Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 15

“Nitakomesha Ukahaba Wako”

“Nitakomesha Ukahaba Wako”

EZEKIELI 16:41

WAZO KUBWA: Mambo yenye tunajifunza mu habari kuhusu makahaba wenye kuzungumuziwa mu Ezekieli na Ufunuo

1, 2. Ni kahaba wa je mwenye hali yake inaweza kuchukiza sana?

INALETAKA huruma kuona mutu anakuwa kahaba. Tunajiulizaka ni nini njo ilimufikisha mu ile maisha ya mubaya sana. Je, ni juu walimutendeaka kwa jeuri ao mutu fulani wa familia yake alimutendeaka mubaya kingono wakati alikuwa mutoto? Ao ni umaskini njo ulimufanya ajiuzishe mu ile maisha ya utumwa? Ao ni juu ya kukimbia bwana mukali? Mambo ya vile inatokeaka sana mu hii dunia ya mubaya. Lakini, Yesu Kristo alitendea makahaba fulani kwa upole. Alionyesha kama wale wenye wanatubu na kubadilisha maisha yao wanaweza kuwa na maisha ya muzuri.​—Mt. 21:28-32; Lu. 7:36-50.

2 Hata hivyo, tufikirie sasa kahaba wa namna ingine. Wazia mwanamuke mwenye anachagua maisha ya ukahaba kwa kupenda. Yeye, haone kama ni maisha ya mubaya, lakini anaiona kuwa maisha ya muzuri sana! Anapenda sana kazi ya ukahaba juu ya feza na uvutano wenye ile kazi inamuletea. Ya kushangaza sana, tuseme kama ule bibi alikuwaka na bwana muzuri na muaminifu, lakini akachagua kwa kupenda kuachana naye juu afanye ukahaba! Bila shaka utachukia mwanamuke wa vile na maisha yenye amechagua. Namna unajisikia mu moyo, ni vile Yehova Mungu anajisikia pia, na ni ile ilimufanya atumie tena na tena mufano wa kahaba juu ya kuonyesha mawazo yake kuhusu dini ya uongo.

3. Tutazungumuzia habari gani mu sura hii?

3 Kitabu cha Ezekieli kiko na habari mbili za kushangaza mwenye ukahaba unatumiwa juu ya kuonyesha matendo ya mubaya ya kukosa uaminifu ya watu wa Mungu wa Israeli na Yuda. (Eze., sura ya 16 na 23) Lakini, mbele tuchunguze kwa ukaribu zile habari, ni muzuri tuzungumuzie kwanza kahaba mwingine wa mufano. Ukahaba wake ulianzaka miaka mingi mbele ya wakati wa Ezekieli​—miaka mingi mbele hata Israeli ikuwe—​na ungali unaendelea mupaka leo. Ule kahaba anazungumuziwa waziwazi mu Ufunuo, kitabu cha mwisho cha Biblia.

“Mama wa Makahaba”

4, 5. “Babiloni Mukubwa” ni nini, na juu ya nini tunasema vile? (Ona picha ku mwanzo wa habari.)

4 Mu maono yenye Yesu alipatia mutume Yohana ku mwisho wa karne ya kwanza (1-100) K.K.Y., kahaba fulani anatokea. Anaitwa “kahaba mukubwa,” na pia “Babiloni Mukubwa, mama wa makahaba.” (Ufu. 17:1, 5) Mu miaka mingi, viongozi wa dini na watu wenye elimu mingi ya Biblia wameshindwa kuelewa kama ule kahaba ni nani. Wengine wamesema ni Babiloni, wengine Roma, ao Kanisa Katoliki la Roma. Lakini, tangu miaka mingi, Mashahidi wa Yehova wameelewa kama huyu “kahaba mukubwa” ni nani kabisa. Ni dini zote za uongo. Juu ya nini tunasema vile?

