Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 9

“Nitawapatia Moyo Wenye Kuunganishwa”

“Nitawapatia Moyo Wenye Kuunganishwa”

EZEKIELI 11:19

WAZO KUBWA: Habari kuhusu kurudishwa kwa watu wa Mungu mu inchi yao na namna inazungumuziwa mu maunabii ya Ezekieli

1-3. Namna gani Wababiloni walichekelea waabudu wa Yehova, na juu ya nini?

WAZIA kama uko Muyahudi muaminifu mwenye anaishi mu muji wa Babiloni. Watu wa taifa lenu wamekuwa mu uhamisho miaka makumi tano hivi. Kama vile unazoea kufanya siku ya Sabato, unaenda kukutana na waamini wenzako juu ya kumuabudu Yehova. Wakati unapita mu barabara zenye kujaa watu, unaona mahekalu ya munene-munene na pia fasi zenye kuonwa kuwa takatifu zenye hauwezi kuhesabia. Watu wengi wanakutana ku zile fasi juu ya kutoa matoleo na kuimbia miungu nyimbo, kama vile mungu Marduki.

2 Wakati unakuwa mbali kidogo na vile vikundi vya watu, unakutana na kikundi kidogo cha waabudu wenzako. * Munapata fasi ya kimya​—pengine pembeni ya moja kati ya mifereji ya muji—​kwenye munaweza kusali, kuimba zaburi, na kufikiri pamoja juu ya Neno la Mungu. Wakati munasali pamoja, munasikia makelele kidogo-kidogo ya mashua za mbao zenye zimetia nanga pembeni-pembeni ya mufereji wa maji. Munatulia sababu pale ni fasi ya kimya. Munatumaini kama watu wa ile fasi hawatajua kwenye muko na hawatakuja kuvuruga mukutano wenu kama vile wanazoea kufanya. Juu ya nini wanazoea kufanya vile?

3 Babiloni imeshinda vita mingi, na wakaaji wake wanaamini kama muji wao uko nguvu sababu ya miungu yao ya uongo. Kulingana na mawazo ya Wababiloni, kuharibiwa kwa Yerusalemu kunaonyesha kama mungu wao Marduki iko na nguvu sana kupita Yehova! Kwa hiyo, wanachekelea Mungu wenu na watu wake. Wakati fulani, juu ya kuwachekelea, wanasema hivi: “Mutuimbie moja ya nyimbo za Sayuni”! (Zb. 137:3) Zaburi mingi zinatukuza ushindi wa Sayuni juu ya maadui wa Yehova. Pengine Wababiloni wanapenda kuchekelea zaidi sana maneno ya zile zaburi. Lakini zaburi zingine, zinazungumuzia Wababiloni wenyewe. Kwa mufano, zaburi moja inasema: “Mataifa . . . yamegeuza Yerusalemu kuwa rundo la mabomoko. . . . Wale wenye kutuzunguka wanatuzihaki na kutuchekelea.”​—Zb. 79:1, 3, 4.

4, 5. Unabii wa Ezekieli ulitoa ujumbe gani wa tumaini, na tutazungumuzia nini mu sura hii? (Ona picha ku mwanzo wa habari.)

4 Kuko pia Wayahudi waasi-imani, wenye wako haraka kukuchekelea juu unamuamini Yehova na manabii wake. Hata kama wanakuchekelea vile, ibada safi inakuletea wewe na familia yako kitulizo. Kusali na kuimba pamoja kunafurahisha. Kusoma Neno la Mungu kunatuliza. (Zb. 94:19; Ro. 15:4) Wazia kwamba ile siku, mumoja wa waabudu wenzako ameleta kitu fulani cha pekee ku mukutano wenu​—kitabu cha kukunjwa cha unabii wa Ezekieli. Unapenda kusikia ahadi ya Yehova yenye inasema kama atarudisha watu wake mu inchi yao. Moyo wako unachangamuka wakati unabii sawa ule unasomwa kwa sauti ya juu, na unafikiria namna siku moja wewe na familia yako munaweza kurudia kwenu na kusaidia mu ile wakati ya muzuri sana ya kurudia mu inchi yenu!

5 Unabii wa Ezekieli unajaa sana ahadi za kurudishwa kwa watu wa Mungu mu inchi yao. Tuzungumuzie ile habari yenye kuleta tumaini. Namna gani zile ahadi zilitimia kuhusu wahamishwa? Ile maunabii inatimia namna gani wakati wetu? Tutazungumuzia pia namna itatimia wakati wenye kuja.

“Wataenda Katika Uhamisho, Katika Utekwa”

6. Namna gani Mungu alionya tena na tena watu wake wenye kuasi?

6 Kupitia Ezekieli, Yehova aliambia waziwazi watu wake namna atawapatia azabu juu ya mwenendo wao wa uasi. Yehova alisema: “Wataenda katika uhamisho, katika utekwa.” (Eze. 12:11) Kama vile tuliona mu Sura ya 6 ya kitabu hiki, Ezekieli hata alionyesha namna ile hukumu itakuwa. Lakini ile haikukuwa mara ya kwanza Waisraeli kupewa onyo ya vile. Tangu siku za Musa, karibu miaka elfu moja mbele, Yehova alikuwa ameonya watu wake kama ikiwa wangeendelea kuasi, wangepelekwa mu uhamisho. (Kum. 28:36, 37) Manabii sawa vile Isaya na Yeremia walitoa maonyo ya vile.​—Isa. 39:5-7; Yer. 20:3-6.

