Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kutafuta Hazina Kwenye Milima Maridadi ya Altay

Kutafuta Hazina Kwenye Milima Maridadi ya Altay

Barua Kutoka Urusi

Kutafuta Hazina Kwenye Milima Maridadi ya Altay

NI SIKU yenye kupendeza ya mwezi wa Mei katika Jamhuri ya Altay—nchi maridadi sana iliyo kusini-magharibi ya Siberia. Tunapotazama nje ya dirisha, tunaona msitu mkubwa wa miti ya misonobari; na nyuma yake kuna milima yenye rangi ya bluu hafifu ambayo vilele vyake vimefunikwa kwa theluji. Hilo ni eneo la mbali lenye milima na mabonde la Waaltay—watu wenye asili ya Asia lakini wanaozungumza lugha tofauti na wengine. Watu hao wanaishi kwa furaha kwenye milima hiyo ya Altay, jina linalotokana na neno la Kituruki cha Mongolia ambalo linamaanisha “dhahabu.”

Miaka michache iliyopita, mimi na mke wangu tulijifunza Lugha ya Ishara ya Urusi na tukaanza kutembelea makutaniko ya lugha hiyo na vikundi vidogovidogo vya Mashahidi wa Yehova ambao ni viziwi. Ingawa katika nchi hii kuna jamii zaidi ya 100 na vikundi 70 vyenye utamaduni mbalimbali, wote wanazungumza lugha moja, Kirusi. Nao viziwi walio kati yetu watumia lugha nyingine, Lugha ya Ishara ya Urusi. Viziwi hao wanafurahia muungano wa kitamaduni, na wengi tunaokutana nao wana hamu ya kutuambia kuhusu maisha yao na kutuonyesha ukarimu. Hivyo ndivyo hali ilivyo huko Altay.

Katika jiji la Gorno-Altaysk, tunaelezwa kuhusu viziwi fulani ambao wanaishi katika kijiji kimoja kidogo kilicho umbali wa kilomita 250. Tunajua kwamba kuna Mashahidi wachache katika eneo hilo, lakini hakuna hata mmoja wao anayefahamu lugha ya ishara. Tunataka kujua zaidi kuhusu Waaltay hao walio viziwi na hivyo tunaamua kwenda kuwatafuta. Shauku yetu inawavutia sana Yury na Tatyana, wenzi wa ndoa ambao ni viziwi, nao wanakubali kujiunga nasi. Tunapakia kwenye gari dogo machapisho ya lugha ya ishara yaliyo kwenye DVD na mashine ya kucheza DVD hizo. Pia tunabeba chombo kikubwa cha kuhifadhi vitu vikiwa moto, sandwichi iliyotayarishwa kwa mkate wa rai na soseji za kuchoma, piroshki—keki tamu za Kirusi zilizotoka tu kuokwa, ambazo hutiwa kabeji na viazi. Mwishowe tunajipulizia na kupulizia viatu na mavazi yetu dawa ya kuzuia kupe, kwa sababu katika eneo hilo watu hupatwa na uvimbe wa ubongo unaosababishwa na kupe.

Barabara tunayopitia inajipinda-pinda katikati ya milima yenye mandhari nzuri. Pia, kuna harufu nzuri inayotokana na miti ya yasmini na lilaki. Harufu hiyo inatuchangamsha kwelikweli! Tunasisimka sana kuona kundi la paa wa Siberia wakila nyasi. Waaltay huishi katika makundi ya nyumba za mbao zilizoezekwa kwa mabati. Kando ya nyumba nyingi kuna nyumba nyingine za mbao zinazoitwa ayyl, zenye kuta sita na paa lenye umbo la pia. Baadhi ya nyumba hizo zinafanana na hema lenye umbo la pia lililofunikwa kwa magamba ya miti. Familia nyingi za Waaltay zinaishi katika ayyl hizo kuanzia Mei hadi Septemba, kisha wanahamia katika nyumba zao katika miezi mingine ya mwaka.

