Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 59

Mwana wa Binadamu Ni Nani?

Mwana wa Binadamu Ni Nani?

MATAYO 16:13-27 MARKO 8:22-38 LUKA 9:18-26

  • YESU ANAPONYESHA MWANAUME MUMOJA KIPOFU

  • PETRO ANAPEWA FUNGUO ZA UFALME

  • YESU ANATABIRI KIFO NA UFUFUO WAKE

Yesu na wanafunzi wake wanafika Betsaida. Kisha watu wanamuletea Yesu mwanaume mumoja mwenye kuwa kipofu na wanamuomba amuguse ili amuponyeshe.

Yesu anakamata mwanaume huyo kwenye mukono na kuenda naye inje ya kijiji. Kisha kutema mate kwenye macho ya mwanaume huyo, Yesu anamuuliza hivi: “Unaona kitu fulani?” Mwanaume huyo anajibu hivi: “Ninaona watu, lakini wanaonekana kama miti yenye kutembea-tembea.” (Marko 8:23, 24) Yesu anaweka mikono yake juu ya macho ya mutu huyo na anaanza kuona. Kisha anaambia mwanaume huyo mwenye sasa anaweza kuona muzuri aende nyumbani, na anamuambia asiingie katika kijiji.

Kisha, Yesu na wanafunzi wake wanasafiri kuenda upande wa kaskazini katika eneo la Kaisaria Filipi. Kijiji hicho kiko juu kwenye mulima, na inaomba kutembea kilometre 40 hivi ili kufika huko. Kinapatikana pia kwenye metre 350 juu ya usawa wa bahari, na kwenye upande wa kaskazini-mashariki, kunapatikana Mulima Hermoni ambao unafunikwa na teluji. Inawezekana safari hiyo inawachukua siku mbili hivi.

Wakati fulani katika safari yao, Yesu anaenda peke yake ili kusali. Kunabakia tu karibu miezi kenda ao kumi mbele ya kifo chake, na anahangaikia wanafunzi wake. Hivi karibuni, wengi wameacha kumufuata, na inaonekana kuwa wengine wanavurugika na kuvunjika moyo. Pengine wako wanajiuliza sababu gani alikataa watu wamufanye kuwa mufalme ao sababu gani alikataa kuleta alama ili kuonyesha kabisa yeye ni nani na kumaliza mashaka.

Wakati wanafunzi wanamufuata nafasi kwenye iko anasali, Yesu anauliza hivi: “Watu wanasema Mwana wa binadamu ni nani?” Wanamujibu hivi: “Wamoja wanasema Yohana Mubatizaji, wengine Eliya, na wengine pia wanasema Yeremia ao mumoja wa manabii.” Ndiyo, watu wanafikiri kuwa Yesu anaweza kuwa mumoja wa wanaume hao mwenye amefufuliwa. Ili kujua mawazo yao, Yesu anauliza wanafunzi wake hivi: “Lakini ninyi munasema mimi ni nani?” Petro anajibu bila kukawia: “Wewe ndiye Kristo, Mwana wa Mungu mwenye kuishi.”—Matayo 16:13-16.

Yesu anaambia Petro kama anapaswa kufurahi kuwa ni Mungu ndiye amemufunulia jambo hilo, na anaongeza hivi: “Ninakuambia: Wewe ni Petro, na juu ya mwamba huu nitajenga kutaniko langu, na milango mikubwa ya Kaburi haitalipita nguvu.” Yesu anapenda kusema kama yeye mwenyewe atajenga kutaniko na kama hata Kaburi halitakuwa na uwezo juu ya watu wa kutaniko hilo ikiwa wanabakia waaminifu katika maisha yao duniani. Anaahidi Petro hivi: “Nitakupatia funguo za Ufalme wa mbinguni.”—Matayo 16:18, 19.

Yesu hamufanye Petro kuwa mukubwa kuliko mitume wengine, ao Yesu hamufanye Petro kuwa musingi wa kutaniko. Yesu mwenyewe ndiye Mwamba kwenye kutaniko litajengwa. (1 Wakorintho 3:11; Waefeso 2:20) Lakini, Petro anapaswa kupokea funguo tatu. Atakuwa na pendeleo la kufungulia vikundi vya watu nafasi ya kuingia katika Ufalme wa mbinguni.

Petro angetumia funguo ya kwanza kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33 wakati wetu, kwa kuonyesha Wayahudi na wageuzwa-imani wenye kutubu kile wanapaswa kufanya ili waokolewe. Angetumia funguo ya pili ili kufungulia Wasamaria wenye kuamini nafasi ya kuingia katika Ufalme wa mbinguni. Kisha, katika mwaka wa 36 wakati wetu, Petro angetumia funguo ya tatu ili kutolea nafasi hiyo watu wa Mataifa wenye hawatahiriwe, Kornelio na wengine.—Matendo 2:37, 38; 8:14-17; 10:44-48.

Katika mazungumuzo haya, mitume wa Yesu wanavurugika wakati anatabiri mateso na kifo chenye anakaribia kupata katika Yerusalemu. Petro haelewe kuwa Yesu anapaswa kufufuliwa ili kuenda mbinguni, kwa hiyo anaenda na Yesu pembeni na kumukemea kwa kumuambia hivi: “Jitendee kwa fazili, Bwana; mambo hayo hayatakupata hata kidogo.” Lakini Yesu anageuzia Petro mugongo na kumujibu hivi: “Pita nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu unawaza mawazo ya wanadamu, lakini haiko mawazo ya Mungu.”—Matayo 16:22, 23.

Sasa Yesu anaita wanafunzi wengine zaidi ya mitume wake na kuwaelezea kuwa haitakuwa mwepesi kuwa mufuasi wake. Anasema hivi: “Kama mutu yeyote anataka kunifuata, lazima ajikane mwenyewe, achukue muti wake wa mateso na aendelee kunifuata. Kwa maana kila mutu mwenye anataka kuokoa uzima wake ataupoteza, lakini kila mutu mwenye anapoteza uzima wake kwa ajili yangu na kwa ajili ya habari njema atauokoa.”—Marko 8:34, 35.

Kwa kweli, ili wanafunzi wa Yesu wakubaliwe naye, wanapaswa kuwa na ujasiri na roho ya kujitoa. Yesu anasema hivi: “Kila mutu mwenye ananisikilia haya mimi na maneno yangu katika kizazi hiki chenye uzinifu na chenye zambi, Mwana wa binadamu pia atamusikilia haya wakati atakuja katika utukufu wa Baba yake pamoja na malaika watakatifu.” (Marko 8:38) Ndiyo, wakati Yesu atakuja, “atalipa kila mutu kulingana na mwenendo wake.”—Matayo 16:27.