Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 121

“Musiogope! Mimi Nimepata Ushindi juu ya Ulimwengu”

“Musiogope! Mimi Nimepata Ushindi juu ya Ulimwengu”

YOHANA 16:1-33

  • KARIBUNI MITUME HAWATAMUONA TENA YESU

  • HUZUNI YA MITUME ITAGEUKA KUWA FURAHA

Yesu na mitume wake wanajitayarisha kuondoka katika chumba cha juu kwenye walikulia chakula cha Pasaka. Kisha kuwaonya sana, Yesu anaongeza hivi: “Nimewaambia ninyi mambo haya ili musikwazike.” Sababu gani maonyo hayo yalikuwa yenye kufaa? Anawaambia hivi: “Watu watawafukuza ninyi katika sinagogi. Kwa kweli, saa inakuja wakati kila mutu mwenye atawaua ninyi atawaza amemutolea Mungu utumishi mutakatifu.”—Yohana 16:1, 2.

Pengine habari hiyo inaogopesha mitume. Hata kama Yesu alikuwa amesema kuwa ulimwengu ungewachukia, hakuwaambia moja kwa moja kuwa wangeuawa. Sababu gani? Anasema hivi: “Sikuwaambia mambo haya mwanzoni, kwa sababu nilikuwa pamoja na ninyi.” (Yohana 16:4) Sasa anawaonya mbele ya kuondoka. Hilo lingeweza kuwasaidia wasikwazike kisha hapo.

Yesu anaendelea kusema hivi: “Ninaenda kwa Ule mwenye alinituma; na bado hakuna hata mumoja wenu mwenye ananiuliza, ‘Unaenda wapi?’” Mangaribi hiyo walikuwa wamemuuliza juu ya mahali kwenye alikuwa anaenda. (Yohana 13:36; 14:5; 16:5) Lakini sasa wanaogopa kwa sababu ya mambo yenye alisema juu ya mateso, na hilo linawaletea huzuni sana. Kwa hiyo, wanashindwa kuuliza maulizo mengine juu ya utukufu wenye atapata ao kumuuliza ikiwa hilo litakuwa na matokeo gani juu ya waabudu wa kweli. Yesu anasema hivi: “Kwa sababu nimewaambia mambo haya, huzuni imejaa katika mioyo yenu.”—Yohana 16:6.

Kisha, Yesu anaeleza hivi: “Ninaenda kwa faida yenu. Kwa maana kama siende, musaidizi hatakuja kwenu; lakini kama ninaenda, nitamutuma kwenu.” (Yohana 16:7) Wanafunzi wanaweza kupata roho takatifu ikiwa tu Yesu anakufa na kuenda mbinguni; anaweza kutuma roho hiyo kama musaidizi kwa watu wake nafasi yoyote katika dunia.

Roho takatifu ‘itatolea ulimwengu uhakikisho wenye kusadikisha juu ya zambi na juu ya mambo yenye kuwa sawa na juu ya hukumu.’ (Yohana 16:8) Ndiyo, kosa la ulimwengu la kushindwa kuonyesha imani katika Mwana wa Mungu litaonyeshwa waziwazi. Wakati Yesu atapanda mbinguni jambo hilo litatoa ushuhuda wa uadilifu wake na kuonyesha kuwa Shetani, “mutawala wa ulimwengu huu,” anastahili kupewa hukumu kali.—Yohana 16:11.

Yesu anaendelea kusema hivi: “Ningali na mambo mengi ya kuwaambia, lakini hamutaweza kuyabeba sasa.” Wakati atawamwangia roho takatifu, itawasaidia kuelewa “kweli yote,” na wataweza kuishi kulingana na kweli hiyo.—Yohana 16:12, 13.

Mitume wanavurugika kwa sababu ya maneno yenye Yesu anasema kisha hapo, anasema hivi: “Kisha wakati kidogo hamutaniona tena, na tena, kisha wakati kidogo mutaniona.” Wanaulizana ikiwa Yesu anapenda kusema nini. Yesu anatambua kuwa wanapenda kumuuliza juu ya jambo hilo, kwa hiyo anawaambia hivi: “Kwa kweli kabisa ninawaambia ninyi, mutalia na kuomboleza, lakini ulimwengu utafurahi; mutahuzunika, lakini huzuni yenu itageuka kuwa furaha.” (Yohana 16:16, 20) Wakati Yesu anauawa kisha muchana yenye kufuata, viongozi wa dini wanafurahi sana, lakini wanafunzi wake wanakuwa na huzuni. Kisha huzuni yao inabadilika na kuwa furaha wakati Yesu anafufuliwa! Na furaha yao inaendelea wakati anawamwangia roho takatifu ya Mungu.

Wakati analinganisha hali ya mitume wake na ya mwanamuke mwenye kuwa na maumivu ya kuzaa, Yesu anasema hivi: “Wakati mwanamuke iko anazaa, anakuwa na huzuni kwa sababu saa yake imekuja, lakini kisha kuzaa mutoto, hakumbuke tena taabu kwa sababu anafurahi kwamba mutu amezaliwa katika ulimwengu.” Yesu anatia moyo mitume wake kwa kusema hivi: “Ninyi pia, munahuzunika sasa; lakini nitawaona tena, na mioyo yenu itafurahi, na hakuna mutu mwenye atawanyanganya furaha yenu.”—Yohana 16:21, 22.

Mupaka wakati huu, mitume hawajafanya ombi lolote katika jina la Yesu. Sasa anasema hivi: “Siku hiyo mutamuomba Baba katika jina langu.” Sababu gani watafanya hivyo? Haiko kwa sababu baba hapendi kuwajibia. Kwa kweli, Yesu anasema hivi: “Kwa maana Baba mwenyewe anawapenda ninyi, kwa sababu mumenipenda . . . nikiwa mwakilishi wa Mungu.”—Yohana 16:26, 27.

Pengine maneno hayo yenye kutia moyo ya Yesu ndiyo yalichochea mitume kusema hivi kwa uhakika: “Kwa jambo hili tunaamini kwamba ulitoka kwa Mungu.” Uhakika huo utajaribiwa hivi karibuni. Kwa kweli, Yesu anaeleza mambo yenye yatatokea. Anasema hivi: “Muangalie! Saa inakuja, kwa kweli, imekuja, wakati kila mumoja wenu atatawanyika na kuenda kwenye nyumba yake mwenyewe na mutaniacha peke yangu.” Lakini anawahakikishia hivi: “Nimewaambia ninyi mambo haya ili kupitia mimi mukuwe na amani. Katika ulimwengu mutapata taabu, lakini musiogope! Mimi nimepata ushindi juu ya ulimwengu.” (Yohana 16:30-33) Yesu hatawaacha peke yao. Iko hakika kuwa wao pia wanaweza kupata ushindi juu ya ulimwengu, kama vile yeye amepata ushindi, kwa kufanya mapenzi ya Mungu kwa uaminifu hata kama Shetani na ulimwengu wake watajaribu kuvunja ushikamanifu wao.