Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 7

Unaona Uzima Kama Vile Mungu Anauona?

Unaona Uzima Kama Vile Mungu Anauona?

“Kwako kuko chemchemi ya uzima.”​—ZABURI 36:9.

1, 2. Yehova ametupatia zawadi gani ya maana?

YEHOVA amepatia kila mumoja wetu zawadi ya muzuri sana. Ni zawadi ya uzima. (Mwanzo 1:27) Anapenda tukuwe na maisha ya muzuri zaidi. Kwa hiyo, ametupatia kanuni zenye zinaweza kutusaidia kujua namna ya kufanya maamuzi ya muzuri. Tunapaswa kutumia zile kanuni ili zitusaidie “kufanya tofauti kati ya mambo yenye kuwa sawa na yenye kuwa makosa.” (Waebrania 5:14) Wakati tunafanya vile, tunaruhusu Yehova atuzoeze kufikiri muzuri. Kadiri tunaishi kulingana na kanuni za Mungu na kuona namna zinafanya maisha yetu ikuwe ya muzuri zaidi, tunafikia kuelewa kuwa ni za maana sana.

2 Maisha inaweza kuwa nguvu sana. Mara mingi Biblia haitupatie sheria yenye kuwa wazi juu ya kila hali yenye inaweza kutupata mu maisha. Kwa mufano, tunaweza kuwa na lazima ya kukamata maamuzi juu ya matunzo yenye kuomba kutumia damu. Ni nini inaweza kutusaidia kukamata maamuzi yenye itamufurahisha Yehova? Biblia iko na kanuni zenye kutufundisha namna Yehova anaona uzima na damu. Tutafanya maamuzi ya muzuri na kuwa na zamiri safi kama tunaelewa kanuni hizo. (Mezali 2:6-11) Tuchunguze basi kanuni fulani.

NAMNA GANI MUNGU ANAONA UZIMA NA DAMU?

3, 4. (a) Namna gani Mungu alionyesha mawazo yake juu ya damu? (b) Damu inamaanisha nini?

3 Biblia inatufundisha kuwa damu ni takatifu, juu damu inamaanisha uzima. Na Yehova anaona uzima kuwa wa maana sana. Kisha Kaini kumuua ndugu yake, Yehova alimuambia hivi: “Damu ya ndugu yako iko inanililia kutoka katika udongo.” (Mwanzo 4:10) Damu ilimaanisha uzima wa Abeli; wakati Kaini alimuua Abeli, alimuondoa uzima.

4 Kisha Garika ya siku za Noa, Mungu aliwaambia wanadamu wakule nyama. Lakini aliwaambia hivi waziwazi: “Isipokuwa tu nyama pamoja na uzima wake​—damu yake—​hamupaswe kula.” (Mwanzo 9:4) Ile amri inatumika kwa watoto wote wa Noa, kutia ndani sisi. Ni wazi kuwa, mbele ya Yehova, damu inamaanisha uzima. Sisi pia tunapaswa kuona damu kama yeye.​—Zaburi 36:9.

5, 6. Sheria ya Musa ilisema nini ili kuonyesha mawazo ya Yehova juu ya uzima na damu?

5 Mu sheria yenye Yehova alipatia Musa, Alisema hivi: “Kama mutu yeyote . . . anakula damu ya namna yoyote, hakika nitakunja uso wangu juu ya mutu huyo mwenye anakula damu, na nitamuondoa katikati ya watu wake. Kwa maana uzima wa mwili uko katika damu.”​—Mambo ya Walawi 17:10, 11.

6 Sheria ya Musa ilisema kama mutu yeyote mwenye aliua munyama kwa ajili ya chakula, alipaswa kumwanga damu yake kwenye udongo. Ile ilionyesha kuwa uzima umerudishwa kwa Yehova, Muumbaji wa ule munyama. (Kumbukumbu la Torati 12:16; Ezekieli 18:4) Lakini Yehova hakutazamia Waisraeli wafanye mambo yenye kupita mipaka wakati walichinja munyama. Wakati wangefanya yote yenye wangeweza na kwa usawaziko ili kuondoa damu, wangekula nyama wakiwa na zamiri safi. Kwa kuheshimia damu ya munyama, walionyesha kuwa wanamuheshimia Yehova, Mutoaji wa uzima. Sheria iliwaomba pia Waisraeli watoe wanyama kama zabihu ya kufunika zambi.​—Ona Mafasirio Ingine ya 19 na ya 20.

