Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Sheria ya Mungu kwa Waisraeli Ilitumika kwa Haki na Bila Upendeleo?

Sheria ya Mungu kwa Waisraeli Ilitumika kwa Haki na Bila Upendeleo?

WAKATI fulani uliopita, tribinali za kuhukumu watenda-maovu katika inchi moja ya Mangaribi zilikubali ushuhuda wa uongo uliotolewa juu ya wanaume wawili walioshitakiwa kuwa wauaji na wanaume hao walihukumiwa kifo. Wakati ilijulikana kwamba ushuhuda uliotolewa juu yao ulikuwa wa uongo, wanasheria walijikaza juu chini na wakapata uhuru wa mushitakiwa mumoja. Lakini wanasheria hao wazuri hawangeweza kufanya jambo lolote juu ya ule mwengine kwa sababu tayari alikuwa ameuawa.

Kwa sababu haki inaweza kuvunjwa katika mambo yote yanayohusisha sheria, Biblia inaonya hivi: “Haki—haki utaifuatilia.” (Kumbukumbu la Torati 16:20) Wakati waamuzi wanafuatia haki, raia wanafaidika. Sheria ya Mungu ilitolea taifa la Israeli sheria mbalimbali zilizotegemea kutendea watu bila ubaguzi na bila upendeleo. Acheni tuchunguze Sheria hiyo ili tuone ikiwa ‘njia [za Mungu] zote ni haki.’—Kumbukumbu la Torati 32:4.

WAAMUZI “WENYE HEKIMA NA BUSARA [AO AKILI] NA UZOEFU”

Watu wanafaidika wakati waamuzi ni wenye uwezo, hawana upendeleo, na hawakubali rushwa. Sheria ya Mungu kwa Waisraeli ilionyesha kwamba waamuzi wa namna hiyo walikuwa wa maana sana. Wakati Waisraeli walianza safari yao katika jangwa, Musa aliambiwa atafute ‘wanaume wenye uwezo, wanaomuogopa Mungu, wanaume wenye kutegemeka, wanaochukia faida isiyo ya haki,’ watumike kama waamuzi. (Kutoka 18:21, 22) Miaka 40 baadaye, alikazia tena ulazima wa kuwa na “watu wenye hekima na busara na uzoefu” ili kuhukumu watu.—Kumbukumbu la Torati 1:13-17.

Mamia ya miaka kisha hapo, Mufalme Yehoshafati * wa Yuda aliwaagiza waamuzi hivi: ‘Muone munalofanya, kwa sababu hamuhukumu kwa ajili ya mwanadamu bali kwa ajili ya Yehova; naye iko pamoja nanyi katika jambo la hukumu. Na sasa hofu [ao uoga] ya Yehova na iwe juu yenu. Muwe waangalifu na mutende, kwa maana hakuna ukosefu wowote wa uadilifu [ao haki] wala ubaguzi wala kuchukua rushwa.’ (2 Mambo ya Nyakati 19:6, 7) Kupitia maneno hayo, mufalme aliwakumbusha waamuzi kwamba ikiwa ubaguzi ao pupa ingeharibisha maamuzi yao, Mungu angewaomba watoe hesabu kuhusu jambo lolote mbaya ambalo lingetokea.

Wakati waamuzi wa Israeli walishika kanuni hizo za juu, taifa lao lililindwa na kuwa salama. Lakini Sheria ya Mungu ilitoa pia kanuni zilizosaidia waamuzi wachukue maamuzi bila upendeleo, hata katika hali ngumu zaidi. Kanuni fulani kati ya hizo ni gani?

KANUNI ZILIZOSAIDIA KUFANYA MAAMUZI BILA UPENDELEO

Hata ikiwa waamuzi waliochaguliwa walipaswa kuwa wenye hekima na wanaume wenye uwezo, hawakuachwa wafanye maamuzi kwa kutegemea uwezo wao wenyewe ao akili yao. Yehova Mungu aliwapatia kanuni ao miongozo iliyowasaidia kufanya maamuzi yaliyo sawa. Ona miongozo fulani yenye waamuzi Waisraeli walipewa.

Mufanye uchunguzi kwa uangalifu ili kujua mambo yote. Kupitia Musa, Mungu aliwaagiza waamuzi Waisraeli hivi: ‘Munaposikiliza kesi kati ya ndugu zenu, muhukumu kwa uadilifu [ao haki].’ (Kumbukumbu la Torati 1:16) Waamuzi wangeweza kuamua kwa haki ikiwa tu walijua mambo yote juu ya hali  fulani. Ndiyo maana Mungu aliwaagiza hivi watu walioshugulikia mambo ya sheria: ‘Mutatafuta na kupeleleza na kuuliza habari kabisa.’ Waamuzi katika tribinali walipaswa kuhakikisha kwamba jambo lililoshitakiwa juu ya mutu muovu ‘limesibitika [ao limehakikishwa] kuwa kweli’ mbele ya kuanza masambo.—Kumbukumbu la Torati 13:14; 17:4.

