Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Wakati Tunapopaswa Kukaa Macho

Wakati Tunapopaswa Kukaa Macho

Wafundishe Watoto Wako

Wakati Tunapopaswa Kukaa Macho

HUENDA unakubali kwamba ni muhimu kukaa macho unapokuwa shuleni. Wengi husinzia wanapokuwa darasani, lakini ni lazima ukae macho ili ujifunze. Labda pia unaenda mikutanoni ambapo unajifunza Biblia.

Unafikiri unaweza kufanya nini ili uweze kukaa macho? * Jambo moja ni kulala mapema. Labda kulala kwa muda mfupi alasiri kutasaidia pia. Acha tuone yale tunayoweza kujifunza kutokana na yaliyompata kijana mmoja ambaye alilala usingizi katikati ya usiku wakati mtume Paulo alipokuwa akitoa hotuba. Soma katika Biblia Matendo sura ya 20, mstari wa 7 mpaka 12, uone kilichotokea.

Paulo alikuwa ametembelea kutaniko lililokuwa katika jiji lenye bandari la Troa. Biblia inasema kwamba Paulo ‘alipaswa kuondoka siku iliyofuata’ kwa mashua. Kwa hiyo, “akarefusha hotuba yake mpaka katikati ya usiku.” Tunasoma hivi: “Kijana fulani anayeitwa Eutiko, aliyekuwa ameketi dirishani, akalala usingizi mzito huku Paulo akiendelea kuongea.” Ni nini kilichotokea?

Eutiko alianguka “chini kutoka ghorofa ya tatu.” Paulo na wengine waliteremka haraka iwezekanavyo kutoka ghorofani. Eutiko alikuwa chini—amekufa! Unaweza kuwazia huzuni iliyowapata wote?— Biblia inasema Paulo alimchukua Eutiko mikononi mwake na kumkumbatia. Kisha, Paulo akasema hivi kwa furaha: ‘Msiwe na wasiwasi, yuko salama!’ Mungu alikuwa amemfufua Eutiko!

Tunaweza kujifunza nini kumhusu Mungu kutokana na yale yaliyompata Eutiko? Jambo moja ni kwamba Yehova, Baba yetu wa mbinguni, anaweza kuwafufua wafu, kutia ndani watoto. Yehova anakuelewa na anakupenda, ndiyo, hata anakupenda zaidi ya vile wazazi wako wanavyokupenda. Yesu alipokuwa duniani, alionyesha jinsi Baba yake alivyo kwa kuwachukua watoto wadogo mikononi mwake na kuwabariki. Pia, aliwafufua watoto, kutia ndani msichana mwenye umri wa miaka 12.

Unahisi namna gani unapojua kwamba Baba yako wa mbinguni anakupenda?— Jambo hilo linafanya tumpende Yehova pia na kutaka kufanya anayosema. Je, unajua jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunampenda?— Njia moja ni kusema kwamba tunampenda. Yesu alisema: “Ninampenda Baba.” Lakini Yesu alifanya mengi zaidi ya kusema tu kwamba anampenda Mungu. Alionyesha jambo hilo kwa matendo.

Yesu alimtii Mungu. “Sikuzote mimi hufanya mambo yanayompendeza,” Yesu akasema. Tukifanya hivyo, tutajitahidi tunavyoweza kukaa macho shuleni na mikutanoni ili kumpendeza Yehova na Mwana wake Yesu.

Soma katika Biblia Yako

Matendo 20:7-12

Luka 8:49-56

Yohana 8:29; 14:31

[Maelezo ya Chini]

^ Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.