Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kwa Nini Ni Vibaya Kuwasiliana na Pepo?

Kwa Nini Ni Vibaya Kuwasiliana na Pepo?

Kwa Nini Ni Vibaya Kuwasiliana na Pepo?

Tangu utotoni, Barbara * alikuwa akipata maono, akisikia sauti, na alikuwa na uhakika kwamba anawasiliana na watu wake wa ukoo waliokufa. Yeye na mume wake, Joachim, walisoma vitabu kuhusu uchawi na wakawa na ustadi wa kusoma kadi za ubashiri. Kadi hizo zilionyesha kwamba wangepata pesa nyingi katika biashara, na ndivyo ilivyokuwa. Siku moja, kadi hizo ziliwaonya kwamba watu hatari wangekuja nyumbani kwao na zikawaambia wanapaswa kujilinda.

INGAWA huenda imani katika mambo ya uchawi ikaonekana imepitwa na wakati, watu wengi wanavutiwa na uwezo unaopita ule wa kibinadamu. Watu wengi ulimwenguni wanavaa hirizi, wanatumia mbao za kufanya uaguzi, na wanaenda kwa watu wenye uwezo wa kuwasiliana na pepo ili wajue wakati wao ujao au kujilinda kutokana na uovu. Gazeti linaloitwa Focus la Ujerumani lilikuwa na makala yenye kichwa “Kompyuta na Ibilisi,” ambayo ilisema hivi: “Intaneti inachochea watu wavutiwe au watake kujua mengi zaidi kuhusu mambo ya uchawi.”

Je, unajua kwamba Biblia inazungumza kuhusu kuwasiliana na pepo? Mambo inayosema kuhusu zoea hilo yanaweza kukushangaza.

Biblia Inasema Nini Kuhusu Kuwasiliana na Pepo?

Sheria ambayo Mungu aliwapa watu wake katika Israeli la kale ilisema: “Asipatikane ndani yako . . . yeyote anayefanya uaguzi, mwenye kufanya uchawi au yeyote anayetafuta ishara za bahati au mlozi, au anayefunga wengine kwa kuwatakia maovu au yeyote anayetafuta ushauri kwa mwenye kuwasiliana na pepo au mjuzi wa kubashiri matukio au yeyote anayeuliza habari kutoka kwa wafu. Kwa maana kila mtu anayefanya mambo hayo ni chukizo kwa Yehova.” (Kumbukumbu la Torati 18:10-12) Kwa nini sheria ya Yehova ilipinga kabisa zoea la kuwasiliana na pepo?

Kama utangulizi wa makala hii unavyoonyesha, watu wengi wanaamini kwamba watu walio hai wanaweza kuwasiliana na wafu na habari zinazopatikana kupitia mambo ya uchawi zinatokana na wafu. Imani hizo zinatokana na jambo ambalo linafundishwa na dini nyingi—kwamba watu wanapokufa wanaenda kuishi katika makao ya roho. Lakini, tofauti na fundisho hilo, Biblia inataja hivi waziwazi: “Wafu, hawajui lolote kamwe.” (Mhubiri 9:5) Kulingana na andiko hilo, wafu wanalinganishwa na watu ambao wamelala usingizi mzito, wakiwa hawajui lolote linaloendelea. * (Mathayo 9:18, 24; Yohana 11:11-14) Ikiwa ni hivyo, huenda ukajiuliza, Tunawezaje kueleza mambo ambayo watu wanaowasiliana na pepo wamejionea? Ni nini chanzo cha mawasiliano hayo?

Kuwasiliana na Viumbe wa Roho

Masimulizi ya Injili yanaonyesha kwamba Yesu alipokuwa duniani aliwasiliana na viumbe wa roho. Andiko la Marko 1:23, 24, linasema kwamba “roho mchafu” alimwambia Yesu: “Ninajua wewe ni nani.” Bila shaka, roho waovu wanakujua pia. Lakini wewe unawajua?

Kabla ya kuwaumba wanadamu, Mungu aliumba wana wengi sana wa roho, au malaika. (Ayubu 38:4-7) Malaika ni viumbe wa hali ya juu kuliko wanadamu. (Waebrania 2:6, 7) Wana nguvu na akili nyingi sana, na waliumbwa ili wafanye mapenzi ya Mungu. Mtunga-zaburi aliimba hivi: “Mbarikini Yehova, enyi malaika zake, mlio na uwezo katika nguvu, mnaolitenda neno lake.”—Zaburi 103:20.

