Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA 15

Kupigania Uhuru wa Kuabudu

Kupigania Uhuru wa Kuabudu

WAZO KUBWA KATIKA SURA HII

Namna Kristo amesaidia wafuasi wake kupigania haki yao ya kukubaliwa kisheria na haki yao ya kutii sheria za Mungu

1, 2. (a) Ni jambo gani linaonyesha kwamba wewe ni raia wa Ufalme wa Mungu? (b) Sababu gani Mashahidi wa Yehova wamelazimika wakati fulani kupigania uhuru wao wa kuabudu?

WEWE ni raia wa Ufalme wa Mungu? Bila shaka, kwa sababu wewe ni Shahidi wa Yehova! Hauna lazima ya kitambulisho (ao passeport) cha serikali fulani ili kuonyesha jambo hilo. Kwa hiyo, ni nini inaonyesha kwamba wewe kweli ni raia wa Ufalme huo wa Mungu? Ni namna yako ya kumuabudu Yehova Mungu. Ibada ya kweli inamaanisha mambo mengi zaidi ya kuamini tu mafundisho fulani. Inamaanisha pia matendo, ni kusema, kutii sheria za Ufalme wa Mungu. Ibada yetu inaongoza kila jambo katika maisha yetu: namna tunatunza familia yetu na hata namna tunahangaikia aina fulani ya matunzo.

2 Mara nyingi, watu wa ulimwengu hawaheshimu uraia wetu ambao tunafurahia sana ao kanuni za kuwa raia wa Ufalme. Serikali fulani zimejaribu kukataza sehemu fulani za ibada yetu ao kutukataza kabisa-kabisa tusiabudu tena. Wakati fulani, wafuasi wa Kristo wamelazimika kupigania uhuru wao wa kuishi kulingana na sheria za Masiya Mufalme. Hilo ni jambo la kushangaza? Hapana. Historia ya watu wa Yehova wa zamani inaonyesha kwamba mara nyingi watu wa Yehova walilazimika kupigania uhuru wao wa kuabudu.

3. Katika siku za Malkia Esta, watu wa Mungu walilazimika kupigania nini?

3 Kwa mufano, katika siku za Malkia Esta, watu wa Mungu walilazimika kupigania maisha yao. Sababu gani? Waziri Mukubwa Hamani alikuwa mutu mubaya sana. Alimuomba Ahasuero, Mufalme wa Perse, kwamba Wayahudi wote ambao wanapatikana katika utawala wake wauawe kwa sababu “sheria zao ni tofauti na zile za watu wengine wote.” (Esta 3:8, 9, 13) Yehova aliwaachilia watumishi wake? Hapana, Yehova alimusaidia Esta na Mordekai wakati walienda kumuona mufalme wa Perse ili kuwasemea watu wa Mungu.​—Esta 9:20-22.

4. Tutazungumuzia nini katika sura hii?

4 Tuseme nini kuhusu wakati wetu? Kama vile tuliona katika sura ambayo ilitangulia, wakati fulani, serikali zenye nguvu, zilipinga Mashahidi wa Yehova. Katika sura hii, tutazungumuzia njia tatu hivi ambazo serikali hizo zilitumia ili kuzuia sehemu fulani za ibada yetu: (1) haki yetu ya kumutumikia Yehova katika tengenezo lake na kumuabudu kama vile tunapenda, (2) uhuru wetu wa kuchagua namna tunapaswa kutunzwa kulingana na kanuni za Biblia, na (3) haki ya wazazi ya kulea watoto wao kulingana na kanuni za Yehova. Katika kila njia tutaona namna raia waaminifu wa Ufalme wa Masiya wamepigana bila woga ili kulinda haki yao ya kuwa raia wa Ufalme wa Mungu na namna nguvu zao zimebarikiwa.

Kupigania Haki ya Kukubaliwa Kisheria na Kuwa na Uhuru Mbalimbali

5. Kukubaliwa kisheria kunasaidia Wakristo wa kweli watimize mambo gani?

5 Tuna lazima ya kukubaliwa na serikali za wanadamu ili kumuabudu Yehova? Hapana, lakini kukubaliwa kisheria kunatusaidia tuendelee kumuabudu Mungu wetu bila magumu. Kwa mufano, kunafanya tukusanyike waziwazi kwenye Majumba yetu ya Ufame na ya Mikusanyiko, tuchapishe na kusafirisha vichapo vyetu, na pia tuhubirie jirani zetu habari njema waziwazi, bila vizuizi. Katika inchi nyingi, Mashahidi wa Yehova wanakubaliwa kisheria, na kwa hiyo, wana uhuru wa kuabudu kama dini zingine ambazo zinakubaliwa. Lakini, tunafanya nini ikiwa serikali zinakataa kutukubali kisheria, na kujaribu kutuzuia tusitumie uhuru wetu mbalimbali?

