Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

A3

Jinsi Biblia Ilivyotufikia

Mtungaji na Mwanzilishi wa Biblia ndiye aliyeihifadhi pia. Yeye ndiye aliyefanya maneno haya yaandikwe:

“Neno la Mungu wetu hudumu milele.”Isaya 40:8.

Maneno hayo ni ya kweli hata ingawa hakuna hati ya Biblia ya awali ya Maandiko ya Kiebrania na Kiaramu a au Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo iliyopo leo. Kwa hiyo, tunawezaje kuwa na uhakika kabisa kwamba ujumbe ulio katika Biblia leo kwa kweli ndio uliokuwa katika maandishi ya awali yaliyoongozwa na roho ya Mungu?

WANAKILI WALILIHIFADHI NENO LA MUNGU

Kuhusu Maandiko ya Kiebrania, iliwezekana kwa sababu ya desturi ya kale iliyoanzishwa na Mungu, aliyesema kwamba maandishi yanapaswa kunakiliwa. b Kwa mfano, Yehova aliwaagiza wafalme wa Israeli wajiandikie nakala zao za Sheria iliyoandikwa. (Kumbukumbu la Torati 17:18) Pia, Mungu aliwapa Walawi jukumu la kuihifadhi Sheria na kuwafundisha watu kuihusu. (Kumbukumbu la Torati 31:26; Nehemia 8:7) Baada ya Wayahudi kupelekwa utekwani Babiloni, kukawa na kikundi cha wanakili, au waandishi (Wasoferi). (Ezra 7:6, maelezo ya chini) Baada ya muda, waandishi hao walitokeza nakala nyingi za vitabu 39 vya Maandiko ya Kiebrania.

Kwa karne nyingi, waandishi walinakili vitabu hivyo kwa makini. Katika Enzi za Kati, kikundi cha waandishi Wayahudi kilichoitwa Wamasora kiliendeleza desturi hiyo. Hati kamili ya kale zaidi ya Wamasora ni Kodeksi ya Leningrad, ya mwaka 1008/1009 W.K. Hata hivyo, katikati ya karne ya 20, hati 220 za Biblia au visehemu vilipatikana kati ya Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi. Hati hizo za Biblia ziliandikwa zaidi ya miaka 1000 kabla ya Kodeksi ya Leningrad. Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi vinapolinganishwa na Kodeksi ya Leningrad jambo muhimu linathibitika: Ingawa Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi vina tofauti fulani katika maneno, tofauti hizo haziathiri ujumbe wenyewe.

Namna gani kuhusu vile vitabu 27 vya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo? Vitabu hivyo viliandikwa kwanza na baadhi ya mitume wa Yesu Kristo na wanafunzi wa mapema. Kwa kufuata desturi ya waandishi Wayahudi, Wakristo wa mapema walitokeza nakala za vitabu hivyo. (Wakolosai 4:16) Licha ya jitahada za Maliki Mroma Diokletiani na wengine kuharibu maandishi yote ya Wakristo wa mapema, maelfu ya visehemu na hati za kale zimehifadhiwa hadi leo.

Pia, maandishi ya Wakristo yalitafsiriwa katika lugha nyingine. Tafsiri za awali za Biblia zinatia ndani nakala za lugha za kale kama vile Kiarmenia, Kikoptiki, Kiethiopia, Kigeorgia, Kilatini, na Kisiria.

KUCHAGUA MAANDISHI YA KIEBRANIA NA YA KIGIRIKI KWA AJILI YA KUTAFSIRI

Si nakala zote za hati za kale za Biblia zilizo na maneno yanayofanana. Hivyo basi, tunawezaje kujua ujumbe uliokuwa katika hati za awali?

Hali hiyo inaweza kulinganishwa na mwalimu anayewaomba wanafunzi 100 wanakili sura fulani ya kitabu. Hata kama baadaye nakala ya awali itapotea, kulinganisha zile nakala 100 bado kunaweza kufunua ujumbe wa maandishi ya awali. Ingawa huenda kila mwanafunzi akafanya makosa, ni vigumu kwa wanafunzi wote kufanya makosa yaleyale. Vivyo hivyo, wasomi wanapolinganisha maelfu ya visehemu na nakala za vitabu vya Biblia vya kale vinavyopatikana, wanaweza kutambua makosa ya wanakili na kujua maneno yaliyokuwapo awali.

“Inaweza kusemwa kwa uhakika kwamba hakuna maandishi mengine ya kale yaliyowasilishwa kwa usahihi mkubwa hivyo”

Tunawezaje kuwa na uhakika kwamba mawazo yaliyokuwa katika maandishi ya awali ya Biblia yamewasilishwa kwetu kwa usahihi? Akizungumza kuhusu maandishi ya Maandiko ya Kiebrania, msomi William H. Green alisema hivi: “Inaweza kusemwa kwa uhakika kwamba hakuna maandishi mengine ya kale yaliyowasilishwa kwa usahihi mkubwa hivyo.” Kuhusu Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambayo huitwa Agano Jipya, msomi wa Biblia F. F. Bruce aliandika hivi: “Uthibitisho wa maandishi yetu ya Agano Jipya ni mkubwa zaidi kuliko uthibitisho wa maandishi mengi ya waandikaji wa kale, na hakuna mtu anayeweza kutilia shaka usahihi wake.” Pia anasema: “Ikiwa Agano Jipya lingekuwa mkusanyo wa maandishi ya kilimwengu, usahihi wake haungetiliwa shaka kamwe.”

