Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

 Masimulizi Kuhusu Maisha Ya Watu

Maisha Yenye Baraka Katika Kazi ya Mungu

Maisha Yenye Baraka Katika Kazi ya Mungu

Tangu wakati nilikuwa mutoto, nilisumbuliwa sana na ubaguzi wa rangi na kuogopa kushindwa na pia hali yangu ya haya-haya. Nilitazamia kupata faraja kutoka katika Biblia, kwa hiyo, nilienda katika Kanisa Katoliki la eneo letu ili wanisaidie kuielewa. Kwa kuwa sikupata musaada wowote, nilianza kupendezwa na michezo.

Bila kukawia, nilijiingiza katika mazoezi ya mwili na kujenga misuli. Mwishowe, nilifungua nafasi ambapo watu walikuja kufanya mazoezi ya mwili katika San Leandro, California, Amerika, na nikaanza kutumika na watu wanaojenga misuli kwa kunyanyua vitu vizito. Kati ya watu hao kulikuwa mutu aliyeshinda mashindano ya kunyanyua vitu vizito katika Amerika. Hata hivyo, sikutosheka kwa kuwa na ule uliowaziwa kuwa mwili wenye misuli iliyojengwa vizuri.

NINAPATA KITU NILICHOKUWA NINATAFUTA

Rafiki mumoja kwenye nafasi yangu ya mazoezi alikuwa anajua nia yangu ya kuelewa Biblia, kwa hiyo, akaniomba nikutane na mutu fulani aliyefahamiana naye. Asubuhi iliyofuata, Shahidi mumoja wa Yehova alikuja nyumbani kwangu. Kwa saa ine alijibia maulizo yangu kupitia Biblia moja kwa moja. Nilimuomba arudie mangaribi ya siku ileile, na tukazungumuza juu ya Biblia mupaka saa sita ya usiku. Nilipendezwa sana na mambo niliyojifunza na nikamuomba ikiwa ninaweza kumusindikiza siku iliyofuata ili nione namna alikuwa anahubiri. Nilishangazwa na namna alikuwa anafungua Biblia na kuonyesha watu majibu ya maulizo yao. Niliamua kwamba hilo ndilo nililotaka kufanya!

Kwa hiyo, niliacha kazi yangu na nikapitisha siku nyingi katika mahubiri pamoja na huyo painia, kama vile watumishi wa wakati wote wa Mashahidi wa Yehova wanavyoitwa. Katika mwezi wa 5, 1948, nilibatizwa kwenye mukusanyiko uliofanywa katika Uwanja wa Cow Palace, San Francisco, California. Kwenye mwisho wa mwaka huo nikakuwa painia.

Wakati uleule, niliomba Mashahidi wa Yehova wamutembelee mama yangu. Alikubali ukweli na bila kukawia akakuwa mumoja wa Mashahidi wa Yehova. Hata ikiwa familia yake ilimupinga, alibaki muaminifu kwa Mungu kufikia kifo chake miaka mingi iliyopita. Hakuna mutu mwengine wa familia yetu ambaye amekuwa Shahidi wa Yehova.

NINAKUTANA NA YULE ALIYEKUJA KUWA BIBI YANGU

Katika mwaka wa 1950, nilihamia Grand Junction, Colorado, ambako nilikutana na Billie. Alizaliwa mwaka wa 1928 na alikomaa wakati kulikuwa matatizo makubwa ya feza ulimwenguni. Mama yake, Minnie, alikuwa anamusomea Biblia kila siku usiku akitumia mwangaza mudogo wa taa ya petroli. Billie alipokuwa na miaka ine, angeweza kusoma, na alijua historia nyingi za Biblia katika akili. Mwishoni mwa miaka kati ya 1941 na 1950 mama yake alijifunza kupitia Biblia kwamba helo, si nafasi ya mateso , lakini ni kaburi la watu wote. (Mhubiri 9:5, 10) Minnie na bwana yake wakakuwa Mashahidi wa Yehova.