6. Mwanzo-mwanzo wa miaka ya 1940 Mashahidi wa Yehova wa Australia walipambana na magumu gani?

6 Australia. Mwanzo wa miaka ya 1940, gavana mukubwa wa Australia alisema kwamba mafundisho yetu yanavunja watu moyo wasiunge vita mukono. Kwa hiyo, kazi ya Mashahidi wa Yehova ilikatazwa. Hawangeweza kukusanyika ao kuhubiri waziwazi, Beteli ilifungwa, na Majumba ya Ufalme yalinyanganywa. Kuwa tu na vichapo vyetu ilionekana kuwa uvunjaji wa sheria. Kisha kutumika kwa uficho muda wa miaka mingi, ndugu wa Australia walipata kitulizo tarehe 14 Mwezi wa 6, 1943. Siku hiyo, Tribinali Kubwa ya Australia iliondoa sheria ambayo ilikuwa inakataza kazi yetu.

7, 8. Fasiria namna ndugu zetu wa Urusi wamepigania uhuru wao wa kuabudu kwa muda wa miaka mingi.

7 Urusi. Kisha miaka mingi ya kukatazwa na serikali ya Ukoministi, Mashahidi wa Yehova waliandikishwa kisheria katika mwaka wa 1991. Kisha kugawanyika kwa Muungano wa Sovieti ya zamani, katika mwaka wa 1992, Mashahidi wa Yehova walikubaliwa na kuandikishwa kisheria katika inchi ya Urusi. Lakini, bila kukawia maadui wetu fulani, zaidi sana wa Kanisa la Ortodoksi la Urusi, walichukizwa sana na ongezeko letu la haraka. Kuanzia mwaka wa 1995 mupaka mwaka wa 1998, wapinzani walipeleka mashitaka tano kwa wakubwa wa serikali, kwamba Mashahidi wa Yehova ni wavunja-sheria. Kila mara muteteaji wa serikali (procureur) hakupata ushahidi ambao unaonyesha kwamba Mashahidi ni wavunja-sheria. Mwishowe, katika mwaka wa 1998, maadui walishitaki tena Mashahidi wa Yehova. Mwanzoni Mashahidi walipata ushindi, lakini maadui wakakataa uamuzi huo na wakaomba uchunguzwe tena. Katika Mwezi wa 5, 2001 maadui wetu wakapewa ushindi. Jambo hilo lilirudiliwa tena Mwezi wa 10 wa mwaka huo na uamuzi ukatolewa katika mwaka wa 2004. Uamuzi huo ulionyesha kwamba Mashahidi wa Yehova hawakubaliwe tena kisheria Mosko na kwamba kazi zao zimekatazwa.

8 Mateso yaliyo kama mvua kubwa yakaanza kuwapata Mashahidi. (Soma 2 Timotheo 3:12.) Walisumbuliwa na kushambuliwa vikali. Vichapo vilinyanganywa; ilikatazwa kabisa kujenga ao kulipia nyumba kwa ajili ya ibada. Fikiria huzuni ya ndugu na dada wakati walikuwa wanapambana na hali hizo ngumu! Katika mwaka wa 2001, Mashahidi walipeleka tena jambo hilo kwenye Tribinali ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya, na katika mwaka wa 2004 walitolea Tribinali hiyo habari zingine zenye kuhitajiwa. Katika mwaka wa 2010, Tribinali ilitoa uamuzi wake. Tribinali iliona kwamba kazi ya Mashahidi ilikatazwa katika Urusi kwa sababu ya ubaguzi. Ikaamua kwamba hakuna sababu ya kukubali uamuzi ambao ulichukuliwa na tribinali za Urusi, kwa sababu hakuna ushahidi ambao unaonyesha kwamba Mashahidi wa Yehova wamefanya kosa fulani. Tribinali ikaonyesha pia kwamba kukatazwa huko kwa Mashahidi kulikuwa tu na kusudi la kuwanyanganya haki zao za kisheria. Uamuzi wa Tribinali ulionyesha kwamba Mashahidi wana haki ya kuwa na uhuru wa dini. Hata kama wakubwa mbalimbali wa serikali ya Urusi hawakufuata uamuzi wa Tribinali ya Haki za Kibinadamu, watu wa Mungu katika inchi ya Urusi wametiwa moyo sana na ushindi huo ambao wamepata.

Titos Manoussakis (Ona fungo la 9)

9-11. Katika inchi ya Ugiriki, namna gani watu wa Yehova wamejikaza kupata uhuru wa kuabudu pamoja, na wamepata matokeo gani?

9 Ugiriki. Katika mwaka wa 1983, Ndugu Titos Manoussakis alilipia jumba fulani katika Heraklion (Crète), ili kikundi kidogo cha Mashahidi wa Yehova kiwe kinafanyia mikutano hapo. (Ebr. 10:24, 25) Bila kukawia, padiri wa dini ya Kiortodoksi alipeleka mashitaka kwa polisi, ili wakataze Mashahidi kutumia jumba hilo. Sababu gani alifanya hivyo? Ni kwa sababu tu mafundisho ya Mashahidi wa Yehova yanatofautiana na ya Dini ya Kiortodoksi! Ndugu Titos Manoussakis na ndugu wengine watatu wa eneo hilo walishitakiwa kuwa wavunja-sheria. Walilipishwa amande na kuhukumiwa kifungo cha miezi mbili. Kwa kuwa wao ni raia wa Ufalme wa Mungu, Mashahidi waliona hukumu hiyo ya tribinali kuwa haiheshimu uhuru wao wa kuabudu. Kwa hiyo, waliendelea kufuatilia jambo hilo kwenye tribinali zingine za inchi, na mwishowe wakapeleka jambo hilo kwenye Tribinali ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya.