7. Namna gani Daudi alionyesha kuwa aliheshimia damu?

7 Tunaweza kuona kuwa damu ni ya maana sana kupitia jambo lenye Daudi alifanya wakati alikuwa anapigana na Wafilisti. Wakati wanaume wa Daudi waliona kuwa Daudi anasikia kiu sana, waliingia mu eneo lenye hatari la maadui na kutia uzima wao mu hatari ili kumuletea maji ya kunywa. Lakini, wakati walimuletea Daudi ile maji, alikataa kuikunywa na ‘akaimwanga mbele ya Yehova.’ Alisema hivi: “Ni jambo lenye haliwezi kuwaziwa kwa upande wangu, Ee Yehova, kwamba nifanye jambo hilo! Je, nikunywe damu ya wanaume wenye walienda kwa kutia uzima wao katika hatari?” Daudi alielewa kuwa uzima na damu ni vya maana sana mbele ya Mungu.​—2 Samweli 23:15-17.

8, 9. Namna gani leo Wakristo wanapaswa kuona damu?

8 Kufikia wakati wa Wakristo wa kwanza-kwanza, watu wa Mungu hawakupaswa kutoa tena zabihu za wanyama. Lakini walipaswa kuendelea kuwa na mawazo yenye kufaa juu ya damu. “Kujiepusha na . . . damu” ni sehemu moja ya Sheria yenye Wakristo waliombwa kutii. Kufanya vile ilikuwa jambo la maana kama vile kuepuka uasherati ao ibada ya sanamu.​—Matendo 15:28, 29.

Ninaweza kueleza namna gani maamuzi yangu juu ya kutumia visehemu vya damu?

9 Leo pia ni vile. Tukiwa Wakristo, tunajua kuwa Yehova njo Chanzo cha uzima na kuwa uzima wote ni wake. Tunatambua pia kuwa damu ni takatifu na kuwa inamaanisha uzima. Kwa hiyo, tunahakikisha kuwa tunachunguza kanuni za Biblia wakati tunakamata maamuzi yoyote juu ya matunzo yenye kuomba kutumia damu.

KUTUMIA DAMU MU MAMBO YA KINGANGA

10, 11. (a) Namna gani Mashahidi wa Yehova wanaona kutiwa damu ndani ya mishipa, ikuwe damu yote ao sehemu kubwa za damu? (b) Ni maamuzi gani ya kipekee kila Mukristo anapaswa kukamata?

10 Mashahidi wa Yehova wanaelewa kuwa “kujiepusha na . . . damu” hakumaanishe tu kukataa kuikula ao kuikunywa, lakini kunatia ndani mambo mengi zaidi. Inamaanisha kukataa kutiwa damu ndani ya mishipa, kukataa kuitolea watu wengine, na kuepuka kuweka damu yetu wenyewe ili kuirudisha tena ndani ya mwili wetu. Inamaanisha pia kukataa kutiwa moja kati ya sehemu ine kubwa za damu​—chembe nyekundu (globules rouges), chembe nyeupe (globules blancs), vigandisha-damu (plaquettes), na plasma.

11 Zile sehemu ine kubwa za damu zinaweza kugawanywa mu sehemu kidogo-kidogo sana, zenye kuitwa visehemu vya damu. Kila Mukristo anapaswa kuamua kama atatiwa visehemu vya damu ao hapana. Kila Mukristo, anapaswa pia kuamua ikiwa atakubali ao kukataa ufundi fulani wenye unaomba kutumia damu yake mwenyewe. Kila mutu anapaswa kuamua namna damu yake itatumiwa wakati wa upasuaji, wakati wa kupimwa damu, ao wakati wa matunzo yenye kutumiwa wakati huo.​—Ona Mafasirio Ingine ya 21.

12. (a) Sababu gani maamuzi yetu juu ya mambo yenye kuhusu zamiri ni ya maana mbele ya Yehova? (b) Ni nini inaweza kutusaidia kukamata maamuzi yenye hekima kuhusu matunzo?

