Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati 29:1-30

  • Michango kwa ajili ya hekalu (1-9)

  • Sala ya Daudi (10-19)

  • Watu washangilia; utawala wa Sulemani (20-25)

  • Kifo cha Daudi (26-30)

29  Sasa Mfalme Daudi akaliambia kutaniko lote: “Mwanangu Sulemani, ambaye Mungu amemchagua+ ni mchanga na hana uzoefu,*+ na kazi hii ni kubwa, kwa maana si hekalu* kwa ajili ya mwanadamu, bali ni kwa ajili ya Yehova Mungu.+  Nami nimejitahidi kabisa kufanya matayarisho kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu, nimetoa dhahabu ya kutengenezea vitu vya dhahabu, fedha ya kutengenezea vitu vya fedha, shaba ya kutengenezea vitu vya shaba, chuma kwa ajili ya vitu vya chuma,+ mbao+ za kutengenezea vitu vya mbao, mawe ya shohamu, na vito vinavyounganishwa kwa saruji, na vijiwe maridadi vya mviringo, kila aina ya mawe yenye thamani, na mawe mengi sana ya alabasta.  Isitoshe, kwa sababu ninaipenda nyumba ya Mungu wangu,+ ninatoa pia hazina yangu binafsi+ ya dhahabu na fedha kwa ajili ya nyumba ya Mungu wangu, pamoja na vitu vyote nilivyotayarisha kwa ajili ya nyumba hiyo takatifu,  na pia talanta 3,000* za dhahabu ya Ofiri+ na talanta 7,000 za fedha iliyosafishwa, ili zitumiwe kufunika kuta za nyumba,  dhahabu ya kutengenezea vitu vya dhahabu na fedha ya kutengenezea vitu vya fedha, na kwa ajili ya kazi yote itakayofanywa na mafundi. Basi ni nani anayejitolea kuja leo akiwa na zawadi mkononi kwa ajili ya Yehova?”+  Basi wakuu wa koo,* wakuu wa makabila ya Israeli, wakuu wa maelfu na wa mamia,+ na wakuu wa kazi za mfalme+ wakajitolea kwa hiari.  Nao wakatoa kwa ajili ya utumishi wa nyumba ya Mungu wa kweli: talanta 5,000 za dhahabu, dariki 10,000,* talanta 10,000 za fedha, talanta 18,000 za shaba, na talanta 100,000 za chuma.  Mtu yeyote aliyekuwa na mawe yenye thamani aliyatoa kwa ajili ya hazina ya nyumba ya Yehova, chini ya usimamizi wa Yehieli+ Mgershoni.+  Watu walishangilia kwa sababu walitoa matoleo hayo ya hiari, kwa maana walimtolea Yehova matoleo hayo ya hiari kwa moyo kamili,+ na Mfalme Daudi pia alishangilia sana. 10  Kisha Daudi akamsifu Yehova mbele ya kutaniko lote. Daudi akasema: “Na usifiwe, Ee Yehova Mungu wa Israeli baba yetu, kwa umilele wote.* 11  Ee Yehova, ukuu ni wako+ na nguvu+ na uzuri na fahari na utukufu,*+ kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako.+ Ufalme ni wako, Ee Yehova.+ Wewe Ndiye unayejikweza mwenyewe ukiwa mkuu* juu ya vyote. 12  Utajiri na utukufu hutoka kwako,+ nawe hutawala kila kitu,+ na mkononi mwako mna nguvu+ na uwezo,+ na mkono wako unaweza kumfanya mtu awe mkuu+ na unaweza kuwapa wote nguvu.+ 13  Na sasa, Ee Mungu wetu, tunakushukuru na kulisifu jina lako linalovutia. 14  “Lakini, mimi ni nani na watu wangu ni nani hivi kwamba tukutolee matoleo haya ya hiari? Kwa maana kila kitu kinatoka kwako, nasi tumekupa vitu vinavyotoka mkononi mwako mwenyewe. 15  Kwa maana sisi ni wakaaji wageni mbele zako na wahamiaji, kama walivyokuwa mababu zetu wote.