Sura ya 40 ya kitabu cha Isaya katika Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi (ya mwaka wa 125 mpaka 100 K.W.K.)

Yanapolinganishwa na hati za Kiebrania zilizoandikwa miaka elfu moja baadaye, kuna tofauti ndogo tu, hasa katika kuandika maneno

Sura ya 40 ya kitabu cha Isaya katika Kodeksi ya Aleppo, hati muhimu ya Kiebrania ya Wamasora ya karibu mwaka wa 930 W.K.

Maandishi ya Kiebrania: Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kiebrania katika Kiingereza (1953-1960) ilitegemea Biblia Hebraica, ya Rudolf Kittel. Tangu wakati huo, matoleo yaliyoboreshwa ya maandishi ya Kiebrania, yaani, Biblia Hebraica Stuttgartensia na Biblia Hebraica Quinta, yameongeza utafiti wa karibuni unaotegemea Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi na hati nyingine za kale. Maandishi hayo ya wasomi yanafanana na Kodeksi ya Leningrad na yana maelezo ya chini yaliyo na maneno yenye ulinganifu kutoka vyanzo vingine, kutia ndani Pentateuki ya Samaria, Vitabu vya Kukunjwa vya Bahari ya Chumvi, Septuajinti ya Kigiriki, Targumi za Kiaramu, Vulgate ya Kilatini, na Peshitta ya Kisiria. Biblia Hebraica Stuttgartensia na Biblia Hebraica Quinta zilitumiwa katika kuandaa toleo hili la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

Maandishi ya Kigiriki: Mwishoni mwa karne ya 19 , msomi B. F. Westcott na F.J.A. Hort walilinganisha hati za Biblia na visehemu vilivyokuwapo walipokuwa wakiandaa maandishi ya Kigiriki ambayo walihisi yalikaribiana zaidi na maandishi ya awali. Katikati ya karne ya 20 Halmashauri ya Biblia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitumia maandishi hayo kama msingi wa tafsiri yao. Pia, walitumia mafunjo mengine ya kale, yanayodhaniwa kuwa ya karne ya pili au ya tatu W.K. Tangu wakati huo, mafunjo mengi zaidi yamepatikana. Isitoshe, maandishi kama yale ya Nestle na Aland na ya United Bible Societies yana utafiti wa karibuni zaidi wa wasomi. Baadhi ya habari zilizo katika utafiti huo zimetumiwa katika toleo hili.

Kwa msingi wa maandishi hayo, ni wazi kwamba baadhi ya mistari katika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo iliyokuwa katika tafsiri za zamani, kama vile King James Version, kwa kweli ilikuwa imeongezwa na wanakili wa baadaye na haikuwa kamwe sehemu ya Maandiko yaliyoongozwa na roho ya Mungu. Hata hivyo, kwa kuwa kugawanywa kwa mistari ambako kwa kawaida kunakubalika katika tafsiri za Biblia tayari kulikuwa kumeanzishwa katika karne ya 16, kuondolewa kwa mistari hiyo huacha mapengo katika mistari fulani ya Biblia nyingi. Mistari hiyo ni Mathayo 17:21; 18:11; 23:14; Marko 7:16; 9:44, 46; 11:26; 15:28; Luka 17:36; 23:17; Yohana 5:4; Matendo 8:37; 15:34; 24:7; 28:29; na Waroma 16:24. Katika toleo hili lililorekebishwa, mistari hiyo iliyoondolewa ina maelezo ya chini mahali inapopatikana.

Kuhusu umalizio mrefu wa Marko 16 (mistari ya 9-20), umalizio mfupi wa Marko 16, na maneno yaliyo kwenye Yohana 7:53–8:11, ni wazi kwamba mistari hiyo haikuwa katika hati za awali. Kwa hiyo, maandishi hayo yaliyoongezwa hayajawekwa kwenye toleo hili. c

Baadhi ya maneno yamerekebishwa ili kutia ndani mawazo ambayo kwa kawaida wasomi huyakubali kuwa mawazo sahihi zaidi ya maandishi ya awali. Kwa mfano, kulingana na baadhi ya hati, andiko la Mathayo 7:13 linasema: “Ingieni kupitia lango jembamba, kwa sababu lango ni pana, na barabara inayoongoza kwenye uharibifu ina nafasi kubwa.” Katika matoleo yaliyotangulia ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, maneno “lango ni” hayakuwapo. Hata hivyo, uchunguzi zaidi wa hati ulithibitisha kwamba maneno “lango ni” yalikuwa katika maandishi ya awali. Basi yalitiwa ndani kwenye toleo hili. Kuna marekebisho mengine kama hayo. Hata hivyo, marekebisho hayo ni madogo, na hayabadili ujumbe wa msingi wa Neno la Mungu.

Hati ya mafunjo ya 2 Wakorintho 4:13–5:4 ya karibu mwaka wa 200 W.K.

a Kuanzia hapa yanarejelewa kama Maandiko ya Kiebrania.

b Sababu moja iliyofanya hati zinakiliwe ni kwamba hati za awali ziliandikwa kwenye vitu vilivyoharibika haraka.

c Habari zaidi kuhusu kwa nini mistari hiyo inaonwa kuwa ya kuongezwa inaweza kupatikana kwenye maelezo ya chini ya Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya—Yenye Marejezo katika Kiingereza ya mwaka 1984.