Kitabu cha Kwanza cha Samweli 10:1-27

  • Sauli atiwa mafuta kuwa mfalme (1-16)

  • Sauli atangazwa kuwa mfalme mbele ya watu (17-27)

10  Ndipo Samweli akachukua chupa ya mafuta na kuyamimina juu ya kichwa cha Sauli.+ Akambusu na kusema: “Yehova amekutia mafuta uwe kiongozi+ juu ya urithi wake.+  Tutakapoachana leo, utakuta wanaume wawili karibu na kaburi la Raheli+ katika eneo la Benjamini kule Selsa, nao watakwambia, ‘Punda ulioenda kutafuta wamepatikana, lakini sasa baba yako amesahau kuhusu punda hao+ naye ana wasiwasi juu yako. Anauliza, “Nitafanya nini kuhusu mwanangu?”’  Kutoka huko nenda mpaka kwenye mti mkubwa wa Tabori, na huko utakutana na wanaume watatu wakipanda kwenda kwa Mungu wa kweli kule Betheli,+ mmoja akiwa amebeba wanambuzi watatu, mwingine akiwa amebeba mikate mitatu, na mwingine akiwa amebeba mtungi mkubwa wa divai.  Watakusalimu na kukupa mikate miwili, unapaswa kuchukua mikate hiyo.  Kisha utafika kwenye kilima cha Mungu wa kweli, mahali ambapo pana kambi ya kijeshi ya Wafilisti. Utakapofika jijini, utakutana na kikundi cha manabii wakishuka kutoka mahali pa juu, na kinanda na tari na filimbi na kinubi vitapigwa mbele yao huku wakitoa unabii.  Roho ya Yehova itakutia nguvu,+ utatoa unabii pamoja nao, nawe utabadilishwa kuwa mtu tofauti.+  Baada ya ishara hizo kutokea, fanya lolote unaloweza kufanya kwa mkono wako, kwa sababu Mungu wa kweli yuko pamoja nawe.  Kisha ushuke na kunitangulia kwenda Gilgali,+ nami nitakufuata huko ili nitoe dhabihu za kuteketezwa na dhabihu za ushirika. Unapaswa kungoja kwa siku saba mpaka nitakapofika. Halafu nitakujulisha jambo unalopaswa kufanya.”  Mara tu Sauli alipogeuka ili amwache Samweli, Mungu akaanza kuubadili moyo wake uwe kama wa mtu mwingine, na ishara hizo zote zikatimia siku hiyo. 10  Basi wakatoka hapo na kupanda kwenye kilima, na kikundi cha manabii kikakutana naye. Mara moja roho ya Mungu ikamtia nguvu,+ naye akaanza kutoa unabii+ kati yao. 11  Watu wote waliomjua awali walipomwona akitoa unabii pamoja na manabii, wakaulizana: “Mwana wa Kishi amepatwa na nini? Je, Sauli pia ni mmoja wa manabii?” 12  Ndipo mtu fulani wa mahali hapo akasema: “Lakini baba yao ni nani?” Basi kukawa na msemo* huu: “Je, Sauli pia ni mmoja wa manabii?”+ 13  Alipomaliza kutoa unabii, akaenda mahali pa juu. 14  Baadaye ndugu ya baba ya Sauli akamuuliza Sauli na mtumishi wake: “Mlienda wapi?” Akajibu: “Kuwatafuta punda,+ lakini hatukuwapata, kwa hiyo tukaenda kwa Samweli.” 15  Ndugu ya baba ya Sauli akamuuliza: “Tafadhali niambie, Samweli alikuambia nini?” 16  Sauli akamjibu: “Alituambia kwamba tayari punda wamepatikana.” Lakini Sauli hakumwambia jambo ambalo Samweli alisema kuhusu ufalme. 17  Kisha Samweli akawaita watu ili wakusanyike mbele za Yehova huko Mispa,+ 18  akawaambia Waisraeli: “Yehova, Mungu wa Israeli anasema hivi: ‘Mimi ndiye niliyewatoa Waisraeli nchini Misri na kuwaokoa kutoka mikononi mwa Misri+ na kutoka mikononi mwa falme zote zilizokuwa zikiwakandamiza. 19  Lakini leo mmemkataa Mungu wenu+ aliyekuwa Mwokozi wenu aliyewaokoa kutoka katika maovu yenu yote na taabu zenu, nanyi mlisema: “Hatutaki, unapaswa kumweka mfalme atutawale.” Sasa simameni mbele za Yehova kulingana na makabila yenu na kulingana na maelfu yenu.’”* 20  Basi Samweli akaagiza makabila yote ya Israeli yakaribie,+ na kabila la Benjamini likachaguliwa.+ 21  Kisha akaagiza kabila la Benjamini likaribie kulingana na koo zao, basi ukoo wa Wamatri ukachaguliwa. Mwishowe Sauli mwana wa Kishi akachaguliwa.+ Lakini walipoenda kumtafuta, hawakumpata. 22  Kwa hiyo wakamuuliza Yehova:+ “Je, mtu huyo tayari amefika hapa?” Yehova akajibu: “Ndiye yule pale, amejificha kati ya mizigo.” 23  Basi wakakimbia na kumleta kutoka mahali hapo. Aliposimama katikati ya watu, alikuwa mrefu kuliko watu wote nao walimfikia mabegani.+ 24  Samweli akawaambia watu wote: “Je, mnamwona yule ambaye Yehova amemchagua,+ kwamba hakuna yeyote aliye kama yeye kati ya watu wote?” Basi watu wote wakaanza kupiga kelele wakisema: “Mfalme na aishi muda mrefu!” 25  Samweli akawaambia watu kuhusu haki za wafalme+ na kuziandika katika kitabu na kukiweka mbele za Yehova. Kisha Samweli akawaruhusu watu wote waende zao, kila mtu akaenda nyumbani kwake. 26  Sauli pia akaenda nyumbani kwake kule Gibea, akiwa pamoja na mashujaa ambao Yehova alikuwa amegusa mioyo yao. 27  Lakini wahuni fulani wakasema: “Huyu atatuokoaje?”+ Kwa hiyo wakamdharau, nao hawakumletea zawadi yoyote.+ Lakini hakusema jambo lolote kuhusu hilo.*

Maelezo ya Chini

Yaani, methali.
Au “koo zenu.”
Tnn., “Naye alikuwa kama bubu.”