Biblia inafunua kwamba baada ya muda fulani baadhi ya malaika walianza kuwasiliana na wanadamu katika njia ambayo Mungu hakukubali. Wakiwa na kusudi gani? Malaika wa kwanza kufanya hivyo, alitumia uwongo ili kuwafanya wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, wamwasi Mungu aliyewaumba. Kwa kufanya hivyo, alijifanya mwenyewe kuwa Shetani Ibilisi, yaani, mchongezi na mpinzani wa Mungu.—Mwanzo 3:1-6.

Baadaye, malaika wengine ‘waliacha makao yao wenyewe yanayofaa’ huko mbinguni, wakajivika miili ya kibinadamu, na kuanza kuishi duniani na wanawake warembo. (Yuda 6; Mwanzo 6:1, 2) Malaika hao waasi pamoja na wazao wao waliokuwa wakubwa isivyo kawaida walianza kuwatesa wanadamu sana hivi kwamba dunia “ikajaa jeuri.” Huenda unafahamu simulizi hilo la Biblia kuhusu jinsi Mungu alivyokomesha jeuri hiyo na kizazi hicho kiovu kupitia Gharika ya siku za Noa.—Mwanzo 6:3, 4, 11-13.

Maji ya Gharika yaliwalazimisha malaika hao kuacha miili yao ya kibinadamu na kurudi katika makao ya roho. Lakini Muumba hakuwaruhusu warudi katika “makao yao.” Badala yake walifungiwa katika hali ya chini inayolinganishwa na “mashimo yenye giza zito.” (2 Petro 2:4, 5) Biblia inawaita malaika hao waasi “roho waovu.” (Yakobo 2:19) Wao ndio pepo ambao watu huwasiliana nao.

Roho Waovu Wanataka Nini?

Kusudi kuu la roho waovu wanaowasiliana na wanadamu ni kuwachochea watu wasimwabudu Mungu wa kweli, Yehova. Zawadi au nguvu ambazo watu wanaofanya mambo ya uchawi wanadai kuwa nazo ni mbinu ya kukengeusha watu ili wasipate ujuzi sahihi kumhusu Mungu na wasisitawishe uhusiano wa karibu pamoja naye.

Kusudi la pili la roho hao waovu linaweza kuonekana wazi katika jambo ambalo Shetani, kiongozi wao, alijaribu kumshawishi Yesu afanye. Shetani aliahidi kumpa Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo.” Naye alitaka Yesu afanye nini? Shetani alimwambia: “Anguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” Ndiyo, Shetani na roho waovu wanatamani kuabudiwa. Lakini Yesu alikataa kishawishi hicho cha kumwacha Mungu na ibada ya kweli.—Mathayo 4:8-10.

Leo, roho waovu hawawasiliani sana na watu moja kwa moja kama walivyofanya na Yesu. Badala yake, wanajaribu kuwanasa watu ambao hawako macho kwa kutumia mbinu ambazo huenda zikaonekana ni kana kwamba haziwezi kudhuru, kama vile matufe ya kioo, majani chai, kadi za ubashiri, pinduli, na kubashiri kwa kutumia nyota. Usidanganywe na mazoea kama hayo! Mazoea hayo yanahusisha mengi zaidi ya kuwasiliana na viumbe wa roho katika njia isiyoeleweka. Roho waovu wanawavutia watu kwa kutumia mambo ya uchawi ili kuwadanganya na kuwanasa wakiwa na kusudi la kuwakengeusha waache kumwabudu Yehova. Wanaposhindwa kutimiza kusudi lao, mara nyingi roho waovu huwasumbua na kufanya maisha ya wale ambao wamenaswa na mtego wao yawe magumu. Ikiwa unakabili hali hiyo, unaweza kufanya nini ili ujiweke huru kutokana na uvutano wa roho waovu?

