Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 3

Chagua Marafiki Wenye Kumupenda Mungu

Chagua Marafiki Wenye Kumupenda Mungu

“Mwenye anatembea na wenye hekima atakuwa na hekima.”​—MEZALI 13:20.

1-3. (a) Mezali 13:20 inatufundisha nini? (b) Juu ya nini tunapaswa kuchagua marafiki wetu kwa hekima?

UMEKWISHA kuona namna mutoto mudogo anaangaliaka wazazi wake? Hata mbele aanze kusema, anaweka mu ubongo wake mambo yote yenye anaona na kusikia. Kadiri anakomaa, anaanza kuiga wazazi wake hata bila kujikaza. Haishangaze kuona kama watu wakubwa pia wanaweza kuanza kufikiri na kutenda kama wale wenye wanapitisha wakati mingi pamoja nao.

2 Kupitia Mezali 13:20, tunajifunza kuwa: “Mwenye anatembea na wenye hekima atakuwa na hekima.” Katika ile andiko, wazo la “kutembea na” mutu fulani linatia ndani kuchagua kupitisha wakati pamoja naye. Ile inamaanisha zaidi ya kuwa tu pembeni ya mutu fulani. Mutu mumoja mwenye elimu ya Biblia alisema kama kutembea na mutu fulani kunatia ndani wazo la kupenda mutu huyo na kujisikia karibu naye. Tunachochewa zaidi sana na watu wenye tunapitisha nao wakati mwingi, zaidi sana ikiwa tunajisikia karibu nao.

3 Marafiki wetu wanaweza kutuchochea kufanya mambo ya muzuri ao ya mubaya. Mezali 13:20 inaendelea kusema hivi: “Mwenye kufanya urafiki na wajinga ataumia.” Mu luga ya Kiebrania, “kufanya urafiki na” mutu fulani kunaweza kumaanisha ‘kushirikiana’ na mutu huyo, ni kusema, kuwa rafiki yake. (Mezali 22:24; Waamuzi 14:20) Marafiki wenye kumupenda Mungu watatutia moyo tuendelee kuwa waaminifu kwake. Ili tuweze kuchagua marafiki kwa hekima, tuone ni watu wa namna gani Yehova anachagua ili wakuwe marafiki wake.

MARAFIKI WA MUNGU NI NANI?

4. Juu ya nini kuwa rafiki wa Yehova ni pendeleo kubwa? Juu ya nini Yehova alimuita Abrahamu “rafiki yangu”?

4 Yehova, Mutawala Mwenye Mamlaka Makubwa Zaidi mu ulimwengu wote, anatupatia nafasi ya kuwa marafiki wake. Ile ni pendeleo kubwa. Yehova anachagua marafiki wake kwa uangalifu. Anachagua wale wenye kumupenda na wenye wako na imani katika yeye. Waza juu ya Abrahamu. Alikuwa tayari kufanya jambo lolote kwa ajili ya Mungu. Tena na tena, Abrahamu alionyesha kama alikuwa muaminifu na mutiifu. Alikuwa tayari kumutoa hata mutoto wake Isaka. Abrahamu alikuwa na imani kama “Mungu angeweza kumufufua hata kutoka kwa wafu.” (Waebrania 11:17-19; Mwanzo 22:1, 2, 9-13) Abrahamu alikuwa muaminifu na mwenye kutii, na Yehova alimuita “rafiki yangu.”​—Isaya 41:8; Yakobo 2:21-23.

5. Yehova anaona namna gani wale wenye kuwa waaminifu kwake?

5 Yehova anaona marafiki wake kuwa wa maana. Marafiki wake wanahangaikia zaidi kuwa waaminifu kwake kuliko jambo lingine lolote. (Soma 2 Samweli 22:26.) Ni waaminifu na wenye kutii kwa sababu wanamupenda. Biblia inasema kuwa Mungu “anafanya urafiki wa karibu pamoja na watu wanyoofu,” ni kusema, wale wenye kumutii. (Mezali 3:32) Yehova anaalika marafiki wake wakuwe wageni wa pekee mu “hema” yake. Anawaalika wamuabudu na kusali kwake wakati wowote.​—Zaburi 15:1-5.

