Kitabu cha Kwanza cha Samweli 12:1-25

  • Hotuba ya mwisho ya Samweli (1-25)

    • ‘Msifuate vitu vya ubatili’ (21)

    • Yehova hatawaacha watu wake (22)

12  Hatimaye Samweli akawaambia hivi Waisraeli wote: “Tazameni nimefanya* mambo yote mliyoomba nifanye, nami nimemweka mfalme awatawale.+  Sasa huyu ndiye mfalme anayewaongoza ninyi!*+ Lakini mimi ni mzee mwenye mvi, na wanangu wako hapa pamoja nanyi,+ nami nimewaongoza tangu nilipokuwa kijana mpaka leo hii.+  Niko mbele yenu. Toeni ushahidi dhidi yangu mbele za Yehova na mbele ya mtiwa-mafuta wake:+ Nimechukua ng’ombe dume wa nani au punda wa nani?+ Au nimemlaghai nani au kumkandamiza nani? Nimepokea rushwa kutoka kwa nani ili nipotoshe haki?*+ Ikiwa nimefanya hivyo, nitawarudishia.”+  Nao wakasema: “Hujatulaghai wala kutukandamiza wala kupokea kitu chochote kile kutoka mkononi mwa yeyote.”  Basi akawaambia: “Yehova ni shahidi dhidi yenu, na mtiwa-mafuta wake ni shahidi leo kwamba hamkupata shtaka lolote dhidi yangu.”* Nao wakasema: “Yeye ni shahidi.”  Basi Samweli akawaambia watu: “Yehova, aliyemtumia Musa na Haruni na ambaye aliwatoa mababu zenu nchini Misri,+ ni shahidi.  Sasa simameni mahali penu, nami nitawahukumu mbele za Yehova kwa msingi wa matendo yote ya uadilifu ambayo Yehova amewatendea ninyi na mababu zenu.  “Baada tu ya Yakobo kuingia Misri+ na mababu zenu kuanza kumlilia Yehova awasaidie,+ Yehova alimtuma Musa+ na Haruni ili wawaongoze mababu zenu kutoka Misri na kuwawezesha kuishi mahali hapa.+  Lakini walimsahau Yehova Mungu wao, naye akawauza+ mikononi mwa Sisera+ mkuu wa jeshi la Hasori na mikononi mwa Wafilisti+ na mikononi mwa mfalme wa Moabu,+ na maadui hao wakapigana nao. 10  Nao wakamlilia Yehova awasaidie+ na kusema, ‘Tumetenda dhambi,+ kwa maana tumekuacha wewe, Yehova, ili kuabudu Mabaali+ na sanamu za Ashtorethi;+ sasa tuokoe kutoka mikononi mwa maadui wetu ili tukutumikie.’ 11  Ndipo Yehova akamtuma Yerubaali+ na Bedani na Yeftha+ na Samweli,+ naye akawaokoa ninyi kutoka mikononi mwa maadui waliowazunguka, ili mwishi kwa usalama.+ 12  Mlipoona kwamba Nahashi,+ mfalme wa Waamoni amekuja kuwashambulia, mliniambia tena na tena, ‘Hatutaki, tumeazimia kuwa na mfalme wa kututawala!’+ hata ingawa Yehova Mungu wenu ndiye Mfalme wenu.+ 13  Sasa huyu ndiye mfalme mliyemchagua, mliyeomba. Tazameni! Yehova amemweka mfalme awatawale.+ 14  Mkimwogopa Yehova+ na kumtumikia+ na kuitii sauti yake+ na msipoasi agizo la Yehova, na ikiwa ninyi pamoja na mfalme anayewatawala mtamfuata Yehova Mungu wenu, itakuwa vyema. 15  Lakini msipotii sauti ya Yehova na mkiasi agizo la Yehova, mkono wa Yehova utawashambulia ninyi na baba zenu.+ 16  Sasa simameni mahali penu mwone jambo hili kubwa ambalo Yehova anatenda mbele ya macho yenu. 17  Je, huu si wakati wa kuvuna ngano? Nitamwomba Yehova alete ngurumo na mvua; ndipo mtakapojua na kuelewa uovu mkubwa mliofanya machoni pa Yehova kwa kuomba mfalme awatawale.”+ 18  Basi Samweli akamwomba Yehova, naye Yehova akaleta ngurumo na mvua siku hiyo, hivi kwamba watu wote wakamwogopa sana Yehova na pia Samweli. 19  Na watu wote wakamwambia Samweli: “Sali kwa Yehova Mungu wako kwa ajili ya watumishi wako,+ kwa maana hatutaki kufa, kwa sababu tumeongeza uovu mwingine juu ya dhambi zetu zote kwa kuomba tupewe mfalme.” 20  Basi Samweli akawaambia watu: “Msiogope. Kwa kweli mmetenda uovu huu wote. Ila tu msigeuke na kuacha kumfuata Yehova,+ mtumikieni Yehova kwa moyo wenu wote.+ 21  Msigeuke na kufuata vitu vya ubatili,*+ ambavyo havina faida yoyote+ na ambavyo haviwezi kuokoa, kwa sababu ni vitu vya ubatili.* 22  Kwa ajili ya jina lake kuu,+ Yehova hatawaacha watu wake,+ kwa sababu Yehova ameamua mwenyewe kuwafanya ninyi kuwa watu wake.+ 23  Lakini mimi, siwezi kamwe kuwazia kumtendea Yehova dhambi kwa kuacha kusali kwa ajili yenu, nami nitaendelea kuwafundisha njia iliyo njema na iliyo sawa. 24  Ila tu mwogopeni Yehova,+ mtumikieni kwa uaminifu* kwa moyo wenu wote, kwa maana angalieni mambo makuu aliyowatendea.+ 25  Lakini mkifanya uovu bila kujali, ninyi pamoja na mfalme wenu mtafagiliwa mbali.”+

Maelezo ya Chini

Tnn., “nimesikiliza sauti yenu kuhusiana na.”
Tnn., “anayetembea mbele yenu.”
Tnn., “ili inifanye nitazame upande mwingine.”
Tnn., “hamkupata chochote mkononi mwangu.”
Au “vya kuwaziwa.”
Au “vya kuwaziwa.”
Au “kwa unyoofu.”