5 Ule kahaba anahukumiwa juu anafanya uasherati na “wafalme wa dunia,” ao guvernema za dunia. Ile inaonyesha waziwazi kama ule kahaba haiko guvernema za dunia. Tena, Ufunuo inaonyesha kama “wafanyabiashara wa dunia,” ao matengenezo ya biashara ya dunia hii, wanalia sana wakati Babiloni Mukubwa anaharibiwa. Kwa hiyo, Babiloni Mukubwa hawezi kufananisha mufumo wa biashara. Sasa, ni nani? Anashitakiwa kuwa na “mazoea ya kupashana habari na pepo wachafu,” kufanya ibada ya sanamu, na kudanganya watu. Je, hauone kama matengenezo ya dini yenye kupotoka ya dunia hii njo yenye iko inafanya ile mambo? Ona pia kwamba, Biblia inasema kama ule kahaba anapanda juu ya munyama wa pori, ao anaongoza kwa kiasi fulani, watawala wa dunia hii. Tena, anatesa watumishi waaminifu wa Yehova. (Ufu. 17:2, 3; 18:11, 23, 24) Je, hauone kama ile njo mambo yenye dini ya uongo iko inafanya kabisa, mupaka leo?

Babeli ya zamani, yenye kisha wakati fulani iliitwa Babiloni, ilitokeza kila namna ya desturi, mafundisho, na matengenezo ya dini ya uongo (Ona fungu la 6)

6. Juu ya nini Babiloni Mukubwa anaitwa “mama wa makahaba”?

6 Sasa, juu ya nini Babiloni Mukubwa anaitwa “kahaba mukubwa” na tena “mama wa makahaba”? Juu, dini ya uongo iko na migawanyiko yenye hauwezi kuhesabia. Kuko makanisa, mazehebu, vikundi-vikundi vyenye hauwezi kuhesabia. Tangu wakati luga zilivurugwa mu Babeli ya zamani, ao Babiloni, mafundisho na desturi za dini ya uongo za kila namna zimeenea mu dunia yote, na ile imezaa dini ya kila namna. “Babiloni Mukubwa” inatokana na jina la muji wa Babiloni, ile inafaa kabisa sababu pale njo dini mingi za uongo zilianzia! (Mwa. 11:1-9) Kwa hiyo, zile dini zote zinaweza kuonwa kuwa “mabinti” wa tengenezo moja, wa kahaba moja mukubwa. Shetani anatumia mara mingi zile dini juu ya kuingiza watu mu mazoea ya kupashana habari na pepo wachafu, ibada ya sanamu, na mafundisho na desturi zingine zenye zinamuvunjia Mungu heshima. Njo maana Mungu iko na sheria ya kuonya hivi watu wake kuhusu ile tengenezo yenye kupotoka, yenye iko mu dunia yote: “Mutoke kwake, watu wangu, kama hamutaki kushiriki pamoja naye katika zambi zake”!​—Soma Ufunuo 18:4, 5.

7. Juu ya nini tunatii onyo ya ‘kutoka’ mu Babiloni Mukubwa?

7 Je, ulishatii ile onyo? Kumbuka, Yehova njo aliumbaka wanadamu wakiwa na “uhitaji wa kiroho.” (Mt. 5:3) Ni ibada safi ya Yehova peke yake njo inaweza kutimiza ile uhitaji. Watumishi wa Yehova wanapenda kubakia mbali na ukahaba wa kiroho kadiri inawezekana. Lakini, Shetani Ibilisi iko na mawazo tofauti. Anapenda kuchochea watu wa Mungu juu waangukie mu ukahaba wa kiroho. Na mara mingi, ameweza kufanya vile. Kufikia wakati wa Ezekieli, watu wa Mungu walikuwa wameangukia mara mingi mu ukahaba wa kiroho. Ni muzuri tuchunguze historia yao, sababu inaweza kutufundisha mambo mingi kuhusu kanuni za Yehova, haki yake, na rehema yake.

“Ukakuwa Kahaba”

8-10. Ni jambo gani la maana lenye ibada safi inaomba lenye linatusaidia kuelewa mawazo ya Yehova kuhusu kushirikiana na dini ya uongo? Toa mufano.

8 Mu kitabu cha Ezekieli, Yehova anatumia mufano wa kahaba mu njia yenye inaonyesha namna yeye mwenyewe anajisikia. Ezekieli aliongozwa na roho ya Mungu kuandika habari mbili zenye kuonyesha waziwazi namna Yehova aliumia sana na kujisikia kuwa amesalitiwa wakati watu wake walikosa uaminifu na kujiendesha mubaya. Juu ya nini aliwalinganisha na makahaba?