7. Ni mu njia gani Yehova alileta azabu juu ya watu wake?

7 Lakini, ya kuhuzunisha ni kwamba, wengi walifunga masikio. Kisha, Yehova aliumia mu moyo wake juu ya uasi wa watu wake, ibada yao ya sanamu, hali yao ya kukosa uaminifu, upotovu wao kwa sababu ya kuchochewa na wachungaji wabaya. Kwa hiyo, aliwaacha wapatwe na njaa, na ile njaa ilikuwa musiba na jambo la haya, sababu mbele ya pale, inchi yao ilikuwa “inchi yenye kutiririka maziwa na asali.” (Eze. 20:6, 7) Kisha, kama vile alikuwa ametabiri zamani, Yehova aliruhusu watu wake wenye kuasi wapewe azabu ya kupelekwa mu uhamisho. Mu mwaka wa 607 M.K.Y., Nebukadneza wa Babiloni alishambulia kwa mara ya mwisho, kwa kuharibu Yerusalemu na hekalu lake. Wayahudi wengi sana wenye waliokoka walipelekwa mu uhamisho kule Babiloni. Wakati walifika Babiloni, watu waliwacheka na kuwapinga kama vile inaonyeshwa ku mwanzo wa sura hii.

8, 9. Namna gani Mungu alipatia kutaniko la Kikristo maonyo kuhusu uasi-imani?

8 Je, kutaniko la Kikristo limekwisha kupatwa na jambo lenye kufanana na uhamisho wa Babiloni? Ndiyo kabisa! Kama vile Wayahudi wa zamani, wafuasi wa Kristo walipewa maonyo mbele ya wakati. Ku mwanzo-mwanzo tu wa utumishi wake, Yesu alisema: “Mufanye angalisho na manabii wa uongo wenye wanakuja kwenu katika ngozi ya kondoo, lakini ndani wao ni imbwa wa pori wakali.” (Mt. 7:15) Kisha miaka fulani, roho ya Mungu iliongoza mutume Paulo atoe onyo ya vile, kwa kusema: “Ninajua kwamba kisha mimi kuondoka imbwa wa pori wenye kukandamiza wataingia katikati yenu na hawatatendea kundi kwa upole wote, na kutoka katikati yenu wenyewe, watu watasimama na kusema mambo yenye kupotoka ili kuvuta wanafunzi wawafuate.”​—Mdo. 20:29, 30.

9 Wakristo walifundishwa namna ya kutambua na kuepuka watu kama wale, wenye kuwa hatari. Wazee Wakristo waliagizwa kuondoa waasi-imani mu kutaniko. (1 Ti. 1:19; 2 Ti. 2:16-19; 2 Pe. 2:1-3; 2 Yo. 10) Ijapokuwa vile, kama vile ilikuwa kuhusu Israeli na Yuda ya zamani, pole kwa pole Wakristo wengi walifunga masikio na hawakusikiliza ile maonyo yenye upendo. Ku mwisho wa karne ya kwanza (1-100), uasi-imani ulikuwa umetia mizizi mu kutaniko. Yohana, mutume wa mwisho mwenye alikuwa angali muzima ku mwisho wa karne ya kwanza (1-100) K.K.Y., alitambua kama upotovu na uasi mwingi ulikuwa umeenea mu kutaniko. Yeye tu njo alikuwa angali anazuia ile hali ya mubaya isiingie mu kutaniko. (2 Te. 2:6-8; 1 Yo. 2:18) Ni nini ilitokea kisha kifo cha Yohana?

10, 11. Mufano wa Yesu wa ngano na magugu ulitimia namna gani kuanzia karne ya pili K.K.Y. na kuendelea?

10 Kisha kifo cha Yohana, mufano wa Yesu wa ngano na magugu ulianza kutimia. (Soma Matayo 13:24-30.) Kama vile Yesu alikuwa ametangulia kuona, Shetani alipanda “magugu,” ao Wakristo wa uongo mu kutaniko, na kutaniko lilianza kuharibika haraka. Bila shaka Yehova aliumia sana mu moyo wake wakati aliona kutaniko lenye Mwana wake alianzisha linachafuliwa na ibada ya sanamu, sikukuu na desturi za kipagani, na mafundisho ya uongo ya wanafilozofia wenye hawamuogope Mungu na kuchafuliwa pia na mafundisho ya dini za Shetani! Yehova alifanya nini? Kama vile alitendea Waisraeli wenye hawakukuwa waaminifu, Yehova aliacha watu wake waende mu uhamisho. Kuanzia wakati fulani mu karne ya pili (101-200) K.K.Y. na kuendelea, haikukuwa mwepesi kutambua Wakristo wa kweli wenye kufananishwa na ngano kati ya Wakristo wa uongo. Kwa kweli, kutaniko la Kikristo lilikuwa katika uhamisho mu Babiloni Mukubwa, ni kusema, dini zote za uongo, na ile Babiloni Mukubwa yenye kupotoka ilimeza Wakristo wa uongo. Kadiri Wakristo wa uongo waliendelea kuongezeka, Dini Zenye Kujiita Kuwa za Kikristo zilitokea.

