Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 96

Yesu Anamujibu Mutawala Kijana Mwenye Kuwa Tajiri

Yesu Anamujibu Mutawala Kijana Mwenye Kuwa Tajiri

MATAYO 19:16-30 MARKO 10:17-31 LUKA 18:18-30

  • TAJIRI ANAULIZA KUHUSU UZIMA WA MILELE

Yesu angali anasafiri kupitia Perea kuenda Yerusalemu. Kijana mumoja tajiri anakimbia kwenye Yesu iko na kupiga magoti mbele yake. Yeye ni mumoja wa ‘watawala,’ pengine anatumika akiwa musimamizi katika sinagogi ao ni mumoja wa wale wenye kufanyiza Sanhedrini. Anauliza Yesu hivi: “Mwalimu Mwema, ninapaswa kufanya nini ili niriti uzima wa milele”—Luka 8:41; 18:18; 24:20.

Yesu anamujibu: “Sababu gani unaniita mwema? Hakuna mutu mwema isipokuwa mumoja tu, Mungu.” Pengine mwanaume kijana huyo anatumia neno “mwema” kama jina la cheo, kama vile marabi wanafanya. Hata kama Yesu anajua kufundisha muzuri, anapenda mwanaume huyo ajue kama cheo, “Mwema” inamustahili tu Mungu.

Yesu anamushauri hivi: “Kama unataka kuingia katika uzima, ushike amri sikuzote.” Kwa hiyo kijana mwanaume huyo anauliza: “Amri gani?” Yesu anataja amri tano kati ya Amri Kumi, kuhusu kuua, kuzini, kuiba, kutoa ushahidi wa uongo, na kuheshimia wazazi. Kisha anaongeza amri ya maana sana: “Unapaswa kumupenda jirani yako kama wewe mwenyewe.”—Matayo 19:17-19.

Mwanaume huyo anajibu hivi: “Nimeshika yote hayo, nifanye tena nini?” (Matayo 19:20) Pengine anafikiri kwamba hajafanya jambo fulani la ujasiri, lenye litafanya astahili kupata uzima wa milele. Yesu anatambua kwamba ombi lake linatoka katika moyo, kwa hiyo ‘anamupenda.’ (Marko 10:21) Lakini, kuko kikwazo mbele ya mwanaume huyo.

Anapenda sana mali yake, kwa hiyo Yesu anamuambia hivi: “Unakosa jambo moja: Enda, uuzishe vitu vyenye uko navyo na upatie maskini, na utakuwa na hazina mbinguni; kisha ukuje ukuwe mufuasi wangu.” Ndiyo, mwanaume huyo angeweza kugawanya feza zake kwa maskini, wenye hawangemurudishia kitu, na kuwa mwanafunzi wa Yesu. Lakini pengine Yesu anamuangalia kwa huruma wakati anaona akisimama na kuenda akiwa mwenye kuhuzunika. Mwanaume huyo anapenda sana mali yake, “vitu [vyake] vingi,” vinamufunga macho ili asione hazina ya kweli. (Marko 10:21, 22) Yesu anasema: “Itakuwa vigumu sana kwa wale wenye kuwa na feza kuingia katika Ufalme wa Mungu!”—Luka 18:24.

Wanafunzi wanashangaa sana kusikia maneno hayo na maneno haya mengine yenye Yesu anasema: “Ni vyepesi zaidi kwa ngamia kupita katika tundu la sindano ya kushonea kuliko tajiri kuingia katika Ufalme wa Mungu.” Hilo linachochea wanafunzi kuuliza: “Ni nani basi anaweza kuokolewa?” Je, kuokolewa ni jambo la nguvu sana lenye mutu hawezi kufikia? Yesu anawaangalia na kujibu: “Mambo yenye hayawezekane kwa wanadamu yanawezekana kwa Mungu.”—Luka 18:25-27.

Petro anaonyesha kama wao wamefanya uamuzi wa muzuri tofauti na ule mwanaume kijana tajiri. Anasema: “Angalia! Tumeacha vitu vyote na tumekufuata; basi, tutapata nini?” Yesu anaonyesha matokeo ya uamuzi wao wa muzuri. Anasema hivi: “Katika uumbaji-mupya, wakati Mwana wa binadamu atakaa kwenye kiti chake cha ufalme chenye utukufu, ninyi wenye mumenifuata mutakaa pia katika viti vya ufalme kumi na mbili (12), mukihukumu makabila kumi na mbili (12) ya Israeli.”—Matayo 19:27, 28.

Ni wazi kwamba Yesu anafikiria wakati wenye kuja duniani, wakati kutakuwa uumbaji mupya wa hali zenye zilikuwa katika shamba la Edeni. Petro na wanafunzi wengine watapata zawabu yao kwa kutawala pamoja na Yesu juu ya dunia Paradiso. Kwa kweli hiyo ni zawabu yenye inapita vitu vyote vyenye waliacha.

Lakini, hawatapata zawabu tu wakati wenye kuja. Wanapata zawabu ingine kuanzia sasa. Yesu anasema: “Hakuna mutu mwenye ameacha nyumba ao bibi ao ndugu ao wazazi ao watoto kwa ajili ya Ufalme wa Mungu mwenye hatapata mara nyingi zaidi katika kipindi hiki cha wakati, na katika mupangilio wa mambo wenye unakuja, uzima wa milele.”—Luka 18:29, 30.

Ndiyo, kote kwenye wanafunzi wake wanaenda, wanaweza kufurahia undugu pamoja na waabudu wenzao, undugu wa sana na wenye samani sana kuliko hata ule wa watu wa familia moja ya kimwili. Jambo lenye kuhuzunisha ni kwamba, inaonekana kama ule mwanaume kijana tajiri atapoteza baraka hiyo na zawabu ya kuishi katika Ufalme wa mbinguni wa Mungu.

Yesu anaongeza: “Lakini wengi wenye ni wa kwanza watakuwa wa mwisho na wa mwisho watakuwa wa kwanza.” (Matayo 19:30) Anapenda kusema nini?

Kijana tajiri iko kati ya wale wa “kwanza,” kwa sababu iko kati ya wale viongozi wa Wayahudi. Kwa kushika amri za Mungu, anaonyesha kama iko na uwezo mukubwa na alikuwa na wakati wenye kuja muzuri wa kiroho. Lakini angali anatanguliza mali na vitu vyake vingine katika maisha yake. Tofauti na yeye, watu wa kawaida wa inchi wanatambua kwamba mafundisho ya Yesu ni ya kweli na ni njia ya uzima. Kwa maneno mengine, walikuwa wa “mwisho,” lakini sasa wanakuwa wa “kwanza.” Wanaweza kutazamia kukaa kwenye viti vya ufalme huko mbinguni pamoja na Yesu wakitawala juu ya dunia Paradiso.