10 Katika mwaka wa 1996, Tribinali ilitoa uamuzi ambao haukutazamiwa na ambao ulishitua wapinzani wa ibada safi. Tribinali ilionyesha kwamba dini ya Mashahidi wa Yehova inatimiza mambo ambayo sheria ya Ugiriki inaomba ili “dini iwe yenye kujulikana.” Ikaonyesha pia kwamba tribinali za inchi ya Ugiriki zilivunja “kabisa haki ya uhuru wa dini” ya Mashahidi. Tribinali hiyo Kubwa ikaonyesha pia kwamba si kazi ya serikali kuamua kwamba “mafundisho ya dini fulani ndio ya kweli ao kuamulia dini njia ambazo itatumia ili kuhubiri mafundisho yake.” Kwa hiyo, Tribinali ilivunja uamuzi wa serikali ya Ugiriki, na ikaonyesha kwamba Mashahidi wana haki ya kuabudu kwa uhuru!

11 Ushindi huo ulimaliza magumu ya ndugu katika Ugiriki? Kwa huzuni, mambo hayakuwa hivyo. Katika mwaka wa 2012, jambo lingine kama hilo ambalo lilitetewa kwa karibu miaka 12, liliamuliwa katika muji wa Kassandreia, Ugiriki. Ni askofu fulani wa dini ya Kiortodoksi ndiye alipeleka mashitaka kwa wakubwa wa serikali. Baraza Kubwa la Inchi, ambalo ni tribinali kubwa zaidi katika Ugiriki, iliamua jambo hilo na ikawapatia watu wa Mungu ushindi. Tribinali ilitoa uamuzi huo kwa kutumia katiba ya inchi ya Ugiriki ambayo inaruhusu uhuru wa dini na ikatupilia mbali mashitaka ya mara kwa mara kwamba Mashahidi wa Yehova si dini ambayo inajulikana. Tribinali ilisema hivi: “Mafundisho ya ‘Mashahidi wa Yehova’ hayafundishwe kwa siri, na kwa hiyo, dini yao ni yenye kujulikana.” Ndugu wa kutaniko ndogo la muji wa Kassandreia wamefurahi kwamba wanaweza sasa kufanya mikutano yao katika Jumba la Ufalme.

12, 13. Katika inchi ya Ufaransa, namna gani maadui wamejaribu ‘kutunga matatizo kwa njia ya sheria,’ na matokeo ilikuwa nini?

12 Ufaransa. Maadui wa watu wa Mungu wametumia njia ya ‘kutunga matatizo kwa njia ya amri [sheria].’ (Soma Zaburi 94:20.) Kwa mufano, katikati ya miaka ya 1990, wakubwa wa serikali ya Ufaransa wenye kuangalia mambo ya kodi, walianza kufanya uchunguzi juu ya matumizi ya feza ya Association Les Témoins de Jéhovah (ATJ), hilo ni jina la shirika ambalo linajulikana kisheria ambalo Mashahidi wa Yehova wanatumia katika inchi ya Ufaransa. Waziri wa mambo ya feza alifunua kusudi la kweli la uchunguzi huo kwa kusema hivi: “Uchunguzi huo ungefanya majengo na mali yote ya tawi ya Ufaransa yanyanganywe na serikali ao kufanya Mashahidi wa Yehova wahukumiwe kama wavunja-sheria . . .  Jambo hilo lingefanya kazi zao mbalimbali zisifanywe kama inavyofaa ao zisifanywe tena katika inchi yetu.” Hata kama wakubwa wenye kuangalia mambo ya kodi waliona kwamba Association Les Témoins de Jéhovah haina deni yoyote, waliilazimisha kulipa kodi ya feza nyingi sana. Ikiwa mupango huo ungefanikiwa, ndugu zetu wangelazimika kufunga biro ya tawi na kuuzisha majengo ya biro hiyo ili kulipa kodi hiyo ya feza nyingi sana. Jambo hilo lilikuwa jaribu kubwa sana, lakini watu wa Mungu hawakuvunjika moyo. Kwa uhodari, Mashahidi walikataa kodi hiyo isiyo ya haki, na mwishowe katika mwaka wa 2005, wakapeleka jambo hilo kwenye Tribinali ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya.