11 Mu ile miaka ya giza yenye Dini Zenye Kujiita Kuwa za Kikristo zilikuwa zimetia mizizi kabisa, kulikuwa Wakristo fulani wa kweli, ni kusema, “ngano” yenye kutajwa mu mufano wa Yesu. Kama vile Wayahudi wahamishwa wenye kuzungumuziwa mu Ezekieli 6:9, wale Wakristo wa kweli walimukumbuka Mungu wa kweli. Wamoja walipinga bila woga mafundisho ya uongo ya Dini Zenye Kujiita Kuwa za Kikristo. Watu waliwacheka na kuwatesa. Je, nia ya Yehova ilikuwa kuacha watu wake milele mu ile giza ya kiroho? Hapana! Kama vile ilikuwa kuhusu Waisraeli wa zamani, Yehova alionyesha kasirani yake kwa kiasi chenye kufaa na kwa kipindi cha wakati chenye kufaa. (Yer. 46:28) Tena, Yehova hakuacha watu wake bila tumaini. Tuzungumuzie tena wale Wayahudi wenye walikuwa mu uhamisho mu Babiloni ya zamani na tuone namna Yehova aliwapatia ujumbe wa tumaini wenye kuonyesha kama utekwa wao ungekuwa na mwisho.

Mu miaka mingi, Babiloni Mukubwa ilitesa Wakristo wa kweli (Ona fungu la 10, 11)

“Hasira Yangu Itafika Mwisho”

12, 13. Ni nini ingefanya kasirani ya Yehova kuhusu watu wake wahamishwa wa siku za Ezekieli itulie?

12 Yehova hakuficha kasirani yake kuelekea watu wake, lakini pia aliwahakikishia kama kasirani yake kali ya haki haitaendelea milele. Ona kwa mufano, maneno hii: “Hasira yangu itafika mwisho, na kasirani yangu kali juu yao itatulia, na nitatosheka. Nao watalazimika kujua kwamba mimi, Yehova, nimesema kwa kukazia kwamba watu washikamane na mimi tu, wakati nitamaliza kumwanga kasirani yangu kali juu yao.” (Eze. 5:13) Juu ya nini kasirani kali ya Yehova ingetulia?

13 Kati ya watekwa kulikuwa Wayahudi waaminifu wenye walipelekwa mu uhamisho pamoja na wenzao wenye hawakukuwa waaminifu. Zaidi ya ile, kupitia Ezekieli, Mungu alitabiri kama wamoja kati ya watu Wake wangetubu wakati wangekuwa mu uhamisho. Wale Wayahudi wenye kutubu wangeeleza mambo ya haya yenye walikuwa wamefanya juu ya kumuasi Mungu wao, na wangemulilia Yehova awasamehe na kuwaonyesha wema. (Eze. 6:8-10; 12:16) Ezekieli alikuwa kati ya wale wenye walikuwa waaminifu, na pia nabii Danieli na wenzake watatu. Tena, Danieli aliishi miaka mingi mupaka kufikia kuona mwanzo na mwisho wa uhamisho. Sala yake ya kutubu ya kutoka mu moyo, yenye alitoa kwa sababu ya zambi za Israeli iko mu Danieli sura ya 9. Kwa kweli, maneno yake ilionyesha hisia za wahamishwa wengi wenye walitamani sana Yehova awasamehe na kuwabariki tena. Bila shaka, ahadi za Ezekieli zenye ziliongozwa na roho ya Mungu kuhusu kuachiliwa huru na kurudishwa kwa watu wa Mungu mu inchi yao zilikuwa za kupendeza kabisa!

14. Juu ya nini Yehova angerudisha watu wake mu inchi yao?

14 Lakini, kulikuwa jambo fulani la maana sana kuhusu kuachiliwa huru na kurudishwa kwa watu wa Yehova mu inchi yao. Uhamisho wao wa siku mingi ungefikia mwisho, hapana kwa sababu walistahili kuachiliwa huru, lakini kwa sababu ilikuwa tena wakati wa Yehova kutakasa jina lake mwenyewe mbele ya mataifa yote. (Eze. 36:22) Kwa mwisho, wale Wababiloni wangefikia kujua kabisa kama miungu yao ya kishetani, sawa vile Marduki, haiko kitu mbele ya Bwana Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi Yehova! Tuzungumuzie basi ahadi tano zenye Yehova alimuongoza Ezekieli atolee wahamishwa wenzake. Kwanza, tuzungumuzie namna kila ahadi ilitimia juu ya wale Wayahudi waaminifu. Kisha, tutaona namna gani zile ahadi zilitimia mu njia kubwa zaidi.

