Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Je, Ulijua?

Je, Ulijua?

Je, Ulijua?

Kalamu na wino vilivyotumiwa wakati wa zamani ili kuandika, vilikuwa vya namna gani?

Mwishoni mwa barua yake ya tatu, mutume Yohana alisema hivi: “Nilikuwa na mambo mengi ya kukuandikia, lakini sitaki kuendelea kukuandikia kwa wino na kalamu.” Maneno ya kwanza kwanza ya Kigiriki ambayo Yohana alitumia yakitafsiriwa neno kwa neno yanamaanisha kama hakupenda kuendelea kuandika kwa “[wino] mweusi na utete.”​—3 Yohana 13, The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures.

Waandikaji walitumia vipande vya matete magumu ili kuandika. Watu walikata utete kwa namna iliyofanya wapate chongo na kisha walilainisha chongo hiyo. Muandikaji angeweza pia kuchonga chongo hiyo tena na tena kwa kutumia jiwe fulani. Kalamu ya utete ilifanana na kalamu ya leo iliyo na jicho la chuma na ilitumika kama kalamu hiyo.

Mara nyingi, ili kupata wino, watu walichanga majivu ya moto ao ya taa na kitu kingine chenye kunata. Wino huo uliuzishwa ukiwa wenye kukauka na ulipaswa kuchanganywa na maji kidogo mbele ya kutumiwa. Mutu alipokuwa anaandika, wino huo ulikauka kwenye karatasi ao ngozi na wino huo haukuonekana upande wa pili wa karatasi hiyo. Kwa hiyo, muandikaji angeweza kurekebisha makosa kwa vyepesi kwa kutumia kipande cha nguo chenye kulowana, ambacho kilikuwa pia kati ya vyombo vya kazi vya muandikaji huyo. Maelezo hayo juu ya wino uliotumiwa zamani yanatusaidia kuelewa mawazo ambayo waandikaji wa Biblia walikuwa nayo waliposema juu ya majina kuvutwa katika kitabu cha Mungu cha uzima.​—Kutoka 32:32, 33; Ufunuo 3:5.

Paulo alifanya mahema ya namna gani?

Andiko la Matendo 18:3 linasema kama mutume Paulo alikuwa na kazi ya kufanya mahema. Wakati huo, wale waliofanya mahema walisuka manyoya ya ngamia ao ya mbuzi ili kupata nyuzi. Kisha waliunganisha nyuzi hizo pamoja ili kufanya mahema ya wasafiri. Lakini wakati huo mahema mengi yalifanywa kwa ngozi. Mahema mengine yalifanywa kwa kitani, kilichotengenezwa huko Tarso, muji wa Paulo. Inawezekana Paulo alitumia ngozi za wanyama ao kitani, ao vyote viwili. Hata hivyo, Paulo alipokuwa anatumika na Akila, inawezekana alifanya mahema yaliyotumiwa ili kufunika sehemu zilizokuwa wazi za juu za nyumba fulani ili kujilinda na jua.

Labda Paulo alijifunza kazi hiyo alipokuwa kijana. Kuna maandishi fulani kwenye karatasi za zamani za huko Misri (papyrus) yanayoonyesha kama wakati wa utawala wa Waroma, watu walianza kujifunza kazi walipokuwa na miaka 13 hivi. Ikiwa Paulo alikuwa na miaka hiyo alipoanza kazi yake, inawezekana alipokuwa na miaka 15 ao 16, alikuwa amekuwa fundi kabisa katika kukata na kuchora ngozi ao kitani na kushona kwa kutumia vyombo na ufundi mbalimbali wa kuunganisha. Kitabu fulani (The Social Context of Paul’s Ministry) kinasema hivi: “Inawezekana Paulo alipewa vyombo vyake mwenyewe alipomaliza kujifunza kazi ya kufanya mahema.” Tena, kitabu hicho kinasema kama “vyombo mbalimbali alivyopewa vilimuwezesha kufanya kazi hiyo mahali popote,” kazi iliyomusaidia kutimiza mahitaji yake katika utumishi wa umisionere.

[Picha katika ukurasa wa 15]

Kalamu za matete kutoka Misri, wakati wa mitume

[Picha zimetolewa na]

© Image Asset Management/age fotostock

[Picha katika ukurasa wa 15]

Vyombo vilivyotumiwa ili kushona kuanzia wakati wa mitume na miaka ya 100 kisha

[Picha zimetolewa na]

Erich Lessing/Art Resource, NY