Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unaweza “Kumjua Mungu”

Unaweza “Kumjua Mungu”

Mkaribie Mungu

Unaweza “Kumjua Mungu”

YEHOVA MUNGU amefanya hazina yenye thamani iweze kupatikana na anataka tuipate. Hazina hiyo haituletei utajiri wa kimwili, lakini inatuwezesha kupata kitu ambacho pesa zote duniani haziwezi kununua—amani ya akili na maisha yenye kuridhisha. Hazina hiyo ni nini? Maneno ya Mfalme Sulemani mwenye hekima yaliyoandikwa katika Methali 2:1-6 yanaeleza.

Sulemani anasema kwamba hazina hiyo ni “kumjua Mungu,” yaani, kujua ukweli kumhusu Mungu na makusudi yake kama yanavyofunuliwa katika Biblia. (Mstari wa 5) Hazina hiyo ina sehemu kadhaa.

Mafundisho ya kweli. Biblia inajibu maswali kama haya: Jina la Mungu ni nani? (Zaburi 83:18) Ni nini kinachotupata tunapokufa? (Zaburi 146:3, 4) Kwa nini tuliumbwa? (Mwanzo 1:26-28; Zaburi 115:16) Bila shaka, ni muhimu sana kujua majibu ya maswali hayo.

Mashauri yenye hekima. Biblia inatueleza njia bora ya maisha. Unaweza kufanya nini ili ndoa yako idumu? (Waefeso 5:28, 29, 33) Unawezaje kuwafundisha watoto wako kutimiza majukumu yao? (Kumbukumbu la Torati 6:5-7; Waefeso 6:4) Unawezaje kupata furaha maishani? (Mathayo 5:3; Luka 11:28) Bila shaka, mashauri yenye kutegemeka kuhusu mambo hayo yana thamani kwelikweli.

Ukweli kuhusu sifa na utu wa Mungu. Biblia ndiyo chanzo kikuu cha habari za kweli kumhusu Mungu. Ana sifa gani? (Yohana 1:18; 4:24) Je, anatujali? (1 Petro 5:6, 7) Baadhi ya sifa zake kuu ni gani? (Kutoka 34:6, 7; 1 Yohana 4:8) Ni wazi kwamba habari za kweli kumhusu Muumba wetu zina thamani kubwa sana.

Bila shaka, “kumjua Mungu” ni hazina ya kiroho. Unaweza kuipata jinsi gani? Kuna dokezo kwenye mstari wa 4 wa Methali sura ya 2, ambapo Sulemani analinganisha ujuzi na “hazina zilizofichika.” Fikiria hili: Hazina iliyofichika haiwezi kujitokeza tu na kuanguka mikononi mwa mtu asiyefanya lolote. Tunapaswa kujitahidi ili kuipata. Ndivyo ilivyo na kumjua Mungu. Hazina hiyo imefichwa ndani ya Biblia. Ili tuipate tunapaswa kujitahidi.

Sulemani anaeleza kile tunachohitaji kufanya ili “tumjue Mungu.” Maneno, “pokea maneno yangu” na ‘elekeza moyo wako’ yanaonyesha kwamba tunahitaji kuwa na moyo msikivu. (Mstari wa 1, 2) Maneno, ‘kuita’ na ‘kuendelea kutafuta’ yanaonyesha kwamba tunahitaji kuchukua hatua na kutenda kwa bidii. (Mstari wa 3, 4) Hivyo, ili tupate hazina hiyo, tunahitaji kusoma Biblia kwa bidii, na kufanya hivyo kwa moyo mnyofu.—Luka 8:15.

Ikiwa tutachukua hatua na kutenda kwa bidii, Yehova atatusaidia kupata hazina hiyo. vMstari wa 6 unasema: “Yehova mwenyewe anatoa hekima.” Tunaweza kuelewa kweli zinazopatikana katika Biblia kupitia tu msaada wa Mungu. (Yohana 6:44; Matendo 16:14) Unaweza kuwa na uhakika huu: Ukichunguza Neno la Mungu kwa unyofu, utapata “kumjua Mungu”—hazina ambayo itaboresha maisha yako kwa kiwango kikubwa sana.—Methali 2:10-21. *

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa mwezi wa Oktoba:

Methali 1-21

[Maelezo ya Chini]

^ Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote wanajifunza Biblia bila malipo pamoja na wale wanaotaka kuielewa. Tunakutia moyo uwasiliane nao katika eneo lenu au uwaandikie barua ukitumia mojawapo ya anwani zilizo kwenye ukurasa wa 4.