12 Yehova anahangaikia kabisa maamuzi yenye tunakamata juu ya mambo yenye kuhusu zamiri? Ndiyo, kabisa. Yehova anahangaikia mawazo na nia zetu. (Soma Mezali 17:3; 24:12.) Kwa kuwa ni vile, wakati tunakamata maamuzi juu ya matunzo, tunapaswa kusali kwa Yehova atupatie muongozo mbele ya kutafuta matunzo. Kisha kufanya vile, tunatumia zamiri yetu yenye kuzoezwa na Biblia ili kufanya maamuzi. Hatupaswe kuuliza wengine kama wangefanya nini ikiwa wangekuwa mu hali yetu, na hatupaswe kuruhusu wengine wachochee maamuzi yetu. Kila Mukristo “atabeba muzigo wake mwenyewe.”​—Wagalatia 6:5; Waroma 14:12.

SHERIA ZA YEHOVA ZINAONYESHA KAMA ANATUPENDA

13. Sheria na kanuni za Yehova juu ya damu zinatufundisha nini kumuhusu?

13 Kila jambo lenye Yehova anatuomba tufanye ni kwa faida yetu na linaonyesha kama anatupenda. (Zaburi 19:7-11) Lakini hatumutii kwa sababu tu amri zake zinatuletea faida. Tunamutii juu tunamupenda. Upendo wetu kwa Yehova unatuchochea tuepuke kutiwa damu mu mishipa. (Matendo 15:20) Jambo hilo pia linalinda afya yetu. Leo, watu wengi wanajua hatari fulani za kutiwa damu mu mishipa, na wanganga wengi wanaamini kama kufanya upasuaji bila kutumia damu ni muzuri zaidi kwa afya ya wagonjwa. Ni wazi kama sheria za Yehova ni zenye hekima na zenye upendo.​—Soma Isaya 55:9; Yohana 14:21, 23.

14, 15. (a) Ni sheria gani zenye Yehova alipatia watu wake ili kuwalinda? (b) Namna gani unaweza kutumia kanuni zenye kutegemeza sheria hizo?

14 Tangu zamani sheria za Mungu zimekuwa kwa ajili ya faida ya watu wake. Yehova alipatia Waisraeli wa zamani sheria ili kuwaepusha na aksidenti za mubaya sana. Kwa mufano, sheria moja ilisema kama mutu mwenye kuwa na nyumba, alipaswa kujenga ukuta mufupi wenye kuzunguka sehemu ya juu ya nyumba yake ili mutu asianguke. (Kumbukumbu la Torati 22:8) Sheria ingine ilihusu wanyama. Ikiwa mutu alikuwa na ngombe dume mukali, alipaswa kumuchunga muzuri ili asishambulie mutu ao kumuua. (Kutoka 21:28, 29) Ikiwa Muisraeli hakutii sheria hizo, ingekuwa kosa lake kama mutu angekufa.

15 Kupitia sheria hizo, tunajifunza kama Yehova anaona uzima kuwa wa maana sana. Kujua vile kunaweza kutuchochea kufanya nini? Tunapaswa kuonyesha kuwa tunaheshimia uzima kupitia namna tunatunza nyumba na gari, namna tunatembeza, na namna tunachagua mambo ya kujifurahisha. Watu fulani, zaidi sana vijana, wanawaza kama hakuna jambo la mubaya lenye linaweza kuwapata, kwa hiyo wanajiingiza mu hali za mubaya, na kuzarau hatari yenye inaweza kutokea. Lakini Yehova hapendi tufanye vile. Anapenda tuone uzima wote kuwa wa maana​—ikuwe uzima wetu wenyewe ao uzima wa watu wengine.​—Muhubiri 11:9, 10.

16. Namna gani Yehova anaona kitendo cha kutosha mimba?

16 Yehova anaona uzima wa kila mutu kuwa wa maana. Hata uzima wa mutoto mwenye hajazaliwa ni wa maana kwake. Chini ya Sheria ya Musa, ikiwa mutu alimuumiza bila kujua mwanamuke mwenye mimba na mwanamuke huyo akufe ao mutoto wake, Yehova alimuona ule mutu kuwa muuaji. Hata kama alifanya vile bila kujua, uzima ulipaswa kulipiwa kwa sababu mutu alikuwa amekufa. (Soma Kutoka 21:22, 23.) Mbele ya Mungu, mutoto mwenye hajazaliwa ni mutu mwenye kuishi. Kwa kuwa unajua vile, unawaza Mungu anajisikia namna gani wakati mutu anatosha mimba? Na unawaza anajisikia namna gani wakati anaona mamilioni ya watoto wenye hawajazaliwa wakiuawa kila mwaka?

