Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 109

Anakemea Waziwazi Viongozi Wa Dini Wenye Kumupinga

Anakemea Waziwazi Viongozi Wa Dini Wenye Kumupinga

MATAYO 22:41–23:24 MARKO 12:35-40 LUKA 20:41-47

  • KRISTO NI MWANA WA NANI?

  • YESU ANAFUNUA UNAFIKI WA WATU WENYE KUMUPINGA

Viongozi wa dini wenye kumupinga Yesu wanashindwa kumuharibishia Yesu sifa ao kumunasa katika mutego ili wamutoe kwa Waroma. (Luka 20:20) Sasa, wakati angali kwenye hekalu tarehe 11 Mwezi wa Nisani, Yesu anawageukia na kuwaonyesha yeye ni nani. Yeye ndiye anaanzisha mazungumuzo. Anawauliza hivi: “Munawaza nini juu ya Kristo? Yeye ni mwana wa nani?” (Matayo 22:42) Inajulikana muzuri kwamba Kristo, ao Masiya, anapaswa kuwa katika kizazi cha Daudi. Na ni hivyo wanamujibu.—Matayo 9:27; 12:23; Yohana 7:42.

Yesu anauliza: “Basi, sababu gani Daudi kwa kuongozwa na roho anamuita Kristo Bwana, wakati anasema, ‘Yehova alimuambia Bwana wangu: “Kaa kwenye mukono wangu wa kuume mupaka niweke maadui wako chini ya miguu yako”’? Basi, kama Daudi anamuita Bwana, yeye ni mwana wake namna gani?”—Matayo 22:43-45.

Wafarisayo wanabakia kimya, kwa sababu wanatumainia kupata mutu wa kizazi cha Daudi ili awakomboe kutoka katika mikono ya Waroma. Lakini akitumia maneno ya Daudi yenye kupatikana katika Zaburi 110:1, 2, Yesu anaonyesha kwamba Masiya hapaswe kuwa tu mutawala mwanadamu. Yeye ni Bwana wa Daudi, na kisha kukaa kwenye mukono wa kuume wa Mungu, ataanza kutawala. Jibu la Yesu linanyamazisha waandishi na Wafarisayo.

Wanafunzi na wengine wengi wamekuwa wakisikiliza. Sasa Yesu anaanza kuzungumuza nao na kuwaambia wafanye angalisho na waandishi na Wafarisayo. Wao “wamejiikalisha katika kiti cha Musa” ili kufundisha Sheria ya Mungu. Yesu anaelezea hivi wasikilizaji wake: “Mambo yote yenye wanawaambia, muyafanye na kuyashika, lakini musitende kulingana na matendo yao, kwa maana wao wanasema lakini hawatende mambo yenye wanasema.”—Matayo 23:2, 3.

Kisha Yesu anawapatia mifano ya unafiki wao, na kusema: “Kwa maana wanapanua visanduku vyenye kuwa na maandiko ndani vyenye wanavaa kama ulinzi.” Wayahudi fulani walivaa kwenye paji la uso ao kwenye mukono visanduku vidogo kama hivyo vyenye vilikuwa na maneno ya Sheria. Wafarisayo wananenepesha visanduku vyao ili kuonyesha watu kama wako na bidii kuhusu Sheria. Tena, “wanarefusha sehemu za chini za nguo zao.” Waisraeli walipaswa kutia uzi kwenye sehemu ya chini ya nguo zao, lakini Wafarisayo walirefusha sehemu hizo za chini kwenye nguo zao. (Hesabu 15:38-40) Wanafanya yote hayo “ili waonekane na watu.”—Matayo 23:5.

Hata wanafunzi wa Yesu wangeambukizwa na tamaa hiyo ya kutaka makubwa, kwa hiyo anawashauria hivi: “Lakini ninyi, musiitwe Rabi, kwa maana Mwalimu wenu ni mumoja, na ninyi wote ni ndugu. Zaidi ya hayo, musiite mutu yeyote baba yenu duniani, kwa maana Baba yenu ni mumoja, Ule wa mbinguni. Wala musiitwe viongozi, kwa maana Kiongozi wenu ni mumoja, Kristo.” Kwa hiyo basi, wanafunzi wanapaswa kuwa na mawazo gani juu yao na wanapaswa kutenda namna gani? Yesu anawaambia: “Lakini mwenye kuwa mukubwa zaidi kati yenu anapaswa kuwa mutumishi wenu. Kila mutu mwenye kujiinua atanyenyekezwa, na kila mutu mwenye kujinyenyekeza atainuliwa.”—Matayo 23:8-12.

Tena, Yesu anatangazia waandishi na Wafarisayo wanafiki ole mbalimbali zenye kufuatana. Anasema hivi: “Ole kwenu, waandishi na Wafarisayo, wanafiki! kwa sababu munafungia watu Ufalme wa mbinguni; kwa maana ninyi wenyewe hamuingie, na wale wenye wanataka kuingia munawazuia.”—Matayo 23:13.

Yesu anakemea Wafarisayo sababu hawajue mambo ya maana kulingana na mawazo ya Yehova. Kwa mufano, wanasema: “Kama mutu yeyote anaapa kwa hekalu, hakuna ubaya; lakini kama mutu yeyote anaapa kwa zahabu ya hekalu, anapaswa kutimiza kiapo chake.” Kwa kukazia sana akili yao juu ya zahabu yenye kuwa kwenye hekalu kuliko kukazia ibada yenye inapaswa kutolewa kwenye hekalu, wanaonyesha kwamba wao ni vipofu. Na ‘wamepuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, ni kusema, haki, rehema, na uaminifu.’—Matayo 23:16, 23; Luka 11:42.

Yesu anaita Wafarisayo hawa ‘viongozi vipofu, wenye kuchuya imbu lakini wanameza ngamia!’ (Matayo 23:24) Wanatosha imbu katika divai yao wakati wa karamu kwa sababu kidudu hicho hakiko safi. Lakini kupuuza mambo mazito ya Sheria ni kama vile kumeza ngamia mwenye pia wakati wa karamu ni munyama muchafu, tena mukubwa sana.—Mambo ya Walawi 11:4, 21-24.