muda ulivyopita, ndivyo nilivyozidi kuvunjika moyo.

JINSI BIBLIA ILIVYOBADILI MAISHA YANGU: Siku moja, nikiwa na umri wa miaka 17, nilihisi nimevunjika moyo sana. Mama yangu alipotambua kwamba sikuwa na furaha, alinisihi nianze kujifunza Biblia tena. Alinitia moyo nichunguze mafundisho ya Biblia, kisha nijiamulie ikiwa ninataka kuishi kupatana na mafundisho hayo au hapana. Mazungumzo hayo yenye kugusa moyo yalinichochea kufanya mabadiliko. Nilikubali kujifunza Biblia pamoja na dada yangu mkubwa Caroline na mume wake, Akif. Mume wake hakulelewa katika familia ya Mashahidi wa Yehova, bali alijifunza Biblia akiwa mtu mzima. Kwa sababu ya mambo ambayo Akif alipitia zamani, nilihisi kwamba ningeweza kuongea naye waziwazi, jambo lililokuwa muhimu sana kwangu.

Nilijua kwamba Shahidi hakupaswa kuishi kama nilivyoishi, lakini mwanzoni, nilihisi kwamba nilipaswa kujiamulia kile nilichotaka kufanya maishani. Hata hivyo, kwa kujifunza Biblia nilitambua kuwa mwenendo wangu unaweza kumfurahisha Yehova au kumhuzunisha. (Zaburi 78:40, 41; Methali 27:11) Vilevile, baadaye nilielewa kwamba mwenendo wangu uliathiri watu wengine pia.

Nilipoendelea kujifunza Biblia, nilitambua kwamba kuna sababu zinazopatana na akili na zenye kusadikisha kuwa Biblia ni Neno la Mungu. Kwa mfano, nilijifunza kuhusu unabii mwingi sana wa Biblia ambao umetimia kwa usahihi kabisa. Ujuzi huo ulinisaidia kuondoa mashaka niliyokuwa nayo mwanzoni.

Mwaka mmoja hivi baada ya kuanza kujifunza Biblia, mimi na wazazi wangu tulimtembelea ndugu yangu mkubwa aliyekuwa amejitolea kufanya kazi katika ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova nchini Ujerumani. Nilipoona jinsi ndugu yangu alivyokuwa mwenye furaha, niliguswa moyo sana. Hiyo ndiyo furaha niliyokuwa nikitafuta! Pia, nilivutiwa sana na Mashahidi wengine waliokuwa wamejitolea kufanya kazi huko. Walikuwa tofauti kabisa na watu wasio waaminifu na waliotafuta raha ambao nilishirikiana nao mwanzoni. Muda mfupi baadaye, nilisali kwa Yehova kutoka moyoni na kumwahidi kwamba nitamtumikia katika maisha yangu yote. Nilibatizwa nikiwa na umri wa miaka 19, na hivyo kuonyesha kwamba nimejiweka wakfu ili kumtumikia Yehova.

JINSI AMBAVYO NIMEFAIDIKA: Sasa nina kusudi la kweli maishani. Ninapata furaha ninapowafundisha wengine Biblia na kuwasaidia wajifunze kumhusu Yehova na ahadi zake za wakati ujao. Familia yangu pia imefaidika—hawana wasiwasi juu yangu.

Ninatambua makosa niliyofanya zamani, lakini ninajitahidi kutoyafikiria. Badala yake, ninakazia fikira msamaha wa Yehova na jinsi anavyonijali na kunipenda. Ninakubaliana kwa moyo wote na maneno ya andiko la Methali 10:22 linalosema: “Baraka ya Yehova—hiyo ndiyo hutajirisha, naye haongezi maumivu pamoja nayo.”

[Blabu katika ukurasa wa 12]

“Tulikuwa na sherehe nyingi, tukafanya ngono kiholela, tukatumia dawa za kulevya, na kunywa pombe kupita kiasi”

[Blabu katika ukurasa wa 13]

“Ninatambua makosa niliyofanya zamani, lakini ninajitahidi kutoyafikiria”