Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kutimiza Wajibu Wetu Mbele za Mungu

Kutimiza Wajibu Wetu Mbele za Mungu

Mkaribie Mungu

Kutimiza Wajibu Wetu Mbele za Mungu

JE, UMEWAHI kujiuliza, ‘Ni nini kusudi la uhai?’ Yehova hakutuumba tu tukiwa na uwezo wa kuuliza swali kama hilo, bali pia tukiwa na uhitaji mkubwa wa kupata jibu. Kwa kupendeza, Mungu wetu mwenye upendo amefanya iwezekane kupata jibu. Jibu tunalotamani kupata liko katika Neno lake, Biblia. Fikiria maneno ya Mfalme Sulemani katika Mhubiri 12:13.

Sulemani alikuwa katika hali ya pekee sana. Angeweza kusema jinsi ya kupata furaha na kusudi maishani. Akiwa amebarikiwa na hekima isiyo na kifani, utajiri mwingi sana, na mamlaka ya kifalme, alichunguza kwa makini utendaji wa wanadamu, kutia ndani jitihada za kupata utajiri na umashuhuri. (Mhubiri 2:4-9; 4:4) Kisha, akiongozwa na roho ya Mungu alimalizia uchunguzi wake kwa kusema hivi: “Huu ndio mwisho wa mambo, kila jambo limekwisha sikiwa: Mwogope Mungu wa kweli na kushika amri zake. Kwa maana huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.” Maneno hayo yanaonyesha jambo lenye kunufaisha na la pekee zaidi ambalo wanadamu wanapaswa kufuatia.

“Mwogope Mungu wa kweli.” Huenda wazo la kumwogopa Mungu lisipendeze mwanzoni. Lakini woga huo ni mtazamo unaofaa wa moyoni. Tunaweza kuwazia si kuhusu mtumwa anayetetemeshwa na bwana-mkubwa aliye mkali, bali kuhusu mtoto ambaye anajitahidi kumpendeza baba mwenye upendo. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba kumwogopa Mungu ni “mtazamo wenye heshima na woga ambao watu Wake wanamwonyesha kwa sababu Wanampenda na kuheshimu nguvu na ukuu Wake.” Mtazamo kama huo unatuchochea kujitiisha na kufanya mapenzi ya Mungu kwa sababu tunampenda na tunajua kwamba anatupenda. Woga huo unaofaa si hisia tu; unaonyeshwa kwa matendo. Jinsi gani?

‘Shika amri zake.’ Kumwogopa Mungu hutuchochea tumtii. Ni jambo linalopatana na akili kumtii Yehova. Akiwa Muumba wetu, anajua njia bora zaidi ambayo tunapaswa kuishi, kama vile tu mtengenezaji wa bidhaa anavyojua njia iliyo bora ya kutumia bidhaa zake. Isitoshe, Yehova angependa tufanikiwe maishani. Anataka tuwe na furaha, na matakwa yake yamekusudiwa kutusaidia tuwe na hali nzuri. (Isaya 48:17) Mtume Yohana anasema hivi kuhusu jambo hilo: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.” (1 Yohana 5:3) Utii wetu unaonyesha kwamba tunampenda Mungu, nazo amri zake zinaonyesha upendo wake kutuelekea.

“Huo ndio wajibu wote wa mwanadamu.” Maneno hayo yanakazia sababu muhimu ya kumwogopa Mungu na kumtii. Ni wajibu wetu kufanya hivyo. Yehova ndiye Muumba wetu, kwa hiyo yeye ndiye chanzo cha uhai wetu. (Zaburi 36:9) Pia, tuna wajibu wa kumtii. Kwa kuishi kulingana na vile anavyotaka tuishi, tunatimiza wajibu wetu.

Hivyo basi, kusudi la uhai ni nini? Kwa ufupi, hili ndilo kusudi: Tuko hai ili tufanye mapenzi ya Mungu. Hakuna njia nyingine bora ya kufanya uhai wako uwe na kusudi. Tunakutia moyo ujifunze mengi zaidi kuhusu mapenzi ya Yehova na jinsi unavyoweza kupatanisha maisha yako na mapenzi hayo. Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia.

Usomaji wa Biblia unaopendekezwa kwa Mwezi wa Novemba:

Methali 22–31; Mhubiri 1-12; Wimbo wa Sulemani 1-8