Katika mwaka wa 1949, Billie alimaliza masomo yake ya juu katika muji wa Boston na akaanza kujifunza Biblia kwa bidii. Kuliko kuwa mwalimu kwenye masomo, aliamua kutoa maisha yake kwa Mungu. Alibatizwa katika mwaka wa 1950 kwenye mukusanyiko wa kimataifa wa Mashahidi wa Yehova uliofanywa katika Uwanja wa Michezo wa Yankee katika muji wa New York. Muda mufupi kisha hapo, tulikutana, tukaoana, na tukaanza utumishi wa wakati wote pamoja.

Tulianzia utumishi huo katika muji wa Eugene, Oregon, na tukapata marafiki wa muda murefu. Katika mwaka wa 1953 tulihamia Grants Pass, Oregon, ili kusaidia kutaniko ndogo lililokuwa huko. Kwenye mwisho wa mwaka huo, tulialikwa kwenye somo la 23 la Gileadi, masomo ya Mashahidi wa Yehova ya kuzoeza wamisionere. Masomo hayo yalifanywa karibu na South Lansing, New York, kilometa 400 hivi kaskazini-mangaribi mwa New York City.

KAZI YA UMISIONERE KATIKA BRAZIL

Katika Mwezi wa 12, 1954, miezi tano kisha kumaliza masomo ya Gileadi, mimi na Billie tulichukua ndege yenye propela (hélices) mbili ili kuenda Brazil. Kisha kufanya saa moja katika anga, motere moja iliharibika lakini tulishukia Bermuda bila tatizo. Kisha kushuka tena bila mupango katika Cuba na safari yenye kuchosha ya saa 36, tulifika kwenye biro ya tawi ya Mashahidi wa Yehova katika muji wa Rio de Janeiro, Brazil.

Jumba la Ufalme la kwanza katika muji wa Bauru, nafasi ya kukodiwa yenye kuwa na maandishi ambayo niliandika, mwaka wa 1955

Kisha siku fulani, mimi na Billie, pamoja na wamisionere wengine wawili, tulienda Bauru, São Paulo, na tukafungua nyumba mupya ya wamisionere. Muji huo ulikuwa na watu zaidi ya 50000, na tulikuwa Mashahidi wa Yehova wa kwanza huko.

Tulianza kuwatembelea watu nyumbani kwao, lakini mara moja padri wa kanisa Katoliki la eneo hilo alianza kupinga kazi yetu. Alikuwa anatufuata na kuwaambia wenye nyumba wasitusikilize. Hata hivyo, kisha majuma machache, familia moja kubwa ambayo tulikuwa tunajifunza nayo ilikubali ukweli wa Biblia na kubatizwa baadaye. Bila kukawia, wengine pia wakaanza kujifunza.

Familia hiyo iliyobatizwa ilikuwa na mutu wa jamaa aliyekuwa kiongozi wa kikundi fulani chenye kujulikana sana. Nilifanya mupango wa kutumia majengo ya kikundi hicho ili kufanya mukusanyiko. Wakati padri wa eneo hilo alikazia kwamba makubaliano yavunjwe, kiongozi huyo alikutana na watu wa kikundi chake na kuwaambia hivi: “Ikiwa munavunja makubaliano hayo, nitaacha kazi!” Tulipewa ruhusa ya kufanya mukusanyiko huo.

Mwaka uliofuata, ni kusema, mwaka wa 1956, tulialikwa kwenye mukusanyiko wa wilaya katika muji wa Santos, São Paulo. Mashahidi karibu 40 wa kutaniko letu walienda huko kwa treni. Wakati tulirudia Bauru, nilipata barua iliyoniomba nitumike kazi ya mwangalizi anayesafiri ili kutembelea makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Nilifanya kazi hiyo kwa miaka karibu 25 katika inchi ya Brazil, nilizunguka katika sehemu karibu zote za inchi hiyo kubwa.

Katika mwaka moja tu, tulikuwa na kikundi cha wahubiri wa Ufalme wenye bidii katika muji wa Bauru

NAMNA KAZI ILIVYOKUWA

Wakati huo ilikuwa vigumu kusafiri. Tulisafiri inchi yote kwa bisi, treni, gari la kukokotwa, kinga, na hata kwa miguu. Moja kati ya miji ya kwanza tuliyotembelea ilikuwa Jaú, São Paulo. Huko padri mumoja alitushambulia.

Alisema hivi: “Hamuwezi kuhubiri ‘kondoo zangu!’”

