Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Tunafaidikaje kwa Kufuata Sheria za Mungu?

Tunafaidikaje kwa Kufuata Sheria za Mungu?

Jifunze Kutoka Katika Neno la Mungu

Tunafaidikaje kwa Kufuata Sheria za Mungu?

Makala hii inazungumzia maswali ambayo huenda umejiuliza na inakuonyesha mahali unapoweza kupata majibu katika Biblia yako. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuzungumzia majibu hayo pamoja nawe.

1. Kwa nini tunapaswa kumtii Mungu?

Tunapaswa kumtii Mungu kwa sababu alituumba. Hata Yesu alimtii Mungu sikuzote. (Yohana 6:38; Ufunuo 4:11) Sheria za Mungu zinatupa fursa ya kuthibitisha kwamba tunampenda.—Soma 1 Yohana 5:3.

Sheria zote za Yehova Mungu zinatufaidi. Zinatufundisha jinsi ya kuishi maisha bora sasa na kutuonyesha jinsi tunavyoweza kupata baraka za milele wakati ujao.—Soma Zaburi 19:7, 11; Isaya 48:17, 18.

2. Sheria za Mungu zinatufaidije kiafya?

Sheria ya Mungu inayokataza ulevi inatulinda kutokana na magonjwa hatari na aksidenti. Kunywa kupita kiasi kunaweza kufanya mtu awe mraibu wa pombe na kutenda kipumbavu. (Methali 23:20, 29, 30) Yehova anaturuhusu tunywe pombe lakini kwa kiasi.—Soma Zaburi 104:15; 1 Wakorintho 6:10.

Yehova anatushauri pia tusiwe na wivu, hasira isiyothibitiwa, na mitazamo mingine yenye madhara. Tukijitahidi kufuata mashauri hayo, tutafaidika kiafya.—Soma Methali 14:30; 22:24, 25.

3. Sheria ya Mungu inaweza kutulindaje?

Sheria ya Mungu inakataza watu wasifanye ngono nje ya ndoa. (Waebrania 13:4) Wenzi wa ndoa wanaofuata sheria hiyo wanahisi wakiwa salama zaidi na wanawaandalia watoto wao mazingira mazuri zaidi wanapokua. Kwa upande mwingine, mara nyingi kufanya ngono nje ya ndoa kunaleta magonjwa, talaka, jeuri, matatizo ya kihisia, na familia zenye mzazi mmoja.—Soma Methali 5:1-9.

Tukiepuka hali zinazoweza kufanya tushawishike kufanya ngono nje ya ndoa, tutalinda urafiki wetu pamoja na Mungu. Vilevile tutaepuka kuwaumiza wengine.—Soma 1 Wathesalonike 4:3-6.

4. Kuheshimu uhai kunatufaidije?

Watu wanaoheshimu zawadi ya uhai ambayo Mungu ametupatia, wanafaidika kiafya wanapoacha tabia kama vile kuvuta sigara na mazoea mengine yanayohatarisha uhai. (2 Wakorintho 7:1) Mungu anathamini hata uhai wa mtoto anayekua ndani ya tumbo la uzazi. (Kutoka 21:22, 23) Hivyo, hatupaswi kuua kimakusudi mtoto ambaye hajazaliwa. Pia, wale wanaothamini maoni ya Mungu kuhusu uhai wanafuata kanuni za usalama kazini, nyumbani, na wakiwa kwenye magari. (Kumbukumbu la Torati 22:8) Isitoshe, hawahatarishi uhai wao katika michezo, kwa sababu uhai ni zawadi kutoka kwa Mungu.—Soma Zaburi 36:9.

5. Tunafaidikaje kwa kuiona damu kuwa takatifu?

Damu ni takatifu kwa sababu Mungu anasema kwamba inawakilisha uhai, au nafsi, ya kiumbe. (Mwanzo 9:3, 4) Sheria ya Mungu inayoonyesha kwamba thamani ya damu inalingana na thamani ya uhai, inatufaidi. Jinsi gani? Kwa msingi wa Sheria hiyo tunaweza kusamehewa dhambi zetu.—Soma Walawi 17:11-13; Waebrania 9:22.

Damu ya Yesu ilikuwa na thamani hasa kwa sababu alikuwa mkamilifu. Yesu alimtolea Mungu kile kilichowakilisha uhai wake, yaani, damu yake. (Waebrania 9:12) Damu yake iliyomwagwa inatuwezesha kupata uzima wa milele.—Soma Mathayo 26:28; Yohana 3:16.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 12 na ya 13 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.