Kitabu cha Kwanza cha Samweli 1:1-28

  • Elkana na wake zake (1-8)

  • Hana ambaye hakuwa na mtoto asali apate mwana (9-18)

  • Samweli azaliwa na kukabidhiwa kwa Yehova (19-28)

1  Sasa kulikuwa na mwanamume fulani kutoka Ramathaim-sofimu*+ katika eneo lenye milima la Efraimu+ aliyeitwa Elkana,+ mwana wa Yerohamu, mwana wa Elihu, mwana wa Tohu, mwana wa Sufu, Mwefraimu.  Alikuwa na wake wawili, mmoja aliitwa Hana na mwingine aliitwa Penina. Penina alikuwa na watoto, lakini Hana hakuwa na watoto.  Mwaka baada ya mwaka mwanamume huyo alitoka katika jiji lake na kupanda kwenda Shilo kumwabudu* na kumtolea dhabihu Yehova wa majeshi.+ Wana wawili wa Eli, Hofni na Finehasi,+ walitumikia huko wakiwa makuhani wa Yehova.+  Siku moja Elkana alipotoa dhabihu, alimpa Penina mke wake na wanawe na mabinti zake wote sehemu za dhabihu hiyo,+  lakini akampa Hana sehemu ya pekee, kwa sababu alimpenda sana Hana; lakini Yehova hakuwa amempa watoto.*  Isitoshe, mke mwenzake alimdhihaki daima ili kumkasirisha kwa sababu Yehova hakuwa amempa watoto.  Hivyo ndivyo alivyofanya mwaka baada ya mwaka; kila mara Hana alipopanda kwenda katika nyumba ya Yehova,+ mke mwenzake alimdhihaki sana hivi kwamba alilia na kushindwa kula.  Lakini Elkana mume wake alimuuliza: “Hana, kwa nini unalia, na kwa nini huli chakula, na kwa nini umehuzunika sana?* Je, mimi si bora kwako kuliko wana kumi?”  Basi siku moja Hana alisimama baada ya wao kumaliza kula na kunywa huko Shilo. Wakati huo, kuhani Eli alikuwa ameketi kwenye kiti karibu na mwimo wa mlango wa hekalu*+ la Yehova. 10  Hana alikuwa na uchungu mwingi sana,* akaanza kusali kwa Yehova+ na kulia sana. 11  Naye akaweka nadhiri hii: “Ee Yehova wa majeshi, ikiwa utayaona mateso yangu mimi mtumishi wako na kunikumbuka na usiponisahau mimi mtumishi wako, nawe unipe mtoto wa kiume,+ nitamtoa awe wa Yehova sikuzote za maisha yake, na hakuna wembe utakaogusa kichwa chake.”+ 12  Alipokuwa akisali kwa muda mrefu mbele za Yehova, Eli alikuwa akiangalia kinywa chake. 13  Hana alikuwa akisali moyoni mwake, midomo yake tu ndiyo iliyokuwa ikitetemeka, lakini sauti yake haikusikika. Basi Eli akafikiri kuwa amelewa. 14  Eli akamwambia, “Utaendelea kuwa mlevi mpaka lini? Acha kunywa divai.” 15  Ndipo Hana akamwambia, “Sivyo, bwana wangu! Mimi ni mwanamke mwenye mkazo mkubwa sana;* sijanywa divai wala kinywaji chochote chenye kileo, bali ninaimwaga nafsi* yangu mbele za Yehova.+ 16  Usidhani mtumishi wako ni mwanamke asiyefaa kitu, kwa maana muda huo wote nimekuwa nikiongea katika uchungu mwingi na mateso yangu.” 17  Ndipo Eli akamwambia, “Nenda kwa amani, na Mungu wa Israeli akupe ulichoomba.”+ 18  Basi Hana akamwambia, “Mtumishi wako na apate kibali machoni pako.” Ndipo mwanamke huyo akaenda zake, akala chakula, na uso wake haukuwa na huzuni tena. 19  Wakaamka asubuhi na mapema na kuinama mbele za Yehova, kisha wakarudi nyumbani kwao kule Rama.+ Elkana akafanya ngono na Hana mke wake, na Yehova akamkumbuka.*+ 20  Katika muda wa mwaka mmoja* Hana alipata mimba, akazaa mwana na kumwita+ mwana huyo Samweli,* kwa maana alisema, “nilimwomba kutoka kwa Yehova.” 21  Baada ya muda Elkana akaenda pamoja na familia yake yote kumtolea Yehova dhabihu+ ya kila mwaka na pia dhabihu yake ya nadhiri. 22  Lakini Hana hakwenda+ kwa sababu alimwambia hivi mume wake: “Mara tu nitakapomwachisha mvulana huyu kunyonya, nitampeleka mbele za Yehova, naye atabaki huko kuanzia wakati huo na kuendelea.”+ 23  Ndipo Elkana mume wake akamwambia, “Fanya unaloona linafaa.* Kaa nyumbani mpaka utakapomwachisha kunyonya. Yehova na atimize jambo ulilosema.” Basi mwanamke huyo akakaa nyumbani, akaendelea kumnyonyesha mwana wake mpaka alipomwachisha kunyonya. 24  Mara tu alipomwachisha kunyonya, alimpeleka Shilo pamoja na ng’ombe dume wa miaka mitatu, efa* moja ya unga, na mtungi mkubwa wa divai,+ naye pamoja na mvulana huyo wakafika katika nyumba ya Yehova huko Shilo.+ 25  Kisha wakamchinja huyo ng’ombe dume na kumpeleka mvulana huyo kwa Eli. 26  Ndipo Hana akasema, “Niwie radhi, bwana wangu! Kwa hakika kama unavyoishi,* bwana wangu, mimi ndiye yule mwanamke aliyekuwa amesimama pamoja nawe mahali hapa ili kusali kwa Yehova.+ 27  Nilisali nipate mvulana huyu, naye Yehova akanipa nilichoomba.+ 28  Sasa nami pia, ninamkabidhi Yehova mvulana huyu. Siku zake zote, amekabidhiwa kwa Yehova.” Naye* akainama chini mbele za Yehova.

Maelezo ya Chini

Au “kutoka Rama, Msufu.”
Au “kumwinamia.”
Tnn., “alikuwa amefunga tumbo lake la uzazi.”
Au “na kwa nini moyo wako unahisi vibaya?”
Yaani, hema la ibada.
Au “uchungu nafsini.”
Angalia Kamusi.
Au “mwanamke aliyefadhaika sana rohoni.”
Au “akamwelekezea fikira.”
Au labda, “Wakati unaofaa ulipofika.”
Maana yake “Jina la Mungu.”
Tnn., “lililo jema machoni pako.”
Efa ilikuwa sawa na lita 22 au kilogramu 13 hivi. Angalia Nyongeza B14.
Au “Kwa uhai wa nafsi yako.”
Inaonekana ni Elkana.