Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 94

Mambo Mbili ya Lazima Sana​—Sala na Unyenyekevu

Mambo Mbili ya Lazima Sana​—Sala na Unyenyekevu

LUKA 18:1-14

  • MUFANO WA MUJANE MWENYE ANAENDELEA KUOMBA

  • MUFARISAYO NA MUKUSANYA-KODI

Yesu amekwisha kutolea wanafunzi wake mufano kuhusu kuendelea kusali. (Luka 11:5-13) Pengine iko sasa katika Samaria ao katika Galilaya, na anakazia tena kwamba ni jambo la lazima kuendelea kusali. Anafanya hivyo kwa kutumia mufano huu mwengine:

“Katika muji fulani kulikuwa muamuzi mwenye hakukuwa anamuogopa Mungu wala kumuheshimia mwanadamu. Katika muji huo, kulikuwa pia mujane fulani mwenye alikuwa anamuendea na kusema, ‘Hakikisha kwamba ninapata haki kutoka kwa mushitaki wangu.’ Ndiyo, kwa wakati fulani alikuwa anakataa, lakini kisha wakati fulani akasema katika moyo wake, ‘Hata kama simuogope Mungu na simuheshimie mwanadamu yeyote, kwa sababu mujane huyu anaendelea kunisumbua, nitahakikisha kwamba anapata haki, ili asiendelee kuja na kunichokesha na ombi lake.’”—Luka 18:2-5.

Yesu anatoa maana ya mufano huo, kwa kusema: “Musikie mambo yenye ule muamuzi alisema hata kama hakukuwa anafanya mambo yenye kuwa sawa! Kwa hakika, je, Mungu hatahakikisha kuwa haki imefanywa kwa ajili ya wachaguliwa wake wenye wanamulilia muchana na usiku, wakati yeye anaendelea kuwavumilia?” (Luka 18:6, 7) Kwa hiyo, Yesu anafundisha nini kuhusu Baba yake?

Bila shaka, Yesu hapendi kusema kama Yehova Mungu anafanana kwa namna yoyote na muamuzi huyo mwenye hafanye mambo yenye kuwa sawa. Anazungumuzia wazo tofauti: Ikiwa muamuzi mwanadamu mwenye hafanye mambo yenye kuwa sawa anafikia kutimiza ombi la mutu mwenye kuendelea kumuomba, bila shaka Mungu pia atafanya hivyo. Yeye ni Mungu mwenye haki na mwema, na atajibu ikiwa watu wake wanaendelea kusali kwake. Tunaweza kuona hilo kupitia mambo yenye Yesu anaongezea: “Ninawaambia ninyi, [Mungu] atahakikisha kwamba wanatendewa haki haraka.”—Luka 18:8.

Mara nyingi watu wa hali ya chini na maskini hawatendewe kwa haki, lakini watu wenye kuwa na mamlaka na matajiri wanapendelewa. Mungu yeye hafanye vile. Kwa wakati wake, atatenda kwa haki kwa kuhakikisha kwamba waovu wanaharibishwa na kwamba watumishi wake wanapata uzima wa milele.

Ni nani wenye kuwa na imani kama ya ule mujane? Ni watu wangapi wanaamini kabisa kama Mungu “atahakikisha kwamba wanatendewa haki haraka”? Yesu ametoka kuonyesha kwamba ni jambo la maana kuendelea kusali. Sasa, kuhusu kuwa na imani katika uwezo wa sala, Yesu anauliza: “Wakati Mwana wa binadamu atafika, je, kweli atapata imani hii katika dunia?” (Luka 18:8) Yesu anapenda kuonyesha kama, wakati atafika, inawezekana haiko watu wengi ndio watakuwa na imani kama hiyo.

Watu fulani wenye wanamusikiliza Yesu wanajiona kuwa wako na imani. Wanajitumainia kwamba ni wenye haki, hata kama wanazarau wengine. Kwa watu kama hao, Yesu anatoa mufano huu:

“Watu wawili walienda katika hekalu ili kusali, mumoja alikuwa Mufarisayo na mwingine alikuwa mukusanya-kodi. Ule Mufarisayo akasimama na kuanza kusali katika moyo wake, ‘Ee Mungu, ninakushukuru kwa sababu mimi siko kama watu wengine wote—wanyanganyi, watu wenye hawafanye mambo yenye kuwa sawa, wazinifu—ao hata kama mukusanya-kodi huyu. Ninafunga mara mbili kwa juma; ninatoa sehemu moja ya kumi (1/10) ya kila kitu chenye ninapata.’”—Luka 18:10-12.

Wafarisayo wanajulikana kuwa watu wenye kujionyesha mbele ya watu kwamba wao ni watu wenye kufanya mambo yenye kuwa sawa. Wanafanya hivyo ili kushangaza watu. Kwa kawaida siku zenye wanafunga ili kujionyesha ni Siku ya Kwanza na Siku ya Ine, siku zenye masoko makubwa yanajaa watu, wakati wenye watu wengi watawaona. Na wanatoa kwa ukamili sehemu ya kumi hata ya mimea midogo. (Luka 11:42) Miezi fulani yenye ilipita, walionyesha namna wanazarau watu wa kawaida kwa kusema: “Watu hawa wenye hawaujue sheria [kulingana na maoni ya Wafarisayo] ni watu wenye kulaaniwa.”—Yohana 7:49.

Yesu anaendelea na mufano wake: “Hata hivyo ule mukusanya-kodi alikuwa amesimama mbali kidogo, na hakutaka hata kuinua macho yake kuelekea mbinguni, lakini alikuwa anajipiga-piga kwenye kifua, akisema, ‘Ee Mungu, nihurumie, mimi mutenda-zambi.’” Ndiyo, mukusanya-kodi anajua kwa unyenyekevu uzaifu wake. Yesu anamalizia hivi: “Ninawaambia ninyi, mutu huyu alishuka kuenda kwenye nyumba yake na akaonekana kuwa anafanya mambo yenye kuwa sawa mbele ya Mungu kuliko ule Mufarisayo. Kwa sababu kila mutu mwenye kujiinua atapatishwa haya, lakini kila mutu mwenye kujinyenyekeza atainuliwa.”—Luka 18:13, 14.

Kwa hiyo, Yesu anaonyesha kuwa ni jambo la maana kuwa wanyenyekevu. Hilo ni shauri lenye faida kwa wanafunzi wake, wenye wamekomalia katika eneo kwenye Wafarisayo wanaishi; Wafarisayo wenye kujiona kuwa watu wenye kufanya mambo yenye kuwa sawa na wenye kutafuta tu cheo na ukubwa. Na hilo ni shauri la maana kwa wafuasi wote wa Yesu.