6. Namna gani tunaweza kuonyesha kama tunamupenda Yesu?

6 Yesu alisema hivi: “Kama mutu yeyote ananipenda, atashika neno langu, na Baba yangu atamupenda.” (Yohana 14:23) Kwa hiyo, ili kuwa rafiki ya Yehova, tunapaswa pia kumupenda Yesu na kufanya mambo yenye alitufundisha kufanya. Kwa mufano, tunatii amri ya Yesu ya kuhubiri habari njema na ya kufanya wanafunzi. (Matayo 28:19, 20; Yohana 14:15, 21) Kwa sababu tunamupenda Yesu, ‘tunafuata hatua zake kwa ukaribu.’ (1 Petro 2:21) Yehova anafurahi wakati anaona bidii yenye tunafanya ili kufuata mufano wa Mwana wake mu mambo yote yenye tunasema na kufanya.

7. Juu ya nini tunapaswa kuhakikisha kuwa marafiki wetu ni marafiki wa Yehova?

7 Marafiki wa Yehova wako waaminifu, washikamanifu, na watiifu, na wanamupenda Mwana wake. Je, tunachagua marafiki wenye Yehova anachagua? Ikiwa marafiki wako wanafuata mufano wa Yesu, na wanafanya kwa bidii kazi ya kufundisha wengine juu ya Ufalme wa Mungu, wanaweza kukusaidia ukuwe mutu muzuri na ubakie mushikamanifu kwa Yehova.

TUJIFUNZE KUPITIA MIFANO YA BIBLIA

8. Ni nini inakufurahisha kuhusu urafiki kati ya Rutu na Naomi?

8 Mu Biblia, tunaweza kusoma juu ya urafiki mbalimbali, kama vile urafiki kati ya Rutu na mama mukwe wake, Naomi. Wanamuke hao hawakuwa wa inchi moja na walilelewa ao kukomalishwa kwa njia tofauti. Pia, Naomi alikuwa mukubwa zaidi kuliko Rutu. Lakini walifikia kuwa marafiki wa karibu kwa sababu wote wawili walimupenda Yehova. Wakati Naomi alipenda kutoka katika inchi ya Moabu na kurudia katika Israeli, “Rutu akashikamana naye.” Alimuambia Naomi hivi: “Watu wako watakuwa watu wangu, na Mungu wako atakuwa Mungu wangu.” (Rutu 1:14, 16) Rutu alimutendea Naomi kwa wema sana. Wakati walifika mu inchi ya Israeli, Rutu alitumika sana ili kumutegemeza rafiki yake. Naomi alimupenda sana Rutu na alimupatia shauri la muzuri. Rutu alimusikiliza, na kwa hiyo, wote wawili walipata baraka mingi.​—Rutu 3:6.

9. Ni nini inakupendeza zaidi kuhusu urafiki wenye ulikuwa kati ya Daudi na Yonatani?

9 Mufano wa Daudi na Yonatani ni mufano mwingine wa watu wawili wenye walikuwa marafiki wazuri wenye walikuwa washikamanifu kwa Yehova. Yonatani alimupita Daudi karibu miaka 30 na ni yeye njo angekuwa mufalme wa pili katika Israeli. (1 Samweli 17:33; 31:2; 2 Samweli 5:4) Hata hivyo, wakati alijua kama Yehova amemuchagua Daudi ili akuwe mufalme, hakumusikilia wivu ao kushindana naye. Lakini, Yonatani alifanya nguvu yake yote ili kumutegemeza Daudi. Kwa mufano, wakati Daudi alikuwa mu hatari, Yonatani alimusaidia “kupata nguvu katika Yehova.” Alitia hata maisha yake mu hatari kwa sababu ya Daudi. (1 Samweli 23:16, 17) Daudi pia alikuwa rafiki mushikamanifu. Alifanya ahadi ya kuhangaikia familia ya Yonatani, na alitimiza ahadi yake hata kisha Yonatani kufa.​—1 Samweli 18:1; 20:15-17, 30-34; 2 Samweli 9:1-7.