13 Tribinali hiyo ilitoa uamuzi wake tarehe 30 Mwezi wa 6, 2011. Ilionyesha kwamba kuheshimia uhuru wa dini kunapaswa kuzuia inchi, kuamua “ikiwa mafundisho ya dini fulani ndio ya kweli ao kuamua njia ambazo dini itatumia ili kuhubiri mafundisho yake. Inaweza kufanya hivyo tu ikiwa dini hiyo inavuka mipaka. Tribinali ilisema pia kwamba: “Kulipishwa kodi hivyo . . . kulifanya shirika hilo la Mashahidi wa Yehova lisitumie mali yake, na jambo hilo lilifanya Mashahidi wa Yehova wasifanye sehemu mbalimbali za ibada yao kwa uhuru.” Waamuzi wote wa Tribinali hiyo walipatia Mashahidi wa Yehova ushindi! Watu wa Yehova walifurahi sana, kwa sababu, mwishowe serikali ya Ufaransa iliwarudishia Mashahidi wa Yehova feza zote za kodi ambazo walikuwa wamekwisha kuwanyanganya na ikawatilia faida. Na kwa kutii maagizo ya Tribinali, serikali iliondoa uamuzi ambao ilikuwa nao wa kunyanganya majengo ya Beteli ili kulipia deni.

Unaweza kuendelea kusali kwa ajili ya ndugu na dada ambao wanateseka leo kwa sababu wanatendewa isivyo haki kisheria

14. Wewe pia, namna gani unaweza kuunga mukono ndugu ambao wanapigania uhuru wa kuabudu?

14 Kama Esta na Mordekai wa hapo zamani, watu wa Yehova leo wanapigania uhuru wa kumuabudu Yehova kama vile ameamuru. (Esta 4:13-16) Unaweza pia kuwaunga mukono? Ndiyo. Unaweza kuendelea kusali kwa ajili ya ndugu na dada ambao wanateseka leo kwa sababu wanatendewa isivyo haki kisheria. Sala kama hizo zinaweza kusaidia sana ndugu na dada zetu ambao wanapambana na hali ngumu na ambao wanateseka kwa sababu ya imani yao. (Soma Yakobo 5:16.) Yehova anajibu sala hizo? Ushindi mbalimbali ambao tumepata kwenye tribinali unashuhudia jambo hilo!​—Ebr. 13:18, 19.

Uhuru wa Kuchagua Matunzo Kulingana na Imani Yetu

15. Kuhusu matumizi ya damu, watu wa Mungu wanafikiria mambo gani?

15 Kama vile tulijifunza katika Sura ya 11, raia wa Ufalme wa Mungu wamepokea muongozo ulio wazi wa Maandiko ambao unawakataza kutumia damu vibaya, tabia ambayo imeenea sana leo. (Mwa. 9:5, 6; Law. 17:11; soma Matendo 15:28, 29.) Hata kama hatukubali kutiwa damu, sisi na watu ambao tunapenda, tunataka tupate matunzo mazuri kadiri iwezekanavyo, ikiwa tu hayapingane na sheria za Mungu. Tribinali kubwa za inchi mbalimbali zimekubali kwamba mutu ana haki ya kuchagua ao kukataa matunzo fulani kulingana na zamiri yake ao imani yake. Lakini, katika inchi fulani, watu wa Mungu wamepambana na hali ngumu kuhusiana na jambo hilo. Acha tuone mifano fulani.

16, 17. Katika hospitali moja ya Japani, ni matunzo gani waganga walimutolea dada ambayo yalifanya dada awashitaki, na namna gani sala zake zilijibiwa?

16 Japani. Dada Misae Takeda, aliyekuwa na miaka 63, alipaswa kufanyiwa upasuaji. Kwa sababu yeye ni raia mwaminifu wa Ufalme wa Mungu, alimuambia waziwazi muganga kwamba anapenda kutunzwa bila kutiwa damu. Lakini kisha miezi fulani, aliumia sana kusikia kwamba alitiwa damu wakati alifanyiwa upasuaji. Dada Takeda alijisikia kwamba ametendwa isivyo haki na kudanganywa. Kwa hiyo, Mwezi wa 6, 1993, alishitaki muganga huyo na pia hospitali. Dada huyo munyenyekevu na mupole, alikuwa na imani yenye nguvu sana. Hata kama dada huyo alikuwa na nguvu kidogo tu, alishuhudia bila kuogopa mbele ya watu wengi katika chumba cha tribinali. Alifanya hivyo akiwa mwenye kusimama kwa muda wa zaidi ya saa moja. Alipatikana tena kwenye tribinali kwa mara ya mwisho mwezi moja mbele ya kufa kwake. Wewe haushangazwe na uhodari wake na imani yake? Dada Takeda alisema kwamba aliendelea kumuomba Yehova amusaidie kupigana vita hiyo. Alikuwa hakika kwamba Yehova angejibu sala zake. Tunaweza kusema kwamba sala zake zilijibiwa?

