Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kuchunguza Rangi na Vitambaa Nyakati za Biblia

Kuchunguza Rangi na Vitambaa Nyakati za Biblia

Kuchunguza Rangi na Vitambaa Nyakati za Biblia

BIBLIA inataja mambo mengi kuhusu mitindo, rangi, na aina ya vitambaa vilivyotumiwa kushona mavazi ya watu walioishi karne nyingi zilizopita.

Bila shaka, Biblia si kitabu cha mitindo ya mavazi. Hata hivyo, maelezo kama hayo yanayotolewa katika masimulizi ya Biblia yanaweza kumsaidia msomaji apige picha akilini anapoyasoma.

Kwa mfano, tunasoma kuhusu vazi ambalo Adamu na Hawa walijaribu kutengeneza ili kufunika uchi wao—vazi lililoshonwa kwa majani ya mtini ambalo lilifunika sehemu ya chini ya kiuno. Hata hivyo, baadaye walivaa “mavazi marefu ya ngozi” yenye kudumu zaidi ambayo Mungu aliwapa.—Mwanzo 3:7, 21.

Pia, tuna masimulizi yenye habari za kutosha katika kitabu cha Kutoka sura ya 28 na 39 kuhusu mavazi yaliyovaliwa na kuhani mkuu wa Israeli. Mavazi hayo yalitia ndani vazi la ndani lililotengenezwa kwa kitani, kanzu nyeupe, ukumbuu uliosukwa, koti la bluu lisilo na mikono, na efodi iliyopambwa, kifuko cha kifuani, pamoja na kilemba na bamba la dhahabu lenye kung’aa. Kusoma tu kuhusu vitu vingi vyenye thamani vilivyotumiwa kutengeneza mavazi hayo kunatusaidia kupiga picha akilini jinsi mavazi hayo yalivyopendeza.—Kutoka 39:1-5, 22-29.

Mavazi ya nabii Eliya yalikuwa ya kipekee sana hivi kwamba watu walimtambua mara moja walipoelezwa jinsi alivyoonekana: “Mtu mwenye vazi la manyoya, na mshipi wa ngozi umefungwa kiunoni mwake.” Miaka mingi baadaye watu fulani walifikiri kwamba Yohana Mbatizaji alikuwa Eliya, labda kwa sababu mavazi yao yalifanana.—2 Wafalme 1:8; Mathayo 3:4; Yohana 1:21.

Vitambaa na Rangi Biblia inatoa marejeo mengi kuhusu aina ya vitambaa vilivyotumiwa, rangi na vitu vilivyotokeza rangi, pamoja na kusokota, kufuma, na kushona vitambaa hivyo. * Vitambaa vinavyotajwa sana vilitengenezwa kwa sufu ya wanyama wa kufugwa na kitani kilichotengenezwa kutokana na mmea wa kitani. Biblia inamwita Abeli “mchungaji wa kondoo.” (Mwanzo 4:2) Biblia haitaji ikiwa Abeli alifuga kondoo ili apate sufu. Mara ya kwanza Biblia inapotaja kitani ni wakati inaporejelea mavazi ambayo Farao alimvisha Yosefu katika karne ya 18 K.W.K. (Mwanzo 41:42) Biblia haisemi ikiwa Wayahudi walitumia pamba kutengeneza mavazi, lakini ilitumiwa nyakati za kale katika maeneo ya Mashariki ya Kati.

Kitani na sufu zilitokeza nyuzi-nyuzi bora ambazo zilisokotwa pamoja ili kutengeneza nyuzi zenye upana mbalimbali. Kisha nyuzi hizo zilifumwa ili kutokeza vipande vya vitambaa. Nyuzi na vitambaa vilivyofumwa vilitiwa rangi mbalimbali. Kisha kitambaa kingekatwa ili kimtoshee mtu aliyekusudiwa kukivaa. Mara nyingi mavazi hayo yalirembeshwa kwa kutiwa mapambo, kufumwa kwa nyuzi za rangi mbalimbali, na hivyo kufanya mavazi hayo yavutie na yawe ya bei ya juu.—Waamuzi 5:30.