Tunakaribishwa kijijini kwa uchangamfu na Mashahidi wa eneo hilo ambao wanatupeleka kwenye nyumba ya wenzi wa ndoa ambao ni viziwi. Wanafurahi sana kutuona na wanataka kujua tulikotoka na kazi tunayofanya. Tunatambua kwamba wana kompyuta, hivyo tunatoa DVD, na wanasisitiza kuitazama. Mara moja, wanaacha kuzungumza nasi, kana kwamba hatupo. Wanakazia fikira mambo wanayotazama na mara kwa mara wanarudia ishara wanazoona na kutikisa kichwa kwa uthamini. Baada ya kuwasihi sana, wanakubali kutusikiliza hivyo tunasimamisha DVD ili tutazame tena sehemu za kwanza zinazoonyesha dunia paradiso yenye kupendeza. Tunapitia sehemu moja na kuzungumzia mambo ambayo Mungu anakusudia kuwafanyia wanadamu na pia ni watu wa aina gani watakaoishi milele chini ya hali wanazoona. Tunatiwa moyo sana na jinsi wanavyopendezwa na habari hizo na tunapotaka kuondoka, wanatueleza kuhusu wenzi wengine wa ndoa viziwi ambao wanaishi katika kijiji kingine kilicho mbali.

Tunaanza safari tena na kupitia njia ya milimani iliyo katikati ya majabali yenye kuvutia, kisha tunafuata barabara iliyojipinda-pinda na kufika kwenye kijiji fulani kidogo. Hapo tunakuta familia ya viziwi—mume, mke, mvulana wao mdogo, na mama ya mke—ambao wanafurahia kupata wageni wasiotazamiwa. Tunaingia katika nyumba hiyo kupitia mlango mdogo wa ayyl yao, ambapo tunafurahia harufu nzuri ya mbao na siagi ya maziwa. Katikati ya paa lililo na umbo la pia, kuna shimo la mviringo linaloruhusu mwangaza upenye. Kwenye kona moja ya nyumba, kuna jiko la kuokea la matofali yaliyopakwa chokaa na jiko lingine. Kuta za nyumba hiyo zimefunikwa kwa vipande vyekundu vya zulia. Wenzi hao wanatupatia chakula cha Waaltay—donati ndogo zilizokaangwa na chai iliyotiwa ndani ya bakuli ndogo zenye muundo wa Kiasia. Tunawauliza ikiwa wamewahi kufikiria kama inawezekana kuwa rafiki ya Mungu. Wanafikiria swali hilo kwa makini. Mama ya mke anatuambia alipokuwa mtoto, wakati fulani alipeleka chakula milimani kama toleo kwa miungu. “Sijui jambo hilo lilimaanisha nini,” anasema huku akiinua mabega na kutabasamu. “Huo ulikuwa utamaduni wetu.”

Tunawaonyesha DVD inayozungumzia jambo hilo na wanaanza kutabasamu. Wana hamu ya kuendelea na mazungumzo, lakini tutafanyaje hivyo? Ingawa ni rahisi kuwasiliana na viziwi kupitia ujumbe mfupi unaotumwa kwa simu za mkononi, eneo hilo halina huduma za simu za mkononi. Hivyo, tunawaahidi kwamba tutawasiliana kupitia barua.

Jua limeanza kutua na tunawaaga wenyeji wetu kwa shauku na kuanza safari ndefu ya kurudi Gorno-Altaysk, tukiwa tumechoka lakini tumeridhika. Muda fulani baadaye, tunawauliza Mashahidi wa eneo hilo kuhusu familia hiyo nao wanatueleza kwamba yule mume husafiri mara kwa mara kwenda kwenye mji mkubwa zaidi, ambako anajifunza Biblia na kuhudhuria mikutano akisaidiwa na dada fulani ambaye anajua lugha ya ishara. Tunafurahi kama nini kwamba bidii yetu ilikuwa na matokeo mazuri!

Bidii yetu ya kuwatafuta viziwi wenye mioyo minyoofu inaweza kulinganishwa na kutafuta hazina iliyofichwa milimani. Baada ya kutafuta kwa muda mrefu inafurahisha kupata mtu anayependezwa, sawa na kupata jiwe la thamani bila kutazamia. Tutaendelea kukumbuka milima maridadi ya Altay, ambayo sikuzote itatukumbusha watu wanyoofu tuliowapata kwenye vilele vya milima hiyo.