17 Miaka tatu kisha kifo cha Dada Takeda, Tribinali Kubwa Zaidi ya Japani ilimupatia ushindi na kusema kwamba ilikuwa vibaya kumutia damu kinyume na mapenzi yake. Uamuzi ambao ulitolewa tarehe 29 Mwezi wa 2, 2000, ulionyesha kwamba “haki ya kuamua” katika jambo hilo “inapaswa kuheshimiwa na kuonwa kuwa ni haki ya mutu.” Kwa sababu Dada Takeda alipigania sana uhuru wake wa kuchagua matunzo ambayo yanategemea zamiri iliyofundishwa na Biblia, Mashahidi wa Yehova wa Japani wanaweza kutunzwa bila kuogopa kutiwa damu kinyume na mapenzi yao.

Pablo Albarracini (Ona fungo la 18 mupaka 20)

18-20.(a) Namna gani uamuzi ambao Tribinali Kubwa Zaidi ya Arjentina ilitoa uliunga mukono haki ya mutu ya kukataa kutiwa damu kupitia karte Instructions médicales? (b) Kuhusu damu, namna gani tunaweza kuonyesha kwamba tunapenda kuongozwa na Kristo?

18 Arjentina. Namna gani raia wa Ufalme wanajitayarisha wakati inaomba kuchukua uamuzi kuhusu matunzo fulani wakati wamepoteza ufahamu? Tunaweza kuwa na kikaratasi chetu ambacho kinakubaliwa na sheria na ambacho kinaweza kutusemea wakati tumepoteza ufahamu. Ni vile ndugu Pablo Albarracini alikuwa amefanya. Katika Mwezi wa 5, 2012, ndugu huyo alipigwa masasi na wezi ambao walitaka kuiba mahali fulani. Kwa hiyo, alipelekwa kwenye hospitali. Kwa sababu alikuwa amepoteza ufahamu, haikuwezekana afasirie musimamo wake kuhusiana na kutiwa damu. Hata hivyo, alikuwa na karte ambayo inaonyesha waganga mapenzi ya mutu ya kukataa kutiwa damu, ambayo alikuwa amejaza kumepita zaidi ya miaka ine. Hata kama maisha yake yalikuwa katika hatari sana na kwamba waganga fulani waliona kwamba iliomba kumutia damu ili kumuokoa, waganga walikuwa wametayarishwa kupitia karte hiyo kuheshimu mapenzi yake. Hata hivyo, baba ya Pablo ambaye hakuwa Shahidi wa Yehova, alipewa ruhusa na tribinali ya kuenda kinyume na mapenzi ya mutoto wake.

19 Muteteaji wa bibi ya ndugu Pablo alienda mara moja kwenye Tribinali. Kisha saa fulani, Tribinali ilivunja uamuzi wa tribinali hiyo ndogo, na ikaamua kwamba waganga wanapaswa kuheshimia mapenzi ya ndugu Pablo ambayo yanapatikana kwenye karte yake. Uamuzi huo ulimusukuma baba ya ndugu Pablo, kupeleka jambo hilo kwenye Tribinali Kubwa Zaidi ya Arjentina. Lakini Tribinali hiyo ilionyesha kwamba “hakuna sababu yoyote ya kushakia kwamba ndugu Pablo alijaza kwa kupenda, kwa uangalifu na kwa uhuru [karte ambayo inaonyesha musimamo wake wa kukataa kutiwa damu].” Tribinali hiyo ilisema hivi : “Kila mutu muzima iko na uwezo wa kuonyesha mbele ya wakati namna anapenda kutunzwa, na anaweza kukubali ao kukataa aina fulani ya matunzo . . . Maagizo hayo yanapaswa kuheshimiwa na kila muganga.”

Umejaza karte yako Instructions médicales?

20 Mwishowe ndugu Albarracini alipona kabisa. Yeye na bibi yake walifurahi sana kuona kwamba walijaza karte hiyo. Kwa kufanya jambo hilo ndogo, lakini la maana sana, walionyesha kwamba walipenda kuongozwa na Kristo Mufalme wa Ufalme wa Mungu. Wewe na familia yako mumejaza karte hiyo pia?

April Cadoreth (Ona fungu la 21 mupaka 24)

21-24.(a) Namna gani Tribinali Kubwa Zaidi ya Kanada ilifikia kutoa uamuzi ambao unahusu vijana wa chini ya miaka 16 na matumizi ya damu? (b) Habari hii, inaweza kuchochea vijana Mashahidi wa Yehova kufanya nini?

21 Kanada. Kwa kawaida, tribinali zinakubali kwamba wazazi wana haki ya kuchagulia watoto wao matunzo mazuri. Wakati fulani, tribinali zimeamua kwamba, maamuzi ya vijana walio chini ya miaka 16 kuhusiana na namna ya kutunzwa yanapaswa kuheshimiwa. Jambo kama hilo lilimufikia dada April Cadoreth. Wakati alikuwa na miaka 14, April alipelekwa kwenye hospitali kwa sababu damu ilikuwa inamutoka katika sehemu za ndani ya mwili. Miezi kidogo mbele ya hapo, alijaza karte Instructions médicales ambayo inaonyesha kwamba hapaswe kutiwa damu hata kama anapatikana katika hali mbaya sana. Muganga ambaye alipokea April alichagua kutoheshimia mapenzi yake ambayo yalikuwa wazi na akaomba ruhusa kwenye tribinali ili amutie damu. Dada huyo alitiwa damu kwa nguvu. Mwishowe dada April alifananisha jambo hilo na ubakaji (ao kulalwa kinguvu).

