Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

SURA YA 132

“Hakika Huyu Alikuwa Mwana wa Mungu”

“Hakika Huyu Alikuwa Mwana wa Mungu”

MATAYO 27:45-56 MARKO 15:33-41 LUKA 23:44-49 YOHANA 19:25-30

  • YESU ANAKUFA KWENYE MUTI

  • MAMBO YENYE HAYAKO YA KAWAIDA YANATOKEA WAKATI YESU ANAKUFA

Sasa ni “saa sita,” ao katikati ya muchana. Giza lenye haliko la kawaida linatokea “juu ya inchi yote mupaka saa kenda,” kisha muchana. (Marko 15:33) Giza hilo lenye kuogopesha halikutokea kwa sababu mwezi uliingia katikati ya dunia na jua. Hilo linatokea wakati wa mwezi mupya, lakini huu ni wakati wa Pasaka, wakati mwezi wote ni wenye kuenea. Na giza hilo linabakia kwa muda murefu sana kuliko kufanya dakika fulani kama vile inakuwa wakati mwezi unaingia katikati ya dunia na jua. Kwa hiyo, ni Mungu ndiye ameleta giza hilo!

Wazia mambo hayo yalipaswa kuwa na matokeo gani juu ya wale wenye walikuwa wanamuchekelea Yesu. Wakati wa kipindi hicho cha giza, wanamuke ine wanakaribia muti wa mateso. Wanamuke hao ni mama ya Yesu, Salome, Maria Magdalene, na Maria mama ya mutume Yakobo Mudogo.

Mutume Yohana iko pembeni ya “muti wa mateso” pamoja na mama ya Yesu mwenye kuwa na huzuni. Maria anaona namna mutoto mwenye alizaa na kukomalisha anateseka sana kwenye muti wa mateso. Jambo hilo ni kama “upanga murefu” wenye kuingizwa katika mwili wake. (Yohana 19:25; Luka 2:35) Lakini, hata kama Yesu anasikia maumivu makali sana, anahangaikia hali ya mama yake. Anajikaza sana kugeuzia kichwa chake upande wa Yohana na anamuambia mama yake hivi: “Mwanamuke, ona! Mwana wako!” Kisha anamugeukia Maria na kuambia Yohana hivi: “Ona! Mama yako!”—Yohana 19:26, 27.

Yesu anafanya mipango ili mama yake, pengine mwenye kuwa sasa mujane, achungwe na mutume mwenye anapenda sana. Yesu anajua kuwa ndugu zake wadogo, ni kusema, watoto wengine wa Maria, walikuwa hawajamuamini. Kwa hiyo anafanya mipango ili mama yake atimiziwe mahitaji yake ya kimwili na ya kiroho. Huo ni mufano muzuri sana!

Wakati giza linakaribia kuisha, Yesu anasema hivi: “Ninasikia kiu.” Kwa kufanya hivyo anatimiza maandiko. (Yohana 19:28; Zaburi 22:15) Yesu anajisikia kuwa ni kama vile Baba yake ameondoa ulinzi juu yake ili ushikamanifu wake ujaribiwe mupaka mwisho. Kristo anaita hivi pengine katika luga ya Galilaya yenye kutokana na Kiaramu: “Eli, Eli, lama sabaktani?” maana yake ni, “Mungu wangu, Mungu wangu, sababu gani umeniacha?” Watu fulani wenye wanasimama karibu naye hawaelewe maneno yake, kwa hiyo, wanasema hivi: “Munasikia! Anaita Eliya.” Mumoja wao anakimbia, anatia sifongo katika divai yenye kuwa chungu, anaitia kwenye mwisho wa utete, na kumupatia Yesu akunywe. Lakini wengine wanasema hivi: “Mumuache! Tuone kama Eliya atakuja kumushusha.”—Marko 15:34-36.

Kisha Yesu analalamika hivi: “Imetimizwa!” (Yohana 19:30) Ndiyo, ametimiza mambo yote yenye Baba yake alimutuma afanye hapa duniani. Mwishowe, Yesu anasema hivi: “Baba, ninaweka roho yangu katika mikono yako.” (Luka 23:46) Kwa hiyo, Yesu anatia uzima wake katika mikono ya Yehova, na iko hakika kuwa Mungu atamurudishia uzima huo. Yesu anamutegemea kabisa Mungu, kwa hiyo, anainamisha kichwa chake na anakufa.

Wakati huo, tetemeko kubwa la inchi linatokea, linapasua miamba. Tetemeko hilo liko na nguvu sana mupaka makaburi yenye kuwa inje ya Yerusalemu yanafunguka na maiti za watu wenye kufa zinatoka inje. Wapita njia wenye wanaona maiti hizo wanaingia katika “muji mutakatifu” na kusema mambo yenye wametoka tu kujionea.—Matayo 12:11; 27:51-53.

Wakati Yesu anakufa, pazia ndefu na yenye kuwa na uzito sana yenye kutenganisha Mahali Patakatifu na Patakatifu Zaidi inapasuka katika vipande viwili, kutoka juu mupaka chini. Matukio hayo yenye kushangaza yanaonyesha hasira ya Mungu juu ya wale wenye waliua Mwana wake na yanamaanisha kuwa njia ya kuenda Mahali Patakatifu Zaidi, ni kusema, mbinguni, inakuwa sasa wazi.—Waebrania 9:2, 3; 10:19, 20.

Kwa kweli, watu wanaogopa sana. Mukubwa wa jeshi mwenye anasimamia kuuawa kwa Yesu, anasema hivi: “Hakika mutu huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Marko 15:39) Pengine alikuwa hapo wakati Yesu alikuwa anasamba mbele ya Pilato wakati alikuwa anaulizwa ikiwa yeye ni Mwana wa Mungu ao hapana. Sasa iko hakika kuwa Yesu ni mutu mwenye kufanya mambo yenye kuwa sawa na kwa kweli yeye ni Mwana wa Mungu.

Watu wengine wenye waliona matukio hayo yenye kushangaza, wanarudia nyumbani kwao, “wakijipiga-piga kwenye vifua vyao” ili kuonyesha huzuni yao nyingi na haya. (Luka 23:48) Kati ya wale wenye kuangalia kwa mbali ni wanafunzi wanamuke wenye walikuwa wanasafiri pamoja na Yesu kwa wakati fulani. Wao pia wanaguswa sana na matukio hayo makubwa sana.