Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

A1

Kanuni za Kutafsiri Biblia

Mwanzoni Biblia iliandikwa katika Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki cha kale. Leo inapatikana ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 2,600 hivi. Idadi kubwa ya watu wanaosoma Biblia hawaelewi lugha za awali na hivyo lazima wategemee tafsiri. Ni kanuni gani zinapaswa kufuatwa katika kutafsiri Biblia, na zilitumiwaje katika kutafsiri Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya?

Huenda wengine wakafikiri kwamba tafsiri ya neno kwa neno inaweza kuwasaidia wasomaji wapate maana inayokaribiana zaidi na ile iliyo katika lugha za awali. Hata hivyo, si lazima iwe hivyo. Fikiria baadhi ya sababu:

  • Hakuna lugha mbili zinazofanana kabisa katika sarufi, msamiati, na muundo wa sentensi. Profesa wa Kiebrania, S. R. Driver, aliandika kwamba lugha “hazitofautiani tu katika sarufi na mizizi, bali pia . . . jinsi ambavyo mawazo yanaunganishwa katika sentensi.” Lugha tofauti hutumia njia tofauti za kufikiri. “Kwa hiyo,” anaendelea kusema Profesa Driver, “miundo ya sentensi katika lugha mbalimbali hutofautiana.”

  • Hakuna lugha yoyote ya kisasa inayofanana kabisa na msamiati na sarufi ya Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki kilichotumiwa kuandika Biblia, kwa hiyo, huenda tafsiri ya neno kwa neno ya Biblia isieleweke au hata nyakati nyingine ikapotosha maana.

  • Maana ya neno au maneno inaweza kubadilika ikitegemea muktadha.

Katika baadhi ya sehemu, mtafsiri anaweza kutafsiri lugha ya awali neno na kwa neno kwa usahihi, lakini anapaswa kuwa makini sana.

Ifuatayo ni baadhi ya mifano inayoonyesha jinsi tafsiri ya neno kwa neno inavyoweza kueleweka vibaya:

  • Maandiko hutumia maneno ‘kulala usingizi’ kumaanisha usingizi halisi na usingizi wa kifo. (Mathayo 28:13; Matendo 7:60) Maneno hayo yanapotumiwa kwenye muktadha unaorejezea kifo, watafsiri wa Biblia wanaweza kutumia maneno kama ‘kulala usingizi katika kifo,’ ambayo humsaidia msomaji wa kisasa aelewe maana.—1 Wakorintho 7:39; 1 Wathesalonike 4:13; 2 Petro 3:4.

  • Mtume Paulo alitumia maneno yanayopatikana katika Waefeso 4:14 ambayo yanaweza kutafsiriwa neno kwa neno kuwa “katika mchezo wa dadu wa wanaume.” Msemo huo wa kale unarejezea zoea la kuwadanganya watu kwa kutumia dadu. Katika lugha nyingi, tafsiri ya neno kwa neno ya msemo huo haieleweki vizuri. Kutafsiri msemo huo kuwa “udanganyifu wa watu” ni njia iliyo wazi zaidi ya kutokeza maana.

  • Andiko la Waroma 12:11 linatumia msemo wa Kigiriki ambao ukitafsiriwa neno na kwa neno unamaanisha “katika kuchemka kwa roho.” Katika Kiswahili, maneno hayo hayatokezi maana iliyokusudiwa, kwa hiyo katika tafsiri hii yametafsiriwa kuwa ‘kuwaka roho.’

  • MATHAYO 5:3

    Tafsiri ya neno kwa neno: “maskini wa roho”

    Wazo: “wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho”

    Katika mahubiri yake maarufu ya mlimani, Yesu alitumia maneno ambayo mara nyingi hutafsiriwa kuwa “Heri walio maskini wa roho.” (Mathayo 5:3, Union Version) Lakini katika lugha nyingi, tafsiri ya neno kwa neno ya mstari huo haieleweki. Katika visa fulani, tafsiri ya neno kwa neno inaweza kumaanisha kwamba “maskini wa roho” ni watu walio na matatizo ya kiakili au walio dhaifu na wasio na msimamo. Hata hivyo, hapa Yesu alikuwa akiwafundisha watu kwamba furaha yao haikutegemea kutosheleza mahitaji yao ya kimwili, bali kutambua kwamba wanahitaji mwongozo wa Mungu. (Luka 6:20) Kwa hiyo, maneno kama vile “wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho” au “wale wanaotambua kwamba wanamhitaji Mungu” hutokeza kwa usahihi maana ya maneno ya awali.—Mathayo 5:3; The New Testament in Modern English.

  • Katika muktadha mbalimbali, neno la Kiebrania linalotafsiriwa kuwa “wivu” linalingana na maana ya neno la Kiswahili, yaani, kukasirika kwa sababu rafiki wa karibu amekosa uaminifu au kuwaonea wivu watu kwa sababu ya mali zao. (Methali 6:34; Isaya 11:13) Hata hivyo, neno hilohilo la Kiebrania lina maana nzuri. Kwa mfano, linaweza kutumiwa kumaanisha “bidii,” au ulinzi ambao Yehova anawapa watumishi wake au jinsi anavyotaka ‘wamwabudu yeye peke yake.’ (Kutoka 34:14; 2 Wafalme 19:31; Ezekieli 5:13; Zekaria 8:2) Pia linaweza kutumiwa kumaanisha “bidii” ya watumishi wake waaminifu kwa ajili ya Mungu na ibada yake au jinsi ambavyo ‘hawavumilii ushindani wowote’ kumwelekea.—Zaburi 69:9; 119:139; Hesabu 25:11.