9 Juu tuelewe, tunapaswa kwanza kukumbuka jambo moja la maana sana lenye ibada safi inaomba lenye tulizungumuzia mu Sura ya 5 ya kitabu hiki. Mu Sheria yenye alipatia Israeli, Yehova alisema: “Haupaswe kuwa na miungu mingine isipokuwa mimi [ao, “tofauti na mimi,” maelezo ya chini]. . . . Mimi, Yehova Mungu wako, ni Mungu mwenye anataka watu washikamane na yeye tu.” (Kut. 20:3, 5) Kisha wakati fulani, alikazia ile jambo kwa kusema: “Hamupaswe kuinamia mungu mwingine, kwa sababu Yehova anajulikana kuwa Mungu mwenye kutaka watu washikamane na yeye tu. Ndiyo, yeye ni Mungu mwenye anataka watu washikamane na yeye tu.” (Kut. 34:14) Mawazo ya Yehova iko wazi kabisa. Kusudi Yehova akubali ibada yetu, tunapaswa kumuabudu yeye tu.

10 Tukamate mufano wa ndoa. Bwana na bibi wako na haki ya kutazamia kama kila mumoja wao hana mutu mwingine pembeni. Kama mumoja wao anaanza kupendezwa kimapenzi na mutu fulani mwenye haiko bibi ao bwana yake, mwenzake iko na haki ya kusikia wivu na kujisikia kuwa amesalitiwa. (Soma Waebrania 13:4.) Vilevile, kuhusu ibada, Yehova anajisikiaka kuwa amesalitiwa wakati watu wake, wenye wamejitoa juu ya kumutumikia yeye tu, wanageuka na kuabudu miungu ya uongo. Anazungumuzia kwa uzito namna yeye mwenyewe alijisikia kuwa amesalitiwa mu Ezekieli sura ya 16.

11. Yehova alitoa habari gani kuhusu Yerusalemu na mwanzo wake?

11 Sura ya 16 ya Ezekieli iko na ile tunaweza kuita kuwa hotuba ya murefu sana ya Yehova mu kitabu cha Ezekieli​—na moja kati ya maunabii ya murefu sana mu Maandiko yote ya Kiebrania. Yehova anazungumuzia muji wa Yerusalemu juu ya kufananisha Yuda yenye inakosa uaminifu. Anaeleza mambo fulani ya kuleta huzuni na ya kuchukiza kuhusu mwanzo wa Yuda na namna ilimusaliti. Ku mwanzo, Yuda ilikuwa sawa vile mutoto mwenye aliachwa, muchafu na mwenye hana mutu wa kumuhangaikia. Wazazi wake walikuwa Wakanaani wapagani wa inchi. Ni kweli, mu miaka mingi, Yerusalemu ilikuwa inatawaliwa na kabila la Kanaani la Wayebusi, mupaka wakati Daudi alishinda ile muji. Yehova alisikilia huruma ule mutoto mwenye alikuwa ameachwa, akamusafisha na kumupatia mambo yenye alikuwa nayo lazima. Kisha, Yuda ilifikia kuwa kama bibi ya Yehova. Kusema kweli, Waisraeli wenye kisha wakati fulani walikaa mu ile muji walikuwa mu uhusiano wa agano na Yehova, uhusiano wenye walikubali kwa kujipendea mu siku za Musa. (Kut. 24:7, 8) Kisha Yerusalemu kuwa muji mukubwa wa inchi, Yehova aliibariki, aliipatia utajiri, aliifanya ikuwe muji wa kupendeza, aliifanyia mambo mingi ya muzuri sawa vile bwana tajiri na mwenye uwezo anaweza kupatia bibi yake mapambo ya kupendeza.​—Eze. 16:1-14.