10. Unajifunza nini kuhusu urafiki wenye ulikuwa kati ya Waebrania watatu?

10 Shadraki, Meshaki, na Abednego walikuwa vijana watatu Waebrania wenye walitoshwa mu inchi yao wakati walikuwa wangali watoto. Wakiwa mbali na familia zao, walisaidiana kubakia waaminifu kwa Yehova. Kisha, wakati walikomaa, imani yao ilijaribiwa wakati Mufalme Nebukadneza aliwapatia amri ya kuabudu sanamu ya zahabu. Shadraki, Meshaki, na Abednego walikataa kuabudu sanamu hiyo na walimuambia mufalme hivi: “Hatutatumikia miungu yako wala kuabudu sanamu ya zahabu yenye ulisimamisha.” Wakati imani yao ilijaribiwa, marafiki hao watatu walibakia washikamanifu kwa Mungu wao.​—Danieli 1:1-17; 3:12, 16-28.

11. Ni nini inaonyesha kama Paulo na Timoteo walikuwa marafiki wa karibu?

11 Wakati mutume Paulo alimuona kijana Timoteo, aliona kama Timoteo alimupenda Yehova na kuhangaikia sana kutaniko. Kwa hiyo Paulo alimuzoeza Timoteo ili asaidie ndugu na dada mu maeneo mbalimbali. (Matendo 16:1-8; 17:10-14) Timoteo alitumika kwa bidii hivi kwamba Paulo alisema: “Alitumika pamoja na mimi ili kuendeleza habari njema.” Paulo alijua kama Timoteo “atajali kabisa” ndugu na dada. Kadiri walitumika pamoja kwa bidii mu kazi ya Yehova, Paulo na Timoteo walifikia kuwa marafiki wa karibu.​—Wafilipi 2:20-22; 1 Wakorinto 4:17.

NAMNA YA KUCHAGUA MARAFIKI WETU

12, 13. (a) Sababu gani tunapaswa kuchagua marafiki wetu kwa uangalifu hata mu kutaniko? (b) Juu ya nini mutume Paulo alitoa onyo lenye kuwa mu 1 Wakorinto 15:33?

12 Mu kutaniko, tunaweza kujifunza mambo mingi kupitia ndugu na dada na kusaidiana kubakia waaminifu. (Soma Waroma 1:11, 12.) Lakini hata mu kutaniko, tunapaswa kuwa waangalifu kuhusu wale wenye tunachagua ili wakuwe marafiki wetu wa karibu. Tuko na ndugu na dada wengi wazuri kutoka katika desturi mingi na hali mbalimbali za maisha. Wamoja ni wapya mu kutaniko, na wengine wamekuwa wakimutumikia Yehova kwa miaka mingi. Inaomba wakati ili mutu akomalishe urafiki wake pamoja na Yehova, kama vile tu inaomba wakati ili tunda liivye. Kwa hiyo, tunapaswa kuvumiliana na kuonyeshana upendo na kuchagua sikuzote marafiki wetu kwa hekima.​—Waroma 14:1; 15:1; Waebrania 5:12–6:3.

13 Wakati fulani, tatizo fulani kubwa linaweza kutokea mu kutaniko, na tunaweza kuwa na lazima ya kuwa waangalifu sana. Pengine inaweza kuwa ndugu ao dada fulani iko anafanya mambo yenye Biblia inasema kama ni ya mubaya. Ao wamoja wanaweza kuonyesha mutazamo ao tabia ya kunungunika yenye inaweza kuharibisha kutaniko. Hilo halitushangaze, kwa sababu hata mu karne ya kwanza, wakati fulani kulikuwa matatizo mu kutaniko. Kwa kweli, mutume Paulo alionya Wakristo wa wakati huo hivi: “Musidanganywe. Mashirika ya mubaya yanaharibu tabia za muzuri.” (1 Wakorinto 15:12, 33) Paulo alionya pia Timoteo akuwe mwangalifu kuhusu wale wenye alichagua kuwa marafiki wake. Tunapaswa kufanya pia vile leo.​—Soma 2 Timoteo 2:20-22.