+ Kwa kuwa siku zetu duniani ni kama kivuli+—hatuna tumaini. 16  Ee Yehova Mungu wetu, utajiri huu wote ambao tumetayarisha ili kukujengea nyumba kwa ajili ya jina lako takatifu unatoka mkononi mwako mwenyewe, wote ni mali yako. 17  Ee Mungu wangu, najua vizuri kwamba wewe huuchunguza moyo,+ na kwamba unapendezwa na utimilifu.*+ Kwa unyoofu wa moyo wangu, nimetoa kwa hiari vitu hivi vyote, nami nimefurikwa na shangwe kuwaona watu wako walio hapa wakikutolea matoleo ya hiari. 18  Ee Yehova, Mungu wa Abrahamu, Isaka, na Israeli, mababu zetu, idumishe mielekeo hii na fikira hizi katika mioyo ya watu wako milele, na uielekeze mioyo yao kwako.+ 19  Mpe mwanangu Sulemani moyo kamili,*+ ili ashike amri zako, vikumbusho vyako,+ na masharti yako na kufanya mambo haya yote na kujenga hekalu* ambalo nimelifanyia matayarisho.”+ 20  Kisha Daudi akaliambia kutaniko lote: “Sasa msifuni Yehova Mungu wenu.” Na kutaniko lote likamsifu Yehova Mungu wa mababu zao, wakainama chini na kumsujudia Yehova na mfalme. 21  Nao wakaendelea kumtolea Yehova dhabihu na kumtolea Yehova dhabihu za kuteketezwa+ siku iliyofuata, ng’ombe dume wachanga 1,000, kondoo dume 1,000, wanakondoo dume 1,000, na matoleo yake ya vinywaji;+ walitoa dhabihu nyingi sana kwa ajili ya Waisraeli wote.+ 22  Wakaendelea kula na kunywa mbele za Yehova siku hiyo kwa shangwe nyingi,+ nao wakamweka Sulemani mwana wa Daudi kuwa mfalme kwa mara ya pili na kumtia mafuta mbele za Yehova ili awe kiongozi,+ na pia Sadoki kuwa kuhani.+ 23  Na Sulemani akaketi kwenye kiti cha ufalme cha Yehova+ akiwa mfalme baada ya Daudi baba yake, akafanikiwa, na Waisraeli wote walimtii. 24  Wakuu wote,+ mashujaa wote hodari,+ na pia wana wote wa Mfalme Daudi+ wakajitiisha wenyewe chini ya Mfalme Sulemani. 25  Na Yehova akamfanya Sulemani kuwa mkuu sana machoni pa Waisraeli wote na kumpa fahari ya kifalme ambayo hakuna mfalme yeyote wa Israeli aliyewahi kuwa nayo kabla yake.+ 26  Kwa hiyo Daudi mwana wa Yese alitawala Israeli yote, 27  alitawala Israeli kwa miaka 40. Alitawala huko Hebroni kwa miaka 7,+ na Yerusalemu kwa miaka 33.+ 28  Naye akafa akiwa amezeeka kabisa;+ aliishi maisha marefu yenye kuridhisha, akiwa na utajiri, na utukufu; na Sulemani mwanawe akawa mfalme baada yake.+ 29  Historia ya Mfalme Daudi, kuanzia mwanzo mpaka mwisho, imeandikwa katika maandishi ya mwonaji Samweli, nabii Nathani,+ na mwonaji Gadi,+ 30  pamoja na utawala wake wote, ukuu wake, na matukio yanayohusu nyakati zake na nyakati za Israeli na falme zote zilizomzunguka.

Maelezo ya Chini

Au “ngome; jumba la mfalme.”
Au “hana uwezo.”
Talanta moja ilikuwa na uzito wa kilogramu 34.2. Angalia Nyongeza B14.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Dariki ilikuwa sarafu ya dhahabu ya Waajemi. Angalia Nyongeza B14.
Au “milele na milele.”
Au “adhama.”
Tnn., “kichwa.”
Au “hali ya kutokuwa na lawama; unyoofu.”
Au “wenye ujitoaji kamili.”
Au “ngome au jumba la mfalme.”