Musikilize ushuhuda wa mashahidi. Maelezo ya mashahidi yalikuwa ya maana katika uchunguzi. Sheria ya Mungu ilisema hivi: ‘Shahidi mumoja asiinuke juu ya mutu kuhusu kosa ao zambi yoyote, kuhusu zambi yoyote ambayo huenda akafanya. Kwa kinywa cha mashahidi wawili ao kwa kinywa cha mashahidi watatu jambo hilo litasibitishwa [ao kuhakikishwa] vizuri.’ (Kumbukumbu la Torati 19:15) Sheria ya Mungu iliwaagiza mashahidi hivi: ‘Musieneze habari isiyo ya kweli. Musishirikiane [ao musipatane] na mutu muovu kwa kuwa shahidi anayepanga jeuri.’—Kutoka 23:1.

Muepuke udanganyifu katika hatua zote za masambo. Hukumu kwa wale waliodanganya ingekuwa onyo kubwa kwa wale wote waliohusika. Sheria ya Mungu ilisema hivi: ‘Waamuzi watatafuta kabisa, na ikiwa shahidi huyo ni shahidi wa uongo naye ameleta shitaka la uongo juu ya ndugu yake, ndipo mutakapomufanyia kama vile alivyomupangia ndugu yake hila [ao ujanja], nawe utaondolea mbali kilicho kibaya kutoka katikati yako.’ (Kumbukumbu la Torati 19:18, 19) Kwa hiyo, ikiwa mwanaume alidanganya katika masambo ili apewe uriti wa mutu mwengine, hukumu yake ingekuwa kulipa kiasi kinacholingana na kile alichokuwa anataka kunyanganya mwenzake. Ikiwa alidanganya ili mutu fulani asiye na kosa auawe, angeuawa pahali pa mutu huyo. Muongozo huo ulichochea sana watu waseme kweli.

Muhukumu bila ubaguzi. Wakati walipata mambo yote yaliyohitajiwa juu ya hali fulani, waamuzi walichunguza mambo hayo ili kukamata uamuzi. Kuhusu jambo hilo, maelezo haya ya lazima sana ya Sheria ya Mungu yalifaa kabisa: ‘Musifanye ukosefu wa haki katika hukumu. Usiwatendee watu wa hali ya chini kwa njia ya ubaguzi, wala usimupendelee mutu mukubwa. Utamuhukumu mwenzako kwa haki.’ (Mambo ya Walawi 19:15) Katika hali zote, waamuzi walipaswa kuamua jambo namna liko kabisa, si kulingana na namna jambo hilo linaonekana kijuujuu ao kulingana na cheo cha watu waliohusika.

Kanuni hizo, zilizoelezwa waziwazi katika Sheria ya Mungu kwa Waisraeli mamia ya miaka iliyopita, zinaweza kusaidia leo katika mambo ya masambo. Wakati kanuni hizo zinafuatwa, kuhukumu vibaya na kuhukumu bila kufuatia haki kunaweza kuepukwa.

Kuhukumu bila kufuatia haki kunaweza kuepukwa wakati kanuni za Sheria ya Mungu zinafuatwa

WATU WALIOFAIDIKA NA HAKI YA KWELI

Musa aliwauliza Waisraeli hivi: “Kuna taifa gani kubwa lenye masharti na maamuzi ya hukumu ya uadilifu kama sheria yote hii ninayoweka mbele yenu leo?” (Kumbukumbu la Torati 4:8) Kwa kweli, hakuna taifa lingine ambalo lilipata faida hizo. Wakati wa utawala wa Mufalme Sulemani, aliyetafuta kutimiza sheria za Yehova katika ujana wake, watu ‘walikaa salama’ na walipata amani na utajiri, ‘wakikula na kunywa na kushangilia.’—1 Wafalme 4:20, 25.

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba mwishowe Waisraeli walimugeuzia Mungu mugongo. Kupitia nabii Yeremia, Mungu alisema hivi: “Tazama! Wamelikataa neno la Yehova, nao wana hekima gani?” (Yeremia 8:9) Kwa sababu ya jambo hilo, muji wa Yerusalemu ukakuwa ‘wenye hatia ya damu’ na ukajaa “machukizo.” Mwishowe, uliharibiwa na kubaki bila kuikaliwa na watu kwa miaka 70.—Ezekieli 22:2; Yeremia 25:11.

Nabii Isaya aliishi katika kipindi hicho chenye muvurugo cha historia ya Israeli. Alipofikiria wakati huo, alichochewa kusema jambo hili la maana juu ya Yehova na Sheria yake: ‘Wakati kunapokuwa na hukumu kutoka kwako kwa ajili ya dunia, wakaaji wa inchi yenye kuzaa hakika watajifunza uadilifu.’—Isaya 26:9.

Isaya alifurahi sana kwa kuongozwa na roho ya Mungu ili kutoa unabii juu ya Yesu Kristo, Masiya Mufalme. Alisema hivi: “Hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu [ao vizuri] kwa ajili ya watu wapole wa dunia.” (Isaya 11:3, 4) Watu wanaokuwa raia wa Ufalme wa Masiya ulio chini ya uongozi wa Ufalme wa Mungu wanatarajia kwa furaha mambo hayo!—Mathayo 6:10.

^ fu. 6 Jina Yehoshafati linamaanisha “Yehova Ni Muamuzi.”