Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Maisha ya Watu Wakati wa Zamani—Muvuvi wa samaki

Maisha ya Watu Wakati wa Zamani—Muvuvi wa samaki

Maisha ya Watu Wakati wa Zamani​—Muvuvi wa samaki

“[Yesu] alipokuwa akitembea kando ya bahari ya Galilaya aliona ndugu wawili, Simoni anayeitwa Petro na Andrea ndugu yake, wakishusha wavu wa kuvulia samaki ndani ya bahari, kwa maana walikuwa wavuvi. Naye akawaambia: ‘Nifuateni, nami nitawafanya ninyi kuwa wavuvi wa watu.’”​—MATHAYO 4:18, 19.

MANENO samaki, kuvua samaki, na wavuvi wa samaki yanatajwa sana katika Injili. Kama tunavyojua, Yesu alitumia mifano mingi iliyozungumuzia kazi ya kuvua samaki. Na hilo si jambo la kushangaza kwa sababu alipitisha wakati wake mwingi akifundisha watu pembeni ya Bahari ya Galilaya. (Mathayo 4:13; 13:1, 2; Marko 3:7, 8) Bahari hiyo nzuri iliyo na maji baridi ina urefu wa kilometre karibu 21 na upana wa kilometre 11 hivi. Inawezekana mitume 7 kati ya mitume wa Yesu walikuwa wavuvi: Petro, Andrea, Yakobo, Yohana, Filipo, Tomasi, na Nathanaeli.​—Yohana 21:2, 3.

Kazi ya kuvua samaki ilikuwa inafanyika namna gani wakati wa Yesu? Namna gani tunaweza kufaidika kwa kujifunza juu ya wanaume hao na kazi yao ya kuvua samaki? Kufanya hivyo kutakusaidia uwafahamu mitume wa Yesu na uelewe zaidi matendo ya Yesu na mifano yake. Kwanza, acha tuone namna kazi ya kuvua samaki ilivyokuwa ikifanyika kwenye Bahari ya Galilaya.

‘Musukosuko Mukubwa Ukatokea Katika Bahari’

Bahari ya Galilaya iko katika bonde kwenye metre 210 chini ya usawa wa bahari. Inazungukwa na milima yenye majiwe makubwa​-makubwa, na upande wake wa kaskazini kuna mulima murefu sana unaoitwa Hermoni. Katika majira ya baridi, wakati fulani upepo wenye baridi sana unatokeza zoruba kali. Katika majira ya joto, hewa yenye joto inafunika maji. Bila kutazamia, upepo mukali wenye kutokeza mawimbi unaotoka kwenye milima inayozunguka bahari hiyo unaweza kuwashambulia wanamaji wanaofanya safari katika bahari ya Galilaya. Yesu na wanafunzi wake walishambuliwa pia na upepo wenye mawimbi wa namna hiyo.​—Mathayo 8:23-27.

Wavuvi wa samaki waliendesha mashua (aina ya boti) zilizotengenezwa kwa miti ambazo zilikuwa na urefu wa metre 8 hivi na upana wa metre 2 hivi. Mashua zao nyingi zilikuwa na muti uliosimamishwa katikati ambako kitambaa kilifungwa, na zilikuwa na sehemu ya nyuma ambamo mutu angeweza kulala. (Marko 4:35-41) Mashua hizo zilizokuwa ngumu na zilizotembea polepole hazikupinduliwa na upepo, kwa sababu kitambaa kikubwa kilichofungwa kwenye muti wa katikati kilizuia upepo huo na kupeleka mashua upande mumoja huku uzito wa wavu ulikuwa ukiikokotea upande mwengine.

Wanaume waliendesha mashua hizo kwa kutumia kasia zilizofungwa pande zote mbili za mashua. Katika kila mashua mulikuwa wavuvi sita ao zaidi. (Marko 1:20) Tena, mashua ilikuwa na vitu vingi kama vile kitambaa cha kitani (1), kamba ndefu (2), kasia (3), jiwe kubwa lililotumiwa kama nanga ya mashua (4), mavazi ya kujifunika ili kujilinda na baridi (5), chakula (Marko 8:14) (6), vitunga (7), kitu fulani cha kulazia kichwa (Marko 4:38) (8), na wavu (9). Inawezekana walibeba pia vitu fulani vya ziada vya kufanya wavu uelee juu ya maji (10), na vitu vya kuzamisha wavu ndani ya maji (11), vitu vya kutengeneza wavu (12), na vimulikaji (ao taa) (13).

‘Wakakusanya Samaki Nyingi Sana’

Tangu wakati wa mitume mupaka leo, katika Bahari ya Galilaya samaki nyingi zinapatikana karibu na mahali ambapo mito inaingia katika bahari hiyo. Mahali hapo, majani​-majani yanaingia katika bahari na yanavutia samaki. Ili kunasa samaki, wavuvi wa wakati wa Yesu walivua mara nyingi wakati wa usiku kwa kutumia vimulikaji. Siku moja, wanafunzi fulani wa Yesu walivua usiku muzima lakini hawakupata hata samaki moja. Lakini ilipokuwa muchana, Yesu aliwaamuru washushe tena nyavu zao ndani ya maji na hivyo wakanasa samaki nyingi sana hivi kwamba mashua zao zilikuwa karibu kuzama.​—Luka 5:6, 7.