22 Dada April na wazazi wake walipeleka jambo hilo kwenye tribinali ili wapewe haki yao. Kisha miaka mbili, tatizo lao lilichunguzwa na Tribinali Kubwa Zaidi ya Kanada. Hata ikiwa April alishindwa kulingana na yale katiba inasema juu ya matunzo kuhusu mutoto wa chini ya miaka 16, Tribinali iliamua kwamba waamuzi walipaswa kumupatia nafasi ya kujiamulia namna angetunzwa na pia kwamba watoto wengine walio chini ya miaka 16 wanapaswa kupewa nafasi hiyo. Tribinali hiyo ilisema hivi: “Kuhusu mambo ya matunzo, vijana walio chini ya miaka 16 wanapaswa kupewa nafasi ya kutoa maoni yao juu ya uamuzi fulani ambao unahusiana na aina fulani ya matunzo. Kwa kufanya hivyo, wanaonyesha kwamba wamekomaa kabisa kiakili na kwamba wanaweza kutoa mawazo yao kwa uhuru.”

23 Uamuzi huo ulikuwa wa maana sana, kwa sababu Tribinali Kubwa ilitolea vijana walio chini ya miaka 16 haki yao ya kisheria. Mbele ya uamuzi huo kutolewa, Tribinali ya Kanada ingeweza kuruhusu mutoto wa chini ya miaka ya 16 atolewe aina fulani ya matunzo, ikiwa inaona kwamba matunzo hayo yatamusaidia sana mutoto huyo. Lakini kisha uamuzi huo kutolewa, tribinali haingeweza tena kuruhusu matunzo yoyote ambayo yako kinyume na mapenzi ya kijana aliye chini ya miaka 16 bila kumupatia nafasi ya kuonyesha kwamba amekomaa kiakili na kwamba anaweza kujichukulia maamuzi.

“Ninajisikia kuwa mwenye furaha sana wakati ninajua kwamba nimetoa muchango kidogo ili kutukuza jina la Mungu na kuonyesha kwamba Shetani ni muongo”

24 Kupigania haki kwa miaka tatu kulikuwa jambo la lazima kabisa? April anasema, “Ndiyo!” April ambaye ni mwenye afya nzuri leo na painia wa kudumu, anasema hivi: “Ninajisikia kuwa mwenye furaha sana wakati ninajua kwamba nimetoa muchango kidogo ili kutukuza jina la Mungu na kuonyesha kwamba Shetani ni muongo.” Mambo ambayo dada April alikutana nayo yanaonyesha kwamba vijana wetu wanaweza kuonyesha kwamba wao ni raia wa kweli wa Ufalme wa Mungu kwa kuchukua musimamo kwa uhodari.​—Mt. 21:16.

Uhuru wa Wazazi Kulea Watoto Wao Kulingana na Kanuni za Yehova

25, 26. Kisha tu wazazi kuvunja ndoa, ni tatizo gani linatokea wakati fulani?

25 Yehova amewapatia wazazi daraka la kulea watoto kulingana na kanuni zake. (Kum. 6:6-8; Efe. 6:4) Hilo ni daraka ngumu, zaidi sana katika familia ambamo bibi na bwana wamevunja ndoa. Wazazi wanaweza kuwa na maoni tofauti kuhusu namna ya kulea watoto wao. Kwa mufano, muzazi ambaye ni Shahidi anaweza kupenda sana kulea watoto kulingana na kanuni za Kikristo, lakini muzazi ambaye si Shahidi anaweza kukataa jambo hilo. Ni kweli kwamba kuvunja ndoa kunaweza kumaliza uhusiano kati ya bibi na bwana, lakini, muzazi ambaye ni Shahidi anapaswa kujua kwamba jambo hilo halimuzuie kulea watoto wake.

26 Muzazi asiye Shahidi anaweza kuomba kwenye tribinali ruhusa ya kulea mutoto ao watoto ili aweze kufuatilia malezi yao ya kidini. Watu fulani wanasema kwamba kuacha watoto watunzwe na Shahidi wa Yehova inaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya mutoto. Wanaweza kukazia kwamba watoto watakosa mambo fulani kama vile, sherehe za siku ya kuzaliwa, karamu mbalimbali, na kwamba wakati mutoto anagonjwa na inaomba ashugulikiwe kwa haraka, muzazi Shahidi atakataa mutoto atiwe damu ambayo inaweza “kuokoa maisha yake.” Jambo la kufurahisha ni kwamba, tribinali nyingi zinachunguza jambo ambalo linaweza kuletea zaidi mutoto faida, wala si mambo ya dini ya wazazi. Acha tuchunguze mifano fulani.