15. Ni mabadiliko gani ilipaswa kufanywa kuhusiana na desturi za Wayahudi wenye walirudia mu inchi yao?

15 AHADI YA 1. Hakutakuwa tena ibada ya sanamu na desturi zingine za kuchukiza zenye zinahusiana na dini ya uongo. (Soma Ezekieli 11:18; 12:24.) Kama vile Sura ya 5 ya kitabu hiki inaonyesha, Yerusalemu na hekalu lake ilikuwa imechafuliwa na desturi za dini ya uongo, sawa vile ibada ya sanamu. Kwa hiyo, watu walipotoka, na kujitenga na Yehova. Kupitia Ezekieli, Yehova alitabiri kwamba kuko wakati wahamishwa watafanya tena ibada safi, yenye haina uchafu. Baraka zingine zote za kurudishwa kwa watu wa Mungu mu inchi yao zingekuja kama tu mupango wa Mungu kwa ajili ya ibada safi ungerudishwa.

16. Yehova alitoa ahadi gani kuhusu inchi ya watu wake?

16 AHADI YA 2. Wahamishwa watarudia mu inchi yao. Yehova aliambia wahamishwa hivi: “Nitawapatia inchi ya Israeli.” (Eze. 11:17) Ile ilikuwa ahadi ya muzuri sana, sababu Wababiloni, wenye walikuwa wanachokoza watu wa Mungu wenye walitekwa, hawakupatia wahamishwa tumaini lolote la kwamba kuko siku watarudiaka mu inchi yao yenye walikuwa wanapenda sana. (Isa. 14:4, 17) Tena, kadiri wale wenye wangerudia mu inchi yao wangebakia waaminifu, inchi ingekuwa na mbolea na ingezaa sana chakula, kwa hiyo hawangekosa chakula na kazi ya kufanya. Haya yenye walipataka na njaa ingekuwa mambo ya zamani.​—Soma Ezekieli 36:30.

17. Ingekuwa namna gani kuhusu zabihu zenye watu wangemutolea Yehova?

17 AHADI YA 3. Matoleo ya zawadi itaanza tena kutolewa ku mazabahu ya Yehova. Kama vile Sura ya 2 ya kitabu hiki inaonyesha, kulingana na Sheria ya Musa, zabihu na matoleo ilikuwa sehemu ya maana sana ya ibada safi. Kadiri wahamishwa wenye walirudia mu inchi yao wangeendelea kuwa watiifu na kuwa safi kiroho, Yehova angekubali matoleo yao. Kwa hiyo, zambi zao zingeweza kufunikwa na wangeendelea kuwa na uhusiano wa karibu na Mungu wao. Yehova aliahidi hivi: “Nyumba yote ya Israeli, wao wote, watanitumikia katika inchi. Nitafurahishwa nao kule, na nitaomba michango yenu na matunda ya kwanza ya matoleo yenu, vitu vyenu vyote vitakatifu.” (Eze. 20:40) Ibada safi ingerudishwa kabisa, na ile ingeletea baraka watu wa Mungu.

18. Namna gani Yehova angechunga watu wake?

18 AHADI YA 4. Wachungaji wabaya wataondolewa. Watu wa Mungu waliharibika zaidi sana kwa sababu ya kuchochewa na viongozi wao wenye walikuwa wamepotoka. Yehova aliahidi kubadilisha ile hali. Kuhusu wale wachungaji wabaya, aliahidi hivi: “Nitawafukuza ili wasikulishe kondoo wangu . . . Nitakomboa kondoo wangu katika kinywa chao.” Lakini, Yehova alihakikishia watu wake waaminifu hivi: “Nitatunza kondoo wangu.” (Eze. 34:10, 12) Angefanya vile je? Angetumia wanaume waaminifu, washikamanifu kuwa wachungaji.

19. Yehova alitoa ahadi gani kuhusu umoja?

19 AHADI YA 5. Kutakuwa umoja kati ya waabudu wa Yehova. Wazia namna waabudu waaminifu walihuzunika wakati waliona mugawanyiko kati ya watu wa Mungu mbele wapelekwe mu uhamisho. Kwa sababu ya kuchochewa na manabii wa uongo na wachungaji wenye kupotoka, watu waliasi manabii waaminifu wenye walisema katika jina la Yehova; na hata watu waligawanyika mu vikundi-vikundi vyenye kupingana. Kwa hiyo, moja kati ya mambo ya kupendeza sana ya kurudishwa kwa watu wa Mungu mu inchi yao ni ahadi hii yenye ilitolewa kupitia Ezekieli: “Nitawapatia moyo wenye kuunganishwa, na nitatia roho mupya ndani yao.” (Eze. 11:19) Kadiri Wayahudi wenye walirudia mu inchi yao wangeendelea kuwa mu umoja na Yehova Mungu na mumoja na mwenzake, hakuna mupinzani mwenye angewashinda. Wakiwa taifa, wangemuletea tena Yehova utukufu kuliko kumufanya alaumiwe na kuzarauliwa.

20, 21. Ahadi za Mungu zilitimia namna gani juu ya wahamishwa wenye walirudia kwao?

20 Je, zile ahadi tano zilitimia juu ya Wayahudi wenye walirudia kutoka mu uhamisho? Ni muzuri tukumbuke maneno hii ya Yoshua, mwanaume muaminifu wa zamani, mwenye alisema: “Hakuna hata neno moja lenye halikutimia kati ya ahadi zote za muzuri zenye Yehova Mungu wenu aliwaahidi. Yote yametimia kwa ajili yenu. Hakuna hata neno moja kati ya maneno hayo lenye halikutimia.” (Yos. 23:14) Kama vile ilikuwa mu siku za Yoshua, ni vile pia ilikuwa mu siku za wahamishwa wenye walirudia mu inchi yao.

21 Wayahudi waliachana na ibada ya sanamu na desturi zingine za kuchukiza za dini ya uongo zenye zilikuwa zimewatenganisha na Yehova. Hata kama ingeonekana kuwa haiwezekane, walirudia na kuishi tena mu inchi yao, waliilima na kufurahia maisha ya muzuri kule. Moja kati ya mambo ya kwanza yenye walifanya ilikuwa kujenga tena mazabahu ya Yehova mu Yerusalemu na kutoa matoleo yenye kukubalika juu ya ile mazabahu. (Ezr. 3:2-6) Yehova aliwabariki kwa kuwapatia wachungaji wazuri wa kiroho, wanaume kama vile nabii muaminifu na mwandishi Ezra, magavana Nehemia na Zerubabeli, Kuhani Mukubwa Yoshua, na manabii hodari sawa vile Hagai, Zekaria, na Malaki. Kadiri watu waliendelea kufuata maagizo na muongozo wa Yehova, walikuwa na umoja wenye ulikuwa tofauti na ule wenye walikuwaka nao zamani, zamani sana.​—Isa. 61:1-4; soma Yeremia 3:15.

22. Ni nini inatusaidia kujua kama utimizo wa kwanza wa maunabii kuhusu kurudishwa kwa ibada safi ulikuwa unaonyesha kitu fulani kikubwa zaidi?

22 Bila shaka, utimizo wa kwanza wa ahadi za Yehova za kurudishwa kwa watu wa Mungu mu inchi yao ulikuwa wenye kutia moyo sana! Lakini, ule utimizo ulikuwa unaonyesha kitu fulani kikubwa zaidi chenye kingetokea kisha. Ni nini inafanya tuseme vile? Kwanza, zile ahadi zilikuwa na masharti fulani: Yehova angezitimiza kama tu watu wangeendelea kuwa watiifu na wasikivu. Kisha wakati fulani, Wayahudi walikosa tena kutii na wakakuwa waasi. Lakini kama vile Yoshua alionyesha, kile Yehova anasema hakikosake kutimia. Kwa hiyo, zile ahadi zingekuwa na utimizo mukubwa zaidi, wa kudumu sana. Tuone namna gani ile ilitokea.

“Nitafurahishwa na Ninyi”

23, 24. “Wakati wa kurudishwa kwa mambo yote” ulianza wakati gani na namna gani?

23 Sisi wanafunzi wa Biblia, tunajua kama mu mwaka wa 1914, ulimwengu huu muovu uliingia mu kipindi chake cha mwisho, mu siku zake za mwisho. Lakini, kwa watumishi wa Yehova, ile haiko kipindi ya kuhuzunisha. Biblia inaonyesha kama kipindi fulani chenye kufurahisha sana kilianza mu mwaka wa 1914, ni kusema, “wakati wa kurudishwa kwa mambo yote.” (Mdo. 3:21) Tunajua vile namna gani? Kwa kweli, ni nini ilitokea mbinguni mu mwaka wa 1914? Yesu Kristo aliwekwa kuwa Masiya-Mufalme! Namna gani ile tukio ilionyesha kama mambo imeanza kurudishwa mu hali ya muzuri? Kumbuka kwamba, Yehova aliahidi Mufalme Daudi kwamba ufalme utadumu milele mu jamaa yake. (1 Ny. 17:11-14) Ile ufalme ilikatizwa mu mwaka wa 607 M.K.Y. wakati Wababiloni waliharibu Yerusalemu na kukomesha utawala wa wafalme wa kizazi cha Daudi.

24 Yesu, “Mwana wa binadamu,” alikuwa muzao wa Daudi na kwa hiyo alistahili kisheria kuwa muriti wa ufalme wa Daudi. (Mt. 1:1; 16:13-16; Lu. 1:32, 33) “Wakati wa kurudishwa kwa mambo yote” ulianza mu mwaka wa 1914 wakati Yehova alipatia Yesu kiti cha ufalme mbinguni. Sasa, njia ilikuwa wazi kusudi Yehova atumie ule Mufalme mukamilifu juu ya kuendelesha kazi ya kurudisha mambo yote mu hali ya muzuri.

25, 26. (a) Uhamisho wa siku mingi mu Babiloni Mukubwa uliisha wakati gani, na tunajua vile namna gani? (b) Ni nini ilianza kutendeka kuanzia mwaka wa 1919 na kuendelea? (Ona pia kisanduku “Juu ya Nini 1919?”)

25 Moja kati ya mambo yenye Kristo alifanya kisha kuwa Mufalme ilikuwa kujiunga na Baba yake juu ya kuchunguza namna ibada safi inafanyika mu dunia. (Mal. 3:1-5) Kama vile Yesu alitabiri mu mufano wake wa ngano na magugu, kwa miaka mingi ilikuwa nguvu kutofautisha ngano na magugu, ni kusema, Wakristo watiwa-mafuta wa kweli na waasi-imani. * Lakini sasa, kipindi cha mavuno kilifika mu 1914, na tofauti ilikuwa wazi. Miaka fulani mbele ya 1914, wanafunzi waaminifu wa Biblia walikuwa wamefunua makosa makubwa ya Dini Zenye Kujiita Kuwa za Kikristo na walikuwa wameanza kujitenga na ile kikundi ya Wakristo wenye kupotoka. Ilikuwa wakati wa Yehova wa kuwarudisha kabisa mu hali ya muzuri. Kwa hiyo, ku mwanzo wa mwaka wa 1919, miaka kidogo tu kisha “kipindi cha mavuno” kuanza, watu wa Mungu waliachiliwa huru kabisa kutoka mu utekwa wa Babiloni Mukubwa. (Mt. 13:30) Uhamisho ulikuwa umeisha!

26 Maunabii ya Ezekieli kuhusu kurudishwa kwa ibada safi ilianza kutimia mu njia kubwa zaidi kuliko namna watu wa Mungu walijionea zamani. Tuzungumuzie sasa namna zile ahadi tano zenye tumekwisha kuchunguza zimetimia mu njia kubwa zaidi.

27. Namna gani Mungu alitakasa watu wake kutokana na ibada ya sanamu?

27 AHADI YA 1. Mwisho wa ibada ya sanamu na desturi zingine za dini ya uongo. Ku mwisho wa karne ya 19 (1801-1900) na ku mwanzo wa karne ya 20 (1901-2000), Wakristo waaminifu walikuwa wanakusanyika pamoja na walikuwa wanaanza kuachana na desturi za dini ya uongo. Kuabudu Utatu, imani ya kama mutu iko na nafsi yenye haikufake, na fundisho la moto wa mateso, ile yote iliwekwa pembeni sababu ni mafundisho yenye haipatane na Maandiko lakini ni ya dini ya uongo. Ilifasiriwa kwamba, kutumia mifano mu ibada, ni ibada ya sanamu kabisa. Pole kwa pole, watu wa Mungu walifikia pia kuona kwamba kutumia musalaba mu ibada ni aina fulani ya ibada ya sanamu.​—Eze. 14:6.

28. Ni mu maana gani watu wa Yehova walirudishwa mu inchi yao?

28 AHADI YA 2. Watu wa Mungu wanarudishwa mu inchi yao ya kiroho. Kadiri waliachana na dini ya Kibabiloni, Wakristo waaminifu walijikuta mu inchi yao ya muzuri ya kiroho, ni kusema, hali ao mazingira yenye kubarikiwa, kwenye hawangeteseka tena na njaa ya kiroho. (Soma Ezekieli 34:13, 14.) Kama vile tutaona mu Sura ya 19 ya kitabu hiki, Yehova amebariki ile inchi kwa kuimwangia chakula mingi sana ya kiroho mu njia yenye haiyakuwaka.​—Eze. 11:17.

29. Ni nini ilifanywa kuhusu kazi ya kuhubiri mu mwaka 1919?

29 AHADI YA 3. Matoleo ya zawadi inaanza tena kutolewa ku mazabahu ya Yehova. Mu karne ya kwanza (1-100) K.K.Y., Wakristo walifundishwa kwamba walipaswa kumutolea Mungu, hapana zabihu za wanyama, lakini zawadi zenye samani zaidi, ni kusema, maneno yenye walisema juu ya kumusifu Yehova na kuhubiria wengine juu yake. (Ebr. 13:15) Mu ile miaka yote ya uhamisho wa kiroho, hakukuwa mupango wowote wenye ulifanywa juu ya kutoa matoleo ya vile. Lakini, wakati uhamisho ulikaribia kumalizika, watu wa Mungu walikuwa wameanza kutoa zabihu za sifa za ile namna. Walikuwa na mengi ya kufanya mu kazi ya kuhubiri na walikuwa wanamusifu Mungu kwa furaha ku mikutano yao. Kuanzia 1919 na kuendelea, “mutumwa muaminifu na mwenye busara” alitia mukazo mukubwa juu ya kazi ya kuhubiri na aliipanga muzuri kabisa. (Mt. 24:45-47) Kwa hiyo, watu wengi sana walianza kumutolea Yehova zabihu za sifa ku mazabahu yake kwa kusifu jina lake takatifu!

30. Yesu alifanya nini juu watu wake wakuwe na wachungaji wazuri?

30 AHADI YA 4. Kuondolewa kwa wachungaji wabaya. Kristo alikomboa watu wa Mungu mu mikono ya wachungaji wabaya wa dini za uongo, wenye kutafuta tu faida zao. Mu kundi la Kristo, wachungaji wenye walitenda kama wale wachungaji wa uongo waliondolewa ku madaraka yao. (Eze. 20:38) Yesu, Muchungaji Mwema, alihakikisha kama kondoo wake wanachungwa muzuri. Mu mwaka wa 1919 aliweka mutumwa wake muaminifu na mwenye busara. Ile kikundi kidogo ya Wakristo watiwa-mafuta ilisimamia kazi ya kutoa chakula cha kiroho, kwa hiyo watu wa Mungu walichungwa muzuri. Kisha, wazee walipewa mazoezi kusudi wasaidie mu kazi ya kuchunga “kundi la Mungu.” (1 Pe. 5:1, 2) Maelezo yenye kuongozwa na roho ya Mungu yenye kupatikana mu Ezekieli 34:15, 16 imetumiwa mara mingi juu ya kukumbusha wachungaji Wakristo mufano muzuri wa Yehova Mungu na Yesu.

31. Namna gani Yehova alitimiza unabii wa Ezekieli 11:19?

31 AHADI YA 5. Umoja kati ya waabudu wa Yehova. Mu miaka mingi, Wakristo wa uongo wamegawanyika mu makanisa mingi, kutia ndani vikundi na mazehebu yenye kupingana. Lakini, Yehova amefanya jambo fulani la muujiza kuhusu watu wake wenye walirudishwa mu hali ya muzuri. Ahadi yenye alitoa kupitia Ezekieli, ya kama, “nitawapatia moyo wenye kuunganishwa,” imetimia mu njia kubwa zaidi. (Eze. 11:19) Mu dunia yote, Yesu iko na mamilioni ya wafuasi wenye kutoka mu makabila yote, makanisa yote, na hali yote ya maisha. Ijapokuwa vile, wote wanafundishwa kweli zilezile na wanafanya kazi ileile kwa upatano wenye kushangaza sana. Usiku wa mwisho wa maisha yake mu dunia, Yesu alisali sana kwamba wafuasi wake wakuwe mu umoja. (Soma Yohana 17:11, 20-23.) Leo, Yehova ametimiza ile ombi mu njia kubwa zaidi.

32. Unajisikia namna gani juu ya maunabii kuhusu kurudishwa kwa ibada safi? (Ona pia kisanduku “Maunabii Kuhusu Utekwa na Kurudishwa kwa Ibada Safi.”)

32 Je, haufurahi kuishi mu hii wakati ya kurudishwa kwa ibada safi? Leo, tunajionea utimizo wa maunabii ya Ezekieli mu kila sehemu ya ibada yetu. Tunaweza kuwa hakika kama kwa sasa, Yehova anafurahi wakati anatuangalia, kama vile alisema kupitia Ezekieli: “Nitafurahishwa na ninyi.” (Eze. 20:41) Je, unatambua kama uko na pendeleo kubwa la kuwa kati ya watu wa Mungu wenye kuunganishwa, wenye kukulishwa muzuri, wenye kumutolea Yehova sifa mu dunia yote​—watu wenye walikombolewa kisha kupitisha miaka mingi mu uhamisho wa kiroho? Lakini, maunabii fulani ya Ezekieli kuhusu kurudishwa kwa mambo mu hali ya muzuri itatimia mu njia kubwa zaidi mu siku zenye kuja.

“Kama Bustani ya Edeni”

33-35. (a) Unabii wa Ezekieli 36:35 ulikuwa na maana gani kwa Wayahudi wahamishwa? (b) Ile unabii iko na maana gani kwa watu wa Yehova leo? (Ona pia kisanduku “Wakati wa Kurudishwa kwa Mambo Yote.”)

33 Kama vile tuliona, “wakati wa kurudishwa kwa mambo yote” ulianza na kurudishwa kwa ukoo wa kifalme wa Daudi wakati Yesu aliwekwa kuwa mufalme mu mwaka wa 1914. (Eze. 37:24) Kisha, Yehova alimutia nguvu Kristo kusudi arudishe ibada safi kati ya watu Wake kisha wao kufanya miaka mingi mu uhamisho wa kiroho. Lakini, je, kazi ya Kristo ya kurudisha ibada safi iliishia pale? Hapana kabisa! Ile kazi itaendelea mu njia ya ajabu mu siku zenye kuja​—na maunabii ya Ezekieli inatupatia maelezo yenye kuchochea sana.

34 Fikiria kwa mufano, maneno hii yenye iliongozwa na roho ya Mungu: “Watu watasema: ‘Inchi yenye kuwa ukiwa imekuwa kama bustani ya Edeni.’” (Eze. 36:35) Ile ahadi ilikuwa na maana gani kwa Ezekieli na kwa wahamishwa wenzake? Bila shaka hawakutazamia kama itatimia mu njia ya kweli-kweli kabisa, ni kusema, inchi yenye kurudishwa haingekuwa kabisa-kabisa kama bustani ya Edeni ao Paradiso ya kwanza, yenye ilipandwa na Yehova mwenyewe! (Mwa. 2:8) Lakini, bila shaka walielewa kama Yehova alikuwa tu anawahakikishia kama inchi yao yenye kurudishwa itakuwa muzuri na itatoa mazao kabisa.

35 Ile ahadi iko na maana gani kwetu leo? Hatutazamie itimie mu njia ya kweli-kweli kabisa leo, mu ulimwengu huu muovu wenye unatawaliwa na Shetani Ibilisi. Tofauti na ile, tunaelewa kama ile maneno inatimia mu njia ya kiroho leo. Sisi watumishi wa Yehova, tunaishi mu inchi ya kiroho yenye imerudishwa mu hali ya muzuri, ni kusema, hali ao mazingira, kwenye tunafanya kazi yenye kuleta matokeo ya muzuri na kwenye tunatanguliza utumishi mutakatifu mu maisha yetu. Pole kwa pole, inchi hii ya kiroho inaendelea kuwa muzuri zaidi na zaidi. Lakini, itakuwa namna gani wakati wenye kuja?

36, 37. Ni ahadi gani zitatimia mu Paradiso yenye kuja?

36 Kisha vita kubwa ya Armagedoni, Yesu atapanua kazi yake ya kurudisha mambo mu hali ya muzuri, atatengeneza hata dunia yenye tunaishi ndani yake. Wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu, ataongoza wanadamu mu kazi ya kugeuza dunia hii yote kuwa bustani ya Edeni, paradiso, kama vile Yehova alipenda ikuwe tangu zamani! (Lu. 23:43) Kisha wanadamu wataishi kwa upatano mumoja na mwengine na watatunza makao yao ya kidunia na dunia itawazalia mazao kwa wingi. Hakuna fasi kwenye kutakuwa hatari, ao jambo la kuogopesha. Wazia wakati wenye hata ahadi hii itatimia: “Nitafanya agano la amani pamoja nao, na nitaondoa katika inchi wanyama hatari wa pori, ili wakae kwa usalama katika jangwa na kulala katika mapori.”​—Eze. 34:25.

37 Jaribu kuwazia ile ahadi mu akili. Bila kuogopa, utaweza kutembelea eneo lenye utapenda la dunia hii kubwa. Hakuna munyama mwenye atakuumiza. Hakuna hatari yenye itakukosesha amani. Utaweza kutembea peke yako mu mapori ya munene-munene, na uko unafurahia uzuri wake wenye kupendeza, na hata kulala kule bila kusumbuliwa, na uko hakika kama utaamuka kisha kupumuzika muzuri na bila kuumizwa na kitu fulani!

Wazia wakati wenye mutu hataogopa ‘kulala hata katika mapori’ (Ona fungu la 36, 37)

38. Unajisikia namna gani kuhusu kuona utimizo wa ahadi yenye inapatikana mu Ezekieli 28:26?

38 Tutaona pia utimizo wa ahadi hii: “Wataishi katika inchi hiyo kwa usalama na watajenga nyumba na kupanda mashamba ya mizabibu, na watakaa kwa usalama wakati nitaleta hukumu juu ya wale wote wenye kuwazunguka wenye wanawatendea kwa zarau; na watalazimika kujua kwamba mimi ni Yehova Mungu wao.” (Eze. 28:26) Kisha maadui wote wa Yehova kuharibiwa, tutafurahia amani na usalama mu dunia yote. Wakati tutakuwa tunatengeneza dunia, tutakuwa pia na nafasi ya kuhangaikia hali yetu na ya wapendwa wetu, kujenga nyumba za muzuri za kuishi ndani na kupanda mashamba ya mizabibu.

39. Ni nini inakuhakikishia kama maunabii yenye Ezekieli alitoa kuhusu Paradiso itatimia?

39 Je, unaona zile ahadi kuwa ndoto tu? Kama ni vile, kumbuka mambo yenye tayari umejionea wakati huu wa “kurudishwa kwa mambo yote.” Hata kama kuko upinzani mukali sana wa Shetani, Yesu ametiwa nguvu juu ya kurudisha ibada safi mu kipindi hiki cha giza kabisa cha ulimwengu. Ile inatuhakikishia kabisa kama ahadi zote zenye Mungu alitoa kupitia Ezekieli zitatimia!

^ fu. 2 Wayahudi wengi waliishi mu vijiji mbali kidogo na Babiloni. Kwa mufano, Ezekieli aliishi kati ya Wayahudi karibu na muto Kebari. (Eze. 3:15) Lakini, kulikuwa wahamishwa kidogo Wayahudi wenye waliishi mu muji wa Babiloni. Kati yao kulikuwa “wenye kutoka katika uzao wa kifalme na uzao wa watu wenye vyeo.”​—Dan. 1:3, 6; 2 Fa. 24:15.

^ fu. 25 Kwa mufano, hatuwezi kuhakikisha kama ni nani kati ya Watu Wenye Kuleta Marekebisho wa karne ya 16 (1501-1600) alikuwa Mukristo mutiwa-mafuta.