Kitabu cha Kwanza cha Samweli 11:1-15

  • Sauli awashinda Waamoni (1-11)

  • Sauli atangazwa tena kuwa mfalme (12-15)

11  Nahashi Mwamoni+ akapanda na kupiga kambi ili kushambulia Yabeshi+ kule Gileadi. Watu wote wa Yabeshi wakamwambia Nahashi: “Fanya agano* pamoja nasi, nasi tutakutumikia.”  Nahashi Mwamoni akawaambia: “Nitafanya agano pamoja nanyi kwa sharti hili: macho yenu yote ya kulia yang’olewe. Nitafanya hivyo ili kuwaaibisha Waisraeli wote.”  Wazee wa Yabeshi wakamwambia: “Tupe muda wa siku saba ili tuwatume wajumbe katika eneo lote la Israeli. Na ikiwa hakuna yeyote wa kutuokoa, tutajisalimisha kwako.”  Baada ya muda, wajumbe hao wakafika katika jiji la Gibea+ la Sauli na kuwaambia watu wote maneno hayo, na watu wote wakalia kwa sauti kubwa sana.  Lakini Sauli alikuwa akitoka shambani akiwa nyuma ya mifugo yake, naye akauliza: “Watu wana shida gani? Kwa nini wanalia?” Basi wakamwambia maneno yaliyosemwa na watu wa Yabeshi.  Roho ya Mungu ikamtia nguvu Sauli+ alipoyasikia maneno hayo, akawaka hasira.  Kwa hiyo akachukua ng’ombe dume wawili, akawakata vipandevipande, akawatuma wajumbe wavipeleke katika eneo lote la Israeli wakisema: “Mtu yeyote ambaye hamfuati Sauli na Samweli ajue kwamba ng’ombe wake watafanyiwa hivi!” Na watu wakashikwa na hofu ya Yehova hivi kwamba wakatoka wote pamoja.*  Kisha akawahesabu kule Bezeki, Waisraeli walikuwa 300,000 na watu wa Yuda walikuwa 30,000.  Kwa hiyo wakawaambia wajumbe waliokuwa wamekuja: “Hivi ndivyo mnavyopaswa kuwaambia watu wa Yabeshi kule Gileadi, ‘Kesho wakati wa jua kali mtaokolewa.’” Basi wale wajumbe wakaja na kuwaambia watu wa Yabeshi, nao wakashangilia sana. 10  Ndipo watu wa Yabeshi wakasema: “Kesho tutajisalimisha kwenu, nanyi mtatutendea mpendavyo.”+ 11  Siku iliyofuata, Sauli aliwagawa watu katika vikosi vitatu, nao wakaingia katikati ya kambi wakati wa kesha la alfajiri* na kuwaua Waamoni+ mpaka jua lilipokuwa kali. Watu waliookoka walitawanywa hivi kwamba hakuna watu wawili waliobaki pamoja. 12  Kisha watu wakamwambia Samweli: “Ni nani waliokuwa wakiuliza, ‘Je, Sauli atakuwa mfalme wetu?’+ Waleteni watu hao ili tuwaue.” 13  Hata hivyo, Sauli akasema: “Hakuna mtu yeyote anayepaswa kuuawa leo,+ kwa maana leo Yehova amewaokoa Waisraeli.” 14  Baadaye Samweli akawaambia watu: “Njooni twende Gilgali+ tukamtangaze tena mfalme.”+ 15  Basi watu wote wakaenda Gilgali, na huko Gilgali wakamweka Sauli kuwa mfalme mbele za Yehova. Kisha wakatoa huko dhabihu za ushirika mbele za Yehova,+ na Sauli na watu wote wa Israeli wakasherehekea kwa shangwe kubwa.+

Maelezo ya Chini

Au “makubaliano.”
Tnn., “kama mtu mmoja.”
Yaani, kuanzia saa 8 hivi usiku hadi saa 12 asubuhi.