Tukamujibu hivi: “Haiko kondoo zako. Ni kondoo za Mungu.”

Tulifanya mupango ili kuonyesha watu video juu ya kazi yetu ya kuhubiri ulimwenguni pote, yenye kichwa La Société du Monde Nouveau en action, lakini padri huyo alikusanya kikundi cha watu ili watushambulie. Bila kukawia tulijulisha polisi jambo hilo. Wakati padri alifika hapo pamoja na kikundi cha wafuasi wa kanisa lake, walikutana na polisi wengi waliokuwa wanasimama kwenye mwingilio wakiwaelekezea bunduki zao. Watu wengi waliofuata video hiyo waliifurahia kabisa.

Hali hiyohiyo ya chuki na upinzani wa kidini ilienea kila mahali tulitumikia kisha hapo. Kwa mufano, katika muji wa Brusque, karibu na Blumenau, Santa Catarina, tulikuta mapainia wawili wakitumika katika upinzani mukubwa. Lakini walibarikiwa kwa sababu ya uvumilivu na ustahimilivu wao. Leo, kisha miaka zaidi ya 50, kuna makutaniko zaidi ya 60 yenye maendeleo mazuri katika eneo hilo na kuna Jumba nzuri la Mikusanyiko karibu na muji wa Itajaí!

Wakati wa maana sana katika kazi yetu ya kusafiri ulikuwa wakati wa furaha tuliopitisha pamoja na Mashahidi wenzetu ili kufanya matayarisho ya mikusanyiko mikubwa. Katika mwaka wa 1975 mupaka 1977, nilipata pendeleo la kutumika kama mwangalizi wa mukusanyiko katika Uwanja mukubwa wa Michezo wa Morumbi. Tangazo lilitumwa kwa makutaniko karibu mia moja ya karibu-karibu ili kila kutaniko litayarishe watu kumi wa kusafisha uwanja usiku mbele ya mukusanyiko.

Wakati wachezaji wa kabumbu walikuwa wakitoka katika uwanja usiku huo, wamoja wao walisikiwa wakichekelea kwa kusema, “Ona wale wanawake wenye vifagio na vikoropo, wanawazia wanaweza kumaliza kusafisha uwanja wote.” Hata hivyo, kufikia saa sita ya usiku uwanja wote ulikuwa safi! Musimamizi wa uwanja alisema hivi kwa mushangao: “Kikundi changu kingechukua juma muzima ili kufanya kazi ambayo ninyi Mashahidi mulifanya katika saa kidogo!”

TUNARUDIA AMERIKA

Katika mwaka wa 1980 baba yangu alikufa, na muda kidogo kisha hapo tulirudia Amerika ili kumuchunga mama yangu, katika muji wa Fremont, California. Tulipata kazi ya kusafisha majengo usiku na tuliendelea na kazi ya upainia na kusaidia watu waliozungumuza Kireno (Portugais) katika eneo hilo. Kisha tulihamia karibu na San Joaquin Valley, ambako tulitafuta watu wanaozungumuza Kireno katika eneo hilo kubwa kuanzia Sacramento mupaka Bakersfield. Leo katika muji wa California, kuna makutaniko karibu kumi ya luga ya Kireno.

Kisha kifo cha mama yangu katika mwaka wa 1995, tulihamia Florida ili kuchunga baba wa Billie mupaka wakati alikufa. Mama yake alikufa mwaka wa 1975. Katika mwaka wa 2000 tulihamia sehemu ya jangwa yenye kuinuka kusini-mangaribi mwa Colorado na tulihubiri wakati wote katika maeneo ya Navajo na Ute ya Wazaliwa wa Amerika tu. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba Billie alikufa katika Mwezi wa 2, 2014.

Mimi ni mwenye furaha sana kwa sababu zaidi ya miaka 65 iliyopita, nilikutana na Shahidi wa Yehova aliyejibia maulizo yangu mengi kupitia Biblia. Nina furaha ya pekee kwamba nilichunguza ili kuhakikisha kuwa mambo aliyosema ndiyo mambo Biblia inafundisha kabisa. Kufanya hivyo kuliniongoza kwenye maisha yenye baraka katika kazi ya Mungu.