Rangi ya bluu, zambarau, na nyekundu zinatajwa sana katika Biblia kuwa rangi zilizotumiwa kutia vitambaa rangi. Waisraeli waliamriwa waweke “uzi wa bluu juu ya upindo wenye nyuzinyuzi” wa nguo zao kama kikumbusho cha uhusiano wa pekee pamoja na Mungu wao Yehova. (Hesabu 15:38-40) Katika Kiebrania neno tekheʹleth linamaanisha rangi ya bluu, nalo ’ar·ga·manʹ, kwa kawaida hutafsiriwa “zambarau.” Hizo ndizo rangi zinazohusianishwa na mavazi ya kuhani mkuu na vitu vingine vilivyotumiwa kurembesha hema la kukutania na hekalu.

Vitambaa vya Hema la Kukutania na Hekalu Maskani, au hema la kukutania, huko jangwani—na baadaye hekalu huko Yerusalemu—lilikuwa kitovu cha ibada cha Waisraeli. Ndiyo sababu kuna maelezo mengi katika Biblia kuhusu kutayarishwa na kuwekwa kwa vifaa mbalimbali katika hema hilo la kukutania na hekalu la Sulemani. Mbali na vitambaa na rangi, tunapata maelezo kuhusu kufumwa, kutiwa rangi, kushonwa, na kupambwa kwa vifuniko na mapazia ya hema.

Chini ya mwongozo wa Mungu, mafundi wenye ustadi, Bezaleli na Oholiabu, pamoja na wanaume na wanawake wengine, walitimiza mgawo wao wa pekee kwa uaminifu, kwa kutengeneza hema la kukutania lililotumiwa kumwabudu Yehova. (Kutoka 35:30-35) Katika sura ya 26 ya kitabu cha Kutoka, Biblia inazungumzia kwa undani ujenzi wa sehemu mbalimbali za hema la kukutania na vifaa vilivyotumiwa. Kwa mfano, vitambaa vikubwa vya rangi mbalimbali vilifumwa kwa “kitani bora kilichosokotwa na uzi wa bluu na sufu iliyotiwa rangi ya zambarau na kitambaa chenye rangi nyekundu ya kochinili.” Inaelekea kwamba vingi kati ya vitambaa hivyo vilitolewa Misri wakati Waisraeli walipotoka huko. Pazia kubwa lililokuwa na rangi mbalimbali na lililopambwa kwa maumbo ya makerubi liligawanya “Patakatifu na Patakatifu Zaidi” katika sehemu ya ndani ya hema la kukutania. Pazia hilo lilikuwa limetengenezwa kwa uangalifu sana. (Kutoka 26:1, 31-33) Pia, maelezo kama hayo yalitolewa kwa wale waliokuwa wakitengeneza vitambaa vya hekalu la Yerusalemu, chini ya mwongozo wa Mfalme Sulemani.—2 Mambo ya Nyakati 2:1, 7.

Kutokana na habari zilizoandikwa katika Biblia, tunaweza kutambua kwamba Waebrania wa kale walikuwa na ubunifu na ustadi mwingi wa kutumia vifaa walivyokuwa navyo. Habari hizo zinatusaidia kutambua kwamba Waebrania hawakuvalia tu mavazi yasiyovutia na yasiyo na mapambo yoyote, bali walifurahia mitindo ya mavazi yenye rangi mbalimbali, ambayo wangevaa kwa ajili ya matukio tofauti-tofauti, kulingana na majira mbalimbali ya mwaka, na kulingana na uwezo wa mtu binafsi.

Biblia inatuambia kwamba Waisraeli walipewa nchi nzuri, “nchi inayotiririka maziwa na asali,” iwe makao yao. (Kutoka 3:8; Kumbukumbu la Torati 26:9, 15) Kadiri walivyoendelea kufuatia ibada ya kweli ya Yehova, ndivyo walivyofurahia baraka zake. Maisha yalikuwa mazuri, na watu walikuwa wenye furaha na wenye kuridhika. Kwa mfano, Biblia inatuambia: “Yuda na Israeli waliendelea kukaa salama, kila mtu chini ya mzabibu wake mwenyewe na chini ya mtini wake mwenyewe, kuanzia Dani mpaka Beer-sheba, siku zote za [Mfalme] Sulemani.”—1 Wafalme 4:25.

