Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 14

Ukuwe Munyoofu Katika Mambo Yote

Ukuwe Munyoofu Katika Mambo Yote

“Tunataka kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.”​—WAEBRANIA 13:18.

1, 2. Yehova anajisikia namna gani wakati anaona namna tunajikaza sana kuwa wanyoofu?

KIJANA fulani mwanaume anarudia ku nyumba kisha kutoka ku masomo. Wakati iko mu njia, anaona chini mukoba kidogo (ao, porte-monnaie) wenye kujaa feza. Atafanya nini? Anaweza kuikamata ili ikuwe yake. Lakini, kuliko kufanya vile, anairudishia mwenye nayo. Wakati mama anasikia namna mutoto wake alifanya, anajivunia sana mutoto wake.

2 Wazazi wengi wanafurahi sana wakati watoto wao ni wanyoofu (ao, waaminifu). Baba wetu wa mbinguni, Yehova, ni “Mungu wa ukweli,” na anafurahi wakati tuko wanyoofu. (Zaburi 31:5) Tunapenda kumufurahisha na “kujiendesha kwa unyoofu katika mambo yote.” (Waebrania 13:18) Tuzungumuzie basi sehemu ine za maisha mwenye haiwezi kuwa mwepesi kuwa wanyoofu. Kisha tutachunguza faida fulani zenye tunaweza kupata wakati tunajiendesha kwa unyoofu.

TUSIJIDANGANYE SISI WENYEWE

3-5. (a) Namna gani tunaweza kujidanganya sisi wenyewe? (b) Ni nini itatusaidia tuepuke kujidanganya sisi wenyewe?

3 Ili tuweze kujiendesha kwa unyoofu mbele ya wengine, tunapaswa kwanza kuwa wanyoofu katika moyo wetu. Kufanya vile mara mingi haiko mwepesi. Mu karne ya kwanza, ndugu wa kutaniko la Laodikia walijidanganya wao wenyewe kwa kufikiri kama walikuwa wanamufurahisha Mungu, wakati kwa kweli walikuwa hawafanye vile. (Ufunuo 3:17) Sisi pia tunaweza kujidanganya kuhusu kile tuko kabisa.

4 Mutume Yakobo alieleza hivi: “Kama mutu yeyote anawaza yeye ni muabudu wa Mungu lakini hazuie kabisa ulimi wake, anadanganya moyo wake mwenyewe, na ibada yake ni ya bure.” (Yakobo 1:26) Tunaweza kuwa tunajidanganya sisi wenyewe ikiwa tunafikiri kama tukiendelea kufanya mambo fulani ya muzuri, Mungu hataona mubaya hata kama tunakuwa wakosa-adabu na wenye kuzarau wengine ao kusema mambo ya uongo. Ni nini inaweza kutusaidia tuepuke kujidanganya?

5 Wakati tunajiangalia mu kioo, tunaweza kuona namna tunaonekana kwa inje. Wakati tunasoma Biblia, tunaweza kuona ikiwa ndani yetu tuko watu wa namna gani. Biblia inaweza kutusaidia tujue uwezo na uzaifu wetu. Inatusaidia kujua mabadiliko yenye tunapaswa kufanya mu namna yetu ya kufikiri, ya kutenda, na ya kusema. (Soma Yakobo 1:23-25.) Lakini ikiwa tunasema kama hatuna kosa lolote, inaweza kuwa nguvu kufanya mabadiliko yenye kuombwa. Kwa hiyo, tunapaswa kutumia Biblia ili kujichunguza kwa unyoofu. (Maombolezo 3:40; Hagai 1:5) Sala inatusaidia pia kujua tuko watu wa namna gani kabisa. Katika sala tunaweza kumuomba Yehova atuchunguze na atusaidie kuona makosa yetu ili tuweze kuirekebisha. (Zaburi 139:23, 24) Tunakumbuka kama “Yehova anachukia mutu mudanganyifu, lakini anafanya urafiki wa karibu pamoja na watu wanyoofu.”​—Mezali 3:32.