Wakati fulani, wavuvi walikuwa wakivua mahali palipokuwa na maji mengi. Walitumika pamoja kwa kutumia mashua mbili. Walikuwa wakitupa wavu katikati ya mashua hizo mbili; na waliendesha mashua kwa bidii, moja upande wa kuume na ingine upande wa kushoto, wakitupa wavu katika maji na kuzingira samaki. Kisha mashua zilikutana na wavuvi walifunga wavu. Kisha wavuvi walikokota kamba zilizofungwa kwenye wavu, na kisha walipandisha wavu uliokuwa umekamata samaki katika mashua. Wavu ungeweza kufikia urefu wa metre zaidi ya 30 na upana wa metre karibu 2 na nusu; kwa hiyo, ungeweza kukamata samaki nyingi sana kwa mara moja. Kwenye sehemu ya juu ya wavu kulifungwa vitu vyenye kuufanya uelee juu ya maji na kwenye sehemu ya chini kulifungwa vitu vyenye kuufanya uzame ndani ya maji. Wavuvi walikuwa wanatupa wavu ndani ya maji na kuupandisha, wanatupa na kuupandisha tena mara kwa mara na saa baada ya saa.

Mahali ambapo hapakuwa na maji mengi, wavuvi walitumia ufundi mwengine tofauti. Wale waliokuwa katika mashua walichukua upande mumoja wa wavu, waliingia nao katika bahari na kuzingira samaki, kisha walizunguka na kurudi kwenye inchi kavu. Na wale waliokuwa kwenye inchi kavu walikokota wavu uliokuwa na samaki mupaka kwenye inchi kavu, ambako walitenganisha samaki nzuri na mbaya. Walitia samaki nzuri ndani ya vyombo. Waliuzishia watu samaki zingine palepale. Samaki zingine nyingi zilikaushwa na kutiwa chumvi ao vikolezo vingine ili zisioze; zilichungwa katika mitungi ya udongo inayoitwa amphoras, na kupelekwa Yerusalemu ao katika inchi zingine. Samaki ambazo hazikuwa na magamba ao mapezi zilionwa kuwa zisizo safi na kwa hiyo zilitupwa. (Mambo ya Walawi 11:9-12) Yesu alizungumuzia ufundi huo wa kuvua samaki alipofananisha “ufalme wa mbinguni” na wavu na alipofananisha aina mbalimbali za samaki na watu wazuri ao wabaya.​—Mathayo 13:47-50.

Muvuvi aliyevua samaki akiwa peke yake alitumia ndoano iliyokuwa na chakula fulani cha kuvutia samaki (ao chambo). Ao angeweza kutumia wavu ndogo wa kutupa ndani ya maji. Ili kutupa wavu, alipaswa kutembea ndani ya maji, na kuchukua wavu katika mikono yake na kuuzungusha kwanza na kisha kuutupa katika maji. Wavu huo ulijifungua na kujitandaza juu ya maji, na kisha ulizama. Wakati fulani, muvuvi alikuta samaki chache ndani ya wavu wake alipoukokota.

Nyavu zilikuwa bei sana na iliomba kazi nyingi ili kuzichunga vizuri. Kwa hiyo, wavuvi walizitumia kwa uangalifu sana. Wavuvi walitumia wakati mwingi sana ili kutengeneza nyavu zao mahali zilipopasuka, kuzisafisha, na kuzikausha. Walifanya hivyo kila wakati walipomaliza kuvua. (Luka 5:2) Mutume Yakobo na ndugu yake Yohana walikuwa wenye kukaa katika mashua yao wakitengeneza nyavu zao mahali zilipopasuka wakati Yesu aliwaita wawe wafuasi wake.​—Marko 1:19.

Wakati wa mitume, watu walivua samaki za aina nyingi. Kati ya aina hizo kulikuwa tilapia nyingi. Katika Galilaya, watu wengi walikuwa wanapenda kula aina hiyo ya samaki, na inawezekana Yesu alikula samaki hiyo tamu. Labda ni tilapia ao bikwara zenye kukaushwa kwa chumvi ndizo alitumia alipofanya muujiza wa kulisha watu wengi sana kwa samaki mbili. (Mathayo 14:16, 17; Luka 24:41-43) Mara nyingi samaki hizo zinaogelea zikiwa zenye kubeba watoto wao katika kinywa. Lakini, ikiwa hazibebe watoto wao katika kinywa chao, zinaweza kubeba majiwe madogo​-madogo yenye bei ao hata sarafu zenye kungaa zinazopatikana chini ya bahari.​—Mathayo 17:27.

Wakati wa mitume, wavuvi walikuwa wavumilivu, walitumika kwa bidii, na walikuwa tayari kuvumilia hali ngumu ili kupata samaki. Wale waliokubali kujiunga na Yesu katika kazi ya kufanya wanafunzi walihitaji pia kuwa na sifa hizo ili kuwa “wavuvi wa watu” wenye matokeo mazuri.​—Mathayo 28:19, 20.

[Picha katika ukurasa wa 19]

(Ona Kichapo)