Jinsi Unavyoweza Kuacha Kuwasiliana na Pepo

Usidanganyike, roho wanaowasiliana na wanadamu ni maadui wa Mungu, na wataangamizwa. (Yuda 6) Roho hao ni wajanja na waongo, nao hujifanya kuwa watu waliokufa. Ungehisije ikiwa ungetambua kwamba mtu uliyefikiri kuwa ni rafiki yako ni mjanja na anataka tu kukukengeusha ili usifanikiwe? Ungehisije ikiwa ungetambua kuwa umejiingiza katika uhusiano bila kujua na mtu anayewadanganya watu kupitia Intaneti akiwa na kusudi la kuwatendea vibaya kingono? Kujihusisha na roho waovu ni jambo hatari hata zaidi. Unahitaji kufanya yote uwezayo ili uache kuwasiliana nao. Unaweza kufanya nini?

Baada ya kujifunza yale ambayo Maandiko yanasema kuhusu kuwasiliana na pepo, wakaaji fulani wa Efeso la kale waliamua kuharibu vitabu vyao vya ufundi wa uchawi, ingawa vilikuwa vya bei ya juu sana. ‘Waliviteketeza mbele ya kila mtu.’ (Matendo 19:19, 20) Leo, mbali na vitabu, hirizi, mbao za kufanyia uaguzi, na vitu vinginevyo, vifaa vya kiuchawi vinaweza pia kutia ndani habari zinazoweza kupatikana kwenye vifaa vya elektroniki. Epuka chochote kile kinachoweza kuonekana kuwa njia ya kuwasiliana na pepo.

Je, unawakumbuka wale wenzi wa ndoa waliotajwa mwanzoni mwa makala hii? Kwa kutazama kadi zao za ubashiri waliona kwamba watu fulani hatari wangewatembelea nyumbani na kwamba hawakupaswa kuwasikiliza wala kupokea chochote kutoka kwao. Hata hivyo, Mashahidi wawili wa Yehova, Connie na Gudrun, walipowatembelea na kuwaambia kwamba walikuwa na habari njema kumhusu Mungu, Joachim na Barbara waliamua kuwasikiliza. Mwishowe walianza kuzungumza kuhusu kuwasiliana na pepo, na Connie na Gudrun wakawapa habari sahihi kuhusu zoea hilo wakitumia Biblia. Kisha wakawa na mpango wa kuzungumzia Biblia kwa ukawaida.

Muda mfupi baadaye, Joachim na Barbara waliamua kuacha kabisa kuwasiliana na pepo. Mashahidi hao waliwaeleza kwamba inaelekea roho hao hawatafurahia uamuzi wao. Joachim na Barbara walipitia hali ngumu na kushambuliwa kwa njia yenye kutisha na roho waovu. Kwa muda fulani, walikuwa na wasiwasi kila usiku hadi walipohamia nyumba nyingine. Muda huo wote, wenzi hao wa ndoa waliendelea kuwa na uhakika katika maneno ya andiko la Wafilipi 4:13, linalosema: “Kwa mambo yote nina nguvu kupitia yeye anayenipa nguvu.” Yehova alibariki jitihada zao, na mwishowe roho waovu wakaacha kuwatesa. Leo, Joachim na Barbara ni waabudu wenye shangwe wa Mungu wa kweli, Yehova.

Maandiko yanawahimiza hivi wote wanaotaka kupata baraka za Yehova: “Jitiisheni kwa Mungu; lakini mpingeni Ibilisi, naye atawakimbia ninyi. Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yakobo 4:7, 8) Yehova Mungu anaweza na atakusaidia uwe huru kutokana na roho waovu, ikiwa unataka. Joachim na Barbara wanapofikiri kuhusu jinsi walivyowekwa huru kutokana na zoea la kuwasiliana na pepo, wanakubali kwa moyo wote maneno yaliyo katika Zaburi 121:2: “Msaada wangu unatoka kwa Yehova.”

[Maelezo ya Chini]

^ Majina yamebadilishwa.

^ Kwa ajili ya mazungumzo zaidi kuhusu hali ya wafu, ona sura ya 6, yenye kichwa “Wafu Wako Wapi?” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Blabu katika ukurasa wa 21]

Mambo ya uchawi yanawazuia watu wasiwe na uhusiano mzuri na Mungu

[Blabu katika ukurasa wa 22]

“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—YAKOBO 4:8