Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati 28:1-21

  • Hotuba ya Daudi kuhusu ujenzi wa hekalu (1-8)

  • Maagizo aliyompa Sulemani; ampa ramani ya ujenzi (9-21)

28  Kisha Daudi akawakusanya Yerusalemu wakuu wote wa Israeli: wakuu wa makabila, viongozi wa vikundi+ vilivyomhudumia mfalme, wakuu wa maelfu na wakuu wa mamia,+ wasimamizi wa mali zote za mfalme na mifugo yake+ na wa wanawe,+ pamoja na maofisa wa makao ya mfalme na kila mwanamume hodari mwenye uwezo.+  Halafu Mfalme Daudi akasimama na kusema: “Nisikilizeni, ndugu zangu na watu wangu. Moyo wangu ulitamani kujenga nyumba ambamo sanduku la agano la Yehova lingekaa* na ambayo ingekuwa kiti cha miguu cha Mungu wetu,+ nami nilifanya matayarisho ya kuijenga.+  Lakini Mungu wa kweli akaniambia, ‘Hutajenga nyumba kwa ajili ya jina langu,+ kwa maana wewe ni mtu wa vita, nawe umemwaga damu.’+  Hata hivyo, Yehova Mungu wa Israeli alinichagua kutoka katika nyumba yote ya baba yangu niwe mfalme wa Israeli milele,+ kwa maana alimchagua Yuda kuwa kiongozi+ na kutoka katika nyumba ya Yuda aliichagua nyumba ya baba yangu,+ na kati ya wana wa baba yangu alinikubali mimi niwe mfalme wa Israeli yote.+  Na kutoka kati ya wanangu wote—kwa maana Yehova amenipa wana wengi+—alimchagua Sulemani mwanangu+ aketi kwenye kiti cha ufalme wa Yehova juu ya Israeli.+  “Akaniambia, ‘Sulemani mwana wako ndiye atakayeijenga nyumba yangu na nyua zangu, kwa maana nimemchagua yeye kuwa mwanangu, nami nitakuwa baba yake.+  Nitauimarisha kabisa ufalme wake milele+ ikiwa atazishika kwa dhati amri zangu na sheria zangu,*+ kama anavyofanya sasa.’  Basi, nasema machoni pa Waisraeli wote, kutaniko la Yehova, na masikioni mwa Mungu wetu: Shikeni kwa uangalifu na mtafute amri zote za Yehova Mungu wenu, ili mwimiliki nchi nzuri+ na kuwaachia wana wenu kuwa urithi wa kudumu baada yenu.  “Nawe, Sulemani mwanangu, mjue Mungu wa baba yako na kumtumikia kwa moyo kamili*+ na kwa nafsi* yenye shangwe;* kwa maana Yehova huichunguza kabisa mioyo yote,+ naye hutambua kila mwelekeo wa fikira.+ Ukimtafuta, atakuruhusu umpate,+ lakini ukimwacha, atakukataa milele.+ 10  Ona kwamba Yehova amekuchagua wewe ujenge nyumba ili iwe mahali patakatifu. Uwe jasiri, anza kazi.” 11  Kisha Daudi akampa Sulemani mwana wake ramani ya ujenzi+ wa ukumbi+ na ya nyumba zake, maghala yake, vyumba vyake vya darini, vyumba vyake vya ndani, na nyumba ya kifuniko cha upatanisho.*+ 12  Alimpa ramani ya kila kitu alichoambiwa kupitia mwongozo wa roho kuhusu ujenzi wa nyua+ za nyumba ya Yehova, vyumba vyote vya kulia chakula vilivyoizunguka, hazina za nyumba ya Mungu wa kweli, na hazina za vitu vilivyofanywa kuwa vitakatifu;*+ 13  pia kuhusu vikundi vya makuhani+ na Walawi, kuhusu kazi zote za utumishi wa nyumba ya Yehova, na kuhusu vyombo vyote vya utumishi wa nyumba ya Yehova; 14  pia kuhusu uzito wa dhahabu, dhahabu ya vyombo vyote vya utumishi mbalimbali, uzito wa vyombo vyote vya fedha, na vyombo vyote vya utumishi mbalimbali; 15  pia uzito wa vinara vya taa vya dhahabu+ na taa zake za dhahabu, uzito wa vinara mbalimbali vya taa na taa zake, na uzito wa vinara vya taa vya fedha, uzito wa kila kinara cha taa na taa zake kulingana na matumizi yake; 16  pia kuhusu uzito wa dhahabu za meza za mikate ya tabaka,*+ uzito wa kila meza, na pia fedha kwa ajili ya meza za fedha, 17  kuhusu nyuma,* mabakuli, magudulia ya dhahabu safi, na uzito wa mabakuli madogo ya dhahabu,+ uzito wa kila bakuli dogo, na uzito wa mabakuli madogo ya fedha, uzito wa kila bakuli dogo. 18  Pia alimpa uzito wa dhahabu safi kwa ajili ya madhabahu ya uvumba+ na kwa ajili ya mfano wa lile gari,+ yaani, wale makerubi+ wa dhahabu walionyoosha mabawa yao na kulifunika sanduku la agano la Yehova. 19  Daudi akasema: “Mkono wa Yehova ulikuwa juu yangu, naye alinipa ufahamu wa kuandika+ mambo yote kuhusu ramani hii ya ujenzi.”+ 20  Kisha Daudi akamwambia Sulemani mwanawe: “Uwe jasiri na imara na uanze kazi. Usiogope wala usihofu, kwa maana Yehova Mungu, Mungu wangu, yuko pamoja nawe.+ Hatakuacha wala kukutupa,+ lakini atakuwa pamoja nawe mpaka kazi yote ya utumishi wa nyumba ya Yehova itakapokamilika. 21  Na hivi ndivyo vikundi vya makuhani+ na vya Walawi+ kwa ajili ya utumishi wote wa nyumba ya Mungu wa kweli. Una wafanyakazi walio tayari, na wenye ustadi wa kufanya utumishi wa kila aina,+ na pia wakuu+ na watu wote watakaotekeleza maagizo yako yote.”

Maelezo ya Chini

Tnn., “lingepumzikia.”
Tnn., “maamuzi yangu ya hukumu.”
Au “kwa hiari.”
Angalia Kamusi.
Au “wenye ujitoaji kamili.”
Au “nyumba ya kufunika dhambi.”
Au “vilivyowekwa wakfu.”
Yaani, mikate ya wonyesho.
Wingi wa kifaa kinachoitwa uma.