27, 28. Tribinali Kubwa Zaidi ya Ohio ilisema nini kuhusu shitaka la kwamba mutoto akilelewa na muzazi ambaye ni Shahidi hilo linaweza kuwa na matokeo mabaya juu yake?

27 Amerika (États-Unis). Katika mwaka wa 1992, Tribinali Kubwa Zaidi ya Ohio, ilichunguza tatizo moja ambamo baba ambaye si Shahidi alisema kwamba kuacha mutoto wake mwanaume alelewe kama Shahidi wa Yehova kutakuwa na matokeo mabaya juu ya mutoto huyo. Tribinali ndogo ilikuwa imekubali baba daraka la kulea mutoto wake. Lakini mama yake Jennifer Pater, alipewa haki ya kumutembelea mutoto, na akaambiwa kwamba haruhusiwe hata kidogo “kufundisha mutoto mafundisho yoyote ya Mashahidi wa Yehova.” Uamuzi huo ambao tribinali ndogo ilitoa ulimaanisha kwamba Dada Pater hana ruhusa ya kuzungumuza na mutoto wake mwanaume Bobby, kuhusu Biblia ao kuhusu kanuni za mwenendo ambazo zinapatikana katika Biblia! Ingekuwa wewe, ungejisikia namna gani? Jambo hilo lilimuhangaisha sana Jennifer, lakini akasema kwamba alijifunza kuwa muvumilivu na kungojea Yehova atende. Anakumbuka hivi: “Sikuzote Yehova alikuwa pamoja nami.” Muteteaji wake ambaye alisaidiwa na biro ya Betheli ambayo inasimamia mambo ya sheria, alipeleka jambo hilo kwenye Tribinali Kubwa Zaidi ya Ohio.

28 Tribinali Kubwa ilipinga uamuzi wa tribinali hiyo ndogo na kusema kwamba “wazazi wana haki ya kufundisha watoto wao, na pia kuzungumuza nao juu ya kanuni za mwenendo na za dini.” Tribinali ilisema kwamba ikiwa hakuna ushahidi wowote unaoonyesha kwamba mafundisho ya Mashahidi wa Yehova yanaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya afya ya mwili ao ya akili ya mutoto, tribinali haikukuwa na haki ya kuzuia muzazi kulea mutoto kwa sababu tu ya dini yake. Tribinali haikupata ushahidi wowote unaoonyesha kwamba mafundisho ya Mashahidi yanaweza kuwa na matokeo mabaya juu ya afya ya mwili na ya akili ya mutoto.

Tribinali nyingi ziliamua kuwapatia wazazi Wakristo daraka la kulea watoto

29-31. Sababu gani dada mumoja katika inchi ya Danemark alinyanganywa daraka la kumulea mutoto wake, na Tribinali Kubwa Zaidi ya Danemark ilitoa uamuzi gani juu ya jambo hilo?

29 Danemark. Dada Anita Hansen alipambana na tatizo kama hilo wakati bwana yake wa zamani alienda kwenye tribinali ili apewe daraka la kumulea mutoto wake wa miaka 7 ambaye anaitwa Amanda. Hata kama tribinali ya wilaya yake ilimupatia Dada Hansen daraka la kulea mutoto katika mwaka wa 2000, baba ya Amanda alienda kwenye tribinali kubwa, na tribinali hiyo ikamupatia daraka la kulea mutoto. Tribinali hiyo kubwa ilisema kwamba kwa sababu mabishano yao yanatokana na dini ya kila mumoja, ni baba tu ndiye ana daraka la kuamua ni dini gani mutoto anapaswa kufuata. Kwa hiyo Dada Hansen alinyanganywa daraka la kumulea Amanda kwa sababu yeye ni Shahidi wa Yehova!

30 Katika hali hiyo, Dada Hansen alivurugika akili sana na hakujua atasema nini katika sala. Alisema hivi: “Lakini mawazo ya andiko la Waroma 8:26 na 27 yalinitia moyo sana. Kila mara nilijisikia kwamba Yehova alielewa mambo ambayo nilitaka kumuomba katika sala. Yehova alikuwa ananitazama na kila mara alikuwa pamoja nami.”​—Soma Zaburi 32:8; Isaya 41:10.

31 Dada Hansen alipeleka jambo hilo kwenye Tribinali Kubwa Zaidi ya Danemark. Tribinali hiyo iliamua hivi: “Uamuzi juu ya tatizo ambalo linahusu kulea watoto unapaswa kutegemea mambo ambayo yatakuwa na faida juu ya mutoto.” Tena ilisema hivi: Uamuzi kuhusu ni nani ambaye atalea mutoto unapaswa kutegemea namna kila muzazi anatatua matatizo, lakini haupaswe kutegemea “imani na musimamo” wa Mashahidi wa Yehova. Kwa hiyo, Tribinali iliona kwamba Dada Hansen ndiye anastahili kabisa kuwa muzazi na ikamurudishia daraka la kumulea Amanda. Jambo hilo lilimutuliza sana.