TUKUWE WANYOOFU KATIKA FAMILIA

6. Juu ya nini bibi na bwana wanapaswa kutendeana kwa unyoofu?

6 Unyoofu ni wa maana kabisa mu familia. Wakati bibi na bwana wanaambiana kweli, wanajisikia salama na wanaweza kutumainiana kabisa. Bibi na bwana wanaweza kukosa uaminifu mu njia mingi. Kwa mufano, bibi ao bwana anaweza kuanza kuchezea kimapenzi mutu mwingine ao kujiingiza mu tabia ya kuona pornografia ao anaweza kuanza kupendana na mutu mwingine kwa siri. Ona mambo yenye muandikaji mumoja wa zaburi alisema: “Sishirikiane na watu wadanganyifu, na ninaepuka wale wenye kuficha namna wako.” (Zaburi 26:4) Kama hauko muaminifu kwa bibi ao bwana yako hata mu mawazo, ile itaharibu ndoa yenu.

Ukuwe tayari kuachana na jambo lolote lenye linaweza kufanya ndoa yako ikuwe zaifu

7, 8. Namna gani unaweza kutumia Biblia ili kufundisha watoto waone kama unyoofu ni wa maana sana?

7 Watoto pia wanapaswa kujua kama unyoofu ni wa maana. Wazazi wanaweza kutumia Biblia ili kuwafundisha ile jambo. Biblia inazungumuzia mifano ya mubaya ya watu wenye walikosa unyoofu: Akani, mwenye alifikia kuwa mwizi; Gehazi, mwenye alisema uongo ili kupata feza; na Yuda, mwenye aliiba feza na kisha akafikia kumusaliti Yesu kwa vipande 30 vya feza.​—Yoshua 6:17-19; 7:11-25; 2 Wafalme 5:14-16, 20-27; Matayo 26:14, 15; Yohana 12:6.

8 Pia, Biblia iko na mifano mingi ya muzuri ya watu wenye walikuwa wanyoofu: Yakobo, mwenye alichochea watoto wake warudishe feza zenye walikuwa wamepata; Yefta na mutoto wake mwanamuke, wenye walitimiza ahadi yao kwa Mungu; na Yesu, mwenye alikuwa munyoofu hata mu hali ngumu. (Mwanzo 43:12; Waamuzi 11:30-40; Yohana 18:3-11) Ile mifano inaweza kusaidia watoto waelewe kuwa unyoofu ni wa maana sana.

9. Wakati wazazi ni wanyoofu, ile inaweza kuwa na matokeo gani juu ya watoto?

9 Wazazi wanaweza kujifunza kutokana na hii kanuni ya Biblia: “Sasa, je, wewe mwenye unamufundisha mutu mwingine, haujifundishe wewe mwenyewe? Wewe mwenye unahubiri, ‘Usiibe,’ je, unaiba?” (Waroma 2:21) Watoto wanajua wakati wazazi wanafanya jambo tofauti na lenye walisema kama watafanya. Kama tunawaambia watoto wetu wakuwe wanyoofu lakini sisi wenyewe tunakosa kuwa wanyoofu, wanaweza kuvurugika. Ikiwa watoto wanatambua kama wazazi wao wanasema uongo, hata mu mambo kidogo, bila shaka wao pia watafanya vile. (Soma Luka 16:10.) Kwa upande mwingine, wakati watoto wanaona kuwa wazazi wao ni wanyoofu, ile inaweza kuwasaidia wakuwe wazazi wenye kutumainika wakati watakuwa na watoto wao wenyewe.​—Mezali 22:6; Waefeso 6:4.

TUKUWE WANYOOFU KATIKA KUTANIKO

10. Namna gani tunaweza kuwa wanyoofu mu mazungumuzo yetu pamoja na Wakristo wenzetu?

10 Tunapaswa pia kuwa wanyoofu mbele ya ndugu na dada zetu Wakristo. Ni mwepesi mazungumuzo ya kila siku igeuke na kuwa porojo, ao hata usingiziaji. Kama tunasema jambo fulani lenye tulisikia bila kujua ikiwa ni la kweli ao hapana, tunaweza kueneza habari ya uongo. Ni muzuri zaidi ‘kuzuia midomo yetu.’ (Mezali 10:19) Kuwa wanyoofu hakumaanishe kama tunapaswa kusema kila kitu chenye tunawaza, tunajua, ao chenye tumesikia. Hata kama jambo lenye tunataka kusema ni la kweli, pengine jambo hilo halituangalie, ao pengine haiwezi kuwa muzuri ao lazima kulirudilia. (1 Watesalonike 4:11) Watu fulani wanatetea tabia yao ya kukosa adabu kwa kusema: “Napendaka tu kusema kweli.” Lakini kwa kuwa tuko watu wa Yehova, tunapenda maneno yetu ikuwe ya upole na yenye neema sikuzote.​—Soma Wakolosai 4:6.

