Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 25

Anaponyesha Mutu Mwenye Ukoma kwa Huruma

Anaponyesha Mutu Mwenye Ukoma kwa Huruma

MATAYO 8:1-4 MARKO 1:40-45 LUKA 5:12-16

  • YESU ANAPONYESHA MUTU MWENYE UKOMA

Wakati Yesu na wanafunzi wake ine wanaenda wakihubiri katika “masinagogi yao katika Galilaya yote,” habari juu ya mambo ya ajabu yenye Yesu iko anafanya inaenea sana. (Marko 1:39) Habari juu ya matendo yake inafika mupaka muji fulani kwenye kuko mwanaume mumoja mwenye kuwa na ukoma. Munganga Luka anazungumuzia mwanaume huyo kuwa “mwenye kujaa ukoma.” (Luka 5:12) Wakati unakolea, ugonjwa huu wenye kuogopesha unaharibu polepole sehemu mbalimbali za mwili.

Kwa hiyo, hali ya mutu huyo mwenye ukoma iko katika hatari na analazimika kuishi mbali na wengine. Zaidi ya hilo, anapaswa kusema kwa sauti kubwa “Mimi siko safi, mimi siko safi!” wakati watu wako karibu; kwa kufanya hivyo, anasaidia watu wasimukaribie sana na kuwa katika hatari ya kuambukizwa. (Mambo ya Walawi 13:45, 46) Lakini mutu huyo mwenye ukoma anafanya nini sasa? Anamukaribia Yesu na kuinama mbele yake, na kumuomba: “Bwana, kama tu unataka, unaweza kunifanya kuwa safi.”—Matayo 8:2.

Mutu huyo iko kabisa na imani katika Yesu! Na ugonjwa wake umemufanya akuwe katika hali yenye kuhuzunisha! Yesu atatenda namna gani? Ungekuwa pale, wewe ungefanya nini? Kwa huruma, Yesu ananyoosha mukono wake na kugusa kabisa mwanaume huyo. Yesu anamuambia hivi: “Ninataka! Kuwa safi.” (Mathayo 8:3) Inaweza kuwa vigumu kuamini, palepale ukoma wa mwanaume huyo unasafishwa.

Ungependa kuongozwa na mufalme mwenye huruma na mwenye kuwa na uwezo kama Yesu? Namna Yesu anatendea mutu huyo mwenye ukoma inatuhakikishia kuwa wakati Yesu atakuwa Mufalme juu ya dunia yote, unabii huu wa Biblia utatimia: “Atamusikilia huruma mutu wa hali ya chini na maskini, na ataokoa uzima wa maskini.” (Zaburi 72:13) Bila shaka, Yesu atafikia kutimiza tamaa ya moyo wake ya kusaidia wote wenye kuteseka.

Kumbuka kama hata mbele Yesu aponyeshe mutu huyo mwenye ukoma, utumishi wake umekuwa ukiletea watu furaha nyingi. Sasa watu watasikia habari juu ya muujiza huo wenye amefanya. Lakini, Yesu hapendi watu waonyeshe imani katika yeye kwa kutegemea tu mambo yenye wanasikia kupitia wengine. Anajua unabii wenye kusema kuwa “hatafanya sauti yake isikike katika barabara,” ni kusema, kufanya mambo ili tu kujiletea utukufu. (Isaya 42:1, 2) Kwa hiyo, Yesu anaambia mutu huyo mwenye ameponyesha ukoma: “Fanya angalisho, usiambie mutu yeyote, lakini uende, ujionyeshe kwa kuhani, na utoe zawadi yenye Musa aliagiza.”—Matayo 8:4.

Lakini kama vile unaweza kuwazia, mwanaume huyo ni mwenye furaha sana kwa sababu ameponyeshwa hivi kwamba hawezi kuchunga siri juu ya mambo yenye yametoka tu kufanyika. Anaenda na kutangaza habari fasi yote. Watu wanapendezwa zaidi na jambo hilo na wanapenda kujua mengi zaidi, hivi kwamba Yesu hawezi kuenda waziwazi katika muji fulani. Kwa hiyo anabakia kwa wakati fulani mahali kwenye hakuna watu. Hata hivyo, watu wenye kutoka maeneo mbalimbali wanakuja ili awafundishe na kuwaponyesha.