17. Ni nini inaweza kumufariji mwanamuke mwenye alitosha mimba mbele ya kumujua Yehova?

17 Tuseme nini juu ya mwanamuke mwenye alitosha mimba mbele ajue mawazo ya Yehova juu ya kile kitendo? Anaweza kuwa hakika kama Yehova anaweza kumusamehe kwa musingi wa zabihu ya Yesu. (Luka 5:32; Waefeso 1:7) Mwanamuke mwenye alitosha mimba zamani, hapaswe kujilaumu ikiwa alitubu kikweli. “Yehova ni mwenye rehema na huruma . . . Kama vile mahali jua linatokea kuko mbali sana na mahali jua linashukia, ni vile ametia zambi zetu mbali sana na sisi.”​—Zaburi 103:8-14.

EPUKA MAWAZO YENYE CHUKI

18. Juu ya nini tunapaswa kufanya nguvu yetu yote ili kuepuka mawazo yenye chuki?

18 Kuheshimia zawadi ya uzima yenye Mungu ametupatia kunaanzia ndani ya moyo wetu. Kunatia ndani namna tunajisikia kuhusu wengine. Mutume Yohana aliandika hivi: “Kila mutu mwenye anamuchukia ndugu yake ni muuaji.” (1 Yohana 3:15) Bila kujua, kukosa kupenda mutu fulani kunaweza kufanya tufikie kumuchukia. Chuki inaweza kufanya mutu asiheshimie wengine, aseme mambo ya uongo juu yao, na hata kupenda tu wakufe. Yehova anajua namna tunajisikia kuhusu wengine. (Mambo ya Walawi 19:16; Kumbukumbu la Torati 19:18-21; Matayo 5:22) Ikiwa tunatambua kama tuko na mawazo yenye chuki juu ya mutu fulani, tunapaswa kufanya nguvu yetu yote ili kuachana nayo.​—Yakobo 1:14, 15; 4:1-3.

19. Mawazo ya Yehova juu ya jeuri inapaswa kutuchochea kufanya nini?

19 Kuko njia ingine yenye inaweza kuonyesha kuwa tunaona uzima kuwa wa maana. Kupitia Zaburi 11:5, tunajifunza kama Yehova “anachukia mutu yeyote mwenye kupenda jeuri.” Ikiwa tunachagua kujifurahisha na mambo ya jeuri, pengine ile itaonyesha kama tunapenda jeuri. Juu ya nini tutie maneno, mawazo, na picha zenye jeuri mu akili yetu? Kuliko kufanya vile, tunapenda kujaza mawazo safi na yenye amani mu akili yetu.​—Soma Wafilipi 4:8, 9.

USIKUWE SEHEMU YA MATENGENEZO YENYE HAIHESHIMIE UZIMA

20-22. (a) Namna gani Yehova anaona Ulimwengu wa Shetani? (b) Namna gani watu wa Mungu wanaweza kuonyesha kama “hawako sehemu ya ulimwengu”?

20 Ulimwengu wa Shetani hauheshimie uzima, na Yehova anauona kuwa uko na deni la damu, ni kusema, uko na kosa la kuua. Kwa mamia ya miaka, mamlaka za politike zimefanya mamilioni ya watu wakufe, kutia ndani watumishi wengi wa Yehova. Mu Biblia, mamlaka hizo ao serikali, zinafananishwa na wanyama wakali na wenye jeuri. (Danieli 8:3, 4, 20-22; Ufunuo 13:1, 2, 7, 8) Katika ulimwengu wa leo, kuuzisha silaha ni biashara kubwa. Watu wanapata faida kubwa sana kwa kuuzisha silaha hizo zenye kuua. Ni wazi kuwa, “ulimwengu muzima unakaa katika nguvu za ule muovu.”​—1 Yohana 5:19.

21 Lakini Wakristo wa kweli “hawako sehemu ya ulimwengu.” Watu wa Yehova hawaunge mukono upande wowote mu mambo ya politike na vita. Kama vile tu hawaue, hawaunge pia mukono tengenezo lolote lenye kuua watu. (Yohana 15:19; 17:16) Wakati Wakristo wanateswa, hawatende kwa jeuri. Yesu alifundisha kama tunapaswa kupenda hata maadui wetu.​—Matayo 5:44; Waroma 12:17-21.

