Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati 16:1-43
16 Basi wakaliingiza Sanduku la Mungu wa kweli na kuliweka ndani ya hema ambalo Daudi alikuwa amepiga ili aliweke humo;+ nao wakatoa dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika mbele za Mungu wa kweli.+
2 Daudi alipomaliza kutoa dhabihu za kuteketezwa+ na dhabihu za ushirika,+ akawabariki watu katika jina la Yehova.
3 Isitoshe, aliwagawia Waisraeli wote, kila mwanamume na mwanamke, mkate mmoja wa mviringo, keki ya tende, na keki ya zabibu kavu.
4 Kisha akawaweka baadhi ya Walawi wahudumu mbele ya Sanduku la Yehova,+ wamheshimu,* wamshukuru, na kumsifu Yehova Mungu wa Israeli.
5 Asafu+ alikuwa kiongozi, na wa pili Zekaria; naye Yeieli, Shemiramothi, Yehieli, Matithia, Eliabu, Benaya, Obed-edomu, na Yeieli+ walipiga vinanda na vinubi;+ na Asafu alipiga matoazi,+
6 na makuhani Benaya na Yahazieli walipiga tarumbeta daima mbele ya sanduku la agano la Mungu wa kweli.
7 Hiyo ndiyo siku ambayo Daudi kwa mara ya kwanza alitunga* wimbo huu wa kumshukuru Yehova na kumwagiza Asafu+ na ndugu zake wauimbe:
8 “Mshukuruni Yehova,+ liitieni jina lake,Yajulisheni mataifa matendo yake!+
9 Mwimbieni, mwimbieni sifa,*+Tafakarini* kazi zake zote zinazostaajabisha.+
10 Jivunieni jina lake takatifu.+
Mioyo ya wale wanaomtafuta Yehova na ishangilie.+
11 Mtafuteni Yehova+ na nguvu zake,Utafuteni uso* wake daima.+
12 Kumbukeni kazi zinazostaajabisha alizofanya,+Miujiza yake na hukumu alizotangaza,
13 Enyi uzao wa* Israeli mtumishi wake,+Enyi wana wa Yakobo, watu wake aliowachagua.+
14 Yeye ni Yehova Mungu wetu.+
Hukumu zake ziko duniani kote.+
15 Kumbukeni agano lake milele,Ahadi aliyotoa,* hata kufikia vizazi elfu,+
16 Agano alilofanya na Abrahamu,+Na kiapo alichomwapia Isaka,+
17 Alichotoa kama amri kwa Yakobo+Na kama agano la kudumu kwa Israeli,
18 Akisema, ‘Nitakupa nchi ya Kanaani+Kuwa urithi wako uliogawiwa.’+
19 Mlipokuwa wachache,Naam, wachache sana, nanyi mlikuwa wageni nchini.+
20 Walitembeatembea kutoka taifa moja hadi taifa lingine,Kutoka ufalme mmoja hadi ufalme mwingine.+
21 Hakumruhusu mtu yeyote awakandamize,+Lakini kwa sababu yao aliwakaripia wafalme,+
22 Akisema, ‘Msiwaguse watiwa-mafuta wangu,Wala msiwatendee manabii wangu jambo lolote baya.’+
23 Mwimbieni Yehova, dunia yote!
Tangazeni wokovu wake siku baada ya siku!+
24 Tangazeni utukufu wake miongoni mwa mataifa,Kazi zake zinazostaajabisha miongoni mwa mataifa yote.
25 Kwa maana Yehova ni mkuu na anastahili kusifiwa kuliko wote.
Anaogopesha kuliko miungu mingine yote.+
26 Miungu yote ya mataifa ni miungu ya ubatili,+Lakini Yehova ndiye aliyeziumba mbingu.+
27 Mbele zake kuna utukufu* na fahari;+Katika makao yake kuna nguvu na shangwe.+
28 Mpeni Yehova anachostahili, enyi familia za mataifa,Mpeni Yehova anachostahili kwa sababu ya utukufu wake na nguvu zake.+
29 Mpeni Yehova utukufu ambao jina lake linastahili;+Leteni zawadi na mje mbele zake.+
Mwinamieni* Yehova katika mapambo matakatifu.*+
30 Tetemekeni mbele zake, dunia yote!
Dunia imeimarishwa kabisa; haiwezi kusogezwa.*+
31 Mbingu na zishangilie, dunia na iwe na shangwe;+Tangazeni miongoni mwa mataifa: ‘Yehova amekuwa Mfalme!’+
32 Bahari na ingurume na vitu vyote vinavyoijaza;Mashamba na vitu vyote vilivyomo na vishangilie.
33 Wakati uleule miti ya msituni na ishangilie kwa sauti mbele za Yehova,Kwa maana anakuja* kuihukumu dunia.
34 Mshukuruni Yehova, kwa maana yeye ni mwema;+Upendo wake mshikamanifu unadumu milele.+
35 Nanyi semeni, ‘Tuokoe, Ee Mungu wa wokovu wetu,+Tukusanye na kutuokoa kutoka katika mataifa,Ili tulishukuru jina lako takatifu+Na tushangilie kukusifu wewe.+
36 Yehova, Mungu wa Israeli, na asifiweKwa umilele wote.’”*
Na watu wote wakasema, “Amina!”* nao wakamsifu Yehova.
37 Kisha Daudi akamwacha Asafu+ na ndugu zake hapo mbele ya sanduku la agano la Yehova ili wahudumu daima mbele ya Sanduku+ hilo, kulingana na utaratibu wa kila siku.+
38 Obed-edomu na ndugu zake, watu 68, na Obed-edomu mwana wa Yeduthuni, na Hosa walikuwa walinzi wa malango;
39 na kuhani Sadoki+ na makuhani wenzake walikuwa mbele ya hema la ibada la Yehova mahali pa juu kule Gibeoni+
40 ili wamtolee Yehova kwa ukawaida dhabihu za kuteketezwa kwenye madhabahu ya dhabihu za kuteketezwa, asubuhi na jioni, na kufanya mambo yote yaliyoandikwa katika Sheria ya Yehova aliyowaamuru Waisraeli wafuate.+
41 Walikuwa pamoja na Hemani na Yeduthuni+ na wanaume wengine waliochaguliwa na kutajwa majina ili wamshukuru Yehova,+ kwa sababu “upendo wake mshikamanifu unadumu milele”;+
42 nao walikuwa pamoja na Hemani+ na Yeduthuni ili wapige tarumbeta, matoazi, na ala zilizotumiwa kumsifu* Mungu wa kweli; na wana wa Yeduthuni+ walikuwa langoni.
43 Kisha watu wote wakaenda nyumbani kwao, na Daudi akaenda kuwabariki watu wa nyumba yake mwenyewe.
Maelezo ya Chini
^ Tnn., “wamkumbuke.”
^ Au “alichangia.”
^ Au “mpigieni muziki.”
^ Au labda, “Zungumzeni kuhusu.”
^ Au “uwepo.”
^ Au “wazao wa.” Tnn., “mbegu ya.”
^ Tnn., “Neno aliloamuru.”
^ Au “adhama.”
^ Au labda, “kwa sababu ya fahari ya utakatifu wake.”
^ Au “Mwabuduni.”
^ Au “kutikiswa; kufanywa ipepesuke.”
^ Au “amekuja.”
^ Au “milele na milele.”
^ Au “Na iwe hivyo!”
^ Au “na ala za wimbo wa.”