[Maelezo ya Chini]

^ Kwa habari zaidi kuhusu jinsi vitambaa hivyo vilivyotengenezwa, ona masanduku katika makala hii.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 26, 27]

Sufu na Kitani

Nyakati za Biblia, kondoo walifugwa kwa ajili ya maziwa na sufu. Mkulima angeweza kupata sufu ya kutosha kwa ajili ya mavazi ya familia yake kutoka kwa kondoo wachache. Ikiwa mkulima alifuga kondoo wengi, sufu iliyobaki ingeweza kuuziwa watengenezaji wa vitambaa katika eneo lake. Miji fulani ilikuwa na vikundi vya watu walioungana ili kutengeneza vitambaa. Tangu zamani, ukataji wa manyoya ya kondoo ulikuwa sehemu ya kazi ya kila mwaka.—Mwanzo 31:19; 38:13; 1 Samweli 25:4, 11.

Kitani ni aina ya kitambaa kilichopendwa sana ambacho kilitengenezwa kwa nyuzi za mmea wa kitani. (Kutoka 9:31) Mmea huo ulivunwa wakati ulipokuwa karibu kukomaa kabisa. Shina la mmea huo lilikaushwa kwa jua kisha likaloweshwa ndani ya maji ili kulainisha sehemu zake ngumu. Baada ya kukaushwa, shina hilo lingepigwa-pigwa na nyuzi zake kutenganishwa, kisha kusokotwa ili kutokeza nyuzi zilizotumiwa kufuma. Watu wa familia ya kifalme na maafisa wa ngazi za juu walipendelea mavazi yaliyotengenezwa kwa kitani.

[Picha]

Mmea wa kitani uliokaushwa kabla ya kuloweshwa

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 27]

Kusokota

Uzi mmoja, iwe ni wa kitani, sufu, au manyoya ya mbuzi, unaweza kukatika kwa urahisi na ni mfupi sana hivi kwamba ni vigumu kuutumia. Hivyo, nyuzi kadhaa husokotwa pamoja ili kutokeza uzi wenye ukubwa na urefu unaotakiwa. Kuhusu “mke mwenye uwezo,” Biblia inasema hivi: “Ananyoosha mikono yake kushika kijiti cha kusokotea uzi, nayo mikono yake mwenyewe imeshika gurudumu la kusokota nyuzi.” (Methali 31:10, 19) Hayo ni maelezo kuhusu kusokota uzi kwa kutumia kijiti na gurudumu la kusokotea, yaani, vijiti viwili vya kawaida tu.

Kwa mkono mmoja, mwanamke angeshika kijiti cha kusokotea, kilichozungushiwa nyuzi ambazo hazijakazwa. Kwa kutumia mkono ule mwingine angetoa baadhi ya nyuzi hizo, na kuzisokota ili kufanyiza uzi, na kuufunga kwenye chuma fulani chenye umbo la ndoano kilicho upande mmoja wa gurudumu la kusokotea. Upande ule mwingine wa gurudumu la kusokotea ulikuwa na diski nzito, ambayo ilisaidia gurudumu hilo kuzunguka. Akishikilia ile sehemu yenye ndoana ikiwa juu huku ile yenye diski nzito ikiwa chini, mwanamke huyo angezungusha gurudumu hilo ili kusokota uzi wenye ukubwa fulani. Uzi huo unaosokotwa ungezungushwa kwenye kijiti cha gurudumu la kusokotea, na angeendelea kusokota mpaka nyuzi zote kwenye kijiti cha kusokotea ziunganishwe na kuwa uzi mmoja mrefu, ulio tayari kutiwa rangi au kufumwa.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 28, 29]

Kutia Rangi

Baada ya kitambaa kufumwa au nyuzi za sufu na za kitani kusokotwa na kusafishwa, vitu hivyo vinatiwa rangi mbalimbali. Kulowesha kitambaa au nyuzi ndani ya rangi mara kadhaa kunafanya ziwe na rangi iliyokolea. Baada ya kutolewa katika mtungi wa rangi, vitambaa vinakamuliwa ili kutoa rangi ya ziada ambayo inatumiwa tena kwa sababu rangi ni bei ya juu. Kitambaa au nyuzi zilizotiwa rangi zinatandazwa chini ili zikauke.

