Kitabu cha Kwanza cha Mambo ya Nyakati 5:1-26

  • Wazao wa Rubeni (1-10)

  • Wazao wa Gadi (11-17)

  • Wahagri washindwa (18-22)

  • Nusu ya kabila la Manase (23-26)

5  Hawa ndio wana wa Rubeni,+ mzaliwa wa kwanza wa Israeli. Yeye ndiye aliyekuwa mzaliwa wa kwanza, lakini kwa sababu alikichafua* kitanda cha baba yake,+ haki yake ya mzaliwa wa kwanza walipewa wana wa Yosefu+ mwana wa Israeli, kwa hiyo hakuandikishwa katika orodha ya ukoo kwamba ana haki ya mzaliwa wa kwanza.  Ingawa Yuda+ alikuwa mkuu kuliko ndugu zake na kiongozi alitoka kwake,+ haki ya mzaliwa wa kwanza ilikuwa ya Yosefu.  Wana wa Rubeni mzaliwa wa kwanza wa Israeli walikuwa Hanoki, Palu, Hezroni, na Karmi.+  Wana wa Yoeli walikuwa Shemaya mwanawe, Gogu mwana wa Shemaya, Shimei mwana wa Gogu,  Mika mwana wa Shimei, Reaya mwana wa Mika, Baali mwana wa Reaya,  na Beera mwana wa Baali, ambaye Mfalme Tilgath-pilneseri+ wa Ashuru alimpeleka uhamishoni; alikuwa mkuu wa Warubeni.  Ndugu zake walioandikishwa katika orodha ya koo kulingana na koo zao na kulingana na wazao wao walikuwa, Yeieli, aliyekuwa kiongozi wao, Zekaria,  na Bela mwana wa Azazi mwana wa Shema mwana wa Yoeli, aliyeishi Aroeri+ mpaka Nebo na Baal-meoni.+  Naye aliishi upande wa mashariki mpaka mahali ambapo nyika inaanzia kwenye Mto Efrati,+ kwa maana mifugo yao ilikuwa imeongezeka sana katika nchi ya Gileadi.+ 10  Katika siku za utawala wa Sauli, walipigana vita na Wahagri, nao wakawashinda, wakakaa katika mahema yao kwenye eneo lote lililo upande wa mashariki wa Gileadi. 11  Wazao wa Gadi waliishi karibu nao katika nchi ya Bashani mpaka kule Saleka.+ 12  Yoeli ndiye aliyekuwa kiongozi wao, Shafamu alikuwa wa pili, na Yanai na Shafati walikuwa viongozi kule Bashani. 13  Na ndugu zao wa koo* zao walikuwa Mikaeli, Meshulamu, Sheba, Yorai, Yakani, Zia, na Eberi, jumla ya watu saba. 14  Hao ndio waliokuwa wana wa Abihaili mwana wa Huri mwana wa Yaroa mwana wa Gileadi mwana wa Mikaeli mwana wa Yeshishai mwana wa Yahdo mwana wa Buzi. 15  Ahi mwana wa Abdieli mwana wa Guni alikuwa kiongozi wa ukoo wao.* 16  Waliishi Gileadi,+ kule Bashani+ na katika miji yake, na katika malisho yote ya Sharoni kufikia mipakani mwake. 17  Wote waliandikishwa kulingana na koo zao katika siku za utawala wa Mfalme Yothamu+ wa Yuda na katika siku za utawala wa Mfalme Yeroboamu*+ wa Israeli. 18  Watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase walikuwa na mashujaa hodari 44,760 katika jeshi lao waliobeba ngao na mapanga na kujihami kwa pinde,* nao walikuwa wamezoezwa kwa ajili ya vita. 19  Walipigana vita na Wahagri,+ Wayeturi, Wanafishi,+ na Wanodabu. 20  Mungu aliwasaidia kupigana nao, akawatia mikononi mwao Wahagri na wote waliokuwa pamoja nao, kwa maana walimwomba Mungu awasaidie vitani, akasikiliza maombi yao kwa sababu walimtumaini.+ 21  Waliteka nyara mifugo yao—ngamia 50,000, kondoo 250,000, na punda 2,000—na pia watu 100,000. 22  Wengi waliuawa, kwa sababu Mungu wa kweli ndiye aliyepigana vita hivyo.+ Nao waliendelea kuishi katika nchi yao mpaka walipopelekwa uhamishoni.+ 23  Wazao wa nusu ya kabila la Manase+ waliishi katika nchi hiyo kuanzia Bashani mpaka Baal-hermoni na Seniri na Mlima Hermoni.+ Walikuwa wengi sana. 24  Hawa ndio waliokuwa viongozi wa koo* zao: Eferi, Ishi, Elieli, Azrieli, Yeremia, Hodavia, na Yahdieli; walikuwa mashujaa hodari, wanaume maarufu, na viongozi wa koo* zao. 25  Lakini hawakutenda kwa uaminifu kumwelekea Mungu wa mababu zao, wakafanya ukahaba na miungu ya mataifa yaliyokuwa nchini,+ mataifa ambayo Mungu alikuwa ameyaangamiza kutoka mbele yao. 26  Kwa hiyo Mungu wa Israeli akaichochea roho ya Mfalme Pulu wa Ashuru+ (yaani, Mfalme Tilgath-pilneseri+ wa Ashuru) hivi kwamba akawapeleka uhamishoni watu wa kabila la Rubeni, Gadi, na nusu ya kabila la Manase, akawapeleka Hala, Habori, Hara, na mto Gozani,+ nao wako huko hadi leo.

Maelezo ya Chini

Au “alikitia unajisi.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, Yeroboamu wa Pili.
Tnn., “na kukanyaga upinde.”
Yaani, ukoo wa upande wa baba.
Yaani, ukoo wa upande wa baba.