Sulemani aliacha wanamuke wake wa kigeni wamuchochee achafue Yerusalemu kupitia ibada ya sanamu (Ona fungu la 12)

12. Namna gani ukosefu wa uaminifu uliingia mu Yerusalemu?

12 Ona yenye ilitokea kisha. Yehova alisema: “Ulianza kutegemea uzuri wako, na ukakuwa kahaba kwa sababu ya sifa yako. Ulimwanga matendo yako ya ukahaba kwa kila mupita-njia, na uzuri wako ukakuwa wake.” (Eze. 16:15) Mu siku za Sulemani, Yehova alibariki na kufanya watu wake wakuwe matajiri kiasi ya kwamba Yerusalemu ikafikia kuwa muji wenye kupendeza sana, muji muzuri sana mu dunia yote ya zamani. (1 Fa. 10:23, 27) Lakini polepole watu walianza kukosa uaminifu. Juu ya kutafuta kufurahisha bibi zake wengi, Sulemani alianza kuchafua Yerusalemu kupitia ibada ya miungu ya kipagani. (1 Fa. 11:1-8) Na wenye walitawala kisha yeye walifanya mambo ya mubaya hata zaidi, na walifikia kuchafua inchi yote kupitia ibada ya uongo. Yehova alijisikia namna gani kuhusu ile matendo ya ukahaba na ya kumusaliti? Alisema: “Mambo hayo hayapaswe kufanyika, wala hayapaswe kutokea hata kidogo.” (Eze. 16:16) Lakini watu wake waasi waliendelea kuzama mu mwenendo mupotovu!

Waisraeli fulani walitoa watoto wao kuwa zabihu kwa miungu ya uongo, sawa vile Moleki

13. Watu wa Mungu mu Yerusalemu walifanya matendo gani ya uovu?

13 Wazia huzuni na chuki ya Yehova wakati alifunua waziwazi uovu wa watu wake wenye alichagua: “Ulikamata watoto wako wanaume na watoto wako wanamuke wenye ulikuwa umenizalia, na ukawatoa zabihu kwa sanamu hizo ili wamezwe​—je, matendo yako ya ukahaba hayajaenda mbali sana? Ulichinja wana wangu, na ukawatoa kuwa zabihu kwa kuwapitisha katika moto.” (Eze. 16:20, 21) Mambo ya kuchukiza sana yenye watu wa Yerusalemu walifanya inaonyesha namna moyo wa Shetani ni muovu sana. Anapenda sana kuchochea watu wa Yehova wafanye matendo ya kuchukiza! Lakini Yehova anaona yote. Mungu anaweza kuondoa matendo yote ya uovu ya Shetani, hata ikuwe ya uovu wa namna gani, na atatenda haki.​—Soma Yobu 34:24.

14. Mu mufano wa Yehova, dada wawili wa Yerusalemu walikuwa nani, na ni nani alifikia kuwa muovu sana kati yao watatu?

14 Lakini Yerusalemu, hakuchukizwa hata kidogo na uovu wake. Aliendelea na ukahaba wake. Yehova alisema kama Yerusalemu alitenda bila haya ukahaba kuliko makahaba wengine sababu ni yeye njo alikuwa analipa watu juu wafanye naye uasherati! (Eze. 16:34) Mungu alisema kama Yerusalemu alikuwa sawa vile “mama” yake, ni kusema, makabila ya kipagani yenye ilikuwa inatawala inchi zamani. (Eze. 16:44, 45) Mu kuendelea na mufano wa familia, anasema kama dada mukubwa wa Yerusalemu alikuwa Samaria, mwenye alimutangulia mu maisha ya ukahaba wa kiroho. Mungu alitaja pia dada wa pili, Sodoma, yenye inatumiwa hapa mu njia ya mufano sababu ilikuwa imeharibiwa zamani juu ya kiburi na mwenendo wake mubaya sana. Wazo lenye Yehova alitaka kuonyesha ni hili: Yerusalemu alifanya uovu sana kupita dada zake wawili, Samaria na hata Sodoma! (Eze. 16:46-50) Watu wa Mungu walipuuza maonyo mingi yenye walipewa na waliendelea na mwenendo wao wa kuchukiza.