  • Neno la Kiebrania yadh kwa kawaida hutafsiriwa kuwa “mkono,” lakini ikitegemea muktadha, neno hili linaweza kutafsiriwa kuwa “mamlaka,” “ukarimu,” “nguvu,” na kwa njia nyingine nyingi

    Neno la Kiebrania ambalo mara nyingi hurejelea mkono wa mwanadamu lina maana mbalimbali. Ikitegemea muktadha neno hilo linaweza kutafsiriwa kuwa “mamlaka,” “ukarimu,” au “nguvu.” (2 Samweli 8:3; 1 Wafalme 10:13; Methali 18:21) Kwa kweli, neno hilo limetafsiriwa kwa zaidi ya njia 40 tofauti-tofauti katika toleo la Kiingereza la Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

Kutokana na sababu hizo, kutafsiri Biblia kunahusisha mengi zaidi ya kutafsiri neno la lugha ya awali kwa kutumia neno lilelile kila mara. Mtafsiri anapaswa kutumia busara ili kuchagua maneno ambayo yanawakilisha vizuri mawazo ya maandishi ya lugha ya awali. Isitoshe, anapaswa kupanga sentensi katika njia inayofuata sheria za sarufi za lugha inayolengwa, na hivyo kufanya maandishi yasomeke kwa urahisi.

Wakati huohuo mtafsiri hapaswi kupita mipaka anapotumia maneno tofauti ili kueleza maandishi. Mtafsiri ambaye bila kujali anafafanua ujumbe wa Biblia kulingana na jinsi anavyoelewa wazo kuu anaweza kupotosha maana ya maandishi. Jinsi gani? Mtafsiri anaweza kuingiza kimakosa maoni yake kuhusu maana ya maandishi ya awali au huenda akaondoa habari muhimu zilizo kwenye maandishi ya awali. Kwa hiyo, ingawa huenda tafsiri za Biblia zilizofafanuliwa zikasomeka kwa urahisi, nyakati nyingine huenda uhuru huo ukafanya wasomaji wasipate ujumbe halisi wa maandishi.

Ni rahisi kwa mtafsiri kuathiriwa na msimamo wa kidini. Kwa mfano, andiko la Mathayo 7:13 linasema “Barabara inayoongoza kwenye uharibifu ina nafasi kubwa.” Baadhi ya watafsiri ambao labda wameathiriwa na msimamo wa kidini, wametumia maneno “moto wa mateso” badala ya maana halisi ya neno la Kigiriki, yaani, “uharibifu.”

Pia, mtafsiri anapaswa kukumbuka kwamba Biblia iliandikwa kwa kutumia lugha iliyotumiwa na watu wa kawaida, kama vile wakulima, wachungaji, na wavuvi. (Nehemia 8:8, 12; Matendo 4:13) Kwa hiyo, tafsiri nzuri ya Biblia hufanya ujumbe wake ueleweke kwa watu wanyoofu, wa malezi mbalimbali. Maneno yaliyo wazi, ya kawaida, na yanayoeleweka kwa urahisi yanafaa kuliko maneno ambayo hayatumiwi sana na watu wa kawaida.

Idadi kubwa ya watafsiri wa Biblia wamefanya uamuzi usio na msingi wa kuondoa jina la Mungu, Yehova, kutoka katika tafsiri za kisasa ingawa jina hilo linapatikana katika hati za kale za Biblia. (Angalia Nyongeza A4.) Tafsiri nyingi huondoa jina hilo na kutumia jina la cheo, kama vile “Bwana,” na nyingine hata huficha ukweli wa kwamba Mungu ana jina. Kwa mfano, katika baadhi ya tafsiri, sala ya Yesu kwenye Yohana 17:26 inasema: “Nimekufanya ujulikane kwao,” na kwenye Yohana 17:6, “Nimekufunua kwa wale ulionipa.” Hata hivyo, tafsiri sahihi ya sala ya Yesu inasema: “Nimewajulisha jina lako,” na “Nimelifunua jina lako kwa watu ulionipa.”

Kama ilivyotajwa katika utangulizi wa toleo la kwanza la Kiingereza la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya: “Hatufafanui Maandiko. Tumejitahidi kutafsiri neno kwa neno inapowezekana, mahali ambapo misemo ya Kiingereza ya kisasa inaruhusu na mahali ambapo tafsiri ya neno kwa neno haifichi maana.” Kwa hiyo, Halmashauri ya Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya imejitahidi kusawazisha kati ya kutumia maneno na misemo inayofanana na ile iliyo kwenye hati za kale, na wakati huohuo, kuepuka maneno ambayo hayaeleweki au yanayoficha mawazo yaliyokusudiwa. Matokeo ni kwamba Biblia inaweza kusomeka kwa urahisi na msomaji anaweza kuwa na uhakika kabisa kwamba ujumbe wa Biblia ulioongozwa na roho ya Mungu umetafsiriwa kwa usahihi.—1 Wathesalonike 2:13.