22 Dini pia imefanya mamilioni ya watu wakufe. Wakati inazungumuzia Babiloni Mukubwa, ni kusema dini zote za uongo, Biblia inasema hivi: “Ndani yake ilipatikana damu ya manabii na ya watakatifu na ya wale wote wenye wameuawa katika dunia.” Unaelewa ni juu ya nini Yehova anatuambia: “Mutoke kwake, watu wangu”? Wale wenye kumuabudu Yehova hawako sehemu ya dini ya uongo.​—Ufunuo 17:6; 18:2, 4, 24.

23. ‘Kutoka’ katika Babiloni Mukubwa kunatia ndani nini?

23 ‘Kutoka’ katika Babiloni Mukubwa kunatia ndani kuonyesha waziwazi kuwa hatuko tena sehemu ya dini yoyote ya uongo. Kwa mufano, tunapaswa kuhakikisha kuwa jina letu limefutwa ao kuzimwa ku liste ya waamini wa ile dini. Lakini inaomba kufanya mingi zaidi. Tunapaswa pia kuchukia na kuepuka mambo ya mubaya yenye dini ya uongo inafanya. Dini ya uongo inaruhusu na kuchochea mwenendo mubaya, politike na pupa. (Soma Zaburi 97:10; Ufunuo 18:7, 9, 11-17) Kwa miaka mingi, ile imefanya mamilioni ya watu wakufe.

24, 25. Namna gani kumujua Yehova kunaweza kutuletea amani na zamiri ya muzuri?

24 Mbele ya kumujua Yehova, kwa njia fulani, kila mumoja wetu aliunga mukono mambo ya mubaya yenye ulimwengu wa Shetani unafanya. Lakini sasa tumebadilika. Tumekubali bei ya ukombozi na kutoa maisha yetu kwa Mungu. Tunapata “vipindi vya kutuliza . . . kutoka kwa Yehova mwenyewe.” Tuko na amani na zamiri ya muzuri, juu tunajua kama tunamufurahisha Mungu.​—Matendo 3:19; Isaya 1:18.

25 Hata kama wakati fulani tulikuwa sehemu ya tengenezo lenye haliheshimie uzima, Yehova anaweza kutusamehe kwa musingi wa bei ya ukombozi. Tuko wenye shukrani kwa zawadi ya uzima yenye kutoka kwa Yehova. Tunaonyesha shukrani yetu kwa kufanya nguvu yetu yote ili kuwasaidia wengine wajifunze juu ya Yehova, watoke mu ulimwengu wa Shetani, na wakuwe na urafiki wa karibu pamoja na Mungu.​—2 Wakorinto 6:1, 2.

ZUNGUMUZA NA WENGINE JUU YA UFALME

26-28. (a) Ni kazi gani ya pekee yenye Yehova alimupatia Ezekieli? (b) Leo, Yehova anatuomba tufanye nini?

26 Katika Israeli ya zamani, Yehova alimuambia nabii Ezekieli aonye watu kama Yerusalemu ilikuwa karibu kuharibiwa na kuwafundisha mambo walipaswa kufanya ili kuokoka. Kama Ezekieli angekataa kuonya watu, uzima wao ungekuwa juu ya kichwa chake. (Ezekieli 33:7-9) Ezekieli alionyesha kama aliona uzima kuwa wa maana kwa kufanya nguvu yake yote ili kutangaza ule ujumbe wa maana.

27 Yehova ametupatia kazi ya kuonya watu kama hivi karibuni ulimwengu wa Shetani utaharibiwa na kuwasaidia wafikie kumujua Yehova ili waokoke na kuingia mu ulimwengu mupya. (Isaya 61:2; Matayo 24:14) Tunapenda kufanya nguvu yetu yote ili kutangazia watu wengine ule ujumbe. Kama Paulo, tunapenda kusema: “Niko safi kutokana na damu ya watu wote, kwa maana sikuepuka kuwaambia ninyi shauri lote la Mungu.”​—Matendo 20:26, 27.

28 Kuko sehemu zingine za maisha yetu mwenye tunapaswa kuonyesha kama tuko safi. Tutazungumuzia sehemu fulani kati ya zile mu sura yenye kufuata.