15. Yehova alikuwa na kusudi gani wakati aliteta hukumu juu ya Yerusalemu, na ile ilitoa tumaini gani?

15 Yehova angefanya nini? Alipatia Yerusalemu ahadi hii: “Ninakusanya pamoja wote wenye kukupenda wenye umewapatia raha” na, “nitakutia katika mukono wao.” Wapagani wenye walishirikiana na watu wake zamani wangemuharibu, wangemuondolea uzuri wake na vitu vyake vya samani. Alisema: “Watakupiga majiwe na kukuchinja kwa panga zao.” Yehova alikuwa na kusudi gani wakati alileta ile hukumu? Kusudi lake halikukuwa kumaliza kabisa watu wake. Lakini alionyesha kusudi lake kwa kusema: “Nitakomesha ukahaba wako.” Mungu aliongeza: “Nitatosheleza kasirani yangu kali juu yako, na gazabu yangu itageuka kutoka kwako; na nitatulia na sitajisikia tena kuwa nimekosewa.” Kama vile tuliona mu Sura ya 9 ya kitabu hiki, kusudi la Yehova mu ile wakati yote lilikuwa kurudisha watu wake mu hali ya muzuri kisha uhamisho wao. Juu ya nini? Alisema: “Mimi mwenyewe nitakumbuka agano lenye nilifanya pamoja na wewe katika siku za ujana wako.” (Eze. 16:37-42, 60) Tofauti na watu wake, Yehova angeendelea kuwa muaminifu kabisa!​—Soma Ufunuo 15:4.

16, 17. (a) Juu ya nini hatuseme tena kama Ohola na Oholiba wanafananisha Dini Zenye Kujiita Kuwa za Kikristo? (Ona kisanduku “Dada Makahaba.”) (b) Ni somo gani tunaweza kupata mu Ezekieli sura ya 16 na 23?

16 Kupitia hotuba yake ya murefu na yenye mawazo mazito yenye kuandikwa mu Ezekieli sura ya 16, Yehova anatufundisha mambo mingi kuhusu kanuni zake zenye kunyooka, haki yake na rehema yake mingi. Tunajifunza vile pia mu Ezekieli sura ya 23. Leo, Wakristo wa kweli wanachukua kwa uzito maneno yenye iko wazi yenye Yehova alisema kuhusu ukahaba wa watu wake. Hatupendi hata kidogo kumuhuzunisha Yehova sawa vile Yuda na Yerusalemu walifanya! Kwa hiyo, tunapaswa kuepuka kabisa kila namna ya ibada ya sanamu. Ile inatia ndani pupa, kutafuta sana vitu vya kimwili, yenye ni aina ya ibada ya sanamu. (Mt. 6:24; Kol. 3:5) Tunataka kuendelea kuwa na shukrani sababu kwa rehema yake, Yehova amerudisha ibada safi mu siku hizi za mwisho na hataacha hata kidogo ichafuliwe tena! Amefanya “agano la kudumu” na Israeli wa kiroho lenye hakuna siku litafikia kuvunjwa juu ya ukosefu wa uaminifu wala ukahaba. (Eze. 16:60) Tufurahie basi pendeleo lenye tuko nalo leo la kushirikiana na watu wa Yehova wenye wako safi.

17 Lakini, maneno ya Yehova kuhusu makahaba yenye kuzungumuziwa mu Ezekieli inatufundisha nini kuhusu “kahaba mukubwa,” ao Babiloni Mukubwa? Acha tuone.

‘Hatapatikana Tena Hata Kidogo’

18, 19. Kuko mambo gani yenye inafanana kati ya makahaba wa mu Ezekieli na kahaba wa mu Ufunuo?

18 Yehova habadilikake. (Yak. 1:17) Mawazo yake juu ya dini ya uongo haijabadilikaka. Kwa hiyo, hatushangae kuona mambo mingi yenye inafanana kati ya hukumu yenye alitoa juu ya makahaba wa mu kitabu cha Ezekieli na uharibifu wenye unangojea “kahaba mukubwa” wa mu kitabu cha Ufunuo.

19 Kwa mufano, azabu yenye makahaba wa mu unabii wa Ezekieli walipata, haikutoka moja kwa moja kwa Yehova, lakini ilitoka kwa mataifa yenye watu wa Mungu wenye kukosa uaminifu walikuwa wanafanya nayo uasherati wa kiroho. Vilevile, dini za uongo za dunia zitahukumiwa sababu zinafanya uasherati wa kiroho na “wafalme wa dunia.” Lakini azabu yenye zitapata itatoka wapi? Tunasoma kwamba viongozi wa guvernema “watamuchukia ule kahaba na kumuacha bila kitu na uchi, na watakula nyama yake na kumuteketeza kabisa kwa moto.” Juu ya nini guvernema za dunia zitafikia kufanya jambo la kushangaza vile? Juu, Mungu “[atatia] jambo hilo ndani ya mioyo yao ili kutimiza wazo lake.”​—Ufu. 17:1-3, 15-17.

