Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 51

Mutu Anauawa Wakati wa Karamu ya Sikukuu ya Kuzaliwa

Mutu Anauawa Wakati wa Karamu ya Sikukuu ya Kuzaliwa

MATAYO 14:1-12 MARKO 6:14-29 LUKA 9:7-9

  • HERODE ANATOA AMRI ILI YONANA MUBATIZAJI AKATWE KICHWA

Wakati mitume wa Yesu wako wanaendelea na kazi yao ya kuhubiri katika Galilaya, mutu mwenye alitanguliza Yesu hana uhuru kama huo. Yohana Mubatizaji angali katika gereza na amefanya karibu miaka mbili humo.

Yohana alisema waziwazi kuwa haiko muzuri Mufalme Herode Antipa achukue Herodia, bibi ya ndugu-nusu yake Filipo, akuwe bibi yake. Herode alivunja ndoa na bibi yake wa kwanza ili aoe Herodia. Kulingana na Sheria ya Musa, sheria yenye Herode anajitapa kuwa anafuata, ndoa hiyo ni ya uzinifu na haipatane na sheria. Kwa sababu Yohana ameonyesha kuwa ni mubaya kufanya hivyo, Herode anamutupa katika gereza; pengine Herodia ndiye alimuchochea afanye hivyo.

Herode hajue ni jambo gani anaweza kumufanyia Yohana, kwa sababu watu ‘wanamuona kuwa nabii.’ (Matayo 14:5) Lakini, Herodia anajua kile anaweza kumufanyia Yohana. Herodia “alimuwekea Yohana kinyongo,” na kwa kweli, anaendelea kutafuta njia ya kumuua. (Marko 6:19) Mwishowe, nafasi inajitokeza.

Muda kidogo mbele ya Pasaka ya mwaka wa 32 Wakati Wetu, Herode anafanya karamu kubwa kwa ajili ya sikukuu ya kuzaliwa kwake. Watu wa Herode wenye cheo cha juu na viongozi wa jeshi, na pia watu wenye kujulikana sana wa Galilaya, wanakuja kwenye karamu hiyo. Wakati wa karamu, Salome, mutoto mwanamuke wa Herodia mwenye alizaa na Filipo, bwana yake wa kwanza, anatumwa ili kucheza dansi kwa ajili ya wageni. Watu wanapendezwa sana na namna yake ya kucheza.

Herode anafurahishwa sana na binti-nusu yake; kwa hiyo, anamuambia hivi: “Niombe kila kitu chenye unataka, na nitakupatia.” Anafikia hata kumuapia, kwa kusema: “Kila kitu chenye utaniomba, nitakupatia, hata nusu ya ufalme wangu.” Mbele ya kujibu, Salome anaondoka na kuenda kuuliza mama yake: “Niombe nini?”—Marko 6:22-24.

Hii ndiyo nafasi yenye Herodia alikuwa anatafuta! Anajibu bila kukawia: “Kichwa cha Yohana Mubatizaji.” Palepale, Salome anarudia kwa Herode na ombi lake: “Ninataka unipatie sasa hivi kwenye sahani kichwa cha Yohana Mubatizaji.”—Marko 6:24, 25.

Jambo hilo linahuzunisha sana Herode, lakini wageni wake walimusikia wakati alikuwa anamuapia Salome. Atasikia haya ikiwa hatimize ombi hilo, hata kama hilo litamuomba kuua mutu mwenye hakufanya kosa. Kwa hiyo, Herode anatuma mulinzi na kumupatia maagizo ili kufanya jambo lenye kuleta huzuni sana. Bila kukawia, mulinzi huyo anarudia na kichwa cha Yohana Mubatizaji kwenye sahani. Anamupatia Salome, mwenye anakipeleka kwa mama yake.

Wakati wanafunzi wa Yohana wanasikia jambo hilo, wanakuja na kuchukua mwili wake na kuutia katika kaburi. Kisha wanamupelekea Yesu habari hiyo.

Kisha muda fulani, wakati Herode anasikia kuwa Yesu iko anaponyesha watu na kufukuza pepo wachafu, anaogopa. Anajiuliza ikiwa mutu mwenye kufanya mambo hayo, ni kusema, Yesu, ndiye Yohana Mubatizaji mwenye sasa “amefufuliwa kutoka kwa wafu.” (Luka 9:7) Kwa hiyo, Herode Antipa anatafuta sana kumuona Yesu. Kwa kweli, haiko juu ya kusikia mafundisho ya Yesu. Lakini, Herode anapenda kumuona Yesu ili kuhakikisha ikiwa anapaswa kuogopa ao hapana.