Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 102

Mufalme Anaingia Yerusalemu Akiwa Juu ya Mwana-punda

Mufalme Anaingia Yerusalemu Akiwa Juu ya Mwana-punda

MATAYO 21:1-11, 14-17 MARKO 11:1-11 LUKA 19:29-44 YOHANA 12:12-19

  • YESU ANAINGIA YERUSALEMU KWA USHINDI

  • ANATABIRI UHARIBIFU WA YERUSALEMU

Siku yenye kufuata, ni kusema, Siku ya Yenga, tarehe 9 mwezi wa Nisani, Yesu anatoka Betania pamoja na mitume wake na kuenda Yerusalemu. Wakati wanakaribia Betfage, kwenye Mulima wa Mizeituni, Yesu anaambia wawili kati ya wanafunzi wake:

“Muende katika kijiji chenye munaona mbele yenu, na mara moja mutakuta punda amefungwa, na mwana-punda pamoja naye. Muwafungue na kuniletea. Mutu fulani akiwaambia jambo lolote, munapaswa kumuambia, ‘Bwana iko na lazima yao.’ Mara moja ataacha ule punda na mwana-punda.”—Matayo 21:2, 3.

Wanafunzi wanashindwa kutambua kwamba maagizo yenye Yesu anawapatia yanategemea unabii wa Biblia. Lakini, kisha wakati kupita wanaelewa kwamba ilikuwa kutimizwa kwa unabii wa Zekaria. Zekaria alikuwa ametabiri kwamba Mufalme wa Mungu mwenye aliahidiwa, angeingia Yerusalemu akiwa “munyenyekevu, na amepanda juu ya punda, juu ya mwana-punda, mwana wa punda-jike.”—Zekaria 9:9.

Wakati wanafunzi wanafika Betfage na kubeba mwana-punda pamoja na mama yake, watu wenye kusimama karibu wanauliza hivi: “Sababu gani munafungua mwana-punda huyo?” (Marko 11:5) Lakini wakati wanasikia kwamba Bwana iko na lazima ya wanyama hao, wanaacha wanafunzi wawapeleke kwa Yesu. Wanafunzi wanatia nguo zao za inje juu ya punda na juu ya mwana-punda wake, lakini Yesu anapanda juu ya mwana-punda.

Vile Yesu iko anakaribia Yerusalemu, ni vile watu wanakuwa wengi. Watu wengi wanatandika nguo zao kwenye barabara. Wengine wanakata matawi yenye kuwa na “majani katika mashamba” na kuyatandika. Wanasema hivi kwa sauti kubwa: “Umuokoe, tunaomba! Amebarikiwa ule mwenye anakuja katika jina la Yehova! Ubarikiwe Ufalme wenye unakuja wa baba yetu Daudi!” (Marko 11:8-10) Wakati Wafarisayo wenye kuwa kati ya watu wanasikia maneno hayo, wanakasirika. Wanaambia Yesu hivi: “Mwalimu, kemea wanafunzi wako.” Yesu anawajibu hivi: “Ninawaambia ninyi, kama hawa wangebakia kimya, majiwe yangesema kwa sauti kubwa.”—Luka 19:39, 40.

Wakati Yesu anaona Yerusalemu, anaanza kuulilia na kusema: “Kama wewe, ndiyo, wewe ungetambua leo mambo yenye kuleta amani—lakini sasa yamefichwa ili usiyaone.” Muji wa Yerusalemu utapata matokeo mabaya kwa sababu ya kukataa kutii kimakusudi. Yesu anatabiri hivi: “Maadui wako watajenga ngome ya miti yenye kuchongwa kukuzunguka na watakuzunguka na kukusonga kutoka kila upande. Watakuangusha chini wewe na watoto wenye kuwa ndani yako, na hawataacha jiwe juu ya jiwe ndani yako.” (Luka 19:42-44) Maneno ya Yesu yanatimia wakati Yerusalemu inaharibiwa katika mwaka wa 70 wakati wetu.

Wakati Yesu anaingia Yerusalemu, ‘muji wote unakuwa katika fujo, na watu wanauliza: “Huyu ni nani?”’ Watu wengi wanaendelea kusema: “Huyu ndiye nabii Yesu wa Nazareti ya Galilaya!” (Matayo 21:10, 11) Watu wenye kuwa katikati ya watu wengi, wenye waliona Yesu akifufua Lazaro, wanaambia watu wengine juu ya muujiza huo. Wafarisayo wananungunika kwa sababu hawaone tena jambo la kufanya. Wanaambiana hivi: “Ulimwengu wote umemufuata.”—Yohana 12:18, 19.

Kama tu kawaida yake, wakati anatembelea Yerusalemu, Yesu anaenda kwenye hekalu ili kufundisha. Huko anaponyesha vipofu na vilema. Wakati wakubwa wa makuhani na waandishi wanaona mambo yenye iko anafanya na wakati wanasikia watoto katika hekalu wakisema kwa sauti kubwa, “Okoa, tunaomba, Mwana wa Daudi!” wanakasirika. Viongozi wa dini wanauliza Yesu hivi: “Unasikia mambo yenye hawa wanasema?” Yesu akawaambia: “Ndiyo. Je, hamujasoma jambo hili, ‘Kutoka katika kinywa cha watoto wadogo na watoto wenye kunyonya umetokeza sifa’?”—Matayo 21:15, 16.

Yesu anaangalia vitu vyenye kuwa pembeni yake ndani ya hekalu. Sasa wakati umesonga, na Yesu anaondoka pamoja na mitume wake. Mbele Nisani 10 ianze, anarudia Betania, kwenye analala Siku ya Yenga.