20. Ni nini inaonyesha kama hukumu juu ya Babiloni itakuwa ya mwisho kabisa?

20 Kwa hiyo, Yehova atatumia mataifa ya dunia hii juu ya kuleta hukumu yake juu ya dini zote za uongo, kutia ndani Dini mingi Zenye Kujiita Kuwa za Kikristo. Ile hukumu itakuwa ya mwisho kabisa; hakutakuwa huruma, dini ya uongo haitapewa wakati wa kubadilisha matendo yake. Ufunuo inaonyesha kwamba Babiloni ‘hatapatikana tena hata kidogo.’ (Ufu. 18:21) Malaika wa Mungu watashangilia wakati Babiloni Mukubwa ataharibiwa, watasema: “Mumusifu Yah! Na moshi kutoka kwake unaendelea kupanda milele na milele.” (Ufu. 19:3) Ile itakuwa hukumu ya milele. Hakuna dini yoyote ya uongo yenye itaruhusiwa kutokea na kuchafua ibada safi. Mu njia ya mufano, hukumu kali na uharibifu wenye Babiloni atapata itatosha moshi wenye utaendelea kupanda juu milele.

Mataifa yenye Babiloni Mukubwa alichochea na kuongoza mu miaka mingi itamugeukia na kumuharibu (Ona fungu la 19, 20)

21. Uharibifu wa dini ya uongo utakuwa mwanzo wa kipindi gani, na ile kipindi itaisha namna gani?

21 Wakati guvernema za dunia hii zitageukia Babiloni Mukubwa, zitakuwa zinatimiza hukumu ya Mungu, na ile itakuwa tukio kubwa katika utimizo wa kusudi la Yehova. Ile tukio itakuwa mwanzo wa taabu kubwa, wakati wa musukosuko wenye hauyakuwaka. (Mt. 24:21) Ile taabu kubwa itaishia ku Armagedoni, vita ya Yehova ya kuharibu mupangilio huu muovu wa mambo. (Ufu. 16:14, 16) Kama vile sura za kufuata za kitabu hiki zitaonyesha, kitabu cha Ezekieli kiko na mambo mingi ya kutuambia kuhusu namna taabu kubwa itaanza. Lakini mbele ya kufika kule, ni somo gani zenye tunatosha mu Ezekieli sura ya 16 na 23 zenye tunataka kuchunga mu akili na kutumikisha?

Guvernema za dunia hii zitageukia Babiloni Mukubwa, na ile itakuwa kutimiza hukumu ya Mungu (Ona fungu la 21)

22, 23. Kuzungumuzia habari za makahaba mu Ezekieli na Ufunuo kunapaswa kutupatia mawazo gani kuhusu utumishi wetu mutakatifu?

22 Shetani anapenda kupotosha wale wenye wanafanya ibada safi. Hakuna kitu kinaweza kumufurahisha sawa vile kupata nafasi ya kutukokota mbali na ibada safi na kutuingiza mu mwenendo sawa ule wa makahaba wa mu kitabu cha Ezekieli. Kwa hiyo, tunapaswa kukumbuka kwamba Yehova havumilie ushindani wowote mu mambo ya ibada, havumilie matendo yoyote ya kukosa uaminifu! (Hes. 25:11) Tunapaswa kuendelea kujitenga na ibada ya uongo, hatupaswe ‘kugusa kitu chochote kichafu’ ku macho ya Mungu. (Isa. 52:11) Vilevile, tunaendelea kuonyesha uaminifu kwa kuepuka kuunga mukono upande wowote mu mivurugo ya politike ao vita za dunia hii yenye kujaa migawanyiko. (Yoh. 15:19) Tunaona mutu kujivunia sana inchi yake kuwa dini ingine ya uongo yenye Shetani anaendelesha, na tunaiepuka.

23 Zaidi ya yote, tusisahau kama tuko na pendeleo kubwa la kumuabudu Yehova mu hekalu lake la kiroho, lenye liko safi na takatifu. Kadiri tunaendelea kufurahia ile mupango yenye kubarikiwa, tuendelee basi kuazimia kuepuka uhusiano wowote na dini ya uongo na ukahaba wake!