11, 12. (a) Namna gani mutu mwenye amefanya zambi anaweza kufanya mambo ikuwe mubaya zaidi kwa sababu ya kukosa unyoofu? (b) Ni maulizo gani fulani tunaweza kujiuliza? (c) Namna gani tunaweza kuonyesha unyoofu mbele ya tengenezo la Yehova?

11 Yehova amepatia wazee daraka la kusaidia kutaniko. Ni mwepesi zaidi wazee watusaidie kama tuko wanyoofu mbele yao. Juu ya nini? Kama uko mugonjwa na unaenda kuona munganga ili akusaidie, utamuficha alama fulani za ugonjwa wako? Kama unafanya vile, namna gani anaweza kukusaidia? Vilevile, kama tunafanya kosa nzito, hatupaswe kusema uongo kuhusu ile kosa. Lakini, tunapaswa kuona wazee na kuwaambia kweli yote. (Zaburi 12:2; Matendo 5:1-11) Sasa fikiria hii hali yenye kuwa tofauti: Utafanya nini ikiwa unatambua kama rafiki yako alifanya kosa nzito? (Mambo ya Walawi 5:1) Utasema: “Nitachunga siri ili kuonyesha kama niko kabisa rafiki yake”? Ao utakumbuka kama wazee wako pale ili kumutolea musaada wenye iko nao lazima ili atengeneze na kutia nguvu uhusiano wake pamoja na Yehova?​—Waebrania 13:17; Yakobo 5:14, 15.

12 Tunapaswa pia kuwa wanyoofu mbele ya tengenezo la Yehova wakati tunajaza ripoti mbalimbali, kama vile ripoti zetu za mahubiri. Na tunaonyesha pia unyoofu wakati tunajaza ombi la kuwa painia ao la kufanya aina ingine ya utumishi.​—Soma Mezali 6:16-19.

13. Namna gani tunaweza kuonyesha kama tuko wanyoofu wakati tunafanya biashara pamoja na Mukristo mwenzetu?

13 Ndugu na dada Wakristo hawapaswe kuchanga ibada na mambo ya biashara. Kwa mufano, hatufanye biashara wakati tuko ku Jumba la Ufalme ao wakati tuko mu mahubiri. Na hatutumikishe mubaya ndugu na dada zetu mu mambo ya biashara ili kupata faida. Kama unaomba Mashahidi wakufanyie kazi, uwalipe wafanyakazi wako kwa wakati, uwalipe vile mulipatana, na uwatolee faida yoyote yenye kuombwa na sheria. Ile inaweza kutia ndani kulipiwa matunzo ao kulipwa mushahara hata wakati wa mapumuziko. (1 Timoteo 5:18; Yakobo 5:1-4) Na kama unafanya kazi kwa Shahidi mwenzako, usitazamie akutendee kwa njia ya pekee. (Waefeso 6:5-8) Hakikisha kuwa unatumika saa zenye mulipatana na ufanye kazi yenye mulipatana kufanya.​—2 Watesalonike 3:10.

14. Wakristo wanapaswa kufanya nini mbele watumike pamoja mu mambo ya biashara?

14 Sasa, namna gani kama tunatumika pamoja na ndugu na dada fulani katika mambo ya biashara? Ile inaweza kutia ndani kuweka feza pamoja juu ya kusudi fulani ao kujikopesha feza. Mu hali kama zile, kuko kanuni moja ya Biblia yenye inaweza kusaidia sana: Muandike kila kitu! Wakati nabii Yeremia aliuza shamba, aliandika kopi mbili za mapatano, alifanya kopi moja itiwe sinyatire na mashahidi, na alichunga muzuri zile kopi mbili ili kuzitumia wakati wenye ungekuja. (Yeremia 32:9-12; ona pia Mwanzo 23:16-20.) Watu fulani wanawaza kama kuandika mapatano kunaweza kufanya ionekane kama hawatumainie ndugu yao. Lakini kwa kweli, kuandika mapatano kunaweza kuzuia hali ya kukosa kuelewana, kuvunjika moyo, na hata kukosana. Hata mu mambo ya biashara, tukumbuke kama amani ya kutaniko ni ya maana zaidi kuliko mapatano yoyote ya biashara.​—1 Wakorinto 6:1-8; ona Mafasirio Ingine ya 30.