32. Namna gani Tribinali ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya ililinda wazazi Mashahidi wasibaguliwe?

32 Inchi mbalimbali katika Ulaya. Katika hali fulani, mabishano kuhusu ni nani ana daraka la kulea mutoto yametoka kwenye tribinali kubwa zaidi za inchi na kupelekwa kwenye Tribinali ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya (THKU). Kwa hiyo, Tribinali ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya imechunguza pia jambo hilo. Katika mashitaka mawili, Tribinali ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya iliona kwamba tribinali za inchi zilifanya ubaguzi wakati wa kushugulikia tatizo ambalo linahusu muzazi Shahidi na muzazi asiye Shahidi kwa sababu tu ya dini. Kuhusu matendo hayo ya ubaguzi, Tribinali hiyo iliamua kwamba “hairuhusiwe kubagua wazazi kwa sababu tu ya dini.” Mama mumoja Shahidi ambaye alifaidika na uamuzi huo wa Tribinali ya Haki za Kibinadamu ya Ulaya alifurahi sana. Alisema hivi: “Ni jambo lenye kuumiza sana kushitakiwa kwamba ninatendea watoto wangu vibaya, wakati nilikuwa ninafanya yote ambayo ninaweza ili kuwapatia mambo ambayo yatawaletea faida, ni kusema, malezi ya Kikristo.”

33. Namna gani wazazi Mashahidi wanaweza kutumia kanuni ambayo inapatikana katika andiko la Wafilipi 4:5?

33 Kwa kweli, wazazi Mashahidi ambao wanapigania haki ya kufundisha watoto wao kanuni za Biblia wanajikaza kuonyesha usawaziko. (Soma Wafilipi 4:5.) Kwa hiyo, wakati wanafurahia haki yao ya kulea watoto katika njia za Mungu, wanakubali pia kwamba muzazi ambaye si Shahidi, ikiwa anapenda, anaweza pia kutoa muchango wake ili kutimiza madaraka yake ya muzazi. Namna gani muzazi ambaye ni Shahidi wa Yehova anaweza kuonyesha kwamba anachukua daraka la kufundisha mutoto kwa uzito?

34. Mufano wa Wayahudi wa siku za Nehemia unaweza kuwafundisha nini wazazi Wakristo leo?

34 Mufano wa siku za Nehemia unaweza kutufundisha. Wayahudi walitumika sana ili kutengeneza na kujenga upya kuta za Yerusalemu. Walijua kwamba kufanya hivyo kungewalinda na kulinda familia zao na mashambulio ya mataifa adui ambayo yaliwazunguka. Kwa hiyo, Nehemia aliwatia moyo hivi: ‘Mupigane kwa ajili ya ndugu zenu, wana wenu na binti zenu, wake zenu na nyumba zenu.’ (Neh. 4:14) Kwa Wayahudi hao, ilikuwa ni jambo la lazima sana kupigana. Leo pia, wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova wanajikaza sana kulea watoto wao katika kweli. Wanajua kwamba watoto wao wanashambuliwa na mawazo mabaya ya marafiki wao na wanafunzi wenzao. Hata nyumbani wanaweza kushambuliwa na mawazo mabaya kupitia vyombo kama televizyo ao Internete. Kwa hiyo, wazazi musisahau hata kidogo kwamba munapaswa kufanya nguvu yenu yote ili kuwalinda watoto wenu na kuwasaidia waishi katika hali ya usalama ambayo itawasaidia kufanya maendeleo ya kiroho.

Uwe Hakika Kwamba Yehova Atategemeza Ibada ya Kweli

35, 36. Mashahidi wa Yehova wamepata faida gani kwa sababu ya kupigania haki yao ya kuabudu, na umeazimia kufanya nini?

35 Kwa kweli, Yehova amebariki nguvu ambazo tengenezo lake limetumia leo ili kupigania haki ya kuabudu kwa uhuru. Kwa kupigania haki yao, watu wa Mungu wamepata mara nyingi nafasi ya kutoa ushahidi wenye nguvu mbele ya watu wengi na kwenye tribinali. (Rom. 1:8) Faida ingine ni kwamba ushindi ambao wamepata umesaidia watu wengi ambao si Mashahidi kupata haki zao. Hata hivyo, kwa sababu sisi ni watu wa Mungu hatuna kusudi la kubadilisha hali ya maisha ya watu; wala hatujitafutie sifa. Ikiwa Mashahidi wa Yehova wamepigania haki yao kwenye tribinali mbalimbali, sababu kubwa ni kwamba wanataka ibada safi ijulikane kisheria na isonge mbele.​—Soma Wafilipi 1:7.

36 Wale wote ambao wamepigana ili tupate uhuru wa kumuabudu Yehova wametuachia mufano muzuri wa imani. Tusamini sana mufano wao na tuige imani yao! Acheni tuendelee kuwa waaminifu na kuwa hakika kwamba Yehova anategemeza kazi yetu na pia anaendelea kutupatia nguvu ili kufanya mapenzi yake.​—Isa. 54:17.