Kwa sababu watu katika nyakati za kale hawakuwa na rangi za kemikali, walitengeneza rangi mbalimbali zisizochujuka ambazo zilitokana na wanyama na mimea. Kwa mfano, rangi ya manjano ilitengenezwa kutokana na matawi ya mlozi na maganda magumu ya makomamanga, nayo rangi nyeusi ilitengenezwa kutokana na magamba ya mti wa makomamanga. Rangi nyekundu ilitengenezwa kwa kutumia mizizi ya mmea unaoitwa madder au wadudu wanaoitwa kermes. Nayo rangi ya bluu ilitengenezwa kwa kutumia maua ya mnili. Rangi zilizotokana na aina mbalimbali za konokono wa baharini zilichanganywa ili kutokeza rangi tofauti-tofauti, kutia ndani rangi ya zambarau, ya bluu, na nyekundu iliyokolea.

Ni konokono wangapi waliohitajika ili kutokeza rangi ya kutosha kutia kwenye vazi moja? Kila konokono wa baharini anatoa kiasi kidogo sana cha rangi hivi kwamba kulingana na utafiti mmoja, konokono 10,000 walihitajika ili kutokeza rangi ya zambarau ya kifalme ambayo ingetosha kutia rangi vazi moja. Wakati wa utawala wa Mfalme Nabonido wa Babiloni, ilisemekana kwamba bei ya sufu iliyotiwa rangi ya zambarau ilikuwa juu mara 40 kuliko sufu iliyotiwa rangi nyingine. Kwa kuwa jiji la kale la Tiro lilijulikana sana kwa kutokeza rangi hiyo ya bei ya juu, rangi ya zambarau ilikuja kuitwa zambarau ya Tiro.

[Picha]

Kombe la konokono wa baharini

Mtungi wa rangi ya zambarau wa karne ya 2 au ya 3 K.W.K. uliopatikana huko Tel Dor, nchini Israel

[Hisani]

The Tel Dor Project

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 29]

Kufuma

Kitanda cha kufumia kinatumiwa kufuma nyuzi na kutokeza vitambaa vyenye ukubwa unaohitajiwa kwa ajili ya mavazi na vitu vingine. Akiwa na nyuzi zilizofungwa kutoka upande wa juu hadi chini kwenye kitanda cha kufumia, mfumaji, anapitisha uzi tena na tena katikati ya nyuzi hizo, akifanya hivyo kutoka upande wa kushoto hadi wa kulia.

Kitanda cha kufumia kilichotumiwa nyakati za Biblia kililalishwa chini au kusimamishwa. Mfumaji alipotumia vitanda vya kufumia vilivyosimamishwa, alihitaji kufunga vitu fulani vyenye uzito kwenye nyuzi zilizoning’inia. Baadhi ya vitu hivyo vyenye uzito vilivyotumiwa nyakati za kale vimevumbuliwa katika maeneo kadhaa huko Israel.

Ufumaji ulikuwa kazi ya nyumbani, lakini katika sehemu fulani kijiji kizima kingefanya kazi hiyo kwa pamoja. Kwa mfano, andiko la 1 Mambo ya Nyakati 4:21, linataja kuhusu “nyumba ya wafumaji wa vitambaa,” likithibitisha kwamba watu fulani walishirikiana kufanya kazi hiyo ili kujiruzuku.

[Picha katika ukurasa wa 26, 27]

“Uzi wa bluu na sufu iliyotiwa rangi ya zambarau.”—Kutoka 26:1