TUKUWE WANYOOFU KATIKA MAMBO YA KIMWILI

15. Namna gani Yehova anajisikia kuhusu udanganyifu mu mambo ya biashara?

15 Tunapaswa kujiendesha kwa unyoofu mbele ya kila mutu, kutia ndani wale wenye hawako Mashahidi wa Yehova. Kuwa kwetu wanyoofu ni jambo la maana mbele ya Yehova. “Mizani za uongo ni chukizo kwa Yehova, lakini kipimo chenye kuwa sawa kinamufurahisha.” (Mezali 11:1; 20:10, 23) Zamani, mizani ao vipimo vilitumiwa mara mingi mu mambo ya biashara. Lakini wafanyabiashara fulani waliiba watu kwa kuwapatia vitu kidogo kuliko vile walipatana ao kwa kuwafanya walipe feza mingi zaidi kuliko zenye walipaswa kulipa. Kama zamani, leo pia, udanganyifu mu mambo ya biashara ni jambo la kawaida. Na kama vile tu Yehova alichukia tabia ya kukosa unyoofu ile wakati, leo pia angali anaichukia.

16, 17. Ni njia gani mbalimbali za kukosa unyoofu zenye tunapaswa kuepuka?

16 Sisi wote tunapatwa na hali yenye inaweza kufanya tukose unyoofu​—kama vile kujaza vikaratasi vya kutafuta kazi, kujaza vikaratasi vya serikali, ao kufanya mashindano ku masomo. Watu wengi wanawaza kama hakuna ubaya ikiwa mutu anasema uongo, anatia chumvi, ao anatoa majibu yenye haiko ya kweli. Ile haiwezi kutushangaza. Biblia ilitabiri kama katika siku za mwisho za ulimwengu huu, watu watakuwa “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda feza, . . . wenye hawapendi wema.”​—2 Timoteo 3:1-5.

17 Wakati fulani inaweza kuonekana kuwa watu wenye kukosa unyoofu njo wenye wanafanikiwa mu ulimwengu wa leo. (Zaburi 73:1-8) Mukristo anaweza hata kupoteza kazi yake, kulipiwa feza kidogo, ao kutendewa mubaya ku kazi juu ya unyoofu wake. Lakini kujiendesha kwa unyoofu ni kwa maana zaidi hata kama ile inaweza kufanya tuteseke. Juu ya nini?

BARAKA ZA KUWA WANYOOFU

18. Juu ya nini kuwa na sifa ya muzuri ni jambo la maana sana?

18 Sifa ya kuwa mutu munyoofu, mwenye kutumainika, na mwenye kutegemeka ni ya maana sana. Na katika ulimwengu huu ni watu kidogo sana njo wako nayo. Kila mumoja wetu iko na nafasi ya kukomalisha ile sifa. (Mika 7:2) Ni kweli, watu fulani wanaweza kukucheka juu uko munyoofu na wanaweza kukuambia kama hauna akili. Lakini watu wengine wanaweza kufurahia sana unyoofu wako na watakutumainia. Mu dunia yote, Mashahidi wa Yehova wanajulikana kuwa watu wanyoofu. Wakubwa fulani wa kazi wanafurahia kutumikisha Mashahidi wa Yehova juu wanajua kama watakuwa wanyoofu. Na wakati wafanyakazi wengine wanafukuzwa ku kazi kwa sababu ya kukosa unyoofu, mara mingi Mashahidi wa Yehova wanabakia na kazi zao.

Kufanya kazi kwa bidii kunaweza kumuletea Yehova utukufu

19. Kuwa munyoofu kutakuwa na matokeo gani juu ya urafiki wako pamoja na Yehova?

19 Kuwa munyoofu mu mambo yote kutakusaidia ukuwe na zamiri ya muzuri na amani ya akili. Tunaweza kuwa kama Paulo, mwenye aliandika hivi: “Tuko hakika kwamba tuko na zamiri nyoofu.” (Waebrania 13:18) Jambo la maana zaidi ni kuwa, Baba yako mwenye upendo, Yehova, ataona na kufurahia sana bidii yenye unafanya ili kuwa munyoofu mu mambo yote.​—Soma Zaburi 15:1, 2; Mezali 22:1.