14. Namna tunachagua marafiki inaweza kuwa na matokeo gani juu ya uhusiano wetu pamoja na Yehova?

14 Tunapaswa kulinda urafiki wetu pamoja na Yehova. Njo kitu cha maana zaidi chenye tuko nacho. Kwa hiyo, tunaepuka kufanya urafiki wa karibu na mutu yeyote mwenye anaweza kuregeza imani yetu ao kuharibisha uhusiano wetu pamoja na Yehova. Kama vile hatuwezi kutia sifongo (ao, chiffon) mu maji ya uchafu na kutazamia sifongo hiyo ijae maji yenye kuwa safi, vilevile hatuwezi kuwa na marafiki wenye kufanya mambo ya mubaya na wakati uleule tutazamie kuwa itakuwa mwepesi kwetu kufanya mambo ya muzuri. Tunapaswa kuchagua marafiki wetu wa karibu kwa uangalifu.​—1 Wakorinto 5:6; 2 Watesalonike 3:6, 7, 14.

Unaweza kupata marafiki wazuri wenye kumupenda Yehova

15. Unaweza kufanya nini ili ukuwe na marafiki wazuri mu kutaniko?

15 Mu kutaniko, unaweza kupata watu wenye wanamupenda kabisa Yehova. Wanaweza kuwa marafiki wako wa karibu. (Zaburi 133:1) Usitafute tu marafiki kati ya watu wa miaka yako ao watu wenye kuwa na hali ya maisha kama yako. Kumbuka kama Yonatani alikuwa na miaka mingi zaidi kuliko Daudi, na Rutu alikuwa na miaka kidogo zaidi kuliko Naomi. Tunapenda kufuata shauri hili la Biblia: “Mufungue mioyo yenu wazi.” (2 Wakorinto 6:13; soma 1 Petro 2:17.) Na kadiri unamuiga Yehova, ni vile wengine watapenda kuwa marafiki wako.

WAKATI MATATIZO INATOKEA

16, 17. Kama mutu fulani mu kutaniko anatukasirisha, tunapaswa kuepuka kufanya nini?

16 Mu kila familia, watu wako na sifa tofauti-tofauti, maoni, na njia tofauti za kufanya mambo. Ni vile pia mu kutaniko. Jambo hilo linafanya maisha ipendeze, na tunaweza kujifunza mambo mingi kupitia watu wengine. Lakini wakati fulani tofauti hizo zinaweza kufanya tuelewane mubaya na ndugu ao dada zetu na kuwakasirikia. Wakati fulani, tunaweza kukasirishwa ao hisia zetu zinaweza kuumizwa. (Mezali 12:18) Je, tunapaswa kuacha matatizo kama hayo ituvunje moyo ao itufanye tuache kukusanyika?

17 Hapana. Hata kama mutu fulani anatuvunja moyo kwa njia fulani, hatutaacha kukusanyika. Haiko Yehova njo alitukosea. Alitupatia uzima na mambo ingine yote. Anastahili upendo na ushikamanifu wetu kwake. (Ufunuo 4:11) Kutaniko ni zawadi kutoka kwa Yehova yenye inatusaidia tuendelee kuwa na imani yenye nguvu. (Waebrania 13:17) Hatutakataa hata kidogo zawadi yake kwa sababu mutu fulani alitukosea.​—Soma Zaburi 119:165.

18. (a) Ni nini inaweza kutusaidia tusikilizane na ndugu na dada zetu? (b) Juu ya nini tunapaswa kusamehe wengine?

18 Tunapenda ndugu na dada zetu na tunapenda kusikilizana nao. Yehova hatazamie mutu yeyote akuwe mukamilifu, na sisi hatupaswe kutazamia wengine wakuwe wakamilifu. (Mezali 17:9; 1 Petro 4:8) Sisi wote tunafanya zambi, lakini upendo utatusaidia tuendelee “kusameheana kwa kupenda.” (Wakolosai 3:13) Upendo utatuzuia kufanya jambo kidogo tu la kukosa kuelewana likuwe tatizo kubwa. Ni kweli, wakati mutu fulani anatukosea, inaweza kuwa nguvu kusahau ile jambo. Ni mwepesi kukasirika na kumuwekea kinyongo. Lakini ile inaweza kufanya tukose furaha na tukuwe wenye uchungu. Kwa upande mwingine, wakati tunasamehe mutu mwenye alitukosea, tunaweza kuwa na amani ya akili, umoja mu kutaniko na, jambo la maana zaidi, tutakuwa na uhusiano wa muzuri pamoja na Yehova.​—Matayo 6:14, 15; Luka 17:3, 4; Waroma 14:19.

WAKATI MUTU FULANI ANATENGWA NA KUTANIKO

19. Ni wakati gani tunapaswa kuacha kushirikiana na mutu fulani mu kutaniko?

19 Mu familia mwenye wote wanapendana, kila mumoja anafanya sehemu yake ili kusaidia wengine wakuwe na furaha. Lakini wazia kama mumoja anaasi. Kila mutu mu familia anajikaza kumusaidia tena na tena, lakini anakataa musaada. Anaweza kuamua kuondoka ku nyumba, ao kichwa cha familia anaweza kumuomba aondoke. Jambo kama hilo linaweza kutokea mu kutaniko. Mutu fulani anaweza kuchagua kuendelea kufanya mambo yenye kumuchukiza Yehova na kuharibisha kutaniko. Anakataa musaada na anaonyesha kupitia matendo yake kama hapendi tena kuwa mu kutaniko. Anaweza kuamua yeye mwenyewe kutoka mu kutaniko, ao kutaniko linaweza kulazimika kumutenga. Ikiwa hilo linatokea, Biblia inasema waziwazi kuwa tunapaswa ‘kuacha kushirikiana’ naye. (Soma 1 Wakorinto 5:11-13; 2 Yohana 9-11) Inaweza kuwa nguvu sana kufanya vile ikiwa ni rafiki yetu ao ni mutu wa familia yetu. Lakini mu hali kama hiyo, ushikamanifu wetu kwa Yehova unapaswa kuwa wenye nguvu zaidi kuliko ushikamanifu wetu kwa mutu mwingine yeyote.​—Ona Mafasirio Ingine ya 8.

20, 21. (a) Ni nini inaonyesha kuwa kutengwa na kutaniko ni mupango wenye upendo? (b) Juu ya nini ni jambo la maana tuchague marafiki wetu kwa hekima?

20 Kutengwa na kutaniko ni mupango wenye upendo kutoka kwa Yehova. Mupango huo unasaidia kutaniko lilindwe kutokana na watu wenye hawapendi kufuata kanuni za Yehova. (1 Wakorinto 5:7; Waebrania 12:15, 16) Unatusaidia tuonyeshe kama tunapenda jina takatifu la Yehova, kanuni zake za juu, na Yehova mwenyewe. (1 Petro 1:15, 16) Na mupango wa kutengwa na kutaniko unaonyesha upendo kwa ajili ya mutu mwenye haiko tena mu kutaniko. Nizamu hiyo nzito inaweza kumusaidia atambue kama mambo yenye iko anafanya ni ya mubaya na inaweza kumuchochea abadilike. Watu wengi wenye zamani walitengwa na kutaniko walifikia kumurudilia Yehova na walikaribishwa kwa furaha mu kutaniko.​—Waebrania 12:11.

21 Mu njia moja ao ingine, marafiki wetu wanaweza kutuchochea tufanye mambo ya muzuri ao ya mubaya. Kwa hiyo ni jambo la maana tuwachague muzuri. Ikiwa tunapenda wale wenye Yehova anapenda, tutazungukwa na watu wenye wanaweza kutusaidia